Header Ads

LightBlog

Jamii itatulinda

HOJA iko mezani. Viongozi 11 wametuhumiwa na vyama vya upinzani nchini kuwa wametenda, au wamesaidia kutenda au wamenyamazia hujuma na ufisadi nchini kwa kipindi cha miaka saba sasa.

Mwandishi wa habari wa gazeti hili alikuwa kwenye mkutano wa hadhara ambako wapinzani walitaja majina ya watuhumiwa wote, mmoja baada ya mwingine; bila kunong’ona bali kwa sauti ya juu na kwa kupitia vipaza sauti.

Kazi yetu kama chombo cha habari ni kusambaza taarifa hiyo, kama tunavyosambaza habari nyingine; kwa kuwaeleza wasomaji wetu nani alisema, alisema nini, alisemea wapi, alimsema nani na alikuwa akimwambia nani.

MwanaHALISI limefanya hivyo. Hii ni kwa kuzingatia msingi wa kuandika ukweli; kuandika kwa usahihi; likitekeleza haki na wajibu wake kwa jamii.

Lakini tangu tulipoandika majina ya watuhumiwa, tumekuwa tukipokea simu nyingi zikiuliza: Kwa nini mmemtaja mkubwa huyu? Ninyi hamuogopi? Mbona magazeti mengine yanasema watu hao hawapaswi kutajwa hadharani? Mbona yanadai sheria inakataza?

Ni kweli baadhi ya magazeti yameandika, tena siyo mara moja, kwamba hawataji majina ya watuhumiwa kutokana na misingi ya “taaluma na sheria.”

MwanaHALISI linaamini kwamba aliyetajwa Temeke, Dar es Salaam ndiye huyohuyo ambaye Mtwara, Pemba, Kyaka na Kigoma wanataka kujua. Kukataa kutaja jina ni kuendesha ushirikina katikakati ya teknolojia ya habari.

Wananchi waliokuwa kwenye mkutano jana; wakasikia majina yakitajwa na kurudiwa na leo wanaambiwa vyombo vya habari havipaswi kuyataja, wataelewaje vyombo hivyo?

Tunaamini kwamba wananchi wana haki ya kujua na vyombo vya habari vina haki ya kuwapa, kwa usahihi, kile kilichotendeka.

Kama kuna maadili ambayo yanazuia kuandika ukweli ni maadili ya wasiopenda ukweli na siyo uandishi wa habari. Kama kuna sheria inayozuia kuadika ukweli, basi hiyo ndiyo sheria ya kuasi haraka na mapema.

Taaluma ya habari ikifunikwa na siasa, kwa ngonjera na nyimbo za wasifu; na waandishi wa habari wakageuzwa mawakala wa mwanasiasa mmojammoja, haki ya watu ya kupata habari na taarifa itakuwa imezikwa.

MwanaHALISI halitaki kushiriki ushirikina wala njama za kuua haki, uhuru na wajibu wa mwandishi na jamii. Atakayetajwa hadharani ataandikwa. Na katika hili, jamii itasimama nasi.

(Tahariri ya gazeti la MwanaHALISI, toleo maalum juu ya ufisadi – kesho 21 Septemba 2007. Gazeti hili lilitaja majina yote 11 ya viongozi waliotuhumiwa ufisadi yakiwemo ya rais wa sasa Jakaya Kikwete na aliyestaafu, Benjamin Mkapa).

2 comments

Ansbert Ngurumo said...

Asante sana. Tanzania yetu inahitaji waandishi waasi kama wewe. Naona hata kwetu waliingia mtego huo huo wa kutii sheria chafu. Nimeamua kuwataja watuhumiwa katika Maswali Magumu Jumapili hii katika staili ambayo itawalazimisha wahariri wasiyafute majina hayo. Nasubiri kuona kama yametumika. Mmefanya kazi nzuri. Huku ndiko kuandika ukweli. Hongera sana!

Unknown said...

Mimi nawapongeza sana Gazeti la Mwanahalisi, nasema hongera sana na fanyeni kazi yenu bila kuyumbishwa na wenye kukumbatia ufisadi. Kosa lenu liko wapi?? Majina mlitoa kwa mujibu wa Dk Slaa! leo hii wanawatishia kuwapeleka mahakani. Ukweli Unauma. Kazeni Butu.

Powered by Blogger.