Header Ads

LightBlog

DC AKISHINDWA SERIKALI IMESHINDWA

DC Tarime anapokiri kushindwa

Na Ndimara Tegambwage


SITAKI kauli na mipango ya mkuu wa wilaya (DC) ya Tarime, Frank Uhahula aliyoitoa hivi karibuni. Inatishia maisha ya wananchi.

Gazeti hili lilichapisha habari kuwa mkuu huyo ametishia “kufuta shughuli za ufugaji wa ng’ombe mkoani Mara, endapo wenyeji wa mkoa huo wataendelea kuibiana mifugo, hali ambayo inachangia vitendo vya mauaji.”

Kwa kuwa hakuna taarifa zozote za kukanusha taarifa hiyo tangu ichapishwe, 7 Septemba mwaka huu, inaweza kuchukuliwa kuwa ni kweli alitoa kauli hiyo.

Katika hali ya kawaida, kauli hiyo haiwezi kutolewa na mkuu wa wilaya aliyepata mafunzo ya uongozi; aliyekulia katika mfumo wa uongozi au mwenye maarifa juu ya taaluma ya uongozi.

Ni muhimu kurudia, kurudia na kurudia kusema kuwa uongozi ni menejimenti na menejimenti haiji tu kwa kuteuliwa kuwa mkuu wa mahali fulani.

Ama umesomea shuleni, umepata mafunzo kwa njia mbalimbali, umeelekezwa ukiwa kazini na umetenda kwa kutumia misingi husika.

Katika baadhi ya nchi, ukuu wa wilaya na mkoa ni vyeo vinavyojazwa na watumishi ambao wamefikia ngazi fulani katika mpangilio wa madaraka serikalini. Hachomolewi mtu kutoka popote kule na kufanywa DC.

Mahali pengine vyeo hivi hupewa wale waliopata mafunzo na wenye maarifa ya uongozi na wamethibitika kuelewa jinsi ya kutumia taaluma hiyo ya menejimenti ya watu na raslimali zao.

Haikutarajiwa basi, kusikia mkuu wa wilaya ya Tarime akitishia “kufuta ufugaji” ng’ombe mkoani Mara. Amekerwa sana? Hana njia ya kukabili tatizo la wizi? Ameshindwa kazi? Anakiri kwa niaba ya serikali kwamba utawala wa nchi umeshindwa kudhibiti wizi wa mifugo Tarime?

Kama mkuu wa wilaya ameshindwa kazi, si amwambie aliyemteua, tena kimyakimya, “Mzee hapa sipawezi,” ili atafutiwe pengine au aachwe njiapanda? Si kauli ya DC inadhalilisha hata serikali nzima? Na serikali ikishindwa, wananchi wafanyeje?

Hata hiyo kauli ya DC ilitolewa mahali pabaya. Ni pale alipokuwa anazindua kikundi cha ulinzi shirikishi wa wananchi na polisi katika kijiji cha Kitenga. Je, kwa kauli hiyo alitaka kusema kuwa hata uzinduzi wa ulinzi aliokuwa anafanya haukuwa wa maana yoyote?

Kauli ya DC iligongana na kauli ya Polisi Jamii wa Mkoa Maalum wa Tarime-Rorya aliyesema ndani ya polisi kuna askari “wachache” wanaosaidiana na wezi wa mifugo. Alitaka wafichuliwe.

Kumbe tatizo siyo mifugo. Tatizo siyo wafugaji. Tatizo ni wizi. Wizi ni uhalifu endelevu unaoweza kukabiliwa na njia endelevu. Kama hakuna njia hizo endelevu, basi akili za watawala zitakwama; watalia, watalalamika na kujawa ghadhabu; watashindwa kazi.

Kwa kauli ya DC, ambayo ni kauli ya serikali, wizi wa ng’ombe ukiendelea, serikali “itafuta” ufugaji huo. Wizi wa mbuzi ukianza na kupanuka, serikali itafuta ufugaji wa mbuzi. Wizi wa kondoo ukianza na kuenea, serikali itafuta ufugaji wa kondoo; na wizi wa kuku ukishamiri, serikali itafuta ufugaji wa kuku!

Fanya mwendelezo hapa. Kila kinachoshindikana kipigwe marufuku. Watu wakiibiana mno nguo, serikali ifute uvaaji nguo. Wakiibiana mno chakula, serikali ifute kilimo cha mazao ya chakula. Wakiibiana mno fedha, serikali izuie watu kuwa na fedha!

Hii ndiyo dhana ya “Uhahulism” inayotokana na fikra za Uhahula wa Tarime. Huku ndiko kukiri kushindwa.

Uhahula anapendekeza kufuta mifugo. Maana yake ni kwamba hajui uhusiano kati ya wananchi na mifugo yao. Inaonekana hajajitahidi kujifunza mazingira ya watu aliokabidhiwa kuongoza na hana ujuzi na maarifa ya kutawala.

Mifugo ni uhai wa wafugaji. Mifugo ni mali. Mifugo ni fedha. Mifugo ni benki. Mingi au michache kama ilivyo, mifugo ndio utajiri wa pili kwa wafugaji. Kwanza ni watu – ndugu na marafiki ulionao; na pli ni mifugo.

Kwa hiyo kutenganisha wafugaji na mifugo ni kuwaondolea uhai – chakula – lishe ya nyama na maziwa. Ni kuwaondolea usalama wa maisha – watakosa kinga na kimbilio pale watakapokuwa na matatizo ya kiuchumi.

Kufuta mifugo ni kupora mali za wafugaji; ni kuwaibia fedha; ni kubomoa mabenki yao; ni kuua udugu, urafiki na uwezo wa jamii wa kujilisha, kujitunza na kuweka misingi kwa jamii zao za baadaye.

Hili ndilo linadhihirisha hatari iliyopo pale viongozi wanapokuwa hawakutokana na mkondo wa ngazi za utawala; wanapokuwa wa kuotesha tu, na hasa wanapokuwa wanaamini kuwa kila kitu huenda kwa amri na siyo fikra na ushawishi.

Kinachosikitisha zaidi ni kwamba mkutano alikohutubia DC haukuwa wa wezi wa ng’ombe. Ulikuwa wa wafugaji na wananchi wengine, hata kama ndani yake kulikuwa na watuhumiwa wawili au watatu.

Kwa hiyo vitisho vya DC, kama vililenga wezi, basi havikuwafikia au viliwachochea. Kilichofika kwa wengi ni hatua za uonevu ambazo serikali wilayani ilikuwa inaahidi kwa watu na mali zao. Huu siyo uongozi. Siyo utawala.

Kuna haja ya kurudia kuuliza: Serikali ikishindwa kazi ya ulinzi wa watu na mali zao, na ikakiri hivyo, wananchi wafanyeje? Labda wananchi na viongozi wao wa kweli wanajua. Tuwasikilize.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
(Makala hii imechapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili, toleo ya 13 Septemba 2009)

1 comment

James said...

Ndg Mwandishi wa makala haya, kwanza nikupongeze kwa mtiririko mzuri wa uchambuzi huu.

Pili niseme wazi kuwa siyo tu Uhahula peke yake ndio haelewi au kutotambua wafugaji na ufugaji wao, bali serikali hii kwa ujumla; wanasema "hakuna wafugaji Tanzania bali kuna Wachungaji"! Ni jambo la kusikitisha kuona kuwa serikali haiwajali Wafugaji kiasi cha kutishia kufuta ufugaji! Embu ajaribu kutishia kufuta kilimo aone cha mtema kuni!

Nachozungumzia hapa nikwamba WAFUGAJI wa nchi hii wamekuwa wakinyanyaswa sana na serikali mpaka kufikia hatua serikali ikatamka wazi kuwa wafugaji warudi kwao walikotoka kana kwamba wametokea kuzimuni wakaibukia ghafla Tanzania!

Mzee wetu Ndimara, kaelezea vizuri sana kuhusu wafugaji na ufugaji wao kuwa ndio maisha yao, uhai wao na kila kitu bila ufugaji kwao maisha ni bure.

Wafugaji ni wazalendo wa nchi hii wana haki sawa na stahiki kama mkulima, wafanyabiashara wa Kariakoo na tena zaidi ya wawekezaji wabovu na matapeli wanaokumbatiwa na serikali kwa sababu wanazozijua wao.

Aidha kuna dhana potofu iliyozuka na tunafahamu ilikoanzia kuwa WAFUGAJI ni waharibifu wa mazingira, lakini swali la kujiuliza tena rahisi la darasa la pili B; Wafugaji hawakuanza leo kufuga Tanzania, walikuwepo hata kabla ya ukoloni mpaka leo, walikuwa wakihama na makundi makubwa ya mifugo, SWALI: Kama ni waharibifu wa mazingira na vyanzo vya maji, nchi hii si ingekuwa JANGWA? Wanyama wanaotegemea nyasi na maji ambao pia wanaishi na hao wafugaji nao pia si wangetoweka? Je tungekua na urithi wa kujivunia kuwa nasi tuna wanyamapori? Kwa wale waliotembelea mbuga za Ngorongoro watanielewa nachozungumza! Huko Wafugaji na mifugo yao wanaishi pamoja na wanyama na hakuna uharibifu wa mazingira ulotokea. Tujifunze kutoka huko, tusiongee na kuandika tu bila kufanya tafiti( No Research No Right to Speak)!

Nakupongeza tena mwandishi wa makala haya kwa kutambua ukandamizaji, udhalilishwaji na uonevu unaofanywa dhidi ya wafugaji wazalendo na wenye haki zote za kuishi na kuendeleza maisha na ufugaji wao katika nchi yao.

Gideon Sanago.

Powered by Blogger.