Header Ads

LightBlog

MKUTANO WA 8 WA SULLIVAN

Porojo za mkutano wa Sullivan


Na Ndimara Tegambwage

SITAKI Watanzania wajigambe kuwa walifanya kazi kubwa ya kuinadi nchi kwa wajumbe wa Mkutano wa Nane wa Leon Sullivan uliomalizika Alhamisi iliyopita mjini Arusha.

Ni kweli walisema wana ardhi kubwa. Kwamba sehemu kubwa ya ardhi inayoweza kulimwa haijalimwa. Hivyo wanahitajika wawekezaji katika kilimo kikubwa.

Watakuwa wamewaambia wageni wapatao 4,000, wengi kutoka Marekani, Marekani Kusini na Afrika, kwamba nchi ina “utajiri mkubwa” wa mbuga nyingi za wanyama. Wawekeze.

Kwamba wanyama walioko nchini, wigi na aina zake, hawako nchi nyingine yoyote duniani. Hapa ndio kikomo.

Rais Kikwete alifanya kitu kimoja kizuri. Aliwaambia kwamba katika moja ya mbuga kuna simba ambao ni hodari wa kupanda miti. Kwa hiyo waliokuwa wanategemea kupanda miti pindi kasheshe likitokea, wafikirie njia nyingine ya kujikinga!

Wawakilishi wa Tanzania watakuwa wamejieleza kwa wageni kwamba nchi ina mlima mrefu kupita yote Afrika, Kilimanjaro, na kwamba wanaotaka kudumu kwa kijigamba kwamba wamekuwa kileleni mwake, wajiandae kuukwea.

Bila shaka kulikuwa na simulizi zilizokolezwa kwa ngano za kale juu ya uzuri wa Visiwa vya Zanzibar na Pemba na historia ya utumwa na mapinduzi ya mwaka 1964.

Hakuna awezaye kusema kuwa wenyeji hawakueleza kuwa nchi hii ina umoja, amani na utulivu na kwamba hivyo ndivyo vyombo muhimu vilivyolea taifa kwa zaidi ya miaka 47.

Hoja kuu zilikuwa: Wageni karibu sana muwekeze katika kilimo, utalii na miundombinu katika nchi yenye watu wenye upendo na wakarimu.

Yote yalisemwa kuiremba nchi na watu wake. Wageni nao waliimba ngonjera na mashairi juu ya ubora wa Tanzania na utukufu wake kisiasa; uimara wa serikali na bashasha ya watu wake.

Unapokuwa unauza kitumbua, usimwambie mnunuzi ngano ilimwagika wakati mtoto akitoka dukani. Akikuta mchanga “atajiju.” Usimwambie anayenunua maziwa kuwa inzi wawili walikuwa wameanguka humo. Akikuta mbawa atajua la kufanya. Hivyo ndivyo Watanzania walivyoendesha shughuli zao kwenye Mkutano wa Sullivan.

Hawakueleza wageni kuwa ndani ya taifa letu kuna wakwapuaji; tena wakubwa ambao wamefanya wananchi wengi kubaki masikini. Kwa hiyo wakati wawekezaji wanalenga kuimarika na kusaidia kuinua taifa, wakwapuaji wanaweza kuangamiza biashara au uzalishaji.

Hawakueleza kuwa kuna nafasi ya kuanzisha makampuni hewa, yakachota mabilioni ya shilingi na kutokomea nje ya nchi; yakiacha makorongo wizarani, benki kuu, mifukoni na akilini.

Bila shaka hakuna aliyewaeleza kuwa katika taifa hili bado watawala hawajaamua kulinda mitaji yake; kwa hiyo mitaji huburutwa hadi nje ya nchi na kuacha ukame wa fedha na bidhaa.

Hata wanaoanzisha miradi na kukopa kutoka mabenki ili wazalishe na kuuza bidhaa nchi za nje, bado hawajawekewa utaratibu. Kwingineko walikoamka, hupewi fedha mpaka ifahamike utauza wapi na kwamba ni baadhi ya fedha hizo zitakazosaidia kulipa deni la nje la nchi husika.

Wageni hawakupewa sura kamili ya mazingira yawezayo kulinda amani, umoja na utulivu ambao watawala wanapenda sana kutungia nyimbo na ngonjera pindi wapatapo wageni.

Kama ambavyo muuza kitumbua hazungumzii jinsi unga ulivyoingia mchanga, ndivyo watawala walivyoficha mambo ambayo yanaweza kuondoa kile ambacho leo hii wanaita kivutio.

Tuone mifano michache. Kivutio kikuu karibu na Ziwa Natron ni ndege weupe aina ya korongo. Huitwa ‘nyangenyange.” Mradi wa magadi ambao serikali inag’ang’ania ujengwe karibu na ziwa hilo, una uwezekano mkubwa wa kuua kivutio hicho.

Mradi utaathiri vibaya ikolojia ya maeneo hayo; kupunguza maji ya ziwa na hata kulikausha na kusogeza mbali wale nyangenyange kutoka maeneo yao ya asili.

Kibaya zaidi ni kwamba ndege hao wanaweza kuhamia Kenya, kupitia mkondo wa mto ambao ndio chanzo kikubwa cha maji yatiririkiayo ziwani. Hilo wasingeweza kuwaambia wageni. Watetezi wa mazingira wangejiunga nasi kusema “hapana!” na wenyeji wangefadhaika.

Kitumbua kimoja chenye mchanga kimeonjwa na kugundulika. Ni giza la Zanzibar. Serikali iliambiwa kuwa mtambo wa kupokelea umeme Unguja utadumu kwa kati ya miaka 25 na 30. Hadi wiki tatu zilizopita ulipoharibika, inasemekana ulikuwa haujafanyiwa huduma yoyote.

Uko wapi uwekezaji usiokuwa na umeme? Yako wapi mazingira yachocheayo maendeleo bila kuwa na nishati ya umeme? Mwekezaji aje kuwekeza nini na wapi ambako umeme unategemea sala kwa Mwenyezi Mungu? Na kuomba siyo kupata!

Wageni hawakuambiwa majanga yawapatayo wabeba mizigo ya watalii kwenda kileleni Kilimanjaro. Vifo, maradhi, ulemavu na bado hakuna anayejali kurekebisha hali hiyo.

Wenyeji wanatangaza urefu wa mlima, siyo dhiki ya wabeba mizigo, rushwa ndani ya makampuni, rushwa kati ya watalii na makampuni katika tasnia ya utalii na unyanyasaji wafanyiwao waongozaji na wabeba mizigo njia nzima – kileleni na kurudi.

Wageni hawakuelezwa mipango ya kujenga mahoteli makubwa ndani ya mbuga za wanyama ili maeneo yafanane na maghorofa katika miji yao mikuu Ulaya na Marekani. Labda wenyeji waliogopa kuchekwa.

Kwa upande wa siasa, wageni hawakuambiwa malalamiko makubwa ya wananchi kuhusu kuwepo kwa Katiba Mpya; uchaguzi ulio huru na wa haki na umuhimu wa kuwa na mgombea binafsi.

Kama wangesema haya wangekuwa wanawafukuza wageni, kwani ni mazingira yanayozaa ghadhabu, chuki, ukosefu wa uvumilivu na migogoro.

Hustahili kumwambia ndugu au rafiki yako kuwekeza katika mazingira ya migogoro – iliyopo sasa au inayomea na inatarajiwa kukomaa si muda mrefu kutoka sasa.

Kudumu kwa chama kimoja madarakani kwa karibu nusu karne ni ishara ya ukatili, ubabe, ukosefu wa demokrasi; uvunjaji wa haki za binadamu kwa kuziba wananchi midomo na akili; ni sura ya woga wa walioko maradakani.

Kuwaambia watu waje kuwekeza katika mazingira haya kunahitaji pia kuwatahadharisha kuwa “lolote linaweza kutokea, tena wakati wowote.” Hilo bila shaka hawakulieleza.

Sitaki kuandika peke yangu. Wewe pia ongeza ya kwako hapa. “Mgeni” yupi anakuja kuwekeza katika mazingira yapi?

(Makala hii itachapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili, 08 Juni 2008. Mwandishi anapatikana kwa Simu: 0713 614872; imeili: ndimara@yahoo.com)

No comments

Powered by Blogger.