Header Ads

LightBlog

MJADALA WA UFISADI: CCM WATAFUNANA

CCM: Mbele au nyuma?

Na Ndimara Tegambwage

HIVI sasa siasa ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) zinaanza “kunoga.” Kwa nini? Kwa kuwa hata wafanyabiashara wanaanza kutunga baadhi ya viongozi kidole jichoni na kuwaambia “ninyi ni wachafu.”

Inanikumbusha kitabu nilichosoma nikiwa shule ya msingi, katika miaka ya 1950. Kilikuwa na shairi nisiloweza kusahau. Soma sehemu yake:
“Paulo usije kucheza na sisi
Una mikono michafu…”

Najiuliza. Yuko wapi sasa “Paulo” wa kisiasa; Paulo wa CCM? Ni nani huyo ambaye mfanyabiashara wa Zanzibar na mkereketwa wa CCM, Mohamed Raza anasema hapaswi kukaribia viongozi wastaafu ambao anasema ni wasafi?

Raza ambaye aliwahi kuwa mshauri wa masuala ya michezo wa rais mstaafu wa Zanzibar, Dk. Salmin Amour, huwa anachukuliwa kuwa mtu wa mzaha; lakini mara hii kadonoa kitu kizito.

Hoja yake ni hii. Kuna watu wanaotuhumiwa kufanya ufisadi. Wamo ndani ya CCM. Wako jikoni; ndani ya Halmashauri Kuu na Kamati Kuu.

Tujadili hoja. Ni kwamba wale wanaotuhumiwa, wakiendelea kuwa wanachama, wanakipa chama sura ya watuhumiwa – kuanzia mwanachama wa kawaida hadi kiongozi wa juu kabisa wa chama hicho.

Je, wanapokuwa viongozi wa Kamati Kuu? Hakika wanachama ambao ni viongozi wa ngazi ya Kamati Kuu wako jikoni. Ni kamati hii inayosimamia utekelezaji wa maamuzi mengi ya chama na kuandaa ajenda za vikao vya juu.

Sasa iwapo watuhumiwa watakuwa ndani ya chombo hiki, bila shaka kitaathirika kwa njia mbalimbali: Kitatuhumiwa. Kitatiliwa mashaka. Kitadharauliwa. Kitapuuzwa na hatimaye kinaweza kuyeyuka machoni na nyoyoni mwa wengi.

Tusonge mbele. Je, watuhumiwa wanapokuwa ndani ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya chama kilichoko ikulu? Sema sasa! Inakuwaje?

Halmashauri Kuu ya chama kilichoko ikulu ndiyo inayotunga na kusimamia sera za chama, kuandaa ilani ya uchaguzi na kutoa mwelekeo wa utawala nchini ikiwa ni pamoja na kuathiri aina ya uongozi na viongozi wa kitaifa.

Sasa iwapo watuhumiwa wa ufisadi wamo katika chombo hiki kikubwa, kutatokea nini? Kutatokea haya: Wanachama wa chama kilichoko ikulu watakuwa butu; hawawezi kusema lolote katika mijadala inayohusu “siasa safi na uongozi bora.”

Viongozi wa ngazi zote wa chama hicho watakuwa na mashaka makubwa kwa wakubwa zao katika kikao hicho kikuu; watadumu katika uongozi kwa kuwa kuna mafao na siyo hadhi itokanayo na usafi wa viongozi, sera na utawala bora.

Si hayo tu. Wajumbe wengine wa Halmashauri Kuu watawaona watuhumiwa kuwa “wanachafua hewa” ndani ya chama. Wanadhoofisha imani zao na imani za viongozi wengine na wanachama kwa ngazi mbalimbali.

Matokeo: Wajumbe wa Halmashauri Kuu watanyauka au watapooza kisiasa. Unyaukaji au upoozaji huu utaleta baridi ndani ya chama; na ili joto liweze kurejea, sharti watuhumiwa wang’oke au wang’olewe na kuachwa njiapanda huku gari la kisiasa likisonga mbele.

Vinginevyo, watuhumiwa wakiri hadharani – mbele ya chama na mbele ya umma; na kuomba radhi ili angalau, hata wakiendelea na kazi, ifahamike kuwa wameahidi kuwa watu wapya kiuongozi. Wakirudia watoswe.

Twende mbele zaidi. Je, watuhumiwa wanapokuwa bungeni? Hapo napo ni hatari nyingine. Bunge lina kazi nzito: Kuwakilisha wananchi. Kutunga sheria. Kushauri na kusimamia serikali. Kazi nzito kweli.

Je, watuhumiwa wanaweza vipi kufanya uwakilishi wa kweli wakati wanatuhumiwa kusaliti wananchi kwa hujuma mbalimbali?

Hawa wanaweza vipi kutunga sheria safi, zisizo na mizengwe na zinazolenga kuinua wananchi na nchi, iwapo tayari kuna tuhuma kwamba waliishatumia fursa zao kuzima na kuzamisha matakwa ya umma?

Wananchi wategemee sheria za aina gani kutoka kwa wabunge watuhumiwa? Wategemee uwakilishi wa aina gani na wasubiri usimamizi upi wa serikali kutoka kwa wabunge watuhumiwa?

Sasa twende taratibu. Kuna watuhumiwa ndani ya serikali. Wanaendelea na “kazi yao.” Kazi ipi? Kazi iliyosababisha watuhumiwe au wamejirudi na sasa wanafanya kazi sahihi za umma?

Hapo ndipo serikali imekwama. Imekataa kufuata kanauni zake za utumishi: kusimamisha kazi watuhumiwa au kuwapeleka mahakamani. Imekataa. Imewalinda. Imewahifadhi wenye tuhuma.

Huko tutokako, viongozi wakuu walishaapa kwamba hawatamwonea haya mwizi, mhujumu uchumi na fisadi. Mambo yamebadilika. Leo hii viongozi wamekuja juu. Wanasema wanataka ushahidi.

Viongozi wanataka ushahidi. Wao wanataka ushahidi kama nani? Ushahidi huhitajika mahakamani. Sasa viongozi wanataka ushahidi ili waufanyie nini?

Tuchukue mfano mmoja wa watuhumiwa wa ukwapuaji fedha za umma kutoka Benki Kuu (BoT). Odita anayethaminika duniani kasema kuna wizi na kutaja wezi ni akina nani. Orodha ndefu.

Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za serikali tayari amekubaliana na maodita wa Ernst & Young waliogundua wizi BoT. Je, hapa serikali inasubiri ushahidi gani?

Kuna mlolongo wa wakwapuaji fedha za umma kutoka BoT na serikalini kwa ujumla. Hii ni kwa njia ya malipo ya kawaida na kwa njia za mikataba, ujenzi na ununuzi.

Serikali ina tuhuma zote kibindoni. Njia ya kushughulikia tuhuma ni kuchukua hatua. Huwa hakuna mwongozo wa hatua ipi iwe ya kwanza. Ni suala la uamuzi kufuatana na uzito wa suala husika.

Wakati hapa unaweza kuanza uchunguzi, pale unaweza kumsimamisha kazi mtuhumiwa akisubiri uchunguzi; kwingineko unaweza kufungua mashitaka kwa kuwa ushahidi uliopo, kama wa kuchota mabilioni ya shilingi unaonekana; tena kwa karatasi na mihuri.

Ni wazi basi kwamba kisichokuwepo hapa siyo ushahidi. Hakuna utashi wa kupambana na wizi, rushwa na ufisadi. Ukikosekana utashi, tena kileleni mwa utawala, kila kitu kitapwaya na ufisadi utajenga makazi ya kudumu.

Katika fasihi ya kupambana na rushwa na ufisadi, kuna mambo ambayo wananchi wanategemea kuona. Wanatarajia kuona walarushwa wakubwa wakikamatwa na kuswekwa mahakamani.

Kama hilo halitendeki na wananchi wakaendelea kuona hakimu au mwalimu wa shule ya msingi ndiye anashitakiwa kwa rushwa ya Sh. 2,000, wakati wezi wakubwa wanatembelea aina mpya za magari ya kifahari, basi hupoteza imani katika vyombo vya utawala na serikali yao.

Mohammed Raza kachokoza, lakini hajachokoza nyuki. Hatuoni nyuki hapa wa kumuuma; wale nyuki wa kumtandika uvurenje (olubuli) na kumwambia akome, au wa kumgeuzia kibao na kusema kuwa hata yeye ni mtuhumiwa.

Katika ufinyu wake, Raza kasema chake; kwamba watuhumiwa wanawasononesha viongozi wastaafu, Rashid Kawawa na Alhaji Ali Hassan Mwinyi.

Je, Mwenyekiti wa CCM, Jakaya Kikwete hasononeki? Viongozi wengine je? Au Raza kaogopa kusema.

(Makala hii itachapishwa katika gazeti la MwanaHALISI, Jumatano 4 Juni 2008. Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa simu: 0713 614872; imeili: ndimara@yahoo.com na ideacent@yahoo.com)

No comments

Powered by Blogger.