Header Ads

LightBlog

SIKU YA UKIMWI DUNIANI

Serikali inavyopakata UKIMWI

SITAKI wimbo wa UKIMWI. Una beti nyingi zisizokatika. Umetungwa kwa shinikizo. Waumini wa kweli ni wachache. Ambao wangeuimba hawaujui; wanalia na kusaga meno. Wanakufa haraka.

Ni jana. Desemba Mosi. Inaitwa “Siku ya Ukimwi Duniani” (SUD). Kwa waliomo vitani dhidi ya gonjwa hili lisilochanjo wala tiba, akili zimeshonwa kwenye meza za maabara na matokeo mapya ya tafiti katika kukabiliana na gonjwa hili.

Kwa waliopokea kampeni dhidi ya ukimwi kama wimbo usiokatika wa kuombea fedha za kutumbulia katika mahekelu yao mapya pembezoni mwa miji mikubwa, jana ilikuwa siku nyingine ya kuongeza ubeti mpya.

Jana ilikuwa siku nyingine ya kusambaza takwimu za vitisho vya maambukizi; mahitaji makubwa ya fedha za kampeni; umuhimu wa kuwa na tume nyingi za kupambana na ukimwi na asasi lukuki za “ombaomba” waneemekao kwenye mgongo wa ukimwi.

Hiyo ni jana. Ndivyo ilivyokuwa mwaka jana na mwaka juzi. Ndivyo itakavyokuwa mwaka kesho na keshokutwa. Wanaochuma kwenye mgongo wa ukimwi hawataki ukomo wa virushi vya ukimwi (VVU) wala ugonjwa wa ukimwi.

Ugonjwa unaoua, usio na chanjo wala tiba, unatengewa siku moja katika mwaka na dunia; “kuuadhimisha” au kuadhimisha juhudi za kukabiliana nao; au kukumbushana umuhimu wa mapambano dhidi yake.

Siku ya Ukimwi Duniani inatukumbusha mambo mengi. Kubwa kuliko yote ni kwamba watawala hawajawa makini katika vita dhidi ya ukimwi. Bado wanauchekea na kuupakata.

Kwanza, Tanzania ni moja ya nchi zinazoendelea ambako watawala walisukumwa na nchi wafadhili kuanza kujadili ukimwi hadharani na kuingiza mkakati wa kukabiliana nao katika mipango ya nchi.

Pili, ukimwi umeandamana na unyanyapaa. Unyanyapaa maana yake ni ubaguzi dhidi ya walio na VVU au wagonjwa wa ukimwi. Ubaguzi huu maana yake ni kutengwa, kukimbiwa, kuepukwa na ndugu, rafiki na jamii.

Lakini kwa nini wagonjwa wa ukimwi wananyanyapaliwa wakati wagonjwa wa kipindupindu hawafanyiwi hivyo? Kipindupindu kinatokana na “kula mavi” au uchafu. Ukimwi unatokana na mahusiano ya mtu na mtu.

Kwa hiyo basi kuna unyanyapaa pia katika kipindupindu lakini sharti uchimbe zaidi. Kipindupindu hupatikana vichochoroni, katika mazingira machafu; kule wanakoishi hohehahe; makazi yasiyo na mpaka kati ya mifereji ya maji safi na majitaka

Kipindupindi hupatikana katika mazingira ya wasio na sufuria ya pili ya kuchemshia maji; wasio na fedha za kununua maji salama; wasio na fedha za kununulia mkaa wa kuchemshia maji; wasio na fedha za kula sehemu zenye usafi; masikini walao kwenye jalala na wasio na uelewa (elimu) juu ya kujikinga.

Hawa walitengwa zamani kwa mpangilio wa jamii kitabaka. Waliishanyanyapaliwa zamani kutokana na hali zao dhoofu kiuchumi ambamo walisukumwa na mkondo wa uchumi unaotawala.

Leo hii, wenye VVU na ukimwi wananyanyapaliwa kwa madai kwamba mgonjwa wa ukimwi anakufa baada ya mateso makubwa – kuugua kwa muda mrefu, kudhoofu kupindukia, kuhara na kutapika na hatimaye kuwa “mzigo” kwa waangalizi wake.

Ukichanganya haya mawili, kipindupindu na ukimwi, utaona kwamba, kote kuna unyanyapaa. Ni masikini na asiye na elimu ambaye anakufa kwa mahangaiko, kukata taamaa na hata kujiua. Hajui, na hana uwezo kifedha wa kukabiliana na kipindupindu na ukimwi.

Wagonjwa wa ukimwi wenye elimu na mali wanajua kuwa kifo kutokana na ukimwi kinaweza kuahirishwa kwa kupambana na magonjwa virukizi, kwa kula chakula chenye viini muhimu na cha kutosha kuimarisha mwili.

Wenye VVU wamethibitika kuishi maisha yao yote na kufa katika umri mkubwa. Hii ni iwapo wamepewa elimu na wana uwezo wa kunawirisha maisha yao kwa chakula kinachotosha na chenye viini muhimu vya kulinda na kuimarisha miili yao.

Katika nchi ambamo hakufanyiki utafiti juu ya kinga wala tiba ya VVU na ukimwi, kama Tanzania, kwa nini kusiwe na mkakati mkubwa wa kulinda uhai wa watu kwa njia ya elimu na lishe?

Kuna watakaosema tayari kuna asasi za kimataifa, Tume ya Kudhibiti Ukimwi Tanzania (TACAIDS), Mfuko wa Mkapa, asasi mbalimbali za kitaifa, asasi za mikoani na wilayani hadi kwenye kata.

Waandishi wa habari katika darasa langu la uchunguzi wa habari, katika wilaya za mikoa ya Kanda ya Ziwa Viktoria, wamegundua utitiri wa asasi za “kupambana” na ukimwi zilizoanzishwa na maofisa wilayani ili zipokee fedha na kuyeyuka.

Hii ina maana gani? Kwamba elimu iliyotarajiwa haipo; kama ipo haifikii walengwa. Fedha zilizolenga kueneza elimu na kuleta afueni kimaisha, haziwafikii walengwa. Kuna wizi. Lakini pia hakuna usimamizi wa kutosha.

Tanzania ina wizara 25 za serikali. Rais Kikwete anafikiria kupunguza baadhi ya wizara. Huenda zikabakia 15 au 18. Katika hizo 18, kwa nini kusiwemo Wizara ya Kupambana na Ukimwi (WIKUKI) inayoongozwa na wanaharakati wa afya za jamii na siyo lazima waliovaa nguo za kijani?

Ni kweli kuna wizara zilizoshindwa kufanya kazi zake barabara. Lakini hatua ya kuwa na wizara inaonyesha kuwa makini na inaahidi uhakika wa mipango ya elimu juu ya VVU na ukimwi; juu ya dawa za kuahirisha kifo; mipango mizuri ya usambazaji wa fedha na usimamizi na ufuatiliaji wenye tija.

Watawala wakifanya ajizi, wananchi wataendelea kupukutika, na wao kama watakuwa wamesalia, watatawala ardhi na nyasi peke yake, kwani maliasili nyingine kama wanyama, misitu na madini, wameishatoa kibali vihamishwe vyote.

(Makala hii itachapishwa katika safu ya SITAKI katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili, Desemba 2, 2007)Mwandishi anapatikana Simu: 0713 614872; imeili: ndimara@yahoo.com)

No comments

Powered by Blogger.