Header Ads

LightBlog

Mjadala juu ya rushwa na ufisadi Tanzania


Kauli za Warioba zimepitwa na wakati


(Tanzania Daima 20 Septemba 2007)

SITAKI Jaji Joseph Sinde Warioba ajitokeze kuzima hoja nzito kwa visingizio kwamba taifa sasa linapaswa kujadili “kilimo” kwa kuwa ni wakati wa msimu na siyo ufisadi.

Sitaki Warioba afikiri kwamba tuhuma za rushwa zinazojadiliwa hivi sasa, ni mjadala unaopotosha lengo na unaosahaulisha mambo ya msingi kama bei za vifaa vya ujenzi au bidhaa muhimu sokoni, kama mchele.

Sitaki Warioba ajipendekeze kwa Rais Jakaya Kikwete na kutoa kauli za ushawishi kwamba rais “amedhalilishwa” ili mamlaka iweze kuwabughudhi na, au kuwakamata na hata kuwashitaki waliotoa tuhuma.

Tupangue madai ya Warioba; moja baada ya jingine.
Kwanza, katika Tanzania, ni upofu wa watawala unaofanya nchi iwe na “msimu” wa kilimo.

Utaongeaje mambo ya msimu wa kilimo katika nchi yenye mito mikubwa na midogo isiyokauka; nchi yenye maziwa makubwa yaliyosheheni uhai wa viumbe wanaopaswa kuvunwa kila siku na kuleta ustawi kwa jamii?

Kwa nchi yenye utajiri mkubwa wa mito na maziwa kama Tanzania; kila siku, kila mwezi, kila mwaka ni msimu wa kilimo. Warioba upo hapooo?

Lakini waliotawala kwa miaka 46 sasa bila hata kujua jinsi ya kutumia maji tuliyojaliwa, ndio wanaendeleza malalamiko dhaifu ya “msimu” unaotegemea mvua. Huu nao ni msiba.

Ni haohao wanaoendeleza fikra za mazao ya “biashara” na mazao ya “chakula,” kana kwamba mazao ya chakula hayawezi kuuzwa. Nani kama si wao wanaonunua mchele, maharage, pilipili, mapeazi na mapera kutoka nje ya nchi?

Warioba anasema badala ya kujadili ufisadi, tujadili kupanda kwa bei za vifaa na chakula. Kwa nini anakataa kutafuta uhusiano kati ya mporomoko wa thamani ya fedha na kupanda kwa bei, kwa upande mmoja na ufisadi, kwa upande mwingine?

Inawezekana kabisa kwamba bei ya mchele iliyopaa inatokana na hongo na rushwa katika mkondo wa usambazaji. Inawezekana gharama kubwa za bidhaa zinatokana na ukamuaji uliosisiwa kimtandao na walioko kwenye njia ya ugawaji.

Hivyo mjadala juu ya wala rushwa na ufisadi kwa ujumla, hapa na leo hii, ndio mahali pake. Na hakika, wakati wote ni wakati wa kujadili nyendo za wahusika katika utawala, menejimenti na biashara ili kulinda maslahi ya jamii pana.

Kwani Warioba hajui uhusiano kati ya ufisadi na kuendelea kudorora kwa uchumi wa nchi? Hajui kuwa rushwa kubwa na ufisadi vinaneemesha wachache sana katika jamii na kuacha wengi wakilia na kusaga meno?

Kwa mtu anayeamini katika “misimu ya kilimo,” kwa nini, hata siku moja, Warioba asitembelewe na fikra kwamba kunaweza kuwa na “msimu wa mbubujiko wa ufisadi?” Na kama upo, kwa nini usijadiliwe?

Waziri Mkuu wa zamani, Joseph Sinde Warioba anapaswa kujua, na anajua lakini anapuunza, kwamba maadili katika utawala yameporomoka kwa kasi kubwa na mazingira ya sasa hayawezi kufafanishwa na yale ya kale.

Katika mifumo ya awali ya utawala; ile ya uchifu au ufalme, kila mtu alilazimika kuamini kwamba kila kilichomo katika eneo la utawala husika ni cha mfalme.

Ardhi yote – misitu, milima, mito, maziwa, mifugo na wanyama na hata fedha – chochote kile kilichotumika katika biashara – vilikuwa mali ya mtawala. Naye aliamini hivyo.

Kama vitu vyote ni vyake na watu wote wako chini yake, ana haja gani ya kuiba? Kujaribu kuiba ni kujaribu kutoa kitu mfuko huu na kuweka mfuko mwingine, au kuanika nguo kwenye kamba na kuja baadaye ukinyatia na kuichukua kama mwizi.

Hicho ni kichaa. Watawala wa sasa katika nchi nyingi zisizo na mfumo mzuri wa utawala, kwanza hawaamini kwamba vyote viko chini yao, na pili ni walafi kupindukia na wamekuwa vichaa.

Wanajiibia wenyewe. Hapo hapo wanawaibia wananchi waliowapa madaraka ya kusimamia, kulinda, kutumia na kuhifadhi fedha, madini na vito vya thamani na maliasili zote kwa manufaa ya wote.

Ni uporaji huu ambao unafanya mijadala juu ya ufisadi kuwa muhimu leo na siku zote. Huku siyo kupoteza wakati. Siyo kupotosha. Siyo kukashifu. Siyo kukebehi.

Na kilichowekwa mbele ya wananchi ni tuhuma. Kiongozi anayeogopa kutuhumiwa afadhali aachie ofisi ya umma. Washika ofisi za umma sharti wawe watu safi na anjia ya kupima usafi wao ni kuanika mashaka yaliyojificha ili weupe wao uweze kujitokeza.

Warioba anasema kazi hiyo isifanyike, badala yake twende kuwaambia wakulima masikini, “Mvua zinakuja, parura viunga vyenu vinginevyo mtakufa!”

Warioba anajua kuwa, kwa hatua yake ya mahubiri, wakulima hawa hawawezi kusonga mbele wala kubaki walipo. Watarudi nyuma. Watakufa haraka. Kwani wanachotea maji kwenye pakacha. Halihifadhi wala halishibi.

Kauli za Warioba zinaendelea kumomonyoa nafasi yake katika jamii. Hakuna aliyetegemea aseme kwamba amekuwa na orodha ya wanaotuhumiwa kula rushwa. Wengi walidhani hajui lolote.

Kumbe Warioba amekuwa akikalia orodha ya watuhumiwa. Anasema iliyotangazwa na wapinzani karibu ina “mambo yaleyale.”

Ukweli ni huu. Hakuna anayeweza kupambana na rushwa na ufisadi kwa kwenda kimyakimya. Hayupo. Hatua ya wazi ndiyo mwalimu kwa wananchi wote na ndio msingi wa kuamini kuwa kinachotendeka.

Usipowataja na wao wakajua kwamba una orodha yao, wanaweza kukuhonga fedha, mali ainaaina, vyeo ndani na nje ya serikali. Nawe unaweza kuishia kusema, “nina orodha yao, siku moja wakiniudhi nitawalipua.”

Hiyo haitoshi. Siku haitafika. Lakini ikifika, nawe utakuwa tayari mchafu kwani utalipuliwa na wengine. Hili ni somo tupatalo katika kupambana na rushwa.

Sidhani Rais Kikwete ana matatizo na kauli za wapinzani. Kama ni safi atabaki safi na atathibitisha. Hata hivyo rais ni “babu.” Kumwaga ugolo wa babu siyo sababu ya yeye kuapa kukuua au kukufukuza nyumbani.

Sitaki kauli za kujenga chuki kwa waliotaja majina ya watuhumiwa. Sitaki awepo wa kupalilia chuki hizo kwa ujanja. Sitaki visingizio vya misimu ya kilimo. Acha mjadala upambe moto.

(Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa Simu: 0713 614872; baruapepe: ndimara@yahoo.com na www.ndimara.blogspot.com )

No comments

Powered by Blogger.