Header Ads

LightBlog

SERIKALI KICHWA CHINI MIGUU JUU


Serikali haina cha kusherehekea

Na Ndimara Tegambwage

SERIKALI haina sababu ya kuchekelea na kusherehekea kuhusiana na matokeo ya mtihani wa Kidato cha IV.

Wakati inatangaza walioshinda; yenyewe imeshindwa na imelala chali. Iko hoi na haina wa kuifaraji.

Katika shule kumi za kwanza, hakuna shule ya serikali. Wanaomeremeta ni wamiliki wa shule za binafsi na mashirika ya madhehebu ya dini.

Hata ukienda kwa nafasi 10 za pili na za tatu (hadi shule 30), bado utakuta shule zinazong’ara ni za watu binafsi na mashirika ya dini. Zile za serikali ni za kuokoteza.

Hapa tunahesabu washindi wa mtihani wa serikali kama ulivyotungwa na kusimamiwa na Baraza la Taifa la Mitihani (NECTA). Tunahesabu kile ambacho serikali inataka: Kuondoa utata juu ya nani wavuke na kuingia darasa la juu.

Hatuhesabu “ubora wa elimu” iliyopatikana. Inawezekana wameshinda kwa alama na vigezo vya baraza na wizara. Inawezekana wakirudishwa darasani na kutahiniwa juu ya uwezo wa kubuni, kufikiri na kudadisi, wanaweza kubaki hoi kama serikali.

Kwa hiyo katika hatua hii, na sasa, hatutajihusisha na zoezi la ubora ambalo, hata hivyo, serikali ama hulikimbia, hulipuuza au huliogopa. Tujadili mengine ambayo nayo huongeza uwezo mwingine wa mwanafunzi.

Miongoni mwa shule 10 za kwanza hakuna shule hata moja inayofanana na shule za Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Abbas Kandoro. Kwa nini?

Shule 10 za kwanza zina madarasa. Shule zote za Kandoro alizojenga Dar es Salaam zina matundu. Kwa hiyo, kwa mtihani wa kwanza, hizo si shule. Ni mahali pa kukusanyika na kukulia.

Shule 10 za kwanza zina walimu. Zina madarasa yaliyojengwa kwa kupanga na kudhamiria. Zina vitabu vya kiada na ziada. Zina maktaba. Zina maabara na vifaa vinavyohitajika kwa mazoezi.

Shule 10 za kwanza zina walimu, tena wanaoshindana kwa ubora. Zina usimamizi wa wanafunzi na walimu. Kuna mazingira yanayothamini muda, malipo ya mwanafunzi kwa kile alichofuata pale na tija ya kila mwanafunzi.

Shule 10 bora zimejengwa kwenye viwanja vipana. Kuna hewa na sehemu za kuchezea na kunyooshea viungo. Kuna hata vipindi vya mazoezi ya mwili ambavyo ni lazima kwa afya njema. Tusiseme mengi.

Turudi kwenye shule za Kandoro. Kuta zake ni za kutabiri. Yeye mwenyewe ameamuru baadhi ya shule ziruhusu wanafunzi warudi makwao ili zirudiwe kujengwa.

Wanafunzi wanaogopa hata kuegemea kuta zake. Wako hatarini kuangukiwa. Zinazoitwa shule zimejengwa kwa haraka, kwa ujanja na nyingine chini ya viwango na hivyo, kwa ufisadi usiomithilika. Iwapi thamani ya fedha zilizotumika?

Baadhi ya zile zinazoitwa shule za Kandoro, zimejengwa uwani; nyuma ya nyumba za wakazi. Zinapakana na vilabu vya pombe; zimo mabondeni na zinafurika kila mvua zikinyesha; zimezungukwa na vijana wavuta bangi na nyumba za kulala wageni.

Hizi shule za Kandoro hazina madawati; ndio wanaokoteza moja baada ya jingine kwa kushirikisha wazazi. Hazina vitabu vya kiada na ziada. Hazioti siku moja kuwa na maktaba.

Zinazoitwa shule za Kandoro hazina maabara wala vifaa vingine vya kufundishia. Hazina vipindi vya michezo wala elimu ya viungo. Vinakwenda kwa “sera” ya Joseph Mungai, yule waziri wa elimu wa zamani aliyesema hakuna sababu ya kuwa na michezo shuleni.

“Shule” za Kandoro hazina walimu. Walioko ni wale waliookwa kama chapatti – wiki sita – pa, pa! Na wao wanasema wamesomea kwenye matundu hayahaya ya Kandoro; kusikokuwa na walimu, vitabu, maktaba, maabara wala hewa ya kutosha.

Kama hali ndiyo hii, kwa nini serikali isitupwe mbali na kuangukia pua? Utalinganishaji shule na tundu? Utategemeaje wanafunzi wa kupata elimu ya juu kutoka “vijiweni?”

Kwa Kandoro wanapanga watoto wa kwenda sekondari kabla mitihani haijafanywa. Wanajali wingi ili kukidhi takwimu za watoa misaada. Siasa? Malengo ya milenia? Chauchau? Tusishindanishe shule na matundu.

(Makala hii ilichapishwa katika gazeti la MwanaHALISI toleo la 11 Februari 2009)

No comments

Powered by Blogger.