Header Ads

LightBlog

WATAWALA WATONESHA WAPINZANI ZANZIBAR

Posted 24 January 2009


Rais Kikwete anapozomea wapinzani

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI zomeazomea ya Rais Jakaya Kikwete kuhusiana na hali ya kisiasa Zanzibar. Kwa nini? Kwa sababu ni yeye aliyejitwisha jukumu la kumaliza kile kilichoitwa “mpasuko wa Zanzibar.”

Mpasuko bado mbichi. Kamati yake imekumbana na kisiki. Karibu na mwisho wa majadiliano, wajumbe watatu wa CCM kwenye kamati hiyo walisema, tena waziwazi, kwamba wamepata wazo zuri kutoka kwa rais wa Zanzibar, Aman Abeid Karume.

Wazo hilo, walisema ni kwa shabaha ya “kupiku Chama cha Wananchi – CUF” kwa kupendekeza kura ya maoni katika kufikia utawala wa mseto Visiwani. Wakaangua kicheko. Wakaona wamekomoa mpinzani wao. Tangu hapo kamati haijawahi kukutana.

Juzi, Alhamisi Rais Kikwete akanukuliwa na vyombo vya habari akiwapiga vijembe wapinzani wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na serikali yake huko Pemba. Vijembe hivyo vilikuwa vikielekezwa kwa CUF na viongozi wake.

Rais alikaririwa akisema kuwa wapinzani wa serikali wanaweza kuchukua muda mrefu kabla ya kupata nafasi ya kuunda serikali, au pengine wasiipate kabisa fursa hiyo; hivyo akawaambia washirikiane na serikali iliyopo “kuwaletea wananchi maendeleo.”

Ujumbe huo unapenya mfupa, kwa njia ya uchokozi, na siyo kejeli ya kawaida, hasa unapokuwa umeelekezwa kwa yule ambaye mara tatu sasa amekuwa akidai “kuibiwa ushindi.”

Sasa hapa kuna matatu: Ama rais ameshindwa kutekeleza ahadi yake ya “kumaliza mpasuko Zanzibar na sasa anakiri;” au kauli yake ilikuwa inathibitisha kuwa hakuwa na dhamira ya kweli pale alipoahidi kumaliza mpasuko; au kauli hii ilikuwa njia isiyo rasmi ya kuvunja kamati yake.

Na kauli ya rais haina utata. Ina maana iliyokusudiwa. Imetolewa katikati ya ngome ya upinzani, Pemba. Inapata nguvu kutokana na ukweli kwamba, tangu mparanganyiko ulioletwa na wajumbe wake katika Kamati ya Muwafaka, hamasa ya “kumaliza mpasuko” inaonekana kuyeyuka.

Ni hivi. Katika “mazingira mazuri,” kauli ya Kikwete ni tambo za kawaida za wanasiasa; lakini si za wanasiasa wa ngazi yake. Tambo za aina hii huwa zinazaa kisrani na hatimaye mitafaruku mipana; lakini kwa kuwa huwa zimetolewa na wengine, kiongozi mkuu hudondosha tone la hekima na kuzima tanuri.

Sasa kama rais na mwenyekiti wa chama kilichoko ikulu ndiye anafanya zomeazomea na tambo za “sisi ndio wenye dhamana ya kuleta maendeleo,” wananchi ambao hasa ndio wenye dhamana ya kujiletea maendeleo kwa kodi na nguvu zao, wamwelewe vipi rais wao?

Dhamana ya utumishi wa umma hutokana na ridhaa ya umma wenyewe. Mtumishi wa umma aliyetokana na utashi wa umma hahitaji vijembe na tambo kwa umma uliomweka kileleni. Hutumika na kutumikia tu kwa kuwa ana uhalali utokao kwa umma.

Lakini kuna mazingira ambamo “mtumishi” amepatikana kwa mizengwe na hata wale anaodai kuwatumikia hawezi kufanikiwa kuwatumikia labda kwa kufanya yale ya kujikosha ili apate mahali pa kusimama na kutamba.

Na barabara, daraja, maji na hata umeme, si muhimu kama vinawekwa kwa ajili ya kujenga misingi ya kujigamba. Afadhali watembeao gizani kwa ujasiri na matumaini ya kujikomboa; wenye kauli na utashi katika mambo yanayohusu maisha na mapambano yao, kuliko watumwa wanaoishi kwenye nuru ya umeme na barabara pana.

Mgogoro wote wa Zanzibar umeshonwa kwenye dhamana. Katika mazingira ya kidemokrasi, dhamana hutolewa kwa chama au mtu wanayeona anastahili kupitia mfumo maalum na unaodhihirisha utashi wa wananchi.

Haitoshi kukusanya kodi za wananchi, kuomba misaada na mikopo na kujenga mioundombinu. Yeyote anaweza kufanya hivyo hata kama hajapewa dhamana na wananchi; na kwa shabaha yake binafsi. Bali miundombino ya maana ni ile ambayo wananchi wanahitaji kwa sasa; waliyoamua kuwa nayo na inayokidhi matakwa yao ya sasa na baadaye.

Miundombinu pasipo uhuru na utashi wa kuchagua yule ambaye unataka atumikie utashi wenu; penye wizi mpevu wa kura ulio wazi na unaorudiwa mara kwa mara; penye maapizo na tambo za walioko ikulu kwamba wapinzani daima watasikia ikulu ikiimbwa redioni; siko mahali pa Rais Kikwete kufanyia zomeazomea.

Inawezekana kabisa Rais Kikwete alikuwa anafanya mchezo wa “nikune hapa nitakukuna pale.” Akimsaidia Rais Karume kuendeleza vijembe kwa kutegemea Karume kufanya hivyo pindi atakapokwenda Bara.

Achilia mbali uhuru wa rais au Kikwete kuwa na maoni, kauli yake Pemba inapanua ufa katika mgogoro wa Zanzibar. Aidha, inaonekana kuwa mgogoro huu haujaweza kutoa somo au wenyewe kuwa somo kwa watawala na CCM.

Mahali penye “miafaka” miwili; penye mwafaka wa tatu kibindoni; palipomwagika damu; penye watu ambao vifua vyao vimevimba kwa chuki na hasira; penye uzoefu wa wizi wa kura tangu 1995 na penye mvuto wa dunia nzima kuona kama janga linaweza kuepushwa, hapahitaji kauli ya kutonesha.

Nimekuwa nikiandika kwamba tatizo la CUF ni kukubali kuingia mazungumzo na CCM. Bado naendelea kusema kuwa serikali ndiyo inasimamia uchaguzi na kama wizi umetokea, ama umetokana na uzembe wa serikali au umetendwa na serikali.

Chama cha siasa kama asasi ya kiraia, na hapa najadili CUF, kingesimamia kukaba koo serikali iliyotenda jinai na siyo kuingia mjadala na CCM ambamo makosa ya serikali yake yanaweza kuhalishwa.

Kumenyana na CCM kunanyima asasi nyingine za kijamii fursa ya kujiunga katika kupigania haki ambayo imepokonywa na serikali. Badala yake, asasi nyingine zinasema hayo ni “mambo ya kisiasa,” au waache ni “mambo yao.”

Hilo likieleweka vema, na “bahati mbaya” sijawahi kukosolewa kwa msimamo huo, ndipo tunaweza kujua kauli ya Rais Kikwete ina uzito gani na ilipaswa kutolewa lini na wapi.

Kwamba wapinzani wa CCM wanaweza kuchukua muda mrefu kabla ya kupata nafasi ya kuunda serikali, au pengine wasiipate kabisa! Ni kauli bahari. Tunahitaji kufikiri zaidi.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com

(Makala hii itachapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili toleo la 25 Januari 2009 katika safu ya SITAKI)

1 comment

Maka Patrick Mwasomola said...

Ndimara,nimesoma katika vyombo mbalimbali vya habari kuwa eti Rais kayasema hayo!Sitaki kuamini kama kweli Rais wetu kayatamka hayo nafikiri pengine walimnukuu vibaya!Lakini kama ni kweli kayasema hayo basi hakika mambo haya yanatuweka katika maswali yaso na majibu!Lakini kwa kuwa viongozi wetu pia ni binadamu na wala si malaika kama alivyowahi kusema baba wa Taifa hili kuwa wao wasikosee kwani wao ni kina nani kwani wao ni malaika?Basi Mkuu pengine aliteleza!Lakini kama inasisitizwa kuwa hakuteleza kwa kweli tuelekeako si kuzuri.Hatuitaji yote hayo kuona kuwa mpasuko huu ukiendelea kukua siku hadi siku.Wala haukuwa wakati muafaka kwa mkuu kuyasema hayo.Muafaka unatekelezeka hatujachelewa tuanze sasa,umoja ni nguvu,utengano ni udhaifu na wala hatuhitaji udhaifu sisi watanzania.Heshima yetu nje ni kubwa sana sasa tusivae ngozi ya kondoo huko nje tuendelee kuwa na ngozi yetu ya kondoo hapa nyumbani pia ili siku moja tusije tukagundulika kuwa sisi ni chui.Sisi sote ni kitu kimoja tofauti yetu ni katika mitazamo.
Lakini kwa kuwa siasa ni mchezo wa kutafuta udhaifu wa mpinzani wako uko wapi hapo sasa panakuwa na kazi sana hasa kama mkuu alikwenda kwa kofia ya chama chake hapo pana kuwa na kazi kwelikweli.Siasa kosa moja goli moja!Hapa ni sualala muda sijui jamaa wa upande wa pili watakuja na mbinu gani zakusawazisha goli hili!
Kwa matokeo yoyote yale yawe ya sare au ushindi,watanzania lazima tuelewe kuwa hakuna kitu muhimu kama amani.Asante

Powered by Blogger.