Header Ads

LightBlog

Magufuli avunja Mayai ya Maafa


Siyo kila chenye watatu au vitatu ni cha “Utatu.” Ndiyo maana kuna “matatu” ambayo hayana uhusiano na waumini katika Utatu wa Maandiko.

Jina la Matatu la Kenya linatokana na magari madogo ya abiria yaliyokuwa yakitoza “mapeni matatu” – senti 10 tatu – zilizokuwa nauli katika miaka ya 1950 katika miji mingi ya nchi hiyo.

Matatu au utatu wa sasa umetoswa kabla haujachipuka. Ni Rais John Pombe Magufuli aliyetosa utatu wa Rais mstaafu Ali Hassan Mwinyi, Mbunge Juma Mkamia na muumini wa CCM, Lawrence Mabawa.

Mwinyi: Kama siyo kwa Katiba ya nchi, ningependekeza Magufuli awe rais wa kudumu/milele.

Mkamia: Nitawasilisha hoja bungeni ya kuondoa ukomo wa urais wa vipindi viwili.

Mabawa: Nitazunguka nchi nzima nikifanya kampeni kushawishi kuungwa mkono kwamba Rais Magufuli aendelee kuwepo kwa zaidi ya vipindi viwili.

Pote yalipoanza maasi ya aina hii dhidi ya Katiba, yalianza namna hii: Watu wachache. Nje ya Ikulu. Nje ya nyumba ya rais. Mbali na rais. Wakitamani. Wakinong’ona. Wakisema. Wakiimba. Wakifyatuka: Rais aendelee. Na rais alisikia. Alishawishika. Alikubali. Alijiandaa. Alibaki.

Huo ni ushawishi unaotaga mayai ya maafa! Mayai hayo yakiachwa hadi kuanguliwa, huleta vifaranga ambavyo hujenga woga miongoni mwa watawala ambao huanza kushuku kila mmoja kuwa siyo mwenzao, anawapinga; kuwa anawasema vibaya, kuwa anataka kuwang’oa, kuwa ana njama za “kuwamaliza!”

Kadri vifaranga vinavyokua, huchochea uadui usio wa kisiasa dhidi ya wapinzani wa kisiasa; huongeza woga miongoni mwa walio karibu na mtawala wanayetaka aishi madarakani; huanza kutafunana wenyewe kwa wenyewe kama senene – kila mmoja akimshuku mwenzake katika kupigania kupendwa na kuaminiwa; huwaingiza katika ndumba na ushirikina.

Rais Magufuli amenukuliwa wakati wa ziara ya mkoa wa Tanga wiki iliyopita akisema, katika hili atasimamia kulinda Katiba; atatumikia kwa kipindi chake na kipindi hicho kikiisha, atakabidhi “kijiti kwa mwingine.”

Kwa kauli hiyo, amevunja mayai ya husuda kabla hayajaanguliwa na kutawanya sumu ya kutawala milele au kwa muda zaidi ambayo tayari kwingine imeleta kutoaminiana, kusutana, kugombana, kupigana na kuuana.

Lakini nani anasema washawishi wamekoma baada ya kushushuliwa? Wanaweza kuendelea. Wanaweza kuongezeka. Wanaweza kukusanyana na kupeleka ujumbe badala ya kutoa kauli zilizotawanyika. Wanaweza!

Kisingizio chao kitakuwa kwamba wana uhuru wa kufikiri na kutoa maoni. Kweli wanao. Lakini waletacho ni maoni binafsi yenye sumu; yanayolenga kuangamiza misingi mikuu iliyowekwa na Katiba; lakini pia yanayolenga kuua utashi, uhuru na haki za wengi wengine kwa kutumia sheria au marekebisho ya Katiba.

Afrika ina somo moja kuu. Kule wenye fikra hizo walipojaribu na kufanikiwa; hata wanaotawala hawana raha. Hawana furaha ya kuwa madarakani. Hawana amani. Hata kinachoitwa ushindi wa mia kwa mia, hakileti tabasamu kwenye nyuso zilizokunjamana kwa woga; na nyoyo zilizofura kwa mihuri ya suto.


Je, Magufuli anahitaji kukumbushwa mara zote juu ya hili, ili ajenge uthabiti na asitetereke? Au, akumbushwe pia maeneo mengine mengi ambako Katiba imesema na kuzingatia lakini hajapatamka kwa uthabiti huohuo?

No comments

Powered by Blogger.