Header Ads

LightBlog

Kufungia gazeti: Ni woga, ubabe au ulimbukeni?

MwanaHALISI: Nusu mwaka kifungoni
 'Kwa kufunga gazeti wamewaweka pia wasomaji gerezani popote walipo'

LEO ni siku 172 tangu serikali ifungie gazeti la MwanaHALISI “kwa muda usiojulikana.” Siku hizo ni sawa na miezi mitano na siku 22 au miezi sita kasoro siku nane. Ni nusu mwaka.

Kwa muda usiojulikana maana yake ni mpaka serikali itakapotaka (yenyewe). Itakapojisikia. Itakapofurahi. Itakapopigiwa magoti na wamiliki wa gazeti. Itakapoombwa na marafiki wa gazeti. Itakaposhinikizwa vya kutosha na wapigania uhuru wa habari.

Kwa muda usiojulikana yaweza kuwa pale viongozi wa serikali waliofungia gazeti watakapotembelewa na akili na uelewa kuwa hawapaswi/hawakupaswa kuingilia uhuru wa kupata, kutafuta na kukusanya habari; au pale serikali itakapoamuliwa na mahakama; au wenye gazeti watakapoamua kulichapisha kwa mapenzi ya wananchi bila kujali serikali inasema nini. Hilo nalo linawezekana.

Nusu mwaka. Serikali inayojidai kutenda na kulinda haki za raia wake imeamua kuwa wafanyakazi wa gazeti la MwanaHALISI wawe ombaomba mitaani; au wasambaratike kwa kuhama kampuni au wafe kwa njaa – potelea mbali! Kama hii ndiyo haki, basi ni haki ya mashetani.

Imekuwa safari ndefu – nusu mwaka – lakini iliyojaa karaha na kinyaa. Hapa kuna serikali inayojigamba kutawala kwa “misingi ya demokrasia;” lakini ni serikali hiyohiyo inayotaka kutawala gizani – kishirikina; na inayonyakua uhuru wa wananchi wake wa kutoa, kupata na kusambaza taarifa na habari.

Hapa kuna watawala wanaojigamba kuwa wakweli na wawazi lakini wanaficha hata kilichowazi kwa kila mmoja. Wanafungia gazeti kwa nia ya kuua jicho la nyongeza la jamii; kuziba sikio la nyongeza la jamii na kusiliba mdomo wa nyongeza ya jamii. Wanataka jamii mfu – isiyoona uoza, isiyosikia mipango ya “uhaini” dhidi ya jamii na isiyotoa kilio cha wengi.

Kufungiwa kwa MwanaHALISI kulisononesha nyoyo; kukazika shauku, kukanyakua maarifa, kukapora uhuru na kukaondoa mategemeo. Watawala wanajua lakini hawajali.

Hili ni gazeti lililofungiwa wakati habari kuu katika vyombo vyote vya habari nchini ilikuwa “Utekaji na utesaji wa Dk. Steven Ulimboka.” Kufungiwa kwa gazeti, katika mazingira haya, tena kwa muda usiojulikana, kulionekana kwa wasomaji wake, wafuatiliaji na wachunguzi kuwa njia ya kuzima mifereji ya ukweli iliyokuwa ikielekea kumwaga ushahidi mwanana katika macho na masikio ya wasomaji wake.

Funga! Ili lisiandike habari nyeti juu ya unyama aliofanyiwa kiongozi wa madaktari katika kudai vitendeakazi na mazingira bora ya kazi. Funga! Lisifumue taarifa za nyongeza na mkondo wa mawasiliano. Funga! Ili lisiendelee kuumbua wahusika – kuanzia waliobuni “mradi” hadi waliotekeleza. Funga! Ili dunia nje ya Tanzania isije kujua unyama unaohusishwa na serikali.

Leo, kama ilivyokuwa siku ya kwanza ya siku 172 za kifungo cha MwanaHALISI, ninaendelea kukubaliana na wasomaji, wafuatiliaji na wachunguzi juu ya sababu za kufungiwa kwa gazeti: Kuingiza taifa gizani ili lisiweze kuona masuala muhimu ambayo gazeti hili limekuwa likiibua.

Kinachosikitisha ni kwamba watawala, kwa upofu wao, katika suala la Ulimboka, hawakuona kuwa gazeti lilikuwa linatoa taarifa za ndani na za kweli ambazo zingesaidia serikali kujiondoa katika tope la “kutaka kumuua Ulimboka.”

Watawala walishindwa, labda kwa kiwewe tu, kueleawa kuwa taarifa za ndani na za kina zingeonyesha muhusika mmoja na siyo serikali yote wala ikulu yote. Hawakuona kwamba taarifa za kina zingesafisha hata Usalama wa Taifa na Polisi – ambao ndio walikuwa wanatungwa kidole.

Kwa vipi? Ikulu siyo pango la wauaji. Ni makao makuu ya mtawala wa nchi. Haitarajiwi kuwa makazi ya watekaji, watesaji au wauaji. Kwahiyo, kama ikulu kuna mtuhumiwa mmoja, watawala wana haki na sababu ya kuachia wanaojua kazi kuwasaidia kufichua nani anachafua heshima na uhalali wa ikulu.

Vivyo hivyo kwa usalama wa taifa. Hawanabudi kukaa kitako na hata kuomba msaada wa nyongeza kutoka kwa wanaojua kazi yao, ili kufichua wanaotaka “kuharibu sifa” zao. Kwani, kazi ya  usalama wa taifa siyo kuteka, kutesa na kuua. Anayefanya hayo sharti awekwe wazi ili chombo hicho kibaki kikiaminiwa. Vivyo hivyo kwa jeshi la polisi.

Mvumo wa taarifa za gazeti ambao ungetunga wahusika mmojammoja kama shanga katika “sakata la Ulimboka,” ungenusuru ikulu, usalama wa taifa na polisi. Hapo ndipo ukweli na uwazi ambavyo vinaimbwa, vingesaidia serikali kuondokana na uchafu unaoweza kuiondolea imani ya wananchi na uhalali wake.

Tumekuwa tukiiambia serikali, tena mara nyingi tangu 1985 – kwamba iwapo chombo cha habari kitakosea, basi kipelekewe mahakamani ili sheria ichukue mkondo wake. Watawala hawataki hilo, bali wanataka kuonyesha kuwa wako juu ya sheria za nchi. Wanatumia ubabe.

Amini usiamini. Hata madikiteta wanahitaji taarifa na habari sahihi na za kina; hata zile zinazoonyesha wanavyonyukana ndani kwa ndani. Wameachana na ubazazi wa kufikiri kuwa, kama gazeti halikuandika au limezuiwa kuandika, basi jambo husika  halitafahamika na hivyo watatulia. Hawafanyi hivyo leo. Wanakataa kuishi kwa umbeya au vitaarifa vya kuwapongeza, kuwasifu na kuwapakata, wakati halihalisi ni tofauti.

Serikali ambayo haina taarifa juu yake na haijui wananchi wanasema au wanajua nini juu yake na wao wenyewe; haiwezi kuchukua hatua. Sasa serikali inayoua vyombo vya habari hadi itakapopakatwa, kubembelezwa na kupigwa busu, siyo serikali ya wananchi. Hata kama watawala wake watadai kuwa walichaguliwa na wananchi, sharti tukubaliane kuwa ilikuwa kiinimacho. Huwezi kuchaguliwa kutawala halafu ukapora waliokuchagua uhuru wao wa kufikiri na uhuru wa kauli.

Ni siku 172 leo tangu serikali izuie wasomaji kuona kipenzi chao MwanaHALISI. Kwamba vyombo vingine vya habari havijaguswa, haina maana kwamba serikali ina ushoga wa kudumu na vyombo hivyo. Vikitaka haki vitazimwa. Vikitaka uhuru vitaning’inizwa. Vikitaka ukweli vitafungiwa “kwa muda usiojulikana.”

Kisichoeleweka vema na haraka kwa wengi ni kwamba, kufungia MwanaHALISI au gazeti kama hilo au lolote lile lililokwishajitambulisha kuwa mdomo wa umma, ni kuweka kifungoni mamilioni ya watu na kuwaondolea kichocheo cha kufikiri.

Wangapi watakubali kubaki kifungoni bila kuhukumiwa na mahakama; bali kwa utashi dhaifu na “hukumu” ya waliobeba mamlaka ya kisiasa? Binafsi, sikubali!

fuatia pia: ndimara facebook

1 comment

chamso mc said...

nafikiri ni woga kwa serikali kufichuliwa maovu wanayo yatenda."likini tukumbuke kua itafika mahali unaye kandandamzwa naye atachoka tu"

Powered by Blogger.