Header Ads

LightBlog

KATIKA JINA LA HAKI


Miswada ikienda kimyakimya 
watapitisha kanyaboya, tutalia

Kwa zaidi ya miaka mitatu sasa, waandishi wa habari nchini Tanzania wamekuwa wakitaka serikali kuwasilisha bungeni miswada miwili ya habari. Hii ni miswada iliyotokana na juhudi kubwa ya waandishi wa habari, marafiki wa habari, wanaharakati ainaina wanaopigania uhuru wa habari na wananchi – makundi na mmojmmoja – kwa shabaha ya kujenga mazingira bora ya haki na uhuru wa kukusanya, kupewa na kutawanya habari. Ni kazi nzuri ambayo serikali imekalia kwa kipindi chote hicho.

Sasa kuna kinachoonekana kuwa juhudi za kuwataka wabunge kujadili kwa kina “miswada hiyo” ya habari na kuipitisha. Lakini kuna haja ya kujiuliza kwanza: Ni miswada ipi wanataka wabunge wajadili na kupitisha?

Kilichopelekwa serikalini kutoka kwa wadau wa habari, ni mapendekezo. Serikali imeyakalia kwa miaka yote hiyo chini ya mawaziri watatu – anatoka huyu anaingia huyu – bila kuyafanyia kazi. Hatimaye tumeanza kusikia serikali ikisema, kupitia wasemaje wake wanaojikanganya kwa tarehe za kuwasilisha bungeni, kuwa itapeleka miswada hiyo bungeni.

Utaratibu ni kwamba serikali inasoma mapendekezo. Inafanya maamuzi. Inapeleka mapendekezo kwa mwandishi mkuu wa sheria ambaye anaumba maoni na hoja za serikali katika sura ya muswada wenye mwelekeo wa mapendekezo ya wadau wa habari. Tuko pamoja?

Hapa ndipo kuna kazi. Serikali inaweza kuazima na kutumia maneno yaleyale yanayotumiwa katika mapendekezo ya wadau lakini ikaja na “moyo tofauti wa sheria” katika maumbile mapya yanayopelekwa bungeni.

Ninajua kuna wanaoamini serikali kwa asilimia 100/100. Lakini naomba kuwakumbusha mapendekezo ya muswada wa mashirika yasiyo ya serikali. Tuliumba kitu chetu. Tukaipa serikali. Ikachukua. Ikapongeza. Ikampa mwandishi wa sheria. Kilichotoka humo ni kibaya zaidi – katili, nyakuzi, ning’inizi na hatarishi kuliko hali ilivyokuwa kabla ya sheria.

Ikitokea hivyo katika miswada ya sheria, serikali itasema: “Walitaka sheria, tukawapa sheria; sana wanalalamikia kitu gani?” Tutagota upya.

Hoja: Kama serikali inasema ipo tayari kupeleka miswada ya habari bungeni; basi kwa nia njema ifanye hivi: Iweke wazi miswada hiyo kwa waandishi wa habari, wadau wa habari na wananchi; waisome, waijadili, wailinganishe na mapendekezo ya wadau wa habari, waijazie (kama itahitaji kujaziwa), wapendekeze mengine – mapya au ya awali yaliyonyofolewa, kabla ya kuiwasilisha bungeni.

Hili ni muhimu sana. Lisipofanyika, serikali itawaambia wabunge, “Hiki ndicho wadau wamekuwa wakidai. Tunaomba muwapitishie.” Ni wabunge wachache watagundua tofauti au ghiliba; na hao wachache hawatazuia miswada kupitishwa. Tutarudi palepale – kubishana na kuzozana na serikali na wa serikali.

Katika jina la haki, miswada ya serikali iwekwe wazi kwanza; tuione, tuisome, tuijadili na kuijazia. Na kama serikali ingekuwa ya uwazi, kwa kipindi chote tangu ikabidhiwe mapendekezo, ingekuwa imeumba miswada yake, kuiweka mbele ya umma kwa mjadala na kupata miswada muwafaka. Haikufanya hivyo. Sasa yaweza kuleta bomu litakaloua hata chembechembe za kilichokuwepo na kilichotupa fursa ya kudai haki ya habari.

see also ndimara's facebook

No comments

Powered by Blogger.