Header Ads

LightBlog

Nape, CCM na Kadi ya Dk. Slaa



Dk. Willibrod Slaa

Mjadala Kadi ya Dk. Slaa 'kiinimacho'

Sina kadi ya Tanganyika African National Union (TANU) - chama kilichoongoza wananchi kupigania uhuru. Sikuwahi kukata kadi ya chama hicho. Lakini nina kadi ya Umoja wa Vijana wa TANU (Tanu Youth League - TYL). Nilikuwa mwanachama na mwenyekiti wake nikiwa sekondari, Kahororo. Niliishia hapo. Sikuwahi kuwa na kadi ya TANU. Sikuwahi kuwa na kadi ya litoto lake CCM. Sikuwahi kuwa na kadi ya Umoja wa Vijana wa CCM.

Lakini bado nina kadi yangu ya TYL. Kadi hii bado imewekwa mahali salama. Imefanyiwa uzuderi (lamination) isije kupauka. Itakaa sana. Siichani. Siitupi. Simpi mtu. Ni mali yangu. Acha historia inukuu ushiriki wangu hata katika kuchanga senti 50 kwa ajili ya ujenzi wa Jengo la Vijana, Lumumba, Dar es Salaam ambalo sasa "vijana" wa chama kinachoheshimu na kulinda mafisadi (CCM) wameuza kwa pesa mbili.

Pointi: Kadi ni mali yangu. Rudi Darasa la Kwanza miaka yetu. Mwalimu anaanza kutufundisha Kiingereza: This is my book. It is my book. It is mine. 

Sasa rudi kwenye kadi: This is my TYL card . It is my card. It is mine. Nikitaka kugawa, naigawa. Nikitaka kutupa, naitupa. Nikitaka kuchoma moto, naichoma. Nikitaka kuuza kwenye mnada, naiuza. Sasa kwanini Dk. Slaa asibaki na kadi yake na hata nyingine zozote atakazoweza kuwa nazo (sasa na baadaye) hadi pale atakapotaka kuachana nazo?

Bali mjadala wa "Kadi ya Dk. Slaa" una maana pana. Unaonyesha jinsi viongozi wa chama kilichopanga ikulu kwa miaka 51 wanavyoweza kuacha hoja kuu za kufikirisha mtu binafsi na jamii; na badala yake kujiviringisha na kuviringisha wananchi katika malumbano dhaifu (triviality) ili kupoteza muda na kuondoa akili zao kwenye hoja kuu za wakati tuliomo. Ndiyo, ni ndoana. Lakini nani ataimeza wakati anajua ni ndoana?

ndimara

No comments

Powered by Blogger.