Header Ads

LightBlog

ITIKA WA DAUDI MWANGOSI


Masalia ya Daudi Mwangosi



ITIKA HAITIKI

Itika haitiki
Hakuna anayemwita.
Naye Itika haitwi
Aliyemwita hayupo.

Jinale watoto hawajui
Wao siku zote waita "mama"  
Mwenye Itika haitiki
Aliyemwita kabaki vipande.

Itika aliitwa na Daudi
Yule Daudi wa Mwangosi
"Mke" au mama fulani
Kinywani hayakutoka
Itika lilinoga mdomoni
Itika lilikuwa jina
Lakini pia lilikuwa wito
Na Itika na Daudi
Waligwaya kwa vicheko.

Mume kabaki masalia
Yule aliyemwita Itika.
Itika hana cha kuzika
Vidole vitatu na kucha
Na vipande vya miguu?
Pande la baba alobusu
Kwa mbwembwe na madaha
Kila litokapo na kuingia;
Limebaki minofu
Mikononi mwa polisi.

Itika anabumbabumba 
Vitoto vyao vinne
Cha mwisho hakielewi 
Umri umekizonga
Miaka miwili ni kinda
Kingali chafyonza Itika;
Na minofu ya baba
Wadai muhali kuona.

Itika katu haitiki!
Amwitike nani?
Aliyemfungia ngama
Amerudishwa vipande.
Anakabidhiwa furushi
Ni minofu ya mumewe.

Mito na maziwa ya machozi
Ndio kitambulisho cha Itika
Anawaka na kuzimika 
Ukiita haitiki Itika.
Hata kwa mtikiso mnono
Abaki kutetemeka
Alotoka akiwa mtu, 
Akiwa mume
Anarudishwaje minofu?

Vipandevipande kwa chungwa
Hilo halina maswali
Vipandevipande kwa embe
Hilo halina ubishi
Vipandevipande kwa muhogo
Nani atakuuliza 
Vipandevipande kwa mtu -
Kwa Daudi Mwangosi
Itika na mimi hatuelewi.

Wei! Wei! Wei!
Waile minofu yao
Wangu hakuwa minofu
Wangu alikuwa mtu
Wangu alikuwa mume;
Niliyejichagulia
Niliyezaa naye wanne hawa.
Warudishe mume wangu...
Wei! Wei! Wei!

Huulizi swali
Husikii Itika akifoka
Unaona uso ukivimba
Unaona uso ukinyauka
Unaona Itika anatweta
Unaona akibubujikwa machozi
Akikamka jasho
Ghafla ananyauka
Ghafla anaibuka
Ni wewe tu unayeyaona
Kwani Itika haitiki

Ni nini hii?
Ni bahati mbaya nyingine?
Ni bahati mbaya ya makusudi?
Sasa waja na jipya:
Wadai wanafanya uchunguzi
Uchunguzi upi kwa minofu?

Wanachunguza nini?
Kilichomuua mume wa Itika?
Kwani hawakijui
Wanachunguza nani?
Aliyemuua Mwangosi wa Itika?
Kwani hawamfahamu
Kwani hawakumuona
Kwani hawakuwepo
Wanamtania nani
Katikati ya majonzi?

Wauawe wangapi…?
Nauliza wangapi ndipo tunune?
Ndipo tuchukie
Ndipo Itika asikike
Yeye na maelfu wengine
Tukilaani bunduki walizobeba
Tukilaani waliowatuma
Tukilaani walioshindwa kazi
Lakini ving’ang’anizi ofisini?

Wauawe wangapi tuape
Tujiapize kuishi
Kuishi…kui...

Woga watakufa kihoro
Jasiri watasonga mbele
Historia inaandikwa
Wa kileleni wasome nyakati.



MWISHO



Powered by Blogger.