Header Ads

LightBlog

WAZIRI GHASIA ANATETEA SIRI ZIPI?

Waziri Ghasia anayeleta ghasia

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI Hawa Ghasia kwa kuwa analeta ghasia katika mjadala kuhusu siri na hasa kile kinachoitwa “nyaraka za siri za serikali.”

Kauli ya waziri huyu wa Utumishi bungeni wiki hii, inaonyesha kuwa yeye binafsi, na huenda siyo serikali, anataka wananchi watembee wamebana pumzi kwa kuogopa kuwa kila walichonacho mkononi ni siri ya serikali.

Ameonya kwamba yeyote atakayekutwa na nyaraka za siri za serikali, “hata kama ni mbunge,” atachukuliwa hatua za kisheria. Ni onyo kali kutoka kwa Waziri wa Utumishi katika Ofisi ya Rais.

Hoja ya siri imejadiliwa mara nyingi. Nilidhani wahusika serikalini walielewa. Kumbe tulipoifikisha kileleni wengine walikuwa hawajaingia serikalini. Ndio sasa wanajaribu kuitoa kileleni na kuirudisha sakafuni.

Kila serikali duniani ina siri. Siri hizi hupangwa kwa viwango maalum – ndogo, kubwa kidogo, kubwa, kubwa sana, kubwa kabambe, kubwa na nene, kubwa na nzito, kubwa kuliko…

Mtanuo huu wa ukubwa hutegemea mfumo wa utawala na tabia ya wachache walioko madarakani ambao hutunga sheria za kulinda kile wanachoona ni siri za serikali. Wakati mwingine, katika ukorokoroni wa nyaraka, watawala hujikuta wanaona kila kitu ni siri na hakuna viwango tena.

Upele mgongoni mwa serikali huitwa siri. Mba shingoni mwa serikali huitwa siri. Jipu makalioni mwa serikali huitwa siri. Kikohozi cha muda mrefu huitwa siri. Tatizo hapa ni kwamba hufikia wakati hata mkubwa kwenda haja kubwa hadharani huitwa siri!

Ni katika hatua hii, watu huangalia pembeni; hutema kwa kinyaa, huku wakibinua midomo kama waliolamba tone la shubiri na kunong’ona, “Ee, kila kitu siri, siri.”

Siri ya serikali inabidi iwe siri kwa manufaa ya nchi. Haiwezi kuwa kwa manufaa ya watawala au kundi la watawala peke yao. Lakini ainisho hili huleta mgogoro kati ya watawala na watawaliwa.

Ununuzi wa ndege za kijeshi huitwa siri. Ukodishaji ndege za jeshi kwa watu binafsi huitwa siri. Uuzaji ardhi, mikataba ya kuchimbaji madini, mikataba ya uzalishaji na ugavi wa nishati ya umeme, vyote huitwa siri. Vivyo hivyo uuzaji wa raslimali nyingine za taifa nje ya nchi.

Siri hupanuka hadi kuhusisha shughuli za rais nje ya shughuli kuu ya utawala. Mikataba ya ununuzi wa rada na manunuzi mengine panapotumika fedha za umma hufanywa siri pia. Siri za aina hii hufikia wakati zikawakwama kooni wale waliopewa jukumu la kuzilinda, nao wakaamua kuzitoa; siyo kama siri bali kama makabrasha tu.

Hapa ndipo yanapotokea maasi. Ni hapa ambapo serikali inashindwa kuthibitishia hata mlinzi kuwa kile anacholinda ni siri. Ni hapa ambapo mlinzi anaamua kusema, “Potelea mbali. Hata kama nitapoteza kibarua, lakini sharti hili lifahamike kwa wengi.”

Hakuna anayenunua vikaratasi vyenye mikataba na viapo vya wahusika katika mikataba hiyo iliyofanywa siri. Hayupo. Mengi ambayo serikali inaita nyaraka za siri yanatolewa kwa hisani tu na hata bila juhudi za uchunguzi wa kina.

Wanaodaiwa kuwa walinzi wa siri hawajatoa taarifa zozote za kuibiwa kwa nyaraka wala kuvunjwa kwa sefu za nyaraka na kukwapuliwa kwa siri. Taarifa hizo hazipo. Raia wema waliochoka kuona “siri” zisizo siri ndio wanawapelekea “makaratasi” wabunge na waandishi wa habari.

Ukitumia viwango sahihi, na kwa kuzingatia misingi ya uandishi wa habari za uchunguzi, utaona kuwa sehemu kubwa ya kile ambacho wengi wanaita “uchunguzi,” hasa siyo uchunguzi kwa maana halisi.

Taarifa nyingi zinapatikana kwa njia ya nyaraka zilizotolewa kwa hisani – na mara nyingi bila ufundi wala ubunifu – na wakati mwingine bila juhudi za mwandishi au mbunge. Hii waweza kuita “chakupewa.”

Hata hivyo, kwa kutumia ustadi na ufuatiliaji wa kiwango cha “kuku wa kujitafutia,” taarifa hizo zimetoa mwanga wa kile kinachoendelea na wakati mwingine kupanua wigo wa kidogo kilichopatikana kuwa mkubwa zaidi na kuhusisha wengi.

Vyovyote ilivyo, serikali inapaswa kulinda kile ambacho inaita nyaraka zake za siri. Hakuna mwenye uwezo wala mamlaka ya kulinda siri za serikali isipokuwa serikali yenyewe.

Ni serikali itakayobuni na kuweka njia “bora” za kulinda siri zake – ziwe siri kweli au viinimacho. Ni serikali inayostahili kujua nani mwenye uwezo wa kulindia siri na uwezo huo hunawirishwaje, huongezwaje na hulindwaje.

Mpaka hapa ni muhimu basi kukubaliana kuwa kama serikali ina siri, basi ilinde siri zake. Serikali ikishindwa kulinda siri zake; na siri hizo zikatoka, haina sababu ya kulalamikia yeyote – awe mbunge au mwandishi wa habari.

Maswali ambayo huulizwa mara nyingi ni: Kama serikali imeshindwa kulinda siri zake, walioko nje ya serikali watazilinda vipi? Watawajibikaje kuzilinda? Watajuaje kuwa ni siri na kama ni siri za serikali?

Lakini hata wakijua, kwa maelezo rasmi kuwa ni siri, kwanza watajuaje kuwa hazijachoka na ndiyo maana zimeachiwa kuranda mitaani? Pili, watashindwaje kuzitumia katika hoja iwapo wanaona kuwa zina chembechembe za kuinua uelewa wa jamii juu ya mwenendo wa serikali yao?

Tatu, hata wabunge na waandishi wakizisaka kwa mbinu, ufundi na ujanja wao, kwa lengo la kuneemesha jamii na kukuza mwamko na uelewa, bado hilo haliwezi kuwa kosa machoni mwa wananchi ambao walifichwa ukweli husika.

Bali kuna haja ya kuzingatia jambo moja. Mjadala juu ya wizi au matumizi ya nyaraka za siri za serikali unarudi wakati wadau wa utawala bora, wakiwemo waandishi wa habari, wanasheria, wabunge, wanaharakati wengine wanasubiri serikali kuwasilisha bungeni muswada wa Uhuru wa Habari.

Kwa kuzingatia mwelekeo uliotolewa na wadau nje ya serikali, kuhusu umuhimu na njia za “kukomboa habari,” mapendekezo hayo yakizingatiwa katika sheria ya Uhuru wa Habari, yatamaliza malalamiko ya Ghasia.

Kwani hadi sasa, kila kilichosemwa bungeni na kuandikwa na kutangazwa na vyombo vya habari – kile ambacho serikali ilikuwa haijakitoa rasmi – hakina madhara kwa serikali adilifu wala jamii kwa ujumla.

Kama serikali iko makini na inajiandaa kuwatendea haki wananchi wake kwa kutambua uhuru wao wa kupata taarifa na habari, na kusimamia utekelezaji wa uhuru huo, basi Ghasia hana budi kuanza mazoezi ya kuishi nje ya mipaka bandia.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
(Makala hii itachapishwa katika safu ya SITAKI ya gazeti la Tanzania Daima Jumapili la 26 Aprili 2009)

1 comment

dyanna said...

I like your blog.

Powered by Blogger.