Header Ads

LightBlog

KLABU HAI YA WAANDISHI DAR


Klabu ya waandishi wa habari ya Dar es Salaam (DCPC) jana Jumatano (28 Agosti 2013) ilifanya warsha ya siku moja jijini katika Hoteli ya Peacock. Ilihusu utekelezaji shughuli zake chini ya kaulimbiu ya klabu nchini mwaka huu isemayo: Klabu ya waandishi wa habari ni nguzo ya maendeleo ya mkoa. Lifuatalo ni wasilisho la Ndimara Tegambwage aliyealikwa kutoa uchokozi.

SASA TUTENDE TUNACHOTAMANI

NINATAMANI kuwa na klabu ya waandishi wa habari. Iwe ya kujenga umoja na ushirikiano wa waandishi katika eneo letu. Iwe ya kutukutanisha wakati wowote, kwa jambo lolote linalohusu mwanachama, klabu na taaluma.

Ninatamani kuwa na klabu ya waandishi inayosimamia misingi ya taaluma kwa njia ya kuzingatia maadili. Inayohimiza wanachama  wake kusoma na kujisomea ili kuongeza elimu, maarifa na stadi. Inayotafuta fursa za ndani na nje za wanachama wake kupanua upeo wa fikra na utendajikazi.

Ninatamani kuwa na klabu ya waandishi inayojifunza na kufunza wanachama wake mbinu za utendaji kazi na katika mazingira anuai. Inayotafuta jinsi wanachama wake wanavyoweza kujiendeleza – ndani na hata nje ya nchi. Inayotafuta fursa za kukuza na kuimarisha ushirikiano miongoni mwa waandishi wa habari, klabu yao na wadau wa habari.   

Sina uhakika kama hii ndiyo klabu mliyonayo – Klabu ya Waandishi wa Habari Dar es Salaam (KWAHADA).

Fursa za elimu na maarifa

Ninatamani klabu ya jiji kubwa la Dar es Salaam, yenye fursa kedekede za elimu na maarifa. Penye wanataaluma wengi. Penye sifa za kazi za viwango vya juu. Penye utajiri wa uzoefu. Penye wepesi wa mawasiliano ya ndani na nje ya nchi.

Ninatamani klabu yenye mahusiano ya kitaaluma na asasi kama vile Tanzania Media Fund (TMF). Ili ikuze uwezo wa wanachama wake katika nyanja ya habari za uchunguzi. Ikuze stadi na hata kuibua vipaji.

Natamani klabu inayoshirikiana moja kwa moja na asasi kama vile Baraza la Habari Tanzania (MCT). Ili kuwa mtekelezaji na msimamizi wa maadili ya kazi. Ili kulinda na kutetea haki ya uhuru wa kuandika na uhuru wa habari.

Klabu yenye mahusiano na asasi za ndani na nje zinazopigania umuhimu wa waandishi kujisimamia katika utekelezaji wa kazi zao badala ya kushikiwa kiboko na watawala.

Sina uhakika kama hii ndiyo klabu mliyonayo.

Maktaba na Press Centre

Ninatamani klabu ya waandishi yenye makazi maalum – Press Centre. Makazi yenye zana za kazi, maktaba na kituo cha vyanzo maridhawa vya taarifa na habari, kwa matumizi ya waandishi wa ndani na nje ya nchi.

Ninatamani klabu yenye utaratibu wa kila wiki au kila mwezi wa kuwa na mgeni; kutoka ndani au nje ya nchi, kuhojiwa na waandishi juu ya jambo muhimu la wiki au lolote muhimu walilochagua kwa wakati uliopo.

Hii, licha ya kuwa chemchemi mpya ya taarifa, itakuwa kiungo kati ya klabu na wadau wa habari – serikali, waserikali, mashirika, kampuni, asasi, vyombo vingine vya habari na watu binafsi. Hiki ni chanzo cha taarifa, lakini pia ni darasa.  

Ninatamani kuwa na klabu yenye uwezo wa kuandaa ajenda muhimu za kitaifa na kwa kushirikiana na klabu na wadau wengine, kuzifafanua, kuzifuatilia, kuzipigania na kuzing’ang’ania “hadi kieleweke.” Huu utakuwa mbadala wa kudonoa hoja na hata kuzika nyingine zingali hai.

Ninatamani kuwa na klabu itakayokuwa nguvu ya pamoja ya kufuatilia, kuhoji, kukemea na kukabiliana, kwa njia yoyote ile, na lolote linalotishia uhai wa mwandishi mmojammoja; umoja wa waandishi katika klabu, uhai wa klabu na uhai wa jamii tunayotumikia.

Sina uhakika kama hii ndiyo klabu mliyonayo. Niruhusu basi niseme kuwa hivyo ndivyo vipengele vya malengo ambavyo tunahitaji kuwekea mikakati ya utekelezaji.

Klabu na maendeleo

Nimealikwa hapa kujadili mada isemayo, “Klabu ya Waandishi wa Habari ni Nguzo ya Maendeleo ya Mkoa.”

Binafsi sioni mkoa haraka. Ninaona mtu katika kaya, mtaa, kitongoji, kijiji, kata na wilaya. Mtu. Huyu ndiye anapaswa kutumikiwa ili kuleta mabadiliko katika maisha yake. Na mabadiliko ndiyo maendeleo.

Kwahiyo, tunapojielekeza kwenye mkoa, tunalenga kushawishi wasimamizi wa “muungano wa tawala za wilaya” na wataalamu wao – kuona umuhimu na uhalali wa kuwa karibu na klabu ya wanahabari ili kufikia na kuhudumia yule ambaye ni tofali la kwanza kwenye mwili wa jamii: Mtu mmoja.

Ni wazi kwamba bila taarifa na habari, kunakuwa na utupu usionawirisha ubongo. Kile kitekenyi cha mabadiliko kwa njia ya kufikiri kinachotokana na mlisho wa taarifa sahihi, kinakosekana au kinatoweka.

Jukumu la wadau

Kwahiyo, wadau wa habari – watawala (serikali mkoani), watendaji wake, wafanyabiashara wakubwa, mabalozi wa nchi mbalimbali, wananchi kwa ujumla wao – wana nafasi ya kushiriki ujenzi na uimarishaji wa klabu. Baadhi ya serikali duniani (ikiwemo ya Sweden) hutoa ruzuku kwa vyombo vya habari makini, siyo kwa kuvihonga, bali kuviwezesha kuwa chokonozi zaidi, makini zaidi na kufikia jamii pana.

Kuna njia nyingi za wadau kushiriki kujenga klabu ya waandishi wa habari Dar es Salaam. Hapo awali nimejadili kazi za klabu kuwa ni pamoja na kutoa mafunzo kwa wanachama wake ili kuongeza elimu, maarifa na stadi. Utendaji bora unaundwa na kunawirishwa kitaaluma.

Kwahiyo, njia za wadau kushiriki kujenga na kuimarisha klabu ya kudumu ya Dar es Salaam, kwa manufaa ya mkoa na taifa, ni pamoja na kuiwezesha kuwa na makazi ya kudumu, ya hadhi ya jiji (vikiwemo vifaa); kuwa na mfuko kwa ajili ya mafunzo ya nyongeza kwa waandishi; na kuhiari kutoa taarifa kwa waandishi pindi wanapowaendea.

Mwandishi ni mtafutaji. Ni mfuatiliaji. Ni mwanikaji wa alichovuna kwa ajili yako na jamii kuona, kujua na kunufaika. Anatafuta taarifa. Wewe unazo. Mpe. Ameona utekelezaji wa mipango yenu una walakini. Anakuomba maelezo. Mpe. Amenusa wizi/ufisadi ofisini mwako. Anakuomba maelezo. Mwambie.

Mwandishi ameona mafanikio au kukwama katika ofisi, kampuni au shirika lako na anataka kujua siri ya hilo. Mweleze. Una jambo la kuwasilisha kwa umma. Mpe. Kwa njia hii, wewe na yeye mtakuwa mmeshiriki kuleta au kufanikisha maendeleo.

Hitimisho

Tukiwa na klabu ya waandishi wanaothaminika kwa kazi, watendaji watajihisi kuwa na “mchungaji” begani mwao. Maadili hukamilishwa na uchungaji unaoanika matendo ya wenye madaraka. Baya ambalo wangefanya wataliacha. Wataamka saa nane usiku kutoa taarifa za umma.
Watendaji watafungua mafaili kwa mwandishi kupata usahihi. Watakemea ofisa anayeficha taarifa. Watatonya waandishi kipi kinakwenda ovyo. Wataumbua waandishi wanoomba rushwa. Lakini wakificha taarifa hawatasikitika pale watakapozikuta ukutani.

Je, kwa haya na yote tuliyoorodhesha hapo awali, tuanzie wapi? Tuanze lini? Tuanze na lipi? Kazi kwenu.
Mwisho
*Ndimara Tegambwage ni mwelekezaji (mentor) katika habari na mawasiliano. Simu: +255 713614872
imeili: ndimara@yahoo.com;  blogu: ndimara.blogspot.com (uhuru hauna kikomo…)  Inapatikana pia kwenye: www.facebook.com/ndimara.tegambwage/



No comments

Powered by Blogger.