Tuesday, December 25, 2012

UMASIKINI TISHIO LA AMANI


                       

Padri aonya juu ya umasikini uliokithiri

Na Lilian Tegambwage

PADRI Dennis Massawe wa Parokia ya Tegeta nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam amesema, “…wanyonge wa nchi hii wakichoka unyonge wao, yatatokea machafuko makubwa.”

“Tuombe kwa ajili ya wanyonge. Hawa ni wale wanaolala njaa; wanaokwenda hospitali na kuambiwa hakuna dawa; watoto wao wanashindwa kwenda shule kwa kuwa hawana daftari…” amesema Padri Massawe.

Alikuwa akihubiri leo Jumanne, kwenye Misa ya Krismasi katika Kigango cha Mtakatifu Petro cha Parokia ya Tegeta kilichoko Tegeta Masaiti.

Amesema wanyonge wakichoka Tanzania kutatokea “machafuko makubwa sana;” akiongeza, “Tuombe sana kwa ajili yao. Tuombe wasichoke.”

Mahubiri ya Padri Massawe yamechukuliwa kama njia mojawapo ya kukumbusha na kuonya watawala kuhusu “bomu la umasikini” ambalo linaweza kulipuka wakati wowote pale waliotupwa nje ya mzunguko wa kunufaika na raslimali za taifa watakapoamka na kudai haki zao.

Kwa upande mwingine, padri alikuwa akiwatekenya wanyonge wenyewe kuvua unyonge wao na kuelekeza madai ya haki na matakwa yao kwa waliopewa mamlaka ya utawala wa nchi.

Kauli ya padri ilifananishwa na mahubiri ya mapadri wa nchi za Amerika Kusini ambao miongo minne iliyopita walianza kuhubiri kwamba sharti wananchi wao waanze kuishi hapahapa duniani maisha bora ambayo wanahubiriwa.

Ni kauli hizi ambazo ziliunganisha waumini Wakristo na watu wa madhehebu mengine, kwa upande mmoja, na wanaharakati na wapigania mabadiliko, kwa upande mwingine, katika kupigania haki na usawa katika nchi zao.

Akigeukia waumini, Padri Massawe amesema, “…wengine tumekuwa tunakuja hapa kwa mazoea tu. Tunakuja kanisani kujifurahisha. Tukitoka kanisani, sisi ndio tunakuwa vinara wa maovu kama ufisadi, ngono, wizi na chuki.”

Padri alitoa mfano wa waziri mmoja wa India ambaye alimnukuu akisema anampenda sana Yesu Kristo kwa kuwa amefanya kazi kubwa katika dunia; lakini hapendi wakristo kwa sababu hawaishi kama Yesu na kama biblia inavyosema.

Biblia, kiongozi cha madhehebu ya Kikristo, ni moja ya vitabu vilivyosomwa na kuchambuliwa sana duniani; kikiwa kimesomwa na wanaoamini na wasioamini katika madhehebu hayo.

Leo ni siku ya Krismasi inayoadhimishwa rasmi na wakristo kote diniani kwa kumbukumbu ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo zaidi ya miaka 2,000 iliyopita.

Kigango cha Mtakatifu Petro kilifurika waumini waliotumbuizwa na kwaya ya Mtakatifu Andrea ya kigangoni hapo.

Padri aliwaombea waumini wote akisema washerehekee Krismasi kwa amani.

Katika hatua nyingine, washiriki walisimama kwa dakika moja kukumbuka muumini maarufu Erasmus Lunaga, mwenyekiti wa Jumuiya ya Timotheo, Machakani-Sinza, aliyefariki siku ya Krismas mwaka jana.
(Lilian anasomea diploma ya IT (University of Dar es Salaam Computing Centre). Alikwenda kanisani leo asubuhi. Aliporudi nikamwomba anieleze kwa maandishi, kile ambacho kimehubiriwa. Akakaa chini na kuandika taarifa hiyo hapo juu. Nimeongeza aya moja tu. Naona anaweza huko aendako).
  •  Picha juu: Polycap Kardinali Pengo
 
 
 

Saturday, December 15, 2012

Porojo za Msajili John Tendwa

JOHN Tendwa, Msajili wa Vyama vya Siasa ambaye ni mwajiriwa wa serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), hupenda kutishia kufuta vyama vya siasa.

Mwandishi wa habari, Mwangosi alipouawa akiwa mikononi mwa polisi, Tendwa alitishia kufuta vyama "vinavyosababisha mauaji." Polisi wanaotuhumiwa kuua mwandishi ni wa serikali ya CCM. John tendwa hajafanya lolote. Yeye hutumika kuhalalisha au kutetea waliompa ofisi. Amekaa kimya mpaka Saidi Michael akamwona.

Mkuki kwa nguruwe, kwa binadamu mchungu! 

Nape, CCM na Kadi ya Dk. Slaa



Dk. Willibrod Slaa

Mjadala Kadi ya Dk. Slaa 'kiinimacho'

Sina kadi ya Tanganyika African National Union (TANU) - chama kilichoongoza wananchi kupigania uhuru. Sikuwahi kukata kadi ya chama hicho. Lakini nina kadi ya Umoja wa Vijana wa TANU (Tanu Youth League - TYL). Nilikuwa mwanachama na mwenyekiti wake nikiwa sekondari, Kahororo. Niliishia hapo. Sikuwahi kuwa na kadi ya TANU. Sikuwahi kuwa na kadi ya litoto lake CCM. Sikuwahi kuwa na kadi ya Umoja wa Vijana wa CCM.

Lakini bado nina kadi yangu ya TYL. Kadi hii bado imewekwa mahali salama. Imefanyiwa uzuderi (lamination) isije kupauka. Itakaa sana. Siichani. Siitupi. Simpi mtu. Ni mali yangu. Acha historia inukuu ushiriki wangu hata katika kuchanga senti 50 kwa ajili ya ujenzi wa Jengo la Vijana, Lumumba, Dar es Salaam ambalo sasa "vijana" wa chama kinachoheshimu na kulinda mafisadi (CCM) wameuza kwa pesa mbili.

Pointi: Kadi ni mali yangu. Rudi Darasa la Kwanza miaka yetu. Mwalimu anaanza kutufundisha Kiingereza: This is my book. It is my book. It is mine. 

Sasa rudi kwenye kadi: This is my TYL card . It is my card. It is mine. Nikitaka kugawa, naigawa. Nikitaka kutupa, naitupa. Nikitaka kuchoma moto, naichoma. Nikitaka kuuza kwenye mnada, naiuza. Sasa kwanini Dk. Slaa asibaki na kadi yake na hata nyingine zozote atakazoweza kuwa nazo (sasa na baadaye) hadi pale atakapotaka kuachana nazo?

Bali mjadala wa "Kadi ya Dk. Slaa" una maana pana. Unaonyesha jinsi viongozi wa chama kilichopanga ikulu kwa miaka 51 wanavyoweza kuacha hoja kuu za kufikirisha mtu binafsi na jamii; na badala yake kujiviringisha na kuviringisha wananchi katika malumbano dhaifu (triviality) ili kupoteza muda na kuondoa akili zao kwenye hoja kuu za wakati tuliomo. Ndiyo, ni ndoana. Lakini nani ataimeza wakati anajua ni ndoana?

ndimara

Wednesday, November 21, 2012

JIPE MOYO SCHOOL - Kishuro Primary School

                                                 All smiles: Standard VII finalists 2012



Bring Your Child To
JIPE MOYO SCHOOL
For Quality Education      

"ROOTS OF EDUCATION ARE SOUR,
BUT ITS FRUITS ARE SWEETER
THAN YOU CAN IMAGINE"

Contact:

P.O. Box 120, Rubya, Kagera

Phone: 0685 805077 & 0758 979310

kishuronurseryprimarysch@yahoo.com

Wednesday, November 14, 2012

NIPIGE NIKUPIGE

Ni jana tu mjini Dodoma. Upigaji kura za "maruhani" ulishindikana. Msimamizi wa uchaguzi Kizota, Anna Makinda alikuja na utaratibu mpya. Kwanza, kila mkoa upigie katika sanduku lake peke yake. Pili, atakayeona karatasi ya kupigia kura imeharibika, aende kwake apate nyingine. Kumwondoa Kikwete uongozini kama Thabo Mbeki, kumekwama licha ya gharama za kikundi kimoja kudaiwa kupeleka vijana Afrika Kusini kujifunza jinsi ya "kumfungisha virago." Sasa wanaotaka kumwondoa watulie au wahamie chama kingine - kile chama cha washindi.

Wednesday, October 17, 2012

MTANZANIA WA KWANZA KUPANDA MLIMA EVEREST



MTANZANIA KWENYE KILELE CHA EVEREST

Ni Wilfred Moshi. 
Amekuwa Mtanzania wa kwanza kufika kilele cha mlima mrefu kuliko yote duniani.
 
Na Freddy Macha 
kwa ushirikiano wa Urban Pulse

KIJANA Wilfred Moshi, ameweka rekodi ya kuwa Mtanzania wa kwanza kupanda mlima Everest - mlima mrefu kuliko yote duniani.

Huyu ni “Mbongo” wa kawaida tu, mzoefu wa kufanya kazi ya upagazi ya kuwahudumia watalii wanaopanda mlima Kilimanjaro.

Hivi karibuni, Moshi alialikwa nchini Uingereza kutembelea shule mbalimbali za Scotland. Alikuwako kwa majuma matano na kuweza kukutana na takribani wanafunzi 5,000.

Wanafunzi walitaka kufahamu namna alivyopanda mlima Everest wenye mita 8,848 (futi 29, 029). Watu 4,000 wamewahi kupanda mlima huu mgumu kukwea kuliko yote duniani, tangu Edmund Hillary na Sherpa Tenzig Norgay walipofika kileleni mwaka 1953. Watu 200 kati ya waliokwea mlima huo walifariki.

Mwaka huu wanne wameshafariki wakijaribu shughuli hii inayochukua  miezi miwili na kugharimu Dola 100,000 (Shilingi milioni 157,500,000). Hapa, linganisha na Mlima Kilimanjaro unaopandwa kwa siku tano na kwa gharama (ikiwepo ya vifaa husika), Dola 2,000 (Shilingi milioni 3.1).

Wilfred Moshi ni Mtanzania wa kwanza na Mwafrika wa tatu kufikia kilele cha kitendawili hiki cha “Chomolungma” – jina la wenyeji kabla mlima huu haujabandikwa jina la Everest, enzi za ukoloni wa Uingereza.  Alikanyaga kileleni tarehe 19 Mei mwaka huu.

Wilfred alizaliwa mwaka 1979. Alimaliza Kidato cha VI shule ya Kilimanjaro Boys. Amekuwa akipanda Mlima Kilimanjaro tangu angali bado shuleni – akiwa na miaka 19.

Mara baada ya kuwasili Edinburgh, Scotland,  Wilfredalikaribishwa bungeni; akakutana na Waziri wa Sheria, Mheshimiwa Kenneth MacAskill na viongozi wengine. Safari hii ilikirimiwa na shirika la “Twende Pamoja” lililoanzishwa na Mike Knox miaka 30 iliyopita.

“Twende Pamoja” limejenga ushirikiano kati ya wanafunzi wa Scotland na shule 34  za Tanzania. Ni moja  ya mashirika, watu binafsi  na wafadhili mbalimbali duniani waliochangia fedha za kumwezesha Moshi kupanda mlima Everest.

Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Mheshimiwa Peter Kallaghe, naye alisafiri toka London kumtembelea Wilfred Moshi na kumpa heko. Umbali wa London hadi Scotland ni kama Dar es Salaam na Kigoma.

Lakini kwanini Moshi anahusudu kupanda milima.

Yeye anasema, kwanza lengo lake lilikuwa kutimiza ndoto yake ya kuwa Mtanzania wa kwanza kupanda Everest. Ameitimiza.

Pili, upandaji milima ni moja ya njia zinazoweza kusaidia kujenga jamii kwa misaada na fadhila za mashirika yasiyo ya kiserikali (NGO). Tujiulize vipi alisaidiwa na watu wengi kuchanga fedha nyingi kiasi hicho.

Tatu, Moshi amethibitisha ukiwa na moyo na jitihada unaweza kufanya lolote. Ushujaa na ushupavu wake utasaidia kuwahamasisha Watanzania kuwa, ukitaka kufanya jambo lolote lile, unaweza ili mradi uwe na moyo na nidhamu.

Mpanda milima mashuhuri, Mike Hamill, aliyekwishafika vilele vyote vya milima mikubwa saba duniani, anasema katika kitabu chake kipya – Climbing Seven Summits –  kwamba wapanda milima ni watu wenye moyo wa kufikia malengo na kufanikiwa katika maisha yao.

Akiwa Uingereza, Moshi alipanda mlima wa Ben Nevis,  mrefu kuzidi yote katika nchi hii – wenye mita 1,344 (futi  4, 409).

Baada ya kuimudu milima mitatu, sasa Wilfred Moshi ameazimia kupanda milima katika mabara yote saba duniani. Anasema amebakisha milima ya Aconcagua (Marekani ya Kusini ), Kosciuszko (Australia), Vinson Massif (Antarctica), McKinley (Alaska) na  Elbrus (Urusi).

Mungu ambariki Mtanzania huyu mwenye hamasa na anayetuletea sifa.

Soma habari zaidi:
http://wilfredmoshi.wordpress.com/



Sunday, September 9, 2012

Kiatu cha John Tendwa kinapwaya


Polisi, mauaji, polisi, mauaji

Na Ndimara Tegambwage
SITAKI John Tendwa. Amenukuliwa akisema kuwa polisi kuua raia ni jambo la kawaida. Swali linakuja: Kwa hiyo?

Wengi tunajiuliza: Kwa hiyo nini? Kwa hiyo polisi wa Tanzania waue tu? Kwa hiyo waige au waendelee kuua? Kwa hiyo liwe taifa la polisi kuua raia tu badala ya polisi kulinda raia na mali zao? 

Tendwa alinukuliwa akisema hayo Ijumaa usiku katika kipindi cha “Kiti Moto” kupitia kituo cha televisheni cha ITV. 

Kauli ya Tendwa inatokana na utetezi wake wa kile kinachofanyika nchini: Mauaji ya wananchi yanayofanywa na polisi. Wanamjadala wenzake walimpa mifano mingi ambako polisi wameua raia.

Katika mjadala huo, Tanzania ilitajwa kuwa miongoni mwa nchi nne zenye idadi kubwa ya wananchi waliouawa na polisi.

Ikatajwa kuwa polisi wa Tanzania hawana hata chombo cha kuwaangalia au kuchunga mwenendo wao. 

Ikaelezwa kuwa polisi wa Tanzania wakiua wanaunda tume yao kuchunguza mauaji waliyofanya na kumalizia kwa kunyamaza au kuhalalisha mauaji.

Ni hapo Tendwa alipopakua kilichokuwa rohoni mwake kwa kusema mbona hata katika nchi nyingine polisi wanaua wananchi.

Haihitaji akili ya nyongeza kuona kuwa Tendwa anatetea mauaji. Anatetea udhalimu. Anahalalisha mateso na vifo. Anafurahia tendo la polisi kuua.

Tusema tu hapa kuwa kuna baadhi ya askari polisi wanaochukia mauaji. Wapo! Nimeongea nao. Sasa Tendwa anatetea nani?

Jana niliongea na baadhi ya maofisa wa ngazi ya juu katika jeshi la polisi kuwauliza iwapo Tendwa alikuwa anaongea kwa niaba ya jeshi la polisi au alitumwa kufanya hivyo. Wote wanne wakasema hawezi kutumwa kitu kama hicho.

Siyo kweli basi kwamba msajili wa vyama aliishiwa msamiati ndipo akasema aliyosema. Siyo kweli kwamba alipitiwa. Siyo kweli kwamba alikuwa amechoka. Hapana! 

Kauli ya Tendwa ndiyo “mlo” aliokuwa ameandalia wasikilizaji wake katika kipindi cha Kiti Moto. Ndiyo mvinyo aliyotaka isindikize kauli zake nyingine. Kama sivyo, aliingizaje hili la hata katika nchi nyingine polisi huua wananchi?

Mfano wa mauaji wa hivi karibuni ni ule wa Mufindi, Iringa ambako mwandishi wa televisheni Daudi Mwangosi alilipuliwa kwa bomu akiwa mikononi mwa polisi.

Niliwahi kuandika kuwa sitaki John Tendwa, Msajili wa Vyama vya Siasa nchini kwa sababu nyingi nilizotaja moja wapo ikiwa vitisho kwa vyama vya upinzani na kubeba, katika mbeleko, Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Leo simtaki Tendwa kwa kuwa anatetea umwagaji damu. Amevaa kiatu kisicholingana na mguu wake. 

Ni hivi: Tendwa alipewa kiatu. Aliyempa kiatu ni rais. Huyu rais hakumpima. Wala hakumpa kwanza ajaribu. Alimwabia “Vaa hiki hapa!” 

Angalia kiatu chenyewe. Kwa mwonekano ni kizuri. Ni cha gharama kubwa pia. Ni cha heshima. Ni cha kwendea mahali pa wenye hekima. Lakini bahati mbaya saizi ya kiatu hiki ni kubwa mno. 

Tendwa alionekana akivaa kiatu kile, lakini hakika alikuwa anachomeka tu miguu.  Alichomeka. Akavuta. Akavuta, mithili ya mtoto anayeanza kusimama na kutembea huku wazazi wakiimba “…kasimama dede.” Huyooo!

Sasa Tendwa hata kuvuta kiatu kile havuti. Amegundua hakikuwa chake. Matambara na karatasi za kupachika mbele, nyuma na upandeni ili kuimarisha mguu, ama yamekuwa ghali au tendo lenyewe limeleta usumbufu. 

Tendwa sasa anavaa ndala. Hizo ndizo saizi yake. Tatizo ni kwamba pale alipowekwa si mahali pa ndala bali kiatu; tena kiatu kutoka kwa rais.

Sitiari hii inafaa kuelezea jinsi Tendwa alivyoshindwa kufanya kazi yake. Jinsi anavyopwaya katika nafasi hii na jinsi anavyoacha kilichochake na kufanya kisichochake.

Kwa nafasi aliyonayo Tendwa, akionekana anashabikia na hata kufikia hatua ya kutetea walioua; na kuonyesha kuwa hata raia katika nchi nyingine huwa wanauawa na polisi, basi anakuwa ameonyesha mchoko wa aina yake.

Mara chache wateule wa aina yake hujiingiza katika mijadala ya aina hii ambayo inaweza kuchukuliwa kuwa ndio msimamo wa waliowateua. 

Tendwa anafanya yote haya kuhalalisha ubabe wa chama chake. Kila mahali ambapo polisi wanaua, na kama kulikuwa na shughuli ya kisiasa, basi Tendwa atasikika akisema “Nitafuta chama.”

Mara zote ametishia kufuta chama cha siasa. Chama anachotishia kufuta siku zote ni chama cha upinzani. Hawezi kusema lolote kwa CCM. Hawezi kuuma kidole kinachomlisha! Tendwa huyo! 

Haina maana kupendekeza Tendwa afukuzwe kazi. Hatafukuzwa. Haina maana kumwambia ajiuzulu. Hatajiuzulu.

Haina maana kumwambia Tendwa aombe radhi kwa wananchi. Hataomba maana huenda asielewe vilevile kile alichofanya anachostahili kuombea radhi. 

Kitu kimoja ni wazi. Marais wetu watakumbukwa, pamoja na mambo mengine, kwa kuweka watu wasio na uwezo madarakani na wakadumu humo kwa kupakatwa hata walipothibitika kupwaya, kunyauka na kupauka.

Kwani kwa kauli ya Tendwa, na kwa serikali inayojali na kuthamini haki na utu wa watu wake, jamaa huyu angevalia ndala zake nje ya ofisi ya umma.

(Makala hii ilichapishwa katika gazeti la TanzaniaDaima Jumapili tarehe 9 Septemba 2012)