Header Ads

LightBlog

TCRA YAAMKA NA KUTUNISHA MSULI

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
MAMLAKA YA MAWASILIANO TANZANIA

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


KUTOA TAARIFA ZA SIRI KATIKA MAWASILIANO YA ELEKTRONIKI NI KOSA LA JINAI
Hivi karibuni Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imegundua kuzuka kwa tabia ya uvunjaji wa kanuni ya utunzaji wa siri za mawasiliano binafsi ya watumiaji wa huduma za mawasiliano ya simu za mkononi. Mawasiliano hayo yamefikia hatua ya kuchapishwa katika vyombo vya habari.

Mamlaka ya Mawasiliano inapenda kuchukua fursa hii kuwakumbusha wenye makampuni ya Simu na wananchi kwa ujumla kuwa, kutoa taarifa za mawasiliano binafsi ya simu bainA ya watumiaji wa huduma hiyo, ni uvunjaji wa Sheria ya Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta Na. 3 ya mwaka 2010 na Kanuni za Mawasiliano (Kulinda Wateja) za mwaka 2005.

Kifungu cha 98 ya Sheria ya Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta kinasema;

(1) “Mtu yeyote ambaye ni mfanyakazi wa kampuni yenye leseni ya kutoa huduma za mawasiliano, au mwakilishi wake, ana wajibu wa kutunza siri za mawasiliano binafsi na taarifa zozote za siri za wateja kwa mujibu wa sheria hii”

(2) “Mtu yeyote haruhusiwi kutoa taarifa binafsi za mteja yeyote alizopokea au kusikia kwa mujibu wa sheria hii isipokuwa tu mtu huyo ameruhusiwa kwa mujibu wa sheria”

Kifungu cha 123 (1) kinasema:-

Mtu yeyote ambae bila sababu za msingi atasababisha kuingilia au kuzuia kupokewa kwa mawasiliano yeyote ya kielektroniki anafanya kosa and akipatikana na makosa atatakiwa kulipa faini ya shilingi za kitanzania zisizopungua milioni tano au kwenda jela kwa muda wa usiopungua miaka miwili au adhabu zote kwa pamoja”

Kanuni ya 12 ya Kanuni za Mawasiliano za mwaka 2005 za Tanzania (Kulinda Wateja) inasema:-

“Mtoa huduma za Mawasiliano haruhusiwa kuingilia kati, kusikiliza au kutoa taarifa zozote za mazungumzo ya mteja yeyote yaliyopitia kwenye mtandao wa mtoa huduma, isipokuwa kwa ruhusa kulingana na mahitaji maalumu kwa mujibu wa sheria zilizopo”

Kutolewa kwa taarifa za mawasiliano binafsi ya watumiaji wa simu za mkononi ni lazima kunafanywa na mtu mwenye ujuzi na uelewa wa jinsi ya kupata taarifa hizo na wenye ruhusa ya kufanya hivyo katika mtandao wa Kampuni husika ya kutoa huduma ya mawasiliano; ama peke yake au kwa kushirikiana na wenzake kwa kuingia kwenye mtandao kwa makusudi kwa lengo la kuingilia mawasiliano binafsi ya watu, ambayo ni uvunjaji na kinyume na matakwa ya kifungu cha 123 cha Sheria Na. 3 ya Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta.

Mamlaka ya Mawasiliano inayakumbusha Makampuni ya simu kuweka uzuizi na kuhakikisha siri za mazungumzo binafsi ya wateja zinahifadhiwa na hazitolewi kwa yeyote isipokuwa kwa mujibu wa sheria na; kuhakikisha yanafanya uchunguzi kugundua walioiningilia mazungumzo binafsi ya wateja.

Wananchi wanapewa tahadhari kuhusu kutafuta au kutaka kupata taarifa za mawasiliano ya siri kutoka kwa watoa huduma na kuzitumia taarifa hizo binafsi za mawasiliano pasipo kufuata utaratibu ulioruhusiwa kisheria.

Kwa taarifa ambazo zimechapishwa kwenye vyombo mbalimbali vya habari hivi karibuni, Mamlaka ya Mawasiliano inafanya uchunguzi wa uvunjwaji huo wa sheria kwa kutoa taarifa binafsi za wateja kinyume na sheria. Baada ya kuwabaini wahusika, Mamlaka itachukua hatua za sheria kwa yeyote atakayebainika kuvunja sheria hiyo.



Imetolewa na

Mkurugenzi Mkuu
Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA)
22 Desemba 2010

No comments

Powered by Blogger.