SITAKI
Waliozoea kubana upinzani nao wabanwa
Na Ndimara Tegambwage
SITAKI kuwa mtovu wa shukrani kwa waliosoma makala yangu ya wiki iliyopita juu ya ahadi za mgombea urais Jakaya Kikwete alizotoa mkoani Kagera na ambao wamenipelekea maoni; hasa wakazi wa Bukoba, Ukerewe na Kigoma.
Ni kilio kitupu. Tuanze na aliyesahihisha tukio la kihistoria. Huyu alisema meli ya mv Viktoria iliingia ziwani Viktoria mwaka 1963 (siyo 1965) baada ya kukata maji kwa “kipindi kirefu” katika mto Thames nchini Uingereza. Namshukuru.
Mwingine akasema nilionekana kuonyesha kuwa mv Viktoria bado inafanya kazi. Ameniuliza, “Watu wangapi wanapanda meli yako hiyo? Siku hizi watu hawana imani nalo. Wanapanda mabasi. Kutoka Bukoba saa 12 asubuhi unakuwa Mwanza kabla ya saa sita mchana siku hiyohiyo. Nani atapanda mzoga. Limebaki kubeba mikungu ya ndizi.”
Huyo naye amejitambulisha kuwa anatoka Bukoba. Sasa huyu mwingine anatoka Ukerewe. Anasema mv Serengeti iliyokuwa ikienda kisiwani humo imeegeshwa gatini. Hawana huduma.
Amesema “ka-meli kengine kanakoitwa Butiana, miezi mine au mitano iliyopita, kalizimikia ziwani” ambako walikwama na hatimaye kukokotwa saa sita baadaye. Hakuna usafiri.
Nacho kivuko cha Clarias, ambacho kina umri mkubwa kuliko mbao zilizokiunda, kimeanza kuwa na mwendo usioweza kukifanya kishinde iwapo kitashindanishwa na kinyonga. Ukerewe wanalia. Si leo. Si jana. Si juzi. Kilio cha miaka mingi kama kile cha Bukoba.
Mwingine huyu hapa. Anatoka Bunazi. Anajadili mambo mawili; tena kwa ufupi. Kwanza, anasema mkuu wa wilaya amesema hawezi kushiriki kugawa eneo la ranchi ya Kakunyu ambalo mgombea urais wa Chama Cha Mapinduzi (rais) aliagiza likatwe na kugawiwa wananchi wenye uhaba wa ardhi, badala ya kuwafukuza.
Anasema mkuu wa wilaya amesema kauli ya mgombea haitoshi. Kwamba kilichopatikana kwa karatasi (hati ya kisheria), sharti kuondolewe katika hadhi hiyo kwa karatasi pia. Shaka imejengeka hasa.
Pili, anasema mgombea aliahidi uwanja wa ndege wa kimataifa lakini wananchi wana shaka kubwa. Anasema, makao makuu ya nchi, Dodoma hayana uwanja wa ndege wa kimataifa; Mwanza mji wa pili kwa ukubwa nchini hauna uwanja wa kimataifa.
Anasema uwanja wa Songwe, Mbeya ambao “wanatwambia utakuwa wa kimataifa, haujakamilika. Tunajiuliza kuna kitu gani kikubwa Misenyi (Bunazi) ambacho kinaweza kufanya serikali ijenge haraka uwanja wa ndege wa kimataifa, kilometa 40 au 50 kutoka mjini Bukoba.”
Lakini mkazi wa Kigoma/Ujiji ndiye ametoa mpya. Anaandika, “…acha haya ya kununuliwa meli mpya Bk; sisi Kigoma amesema anataka iwe kama Dubai, wakati umeme tu ni mtihani huku tuna maporomoko ya mto Maragalasi.”
Ahadi hizi zote Bukoba na mkoani Kagera kwa jumla, ni kama ahadi nyingine zilizotolewa na zinazoendelea kutolewa na mgombea wa CCM na baadhi ya wagombea wengine wa urais na ubunge wa chama hicho na vyama vingine nchi nzima.
Kinacholeta tofauti kati ya mgombea wa CCM na wagombea wa avyama vingine, ni kwamba Kikwete hawezi kujitofautisha na urais. Mara nyingi pia, anaongea kwa mamlaka ya rais.
Kwa mfano, anapoagiza wananchi wakatiwe vipande vya ardhi kutoka kwenye ranchi, anaongea kwa kofia ya mwenye mamlaka juu ya ardhi, kwa mujibu wa sheria – rais – hata kama kauli yake itapingwa na kupinduliwa na wateule wake.
Lakini wingi wa ahadi, hasa zinazohusisha hata ujenzi wa viwanja vya ndege, Dubai ya Kigoma, meli, vivuko, bajaji kwa wajawazito (ahadi ya zamani); ahadi za kulipa mishahara ya wafanyakazi wa mgodi wa mkaa wa mawe Kiwira na kufufua mgodi huo, zinaonekana wazi kuwa zinatoka kwa kiwewe.
Ndiyo maana mmoja wa wasomaji ameandika, “Kikwete si anajua kuwa ni awamu ya mwisho. Hata akiahidi yasiyotekelezeka, alimradi anamalizia muda wake ikulu; atakayemrithi aweza kusema ‘siyo mimi niliyeahidi.’”
Kauli hii ya msomaji inaleta mazingira ambamo anayetoa ahadi na amri, atakuwa ameshinda. Haingalii upande mwingine. Bali hiyo siyo hoja ya msingi.
Hoja kuu ni kinachomsukuma Jakaya Kikwete kutoa ahadi nyingi na kwa wingi mara hii. Hiki kinaweza kupatikana katika kuchunguza mazingira ya kisiasa ya wakati tuliomo.
Kwa mara ya kwanza, tangu kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi, serikali imewambwa msalabani katika kampeni za uchaguzi mkuu wa rais na wabunge. Nayo imekiri.
Hoja za vyama vya upinzani zimelenga kuonyesha udhaifu katika sera na mipango ya serikali ya CCM. Zimeibua vitendo vya wizi na ufisadi chini ya serikali ya chama cha umri mkubwa. Zimeweka wazi uongo, uzemba na usanii wa viongozi.
Mara hii hoja siyo za maneno matupu. Zimesheheni takwimu na vielelezo juu ya kilichotendeka; alitenda nani, lini, wapi na katika mazingira yapi. Ni hivi: Hoja zimepangwa na kila hoja ina ushahidi mwanana ambao haupingiki. Ambao hauwezi kupuuzwa.
Rais mtaafu Benjamin William Mkapa, waziri mkuu mstaafu Frederick Sumaye na Rais Amani Abeid Karume, wamenukuliwa wakijadili mazingira ya sasa katika kampeni kuelekea uchaguzi mkuu.
Kwenye sherehe ya harusi ya mtoto wa Karume, mjini Zanzibar, kama miezi miwili iliyopita, viongozi hao walinukuliwa wakijadili “uimara” wa hoja za upinzani na umakini wa Dk. Willibrod Slaa.
Yalikuwa mazingira ya sherehe lakini mmoja wa viongozi hao alinukuliwa akisema kuwa chama chao kimezoea kutoa takwimu bila ufafanuzi; lakini safari hii kuna mahiri (Dk. Slaa) wa kutafsiri na kutoa takwimu nyingine zenye fafanuzi ambazo zitakuwa kisiki kwa mgombea wa CCM.
Kwa kauli hizo, alikuwa amepatikana wa kuvunja pingu za takwimu ambazo watawala walizoea kumwagwa mbele ya wananchi bila fafanuzi au walizitumia kujikweza.
Kwa mfano, kutaja wingi wa vyumba vya madarasa kama maendeleo wakati havina madawati, walimu, vitabu, chaki, maabara, maktaba na vifaa vingine.
Hizi ni takwimu zilizopeperushwa na watawala – ghiliba ya wazi kabisa – na kujikinga nyuma yake wakisubiri kupigiwa makofi na kupewa kura. Mifano ya takwimu hizi ni mingi.
Ni takwimu zinazokidhi mahitaji ya mitaji mikuu mitatu ya watawala walioko madarakani kwa miaka 50 sasa. Mitaji hiyo imekuwa ujinga, umasikini na woga.
Ujio wa mageuzi uliondoa woga mkubwa uliokuwa umetanda na kwa kiwango kikubwa kupandikiza ujasiri wa kuuliza maswali na kudai majibu.
Ujinga na umasikini viliendelea kushamirishwa na takwimu malaya zilizopewa tafsiri yoyote ile kukidhi mahitaji ya wakati uliopo.
Kuibuka kwa tafsiri ya takwimu basi, na kutolewa takwimu zinazokinzana na zile zilizokuwa zikighubika akili za wengi, kumekuwa njia muwafaka ya kuongea na umma na kuuondoa katika kiza nene.
Aidha, kuibuka kwa uchanganuzi mwanana kunafuatia pia kudhihirika kwa vitendo vya wizi mkubwa na ufisadi wa mabilioni ya shilingi unaodaiwa kufanywa na, au kwa baraka za watawala.
Mazingira haya ndiyo yanasaidia kujenga hoja nzito kuhusu mustakbali wa taifa – lakini siyo chini ya uongozi na utawala wa sasa unaotuhumniwa kutenda au kushiriki au kunyamazia yale ambayo yamekuza ujinga na kuongeza umasikini.
Hakika hoja za aina hiyo ni ngumu sana kukabili. Watawala wa sasa, wakiongozwa na anayegombea urais kwa chama kilichoko ikulu, hawana majibu. Hawana!
Wanachoweza kufanya ni kuambaa nchi nzima; wakitoa kila ahadi kwa kubakiza moja tu wasiloweza kuahidi – ufalme wa mbiguni. Basi.
Hilo ndilo chimbuko la ahadi nyingi za Kikwete. Zitakuwa zaidi ya tulizosikia. Hata hivyo, ahadi hazijibu hoja. Zitabaki ahadi na maelezo yake na wakati mwingine amri na maelekezo.
CCM itakiri, leo au kesho – na siyo suala la ushabiki bali uchambuzi sahihi – kuwa hoja za sasa za upinzani hazijibiki. Kama kuchaguliwa itakuwa ni kwa mazoea tu yaliyodumishwa na mitaji yake miwili iliyobakia: ujinga na umasikini.
Kwani kinachofanyika hivi sasa na ambacho hakijawahi kufanywa, ni kwamba CCM na serikali vimechukua upande ule ambako vimekuwa vikisukumiza wapinzani na wananchi – ule wa kujitetea; wa kujihami.
Kwa chama kilichoko ikulu kuwa katika nafasi ya kujikinga, kujihami na kujitetea wakati wote; kuna maana kuwa “yamewafika.” Kuwa mabadiliko yaja.
0713 614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com
Sunday, October 10, 2010
UJINGA ULIOPATA DIGRII, UPROFESA

SITAKI
Prof. Maghembe anavyokana siasa
Na Ndimara Tegambwage
SITAKI Profesa Jumanne Maghembe awe mfano wa jinsi usomi unavyoweza kuota kutu, kuwa butu na hata kuwa sumu.
Profesa huyu ndiye waziri wa elimu na mafunzo ya ufundi; mbunge anayejaribu kutetea kiti chake, lakini kiongozi ambaye wizara yake ina ndimi mbili juu ya haki ya wanafunzi kupiga kura mwaka huu.
Maelfu ya wanafunzi wa vyuo vikuu vya serikali walijiandikisha kupiga kura pale vyuoni kwao. Wizara ilijua hilo. Tume ya Uchaguzi ilijua na kupanga hivyo. Wanafunzi walijua watakuwa vyuoni. Serikali kwa jumla ilijua hilo.
Ghafla serikali ikasema muhula mpya wa masomo katika vyuo vyake utaanza mapema Novemba na siyo mwishoni mwa Oktoba – tofauti ya siku kumi tu.
Maana ya maamuzi hayo ni kwamba wanafunzi hawatakuwa kwenye maeneo walikojiandikisha kupiga kura. Hawatapiga kura. Hapa ndipo zimetokea kauli mbili za serikali zinazoleta utata.
Kauli ya kwanza ni kwamba maandalizi ya malipo kwa wanafunzi wanaoomba mikopo hayatakuwa yamekamilika mwishoni mwa Oktoba.
Kauli ya pili na iliyotolewa na waziri wiki iliyopita ni kwamba, vyuo vitafunguliwa mapema Novemba kwa sababu kumekuwa na mabadiliko katika mfumo wa udahili.
Waziri anataka kila mmoja amwamini, yeye na serikali yake, kuwa katika siku 10 (kumi tu), ambazo ni tofauti kati ya tarehe ya awali ya kufungua vyuo na tarehe mpya, maandalizi ya malipo yatakuwa tayari na tofauti ya muda wa udahili itakuwa imetoweka.
Hivi ni visingizio. Ni njia ya kuwapora wanafunzi fursa na haki yao ya kupiga kura, hasa wale ambao wazazi wao hawana uwezo wa kuwawezesha kwenda vyuoni mapema; au kuwa karibu na vyuo ili wapige kura na siku 10 baadaye waingie vyuoni.
Katika baadhi ya nchi duniani, kuna mifumo ya kuhakikisha raia wake waishio ughaibuni, wanashiriki zoezi la uchaguzi huko watokako. Serikali huhakikisha kila kura inakusanywa.
Walioko katika ofisi za kibalozi nje ya nchi, wafanyabiashara, wanafunzi na hata walioko katika majeshi, huwezeshwa kupiga kura makwao kutoka pale walipo.
Tanzania, hapahapa, humuhumu, maelfu ya kura yanaachwa hivihivi, njenje. Kuna tatizo. Siyo rahisi kufikiri kuwa siyo njama za kuzika utashi wa maelfu ya wanafunzi. Kwa kadri hali ilivyo, kuna uwezekano mdogo sana kwa serikali kubadili mwelekeo.
Hapa ndipo kuna mtihani wa nyongeza kwa wanafunzi vyuoni: Kufanya vyovyote iwavyo, kuwa maeneo walikojiandikisha – bila kusikiliza waziri wala tume – ili waweze kupiga kura.
Hatua hiyo, inayoweza kufanywa na wanafunzi wachache, wengi au wote, yaweza kuwa ushahidi wa kudumu wa kupigania haki na kichocheo kwa vijana wengi katika kuthamini na kupigania haki zao.
Ni hatua hii pia itakayoweza kumrudisha darasani Prof. Maghembe, mara hii akifundishwa na wanafunzi wa umri mdogo, juu ya haki ya raia ya kupiga kura kuchagua yule anayeona anafaa kumwongoza.
Kwani ni Maghembe aliyekaririwa wiki iliyopita akisema kuwa anawashangaa wanafunzi kuweka shinikizo la kuwa vyuoni mapema ili waweze kupiga kura.
Amenukuliwa pia akisema vyuo vya elimu ya juu siyo taasisi za kuendesha siasa bali ni “…maeneo yanayotumika kufundishia wataalamu wa kada mbalimbali.”
Tayari wanafunzi wamemjibu profesa. Wamemuuliza: Kama vyuo ni mahali pa kazi pekee ambayo waziri ametaja, kwa nini chuo kiliruhusu uandikishaji wanafunzi, tena hapo vyuoni?
Prof. Maghembe hawezi kupata jibu kwa swali hili kama ambavyo hawezi kupata majibu kwa maswali mengine kuhusiana nalo.
Kwa mfano, profesa anasema nini kuhusu siasa kuwa moja ya masomo muhimu na kwamba chuo kikuu ni eneo la kuoka wataalamu katika sayansi ya siasa? Na hilo linafanyika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Kama hajui hilo, basi kuna kila sababu ya kutilia mashaka nia, shabaha, uwezo wake wa uelewa na elimu yake, kwani kupiga kura siyo zoezi la ndimu mchangani.
Pamoja na kuoka na kuipua wataalamu katika sayansi ya siasa, elimu ya kiwango cha chuo kikuu inapaswa kuwa ufunguo wa akili katika nyanja mbalimbali za maisha, ikiwemo siasa.
Aidha, siyo lazima uwe katika idara au kitivo kinachohusiana na siasa ndipo ujue mazingira yako ya kisiasa na jinsi zinavyokuathiri – wewe na jamii yako.
Hii ni kwa kuwa kila eneo la jamii linahusika na kuathiriwa – vizuri au vibaya – na siasa za wakati uliopo. Ndivyo ilivyo pia katika vyuo vikuu.
Maamuzi yanayotumiwa na watendaji na kufanya nchi hii iendelee kuwa makazi ya watu wengi, woga, masikini na wajinga, ni ya kisiasa.
Taratibu na mazingira yanayosababisha watoto wamalize madarasa saba bila kujua kusoma na kuandika; yanayolea wizi mkuu na ufisadi usiomithilika; ama zimetokana au zimeathiriwa na maamuzi ya kisiasa ya wakati huu.
Mfumo wa maisha unaofanya waliohitimu chuo kikuu, hata maprofesa, wapauke haraka na wengine hatimaye kupoteza uwezo wa kufanya maamuzi na hata kusoma na kuandika; umeathiriwa kwa kiwango kikubwa na siasa za nyakati tulizomo.
Wahitimu vyuo vikuu, wanaokwenda kuwa walimu, wanasheria – mawakili na mahakimu – madaktari, mainjinia, mabwana na mabibi shamba na mifugo, wana-mipango na wengine, hawanabudi kujua mwelekezaji ni siasa.
Mfumo wa utawala wa wanafunzi vyuoni, unaoamuliwa kwa njia ya uchaguzi wa viongozi wao na kushirikisha kila mmoja bila kujali anasomea nini, ndilo rejeo la haraka kwamba wasomi vyuoni wanapaswa kuwa hai juu ya kinachotendeka katika jamii na hasa kinachogusa haki zao.
Kama Profesa Maghembe anafikia hatua ya kusema siasa haziwahusu walioko vyuo vikuu, ama amesahau, amepotoka au amepauka.
Siyo rahisi kuzungumzia elimu ya juu bila kugusa mustakbali wake kwa jamii, kupitia mipango iliyowekwa au kuathiriwa na siasa zilizopo.
Kwa hiyo, kudai kuwa vyuo siyo mahali pa siasa na kuweka vikwazo kwa wanafunzi ili wasifurahie haki yao ya kuchagua viongozi wanaotaka, ni kuendeleza ujuha ambao uliishafukuliwa na kutupwa nje ya vyuo na hata shule nyingi nchini.
Maghembe hasononeki kwa wanafunzi kushindwa kupiga kura. Serikali yake pia haisoneneki. Labda walishajua kuwa wanafunzi hawatapigia kura chama chao.
Lakini walijuaje? Hiyo si kama kufyatua risasi gizani ambako waweza kukuta unaumiza au unaua mkeo, baba au mwanao?
Zimebaki siku 21 kupiga kura katika uchaguzi mkuu. Wanafunzi wa vyuo vikuu bado wanasubiri serikali itende maajabu.
Hayapo. Hayaji aua hayaji haraka.
Kuna kazi moja ambayo wanafunzi wanaweza kufanya iwapo serikali haitabadili msimamo. Wabaki walipo. Wahimize wananchi kuamka mapema na kupiga kura. Wafanye uwakala kwa vyama vyao.
Kufanya hivi siyo kudhalilika. Njia hii ina faida mbili kuu. Kwanza, kuanzia hapo, wataelewa hila na husuda walizonazo watawala na kwamba haziondoki kamwe kwa sala kanisani wala msikitini.
Pili, watajifunza kuchukia na kuchukua hatua – mwanzo na mwisho wa lelemama – kwa njia ya kujiunga na wanaharakati kupigania haki zao na wote, ambao wakati wowote, waweza kunyang’anywa haki zao.
0713 614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com
(Imechapishwa katika Tanzania Daima Jumapili ya 10/10/2010)
Saturday, October 2, 2010
OMBAOMBA YA KIKWETE INANUFAISHA NANI?

Safari za nje na ombaomba ya JK
Na Ndimara Tegambwage
SITAKI kusikia Jakaya Kikwete akisema kuwa asigefanya safari zake nyingi nje ya nchi, basi wananchi wangekufa njaa.
Huyu rais aliyemaliza muda wake anataka kusema kuwa alikuwa anakwenda kuhemea; kuomba kishika-roho ili Watanzania wasife njaa.
Ndivyo alivyonukuliwa akisema kwenye mikutano ya hadhara ya kuomba kura katika majimbo mawili ya uchaguzi ya Urambo – Mashariki na Magharibi mkoani Tabora.
Wakati mgombea urais akisema hayo, Bolozi wa Ujerumani nchini, Guido Herz anawaambia waandishi wa habari jijini Dar es Salaam kuwa nchi yake inashangazwa na umasikini ulioko nchini, tena katikati ya “raslimali nyingi.”
Balozi anarudia yale ambayo yamesemwa kwa miaka nendarudi kuwa nchi hii, pamoja na raslimali nyingine, ina mito, maziwa, bahari, ardhi nzuri kwa kilimo na vivutio vya utalii.
Balozi anasema, “Kwa hakika siwezi kutaja sababu ya kuifanya Tanzania isipige hatua ya maendeleo,” bila shaka na kuondokana na umasikini wa kipato (ajira), chakula, elimu, mavazi, usafiri, maji, umeme na mahitaji mengine ya jamii.
Ni njaa ipi ya Watanzania anayosema Jakaya Kikwete ambayo imekuwa ikimpeleka nje ya nchi?
Hapa ndipo tunaweza kushona alichowahi kusema Mwalimu Julius Nyerere kuwa, ni upumbavu kufa kwa njaa wakati unaishi katika bonde lenye rutuba.
Katika mazingira haya, ni vigumu kumruhusu mgombea urais wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kutumia kampeni za uchaguzi mkuu kujidhalilisha, yeye na watawala waliomtangulia.
Hakika hapa Jakaya Kikwete anajianika, kwamba ameshindwa kazi; na kwa njia ya ushauri wa bure, asijaribu kurudia kauli ile mbele ya wakulima masikini anaowaomba kura. Watamnyima.
Wakulima wamejilisha kwa ndizi, muhogo, mahindi, viazi, mtama, uwele, ulezi, karanga, maharage na mazao mengine.
Wamejipatia matumizi kwa kuuza mazao yaliyotajwa hapo juu, pamoja na pamba, miwa, korosho, nazi, alizeti, karafuu na kahawa. Wafugaji wamelinda maisha yao kwa mifugo – mbuzi, kondoo na hasa ng’ombe.
Wananchi masikini wamevua samaki kutoka mito na maziwa ambayo husema kila siku kuwa wamejaliwa na Mwenyezi Mungu; wamekula na kuendelea na maisha.
Wengine wamefukua dhahabu, almasi, tanzanite na madini mengine “tuliyojaliwa na Mwenyezi Mungu” kwa kutumia vijiti, majembe na koleo – alimradi wamepata vipande vya kuuza, kupata fedha na kusogeza miaka mbele.
Pamoja na kilimo, ufugaji, uvuvi na uchokonoaji madini kwa njia za kale, wananchi wengi wamebaki masikini. Wanatumia nyenzo duni.
Wengi wana mashamba madogo. Maeneo madoyo ya kulima na kuchungia. Wanapata mazao kidogo. Wanakula kidogo. Wanauza kidogo. Wanabakia na kidogo. Wanajiviringisha katika udogo-udogo ambao ni umasikini usioisha.
Hili ni somo pana lisoloweza kuenea kwenye kipande hiki cha ukurasa. Bali ni somo linaloeleweka vema kwa wakulima, wafugaji, warinaasali na wakusanya matunda porini; wafanyakazi na wasio na kazi, kwa kuwa ndio wanaishi maisha hayo.
Ukichunguza utaona udogo unaojadiliwa unatokana na “ubongo mdogo wa watawala,” kwa maana tatu.
Kwanza, kukosa uwezo wa kufikiri. Pili, kukosa utashi katika kutumikia wananchi. Tatu, uroho wa kijuha – wizi, matumizi ya kutanua na ushirika na watu wa nje katika kuibia nchi.
Huwezi kusema unakwenda kuhemea nje ya nchi kwa ajili ya mtu ambaye umemnyang’anya ziwa ambalo limekuwa chanzo cha mapato yake (samaki na fedha) na kiungo cha uhai wake.
Wananchi wanalia – nyavu zao na mitumbwi vimechomwa moto; wamekamatwa, kupigwa viboko na kuchomewa nyumba ili mwekezaji ziwani apate usalama wa kukomba “samaki wa mungu.”
Hilo bakuli la ombaomba wa kitaifa, limemletea nini huyu aliyeachwa utupu na ambaye watawala hawataki kusikiliza kilio chake?
Haiingii akilini kudai unakwenda kuhemea nje ya nchi kwa ajili ya mfugaji wa Kilosa ambaye watawala wamenyang’anya ng’ombe 600 au 1,000 na hata 2,000. Kuna nini lake ndani ya pochi ya mhemeaji aliyeacha amemfukarisha?
Hakuna mtawala awezaye kwenda kuhemea kwa ajili ya wafugaji ambao ng’ombe wao wameswagwa na kupotea porini, nyumba zao kuchomwa moto na wao kuamriwa, kwa mtutu wa bunduki, kuhamia wasikojua – kwa kauli za “rudi kwenu.”
Anayekwenda kuhemea atawakuta wapi watu hawa ili awape alichopata? Kama siyo mzaha basi ni ukatili usiomithilika.
Chukua wachimbaji wadogo – wale wa vijiti, majembe na koleo. Wameswagwa kutoka walikoishi uhai wao wote. Wametengwa na chanzo cha “uchumi” na maisha yao. Sasa ni jinai kukutwa na madini “waliyopewa na Mwenyezi Mungu.”
Nani ataamini kuwa hata makombo kutoka kapu la mhemeaji Jakaya Kikwete, yataweza kuwafikia watu hawa, licha ya madai kuwa anakwenda nje kuhemea ili wasife njaa? Yatawakuta wapi?
Nenda Rukwa, Ruvuma, Mbeya na Iringa – mikoa inayozalisha mahindi kwa wingi mpaka ikaitwa “Wababe Wanne.” Mazao wanayo. Hayana soko la ndani. Wanazuiwa kuuza kokote wanakotaka.
Ndivyo ilivyo kwa wakulima wa kahawa Kagera na wakulima wa karafuu Unguja na Pemba. Bado kuna ukiritimba ambao hauendani na siasa za watawala za soko huria.
Hakuna mwenye haki wala wajibu wa kuhemea kwa niaba ya wakulima hawa. Wana uwezo wa kijilisha; bali serikali imekuwa ikiwanyang’anya uwezo huo ili iweze kuwatawala kwa urahisi.
Serikali imekataa kufanya hata jambo dogo na kununua nafaka kutoka kwa wakulima, kwa bei nzuri kwa ajili ya kutunisha mfuko wa akiba (GSR). Kwa njia hii yaweza kuchochea mashindano katika kilimo na hivyo wananchi kulima zaidi na chakula kuwa kingi.
Serikali ikishindwa kujenga mazingira ya kutumia mabonde, ardhi yenye rutuba, mito, maziwa, bahari, madini, misitu na mbuga za wanyama; badala yake ikadai rais wake anakwenda kuomba chakula nje ya nchi, ijue imeshindwa kazi.
Hakuna awezaye kuelewa mantiki ya kuwa ombaomba katikati ya utajiri wa aina hii wa raslimali; wala hakuna atakayehusudu ombaomba katika mazingira ambamo watawala wenyewe ndio, ama chanzo au kichocheo cha njaa na umasikini.
Kwa nini basi tusikubaliane kuwa, watawala wetu wanakwenda nje ya nchi kutafuta utumwa; kwani hawataki kuishi kwa uhuru unaotokana na rasliamli lukuki zinazopaswa kuendelezwa kwa manufaa ya watu, ndani na nje ya nchi yao.
0713 614872
ndimara@yahoo.com