Thursday, September 23, 2010

MARUHANI WALINDA IKULU DAR




SITAKI

Kikwete anayelindwa na mashetani

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI kusikia na kuamini kuwa vyombo vya ulinzi nchini vimeshindwa kazi – Polisi, Jeshi la Wananchi (JWTZ) na Usalama wa Taifa.

Sitaki kuamini kuwa tayari walinzi wanakaa tu; lakini wanalipwa mishahara na marupurupu mengine – wanatumbukiza mifukoni na matumboni – bila kufanya kazi yoyote ya kumlinda “Rais wa Jamhuri ya Muungano.”

Sitaki kuamini kuwa nadharia za kisasa za ulinzi, silaha za kisasa na uvumbuzi unaoendelea katika medani ya ulinzi, vinaweza kutupwa chini na badala yake akatafutwa mtu, watu au vikundi vya kumlinda rais.

Sitaki kukubali wawepo watu binafsi, vikundi na makampuni ya ulinzi; tena ya kumlinda rais – na huenda na wananchi na mali zao – ambavyo havitambuliki kikatiba.

Sitaki kuamini kuwa walinzi – waliosomea kazi hiyo na hata waliopendelewa kuwa katika nafasi hiyo muhimu – wanaweza kukubali “kuwekeana mikataba” na watu binafsi, makampuni na mataifa ili kulinda nchi yao.

Sitaki kuamini pia kuwa walinzi – wataalam wa zana na wenye maarifa makuu – wanaweza kujisalimisha kwa Sheikh Yahya Hussein ambaye anaona ulinzi wa rais na ikulu sharti uwe mikononi mwake.

Sitaki kuamini kuwa rais wa Jamhuri ana taarifa kuwa walinzi wake hawatoshi kumlinda; hawawezi kumlinda na kwamba zana zao na maarifa yao vimeshindwa kumwekea usalama unaostahili.

Sitaki kuamini kuwa rais anaamini kuwa hana ulinzi wa kutosha; kwamba majeshi yake yamechoka na kuchakaa na sasa sharti atake, apewe au atafutiwe ulinzi wa nyongeza nje ya silaha na maarifa yanayotambuliwa kitaifa na kikatiba.

Sitaki kuambiwa kuwa rais anaweza kukubali kulindwa na vyombo vingine nje ya vile tunavyofahamu kitaifa na kikatiba. Atakuwa amedharau nchi yake, watu wake, majeshi yake na katiba ya nchi yake.

Lakini mnajimu Sheikh Yahya Hussein anasema, bila woga wala aibu kuwa “sasa atamlinda Rais Jakaya Mrisho Kikwete” kwa ulinzi maalum ambao hauonekani.

Mnajimu huyo wa Magomeni, Dar es Salaam, alisambaza waraka katikati ya wiki hii akielezea jinsi Rais Kikwete alivyoandamwa na wabaya na kwamba kuishiwa nguvu uwanjani Jangwani tarehe 21 mwezi uliopita, kulitokana na uchawi.

Haijafahamika iwapo Sheikh Yahya ndiye alitangua uchawi uliomwangusha Kikwete; ulikuwa uchawi wa kiwango gani; uliolenga nini na uliotoka kwa nani.

Kwa kauli ya mnajimu, haikufahamika “amemwokoa” mara ngapi, amemkinga mara ngapi na anaaminika kwa kiwango gani kwa mkuu wa nchi.

Mwaka jana alipotabiri kuwa atakayejitokeza kushindana na Kikwete, ndani ya chama chake, atakufa kifo cha ghafla, ndipo wengi walianza kumhusisha Yahya na wapangaji wa ofisi kuu ya nchi.

Kwa nia njema na labda kwa kutambua kazi yake nzuri, msemaji wa ikulu alipoulizwa juu ya kauli ya Yahya, alisema kuna haja ya “kuheshimu kauli” ya kila mmoja. Lakini Jakaya Kikwete hakusikika akisema lolote.

Haikufahamika iwapo kwa “kuheshimu kauli” msemaji wa ikulu alikuwa na maana ya kila mmoja kuwa na haki ya kutoa kauli au alikuwa anasisitiza umuhimu wa kutambua na kuzingatia utabiri wa Sheikh Yahya.

Wakati huo, Sheikh Yahya hakusema iwapo amemwekea kinga Rais Kikwete. Hakusema kifo cha ghafla kitaletwa na nani na nini – nyota, mwezi, mizimu katika mzunguko wa kinga-nikukinge au ua-nikuue.

Bali vyovyote iwavyo, kuibuka tena kwa mnajimu zikiwa zimebakia siku 51 kufanya uchaguzi mkuu, kumechukuliwa na wengi kuwa njia ya kuimarisha utabiri wake; kuongeza nguvu za “kinga” yake na hata kuonyesha “mteja wake” kuwa hajamtupa mkono; pamoja na yote yanayojitokeza.

Hii ni mara ya kwanza kwa Sheikh Yahya kusema analinda rais aliye ikulu. Uhusiano huu kati ya mtu binafsi na ofisi kuu hauwezi kuwa umejitokeza ghafla.

Yawezekana pia uhusiano huu umekuwepo kati ya mganga huyu mwenye “ulinzi” (unaozidi ule wa maaskari na mashushushu) na marais waliotangulia; bali hapa hatuna uwezo wa kuwasemea.

Swali la haraka ambalo kila mmoja anaweza kujiuliza ni: Mlinzi huyu wa majeshi yasiyoonekana, analipwa posho au mshahara? Analipwa kiasi gani?

Nani anamlipa mlinzi huyu? Fedha hizo zinatoka kwenye kodi za wananchi au yule ambaye anajisikia amelindwa na kufanikisha matakwa na malengo yake?

Nikiwa bungeni pale Dodoma, mwaka 1997, mbunge mmoja wa CCM aliyekuwa akifurahia hoja zangu, alinitambulisha kwa wageni kutoka jimboni mwake ambao ambao pia walitambulishwa kwa wawakilishi bungeni.

Alitambulisha wageni saba; wakiwa wanawake watatu na wanaume wanne. Alinieleza kuwa aliyemtambulisha mwishoni “ndiye mtu wangu muhimu” – mganga/mlinzi.

Uganga na kinga ndani ya nyumba za watu binafsi. Uganga ndani ya ofisi za serikali. Uganga ndani ya bunge. Uganga ndani ya ikulu – kwa kuombwa au kwa kujipendekeza. Uganga!

Nimekumbuka ikulu ya Banjul, Gambia ambako tuliambiwa mapema mwaka jana kuwa Rais Sheikh Profesa Alhaj Dk. Yahya Abdul-Aziz Jemus Junkung Jammeh, naye ni mganga wa aina yake; pamoja na “kutibu ukimwi.”

Katikati ya ulofa huu unaoitwa kinga, watoto wa kike wa hata umri wa miaka 12, wanabakwa na wazungu – katika mahoteli na mabaa yaliyotapakaa mjini Banjul; kufanywa wajawazito na kutupwa mitaani wakilia na kusaga meno. Umasikini wa kutaga mayai!

Imani za “kukinga” zimedumaza akili; zimekwamisha uwezo wa kufikiri; zimezamisha matumaini ya wengi huku zikifanya watawala washughulikie kitu kimoja tu: kujikinga.

Bila shaka hapa Sheikh Yahya alikuwa anajitangaza ili wagombea nafasi mbalimbali wapate kumkumbuka na kumwendea, hasa wakizingatia kuwa ndiye mtoa kinga kwa rais badala ya vyombo vya dola.

Wale askari wasioonekana; zile silaha zisizoonekana; ule utaalam usiosomewa vyuoni wala kufundishwa majumbani; ni mashetani ambao mnajimu anataka yamlinde Kikwete.

Tunasubiri mgombea urais wa CCM kukubali kwa faragha au hadharani kupata ulinzi huo; jambo ambalo litakuwa na maana moja tu: kwamba amefukuza kazi majeshi yote nchini na kuajiri mashetani.

Haitakuwa ajabu kuona hata walinzi wake kwenye msafara wake wa sasa wakiondolewa na yeye kubaki na wapiga debe wa umoja wa vijana wa chama chake. Tunasubiri.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com

SHERIA YA MABWEGE HII HAPA




SITAKI

Na Ndimara Tegambwage

Lugha ya Tume ya Uchaguzi Haieleweki

SITAKI uamuzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) wa kulazimisha matumizi ya Kiswahili peke yake katika kampeni za uchaguzi mkuu.

Nakumbuka ilikuwa hivyo mwaka 1995 wakati nagombea ubunge jimbo la Muleba Kaskazini. Bado ni hivyo hata leo. Safari hii matumizi ya lugha yamekuwa moja ya masharti ambayo vyama vimelazimishwa kusaini.

Kiswahili ni lugha ya taifa. Ni lugha kuu inayotumiwa na wengi ndani ya soko la ajira – serikali na makampuni yake, shuleni na baadhi ya vyuo; katika biashara za kati, ndogo na katika mawasiliano ya kawaida.

Kiswahili kimeenea mijini – miji mikubwa na midogo na katika baadhi ya vijiji ambako kimetumiwa kwa muda mrefu au wakazi wake wamekuwa na mwingiliano mkubwa na wale wanaozungumza lugha hii.

Kwingineko Kiswahili kimeenezwa na shule za msingi na sekondari ambako walimu na wanafunzi wameathiri matumizi ya lugha za asili, bila kusahau juhudi za makusudi za kupambana na ujinga kwa njia ya Elimu ya Watu Wazima (Kisomo Chenye Manufaa).

Kampeni za kisiasa nazo zimekuwa na mchango mkubwa kwa uenezi wa lugha hii, zikiongezea kwa mipango ya awali, mara baada ya uhuru, ya kusambaza vipeperushi na filamu juu ya matakwa na mbinu za “maendeleo” katika Kiswahili.

Pamoja na yote hayo, bado nchini Tanzania kuna maeneo ambako kuta za lugha za asili zingali imara; na hasa imara sana.

Ni lugha hizi za asili ambazo zimeendelea kuwa chimbuko la misamiati na istilahi mbalimbali kwa matumizi ya sasa ya kukuza Kiswahili na hata kueleza maana halisi ya kile wanachosema wale wanaotumia lugha yao.

Siyo bahati mbaya basi kwamba Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kuna idara inayoshughulikia lugha za asili. Watafiti katika eneo hili hawafanyi kazi ya “kuzienzi” lugha hizi za asili – iwapo tutaazima vineno vya kisiasa – bali wanavuna maarifa ndani ya lugha hizo na kupitia lugha hizo.

Kuwepo kwa lugha hizo kunakoweza kusaidia kuelewa jamii na utamaduni wake – kwa kudhamiria au kwa utuki tu – kumekuza na kunawirisha Kiswahili na hata lugha nyingine za asili.

Hii ndiyo maana kumekuwa na wanaharakati wa ngeli na ngeli wakitetea kuendelea kuwepo lugha za asili zilizohifadhi hekima na falsafa za jamii ambako zinatumika.

Aidha, ni lugha hizi ambazo watafiti wanaoumba kamusi za Kiswahili na hata lugha nyingine zinazotumika katika maeneo haya, wanakimbilia kupata maneno halisi – hasa istilahi katika ufundi na teknolojia ya kale na sasa.

Hizi basi siyo lugha za kuua hivihivi tu kisiasa. Bado zina nafasi muhimu katika jamii kama vile walivyo watu wanaozitumia; na wanaendelea kuwa Watanzania hata kama hawawezi kuongea Kiswahili.

Sasa Tume ya Uchaguzi inasema wanasiasa wanaotafuta kura katika uchaguzi mkuu wasitumie lugha nyingine yoyote ile isipokuwa Kiswahili.

Maagizo ya tume yanafanana na kanuni za Wizara ya Habari zinazolazimisha kila chombo cha habari kilichosajiliwa nchini, kutumia ama Kiswahili au Kiingereza – lugha mbili peke yake.

Ukichanganya haya ya maeneo mawili, utaona kuwa wasiojua Kiswahili hawapaswi kujua kinachotangazwa redioni au kinachoandikwa kwenye magazeti.

Ni hivi: Kama hawajui lugha hizo – Kiingereza na, au Kiswahili – basi potelea mbali. Ndiyo tafsiri ya kile ambacho Tume inasema na ambacho serikali inasisitiza. Ndivyo wenye vyama walivyoweka saini kutetea.

Anayeomba kura, aingie Usukumani. Maeneo ambako Kiswahili hakitumiki kwa kiwango kikubwa. Pale ambako maneno ya Kiswahili yanatumika kwa ushabiki tu – ama kueleza kuwa anayeyajua ni “mkora” au “mwerevu” kutoka mjini.

Hapa, Tume inataka anayeomba kura atumie Kiswahili. Atatumia. Baada ya hotuba kuna kipindi cha maswali. Hakuna anayeuliza kwa kuwa hakuna aliyeelewa. Kuna haja gani basi ya kufanya kampeni katika “lugha ya kigeni?”

Nendeni Loliondo vijijini, katika mkoa wa Arusha. Kuna shule za msingi. Wanafunzi na walimu wana akili nzuri. Wanajua kuwa Kiswahili na Kiingereza, zote ni lugha za ngeni.

Baadhi ya walimu wanafundisha kwanza kwa Kimasai na baadaye kuweka katika Kiswahili. Njia bora kabisa. Ni kwa misingi sahihi kwamba lugha ya kufundishia iwe ile ambayo mwalimu na mwanafunzi wanaelewa. Mara hii ni Kimasai.

Wazazi katika eneo hili ambao ndio wapigakura, wanajua vema lugha yao moja – Kimasai. Wanaokwenda magulioni mara kwa mara ndio wameokoteza istitahi za kibiashara katika Kiswahili.

Sasa aende mwanasiasa anayetafuta kura. Amwage hapa kampeni yake kwa Kiswahili. Ataondoka kama alivyokwenda. Mtupu. Bila kura hata moja. Kwa nini? Kwa kuwa hawakumwelewa; lakini pia kwa kuwa naye ni mpumbavu – anatumia lugha ambayo anajua vema kuwa anaowaambia hawaijui.

Hili lina tafsiri moja kuu. Kwamba kwa miaka 50 ya utawala wa chama kimoja, watawala wamekuwa wakiimba na kijipiga vifua kuwa wana “lugha ya taifa – Kiswahili.”

Kumbe yamekuwa majigambo yasiyo na mashiko. Wameshindwa kueneza lugha hiyo hapa nchini kama walivyoshindwa kutumia wataalam wake kuigeuza kuwa “bidhaa” ya kuingiza fedha za kigeni.

Wameshindwa kukuza Kiswahili; wameshindwa kukuza lugha za asili; wameshindwa kutoa ajira kwa wanaojua lugha hizo ili wawe wakalimani kwa wasiojua lugha za kigeni; wamebakia na amri – “Tumia Kiswahili!”

Kwa amri na mantiki ya Tume, wasiojua Kiswahili “shauri yao.” Hii siyo haki.

Wananchi wanaojua lugha zao wanastahili kupelekewa kampeni katika lugha zao; na kama njia ya kueneza lugha kuu, wapiga kampeni waombwe kudondosha maneno ya Kiswahili hapa na pale kama kupanda mbegu.

Vinginevyo itafikiriwa kuwa serikali, na vyombo vyake, imeamua kuwatenga, kuwatelekeza, kuwasahau na kuwanyima haki ya kushiriki siasa za nchi yao, wale wote ambao hawajui Kiswahili au Kiingereza.

Sheria, kanuni na taratibu zinazoondoa haki ya mtu; kupoteza utashi wake, tena ndani ya nchi yake, hazistahili kuheshimiwa na haitakuwa mara ya kwanza kukataa kuzishemu.

Njia bora ya kuzipinga ni kuongea na wananchi katika lugha yao. Wananchi ndio watakuwa watetezi.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com

UNYANYASAJI WANAWAKE WAENDELEA

SITAKI
Makongoro anavyonyanyasa shemeji yake

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI Makongoro Nyerere aanzishe mgogoro kati yake na Leticia Nyerere, mke wa zamani wa ndugu yake, Madaraka Nyerere.
Vyombo vya habari vimemnukuu Makongoro akisema, kwenye mkutano wa hadhara jimboni Kwimba, kwamba Leticia asijaribu kujihusisha na ukoo wa Nyerere kwa kuwa tayari aliishachika.

Siyo rahisi kujua iwapo Makongoro ameagizwa na Madaraka kusema aliyoyasema; kwani hakusema hivyo. Haijafahamika iwapo kulikuwa na kikao cha ukoo kuamua juu ya matumizi ya jina la Nyerere.

Lakini muhimu zaidi ni kwamba, haijafahamika kuwa kila anayejitambulisha kuwa wa ukoo wa Nyerere anapendwa zaidi, anaaminika na kupewa kura.
Hapa kuna upogo katika jamii ambao umefanya wanawake watupilie mbali majina ya wazazi wao na badala yake kujibandika majina ya waume zao.

Ni upogo uliogeuka mtindo, hasa mume anapokuwa mtu wa kujiweza na mke anapenda kuitwa Mrs. Fulani – mwenye mali, nyumba nzuri, magari na fedha zisizokauka mfukoni.
Bali ni kupoteza utambulisho. Kipi bora, kujitambulisha kama mtoto wa Fulani au mke wa Fulani? Tukiwa sekondari kulikuwa na mwanafunzi mmoja aliyeitwa Festo Kokugonza. Mwendelezo mwingine huo.

Kwamba siyo lazima kuwa na ubini wa baba. Waweza pia kuwa na ubini wa mama na maisha yakasonga mbele bila kelele wala mikwaruzo.

Lakini hebu turudi kwa Leticia Nyerere. Je, haijulikani kweli kwamba alikuwa ameolewa katika ukoo wa Nyerere? Si taarifa hizi ziko wazi kwa kila mmoja kujua, hasa wakati huu wa kutafuta ufalme wa kisiasa?

Je, ni lazima kufuta jina la mume pale mwanamke anapomwacha mume au anapoachika? Je, kuendelea kulitumia kuna maana kwamba unataka kurudi au hutaki kuharibu utambulisho uliokuwa tayari umejengeka?

Je, kuendelea kulitumia jina hilo kwa utambulisho tu kuna maana kuwa unalithamini sana au sasa ni lebo maalum ambayo kuibadili kunaweza kukugharimu?

Je, kujigamba tu kwamba mtu anatoka katika ukoo fulani kunaweza kuleta manufaa yoyote wakati anaowaambia wanajua kuwa sivyo ilivyo?

Je, hata kama mtu atajidai na kujinadi kuwa ni wa ukoo fulani, ukoo huo una kitu gani cha ajabu na cha manufaa kwa jamii kiasi kwamba kujitambulisha nao tu wewe utakuwa umenufaika?

Nyerere alionyesha mfano mmoja mkubwa ambao mabwege wengi huutumia kumlaumu. Alijua watoto wake ni watoto kama watoto wa watu wengine.

Hakuwapendelea kwa kuwapeleka shule zenye majina makuu au kuwapeleka Ulaya na kuwaficha huko na ujinga wao, ili warejee hapa kwa mbwembwe wakati hawana akili; kama viongozi wengine wanavyofanya.

Kama kuna lolote katika ukoo wa Nyerere ni kwamba ulimzaa Julius Kambarage Nyerere; aliyetokea kuwa jasiri, mwenye uwezo wa kiakili na aliyeongoza harakati za kuleta uhuru wa Tanganyika.

Kama kuna lolote katika ukoo huu ni kwamba, hatuhitaji kutafuta zaidi, bali kwa ufupi tu, ulitoa Nyerere kama tulivyomwona, tulivyomfahamu na tulivyomwelewa. Basi.
Waliobaki – mke wake, watoto wake na wengine katika ukoo – sharti wajisimamie na hawawezi kwenda kwa sifa ya ukoo wa Nyerere.

Jamii itawaona na kuwaelewa kama mtu mmojammoja, mwenye sifa yake binafsi, udhaifu wake binafsi, ubora wake binafsi; kwani hakuna kitu maalum kinachoweza kuitwa alama ya ukoo wa Nyerere.

Hii ndio maana, pale Butiama na katika ukoo, hakuna kinachomwakilisha Nyerere kama Nyerere – akili yake, uwezo wake, siasa zake, visheni yake, utashi wake na mengine mengi.

Alichokumbuka Makongoro – ng’ombe 30 – ambao baba yake alitoa ili Madaraka amwoe Leticia, ni historia isiyofutika na ambayo inamwingiza mama huyo katika familia mpya, ukoo mpya hata usingekuwa wa Nyerere.

Isipokuwa siyo siri, kwamba akili na uwezo wa Nyerere havikuwa mali ya ukoo; vilikuwa mali yake binafsi, lakini kwa uchambuzi mpana – hazina ya taifa.
Bahati mbaya hakuvirithisha kwa yeyote – awe mke wake, watoto au ukoo wake. Ukitaka waweza kusema hivi; kwamba wanaovitambua, kuviheshimu na kuvienzi, ni watu wengine, wakiwemo wa mataifa na wala siyo hata chama chake alichoanzisha – CCM.

Kuna mamia kwa maelfu ya watu ambao wanaweza kumtetea Nyerere; kutaka asichafuliwe kwa hoja kubwa na nzito kwa kuangalia aliyoyafanya kuliko kung’ang’ania ukoo.

Vyovyote itakavyokuwa, kwa kuwa Leticia ameingia ulingoni, ataulizwa anatoka wapi; hilo jina la Nyerere alilipataje; huyo Nyerere ni yupi na yuko wapi? Atajieleza.

Watakaopenda kumshangilia kuwa aliishaonja maisha katika moja ya nyumba ya watoto wa Julius Nyerere, acha waseme. Watakaosema “unyerere” wake hauna uzito, acha wapuuze.
Bali kwa Makongoro kufunga safari kutoka Musoma hadi Kwimba kumwambia shemeji yake asijitambulishe na ukoo wa Nyerere, hakika ni njia nyingine ya udhalilishaji.

Julius Kambarage Nyerere hakuwahi kuwa, na siyo mali ya ukoo. Inawezekana Leticia anamtaja leo baada ya kuingia katika siasa, kama wengine wanavyomtaja.

Huwezi kukaa na Nyerere, kwa mfano, akichimba mtaro wa mabomba ya maji wa Ntomoko; akijenga nyumba za wanakijiji Kibondo kwa wiki mbili; halafu ukamsahau, wakati una rais anayewekewa mkeka na kuvalishwa glovu mikononi ndipo apande mti.

Huwezi kusoma vitabu na maandishi mengine ya Nyerere; ukaelewa fikra zake halafu ukashindwa kumuunga mkono au kumpinga na hata kumsema mara kwa mara kufuatana na jinsi ulivyomwelewa; hasa unapokuwa na rais asiye na hoja za kutoa changamoto kwa ubongo.

Huwezi kuwa na Nyerere anayeanzisha chama cha siasa na baadaye kusema kinanuka rushwa na kutishia kukikimbia akisema “siyo baba, siyo mama;” wakati una utawala ambao unachefua kwa rushwa, wizi na ufisadi usiomithilika.

Ushauri wangu kwa rafiki yangu Makongoro Nyerere ni kwamba, siyo tu amwache shemeji yake Leticia achanje mbuga na kutafuta ubunge kwa uhusiano wowote ule; bali awaache wote wanaomtaja Nyerere, kwa wema au ubaya na kwa sababu yoyote iwayo.

Nyerere siyo mali ya mtu mmoja, familia au ukoo. Na Nyerere hahitaji utetezi; bado anajiweza, hata baada ya kuaga dunia.

Aidha, tusisahau kuwa upogo uliogeuka mtindo, utaendelea kutumiwa na wanaume wengi kudhalilisha wanawake, wakidhani kuwa hata wanapokuwa hawawagharamii tena, bado wananufaika kwa majina yao.

Huu siyo tu uongo, bali ujinga ulioambatana na ubabe wa miaka mingi na unaoendelezwa na ulimbukeni miongoni mwa wanaume, wakifikiri au kudhani tu kwamba majina yao yana ulimbo wa maisha bora.


Mwisho

AHADI LUKUKI ZA CCM




SITAKI

Ahadi nyingi za kiwewe za mgombea urais

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI kampeni zilizosheheni ahadi kebekebe na zisizokuwa na ukomo; hasa zinapokuwa zinatolewa na mgombea anayetaka kubaki ikulu kwa miaka mingine mitano.

Akihutubia mkutano wa kampeni mjini Bukoba mapema wiki hii, mgombea urais wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Jakaya Mrisho Kikwete alinukuliwa akisema serikali itanunua meli kubwa na mpya itakayofanya kazi katika ziwa Viktoria na kupunguza kero ya usafiri kwa bandari za ziwa hilo.

Hivi sasa, meli ya mv Viktoria ndiyo kubwa inayofanya safari ziwani humo, baada ya mv Bukoba kupinduka na kuua zaidi ya watu 1000 Mei 1996.

Kikwete ametonesha vidonda hai. Tangu mwaka 1996 serikali imekaa kimya. Benjamin William Mkapa alimrithisha Kikwete kimya hicho. Kikwete amekuwa kimya kwa miaka mitano. Bila shaka kuna sababu ya Kikwete kuahidi ununuzi wa meli. Tutaona.

Nakumbuka mama yangu alizimia muda mfupi baada ya kuambiwa kuwa meli imezama na kuua watu wengi. Siku ya tatu baadaye aliaga dunia.

Ilikuwa hivi: Kaka yangu alimwambia mama yetu kuwa meli imezama na kuua watu wengi. Alimwambia kuwa yeye alikuwa asafiri kwa meli hiyo, lakini alipoona imejaa, akaamua kubaki pale bandari ya Kemondo ili asafiri siku nyingine. Hiyo ndiyo ilikuwa safari ya mwisho ya mv Bukoba.

Ndani ya meli hiyo aliteketea mke wa kaka yangu na watoto wake wawili. Aliteketea mpwa wangu Evelyn, mtoto wake na binti mmoja ambaye alikuwa amemchukua kutoka kijijini kwetu Bushumba ili amsaidie shughuli za nyumbani.

Nasimulia. Ilikuwa hivi: Baada ya kaka kumwambia mama yetu kuwa meli imezama na kuua wengi, mama aliuliza, “…na Ndimara alikuwemo?” Kaka alijibu, “Hapana. Ndimara yuko nje ya nchi.” Mama alijibu, “…hivyo ndivyo wamezoea kunidanganya…” Alikaa kimya hadi alipoaga dunia, siku ya tatu.

Hakika nilikuwa nje ya nchi. Nilikuwa mji wa Kariba kwenye bwawa la Kariba lililoko mpakani mwa Zambia na Zimbabwe. Tulikuwa kwenye mkutano wa waandishi wa habari tukijadili “Sheria, Demokrasi na Vyombo vya Habari.” Nilipata taarifa kwenye televisheni iliyoonesha meli ilivyozama.

Niliomba gari kutoka ubalozi wa Sweden nchini Zambia. Nilipewa. Ni kilometa 249 kutoka Kariba hadi Lusaka. Kesho yake niliunganisha na ndege, wakati huo Shirika la Ndege Tanzania (ATC) iliyokuwa inapitia Harare na kurudi Dar es Salaam.

Nilifika Dar es Salaam jioni ya saa 12. Niliondoka Dar es Salaam kwenda Bukoba kesho yake asubuhi. Nilifika kijijini Bushumba siku hiyohiyo saa 10.30 na kukuta wananawa mikono – wamemaliza kumzika mama.

Mjini Mwanza nilikuwa nimemwacha kaka yangu, Gration Tegambwage akichuruzika machozi yasiyoisha – amepoteza mke na watoto wawili. Nilimwachia andishi lililokuwa limeandikwa kwa njia ya shairi awe analisoma na kuona iwapo lingemsaidia kutuliza roho; lakini siyo kusahau.

Asingeweza kusahau haraka au polepole kwani kila baada ya muda, maiti zilizoopolewa ziliwekwa uwanjani Nyamagana na alilazimika kufunua kila maiti kuona iwapo atamwona mpenzi wake – mkewe au angalau mmoja wa watoto wake. Ni majuto. Ni machozi yasiyokauka. Hakuona yeyote.

Vilio hivi vimeendelea ndani ya mitima ya wengi. Serikali imekaa kimya. Miaka mitano imepita. Rais akaomba kura tena. Akapata. Akatulia ikulu. Akasahau. Miaka ikapita. Akaondoka. Akaja mwingine – Jakaya Mrisho Kikwete.

Naye Kikwete amekaa miaka mitano. Sasa anaomba kura ili aendelee kupanga ikulu kwa miaka mingine mitano. Ndipo anaahidi meli.

Kwa kumbukumbu zangu mv Viktoria iliingia ziwani Viktoria mwaka 1965. Tunaambiwa haikuwa mpya. Huenda ni kweli. Tangu hapo imekata maji usiku na mchana hadi ikazeeka.

Meli hii imezimika mara kadhaa ikiwa safarini. Imeshindwa kuendelea na safari na kuwekwa ghatini kwa vipindi vingi. Imekarabatiwa na kukarabatiwa. Baadhi ya wafanyakazi melini humo wamesikika wakisema, “...nalo hili limeoza.”

Hii ina maana gani? Kwamba abiria wanasafiri kwenye mgongo wa mauti. Kwamba lolote laweza kutokea. Lolote lipi? Bila kutabiri majanga, lakini linajulikana: kuzama, kupinduka na kuua abiria mithili ya mv Bukoba.

Kinachouma ni kwamba mgombea wa CCM alipotoa ahadi ya meli, wananchi wa Bukoba walishangilia. Wachache walitikisa vichwa kwa masikitiko. Wachache au hakuna waliojiuliza kwa nini mgombea atoe ahadi siku hiyo na siyo miaka kadhaa iliyopita.

Niliwahi kuhutubia mkutano wa hadhara mjini Bukoba, miaka mingi iliyopita nilipokuwa mwakilishi wa Muleba Kaskazini. Niliwaambia wananchi, pamoja na mambo mengine kuwa, “…nimushekelela olufu nk’omunyima.”

Omunyima ni mnyama ndogo mweusi ambaye, hata anapofukuzwa na kupigwa, kwa nia ya kumuua, bado anaendelea kutoa sauti kama anayecheka. Ndipo wenye lugha yao wakasema “unachekea mauti kama mnyima.”

Wakazi wa Magharibi mwa Ziwa Viktoria wamekuwa wakichekea mauti kama mnyima. Kuna majanga mengi yaliyowakumba na serikali ikakaa kimya; lakini wao waliendelea kuonyesha tabasamu. Ni mengi na yanajumuisha vita vya Uganda na hata ukimwi uliokingiwa magego hadi watu walipoanza kupukutika.

Nilitoka Bukoba siku ya Jumatano ambayo mgombea wa CCM alikuwa ahutubie mjini hapo. Nilikutana na wanaume wawili na mwanamke mmoja – wote wa makamo – kwenye hoteli ya Victorius Perch.

Ni mwanamke aliyekuwa wa kwanza kueleza kuwa kuna mkutano wa mgombea urais wa CCM siku hiyo. Maneno yake yalidakwa na mmoja wa wanaume, na kama kawaida katika lugha yao. “Nani? Ekikwanga okyanga” – anayekukataa nawe huna budi kumkataa!

Ni ujumbe mkataa. Inaonekana hao hawachekei mnyima tena. Wanajadili mengi ambayo serikali imefanya lakini imesahau au imedharau wasafiri kwenye ziwa Viktoria wanahitaji na hakika wanastahili chombo imara cha usafiri.

Mmoja anang’aka, “Naona wanafikiri kuwa sisi tuna uzoefu wa kufa.” Mwingine anaorodhesha yale ambayo serikali imefanya na kutaja uwanja mpya wa taifa jijini Dar es Salaam kuwa ndio watawala wameona ni muhimu kuliko meli.

Kikwete atakuwa amebanwa sana katika kampeni za sasa za kutafuta urais hadi kufikia hatua ya kuahidi meli ziwani Viktoria ambayo hajawahi kutamka katika mipango yake.

Ni kama alivyofanya kwa wakazi wa Misenyi mkoani Kagera ambao wamekuwa wakifukuzwa kutoka maeneo yao ya asili kwa madai kuwa ni eneo la ranchi iliyobinafsishwa. Sasa anasema wapimiwe viwanja ndani ya ranchi.

Mgombea urais wa CCM anajua kuwa nani walinunua na wanamiliki ranchi ya Misenyi. Tumeambiwa ni baadhi ya marafiki zake. Alikuwa wapi hadi juzi ndipo aseme hilo? Mbona hakusikia vilio vya wananchi pale mkuu wa mkoa alipokuwa akiwakomalia kuwa wataweza kuhamishwa “hata kwa mtutu wa bunduki?”

Ahadi za Kikwete zitakuwa nyingi mwaka huu. Anayejua sababu ni yeye mwenyewe na chama chake. Kinachoonekana ni kwamba katika maeneo mengi, kama Bukoba na Misenyi, anajichongea.
Huenda kura zisitimie.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com

UCHOVU NA UMBEYA WA WAKUBWA

SITAKI


Wachovu wa CCM na umbeya wao


Na Ndimara Tegambwage

SITAKI wananchi waingizwe kwenye ubishi wa kipuuzi unaopaliliwa na kunawirishwa na wachovu wa siasa.

Wiki hii tumesikia baadhi ya viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wakidai kuwa watashitaki Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).

Wamesema watapeleka malalamiko kwa Tume na Msajili wa Vyama vya Siasa kwamba Chadema imefanya kampeni kabla ya Tume kuruhusu.

Kinachotia kichefuchefu ni baadhi ya wanasiasa upande wa upinzani kuitikia kibwagizo cha CCM na wao kuimba kuwa Chadema na CCM wanaweza “kuchukuliwa hatua.”

Hali iko hivi: Dk. Willibrod Slaa anateuliwa na chama chake kugombea urais. Chama kinaanua kufanya mikutano katika miji mikuu ya mikoa kadhaa. Kinambeba mteule wake. Hii ni kwa sababu kuu mbili:

Kwanza, kumtambulisha kwa wanachama wake na wananchi. Pili, kuendeleza kazi yake ya kisiasa kama chama chochote kile kilichohai.

Chama kilichohai, kikipata fursa, sharti kiitumie kuwafikia majaji wakuu katika taratibu za kidemokrasia; ambao ni wananchi wapigakura.

Chadema haikufanya hivyo juzi tu. Imekuwa ikifanya hivyo kila inapotaka kuwa karibu na wananchi; na wapigakura.

Hivyo ndivyo CCM imefanya. Imetangaza wagombea wake, halafu ikawapeleka kwenye mikutano ya hadhara – kwa wapigakura – ili wanachama wenzao na wananchi wawafahamu.

Chama kingine chenye ushindani ni Chama cha Wananchi CUF. Hiki hakikuwa na kiongozi wa kutambulisha kwani mgombea urais wake mwaka huu, ni Profesa Ibrahim Lipumba ambaye tayari amepigiwa kura za urais mara tatu.

Hata hivyo, CUF muda mfupi baada ya kutangaza mgombea wake, iliweka wazi kwa mgombea, ambaye pia ni mwenyekiti wa chama hicho kitaifa, atatembelea mkoa wa Dar es Salaam kwa madhumuni ya “kuangalia uhai wa chama.”

Hiyo nayo ni fursa nyingine kwa chama makini kuwa karibu na wananchi na wanachama wake wakati muhimu wa kuelekea uchaguzi mkuu.

Ukiangalia kwa makini, utaona kuwa kila chama kina njia zake za kufanya kazi za kisiasa – iwe asubuhi, adhuhuri, alasiri, mangharibi au usiku.

Muda huu wa maandalizi ya kuingia kipindi maalum cha kampeni na uchaguzi mkuu, hautawaliwi na pingu za NEC. Ni muda na eneo huru la kuzidisha kazi za kisiasa.

Hasa ni kipindi maalum kwa vyama upande wa upinzani, kutekenya jamii, kuizindua, kuielimisha, kuishawishi na kuiandaa kuachana na ukale ulioizonga na kuipa kilema – kudumaa.

Kwa mfano, kwa upande wa Chadema, ni wakati wa kuendeleza na kuhitimisha kwa nguvu, kazi ya kisiasa inayoitwa “Operesheni Sangara” – iliyovuma na kuvuna nyoyo za wengi – kabla ya kuingia katika uchaguzi mkuu.

Kwa upande wa CUF, ni wakati mzuri wa kuendeleza na kuhitimisha kazi ya kisiasa iliyoitwa “Zinduka” – iliyozindua wengi – kabla ya kuingia katika uchaguzi mkuu.

Kwa hiyo, kinachoipa kiwewe CCM, siyo Chadema “kufanya kampeni” kabla ya muda uliopangwa na Tume, bali umaarufu wa mgombea wa Chadema anapolinganishwa na yule wa chama chao.

Kiwewe kinatokana na mgombea mpya anayefahamu vema serikali na nyendo zake. Anayejua serikali ilivyokwama kwenye tope la ufisadi, ukosefu wa ubunifu; ukame wa mbinu mpya na ahadi tuputupu.

Kelele za CCM zinalenga kufanya mwendelezo wa ghiliba kwa wananchi. Chama hiki, kama ilivyo serikali yake, kina midomo mingi na uwezo wa kupakazia.

Kina vyombo vya habari vya serikali (wanadai ni vya umma), ambavyo vinatawaliwa na makada wake. Humu hupitishwa kampeni na propaganda angamizi.

CCM ina “marafiki” wenye vyombo vya habari ambao huipendelea kwa kila hali kuliko hata gazeti lake la UHURU.

Kwa kutumia midomo yake mingi; laghai wake wengi; ujuzi na uzoefu wa kutunga ghiliba na kupakazia, chama hiki kinaweza kuanzisha mjadala finyu, kikaupa mvumo, ukapandikiza mitafaruku na kupotosha wananchi wengi.

Chama hikihiki kinaweza kutumia kauli za nguvu kuyumbisha watendaji serikalini; kutishia walioko madarakani katika sehemu muhimu kama Tume ya uchaguzi na kuogofya wananchi.

Haitakuwa mara kwanza kwangu kujenga hoja kwamba watawala wetu wamekuwa wakitegemea sana ujinga, woga na umasikini wa wananchi (vilivyosimikwa na chama kinachopanga ikulu), kama mitaji yake mikuu katika juhudi za kubaki madarakani kwa nusu karne sasa.

Chama hiki kina watu wenye ujasiri wa kukataa ukweli; wakaidi wa kutaka kila mmoja aone, kwa mfano, kuwa hili ni chungwa wakati ni kiazi kikuu.

CCM isingekuwa hivyo, kama ilivyofafanuliwa hapo juu, viongozi wake wasingejitokeza kupandikiza uzushi kwamba Chadema imefanya kampeni kabla ya NEC kutangaza.

Kwani kampeni za kuwaelimisha wananchi kujua kuwa diwani, mbunge au rais huyu hafai; anayefaa ni fulani kutoka chama kingine, hazisubiri uchaguzi mkuu.

Hii ni kazi ya Oktoba hadi Oktoba, kwa kipindi chote cha miaka mitano ya wanaokuwa madarakani na wanaokuwa wakisubiri kuingia.

Katika kipindi chote hiki NEC inajiandaa kusimamia uchaguzi lakini wanasiasa wanakata mbuga kuandaa wananchi kwa “mavuno.”

Hapa hakuna udhibiti hadi unapoingia rasmi kwenye mchakato wa uchaguzi mkuu. Kazi za kisiasa za chama chochote, haziruhusiwi wala hazipaswi kuzuiwa na Tume. Na pasito zuio kuna uhuru kamili.

Chukua mfano huu: Katika mazingira ambako hakuna sheria inayolazimisha kila mmoja kuvaa tai shingoni, hakuna anayeweza kukamatwa na kushitakiwa kwa kutovaa tai. Hakuna sheria inayombana.

Hiyo ndiyo hali iliyopo katika kipindi ambapo wachezaji watarajiwa wa mchezo wa siasa hawajajifunga kushiriki; na mchezo wenyewe haujaanza.

Huwezi kuwabana. Huwezi kusema aliye nje ya uwanja ameharibu kanuni na taratibu za mchezo. Kudai hivyo ni kupanda mbegu ya uhasama ambao CCM na serikali yake, havina uwezo wa kuzima ndimi zake pale zitakapokuwa zimechomoza.

Hivi sasa, CCM ni chama kinachokwenda kwa mazoea tu. Hakina jipya ingawa kinataka kubaki ikulu, kwa “gharama yoyote ile.”

Na hili la kubaki madarakani kwa gharama yoyote ile, ndilo liwezalo kuleta maafa kwa nchi na watu wake.

Kwani wanajua kuwa kuondoka kwao kutaweka wazi mengi machafu ambayo yamekuwa yakitendeka. Hili, viongozi wake hawataki kuliona wala kulisikia.

Wako tayari kuua mbegu mpya na bora kwa kupitia madai yasiyo kichwa wala miguu, alimradi wamebaki ikulu.

Lakini katika hili la kupakazia kufanya kampeni mapema, tundu limezibwa. Hata kwa mgongo wa “tu-vyama twingine” kwenye upande wa upinzani, kama vile Tanzania Labour Party (TLP) ka Augustine Mrema, CCM itaendelea kukaliwa kooni.

Tayari kuibuka kwa Dk. Slaa kumebadili mwelekeo wa siasa nchini na kuleta uwezekano wa kuifinyaza CCM na mikonga yake.

Bali wananchi wanataka umoja wa vyama; kwa maana ya ushirikiano katika uchaguzi huu ili mradi wa kuadabisha CCM uweze kufanikiwa.

Umbeya na ghiliba ya CCM vyaweza kuzimwa. Je, hili la ushirikiano laweza kufikiwa? Tusubiri.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com