Sunday, November 8, 2009

SERIKALI IKIKIRI KUSHINDWA 'IPUMZIKE'




RAIS APUMZIKIA KARIBU NA MIZOGA YA
MIFUGO NA WAKULIMA WENYE NJAA

Na Ndimara Tegambwage
SERIKALI imesema isilaumiwe kwa ukame au vifo vya mifugo nchini. Rais Jakaya Kikwete amesema, "Wapo …wanaoichukia serikali kutokana na ukame; jamani hata sisi tunaomba Mungu hali iwe nzuri…"

Ni kauli za aina hii ambazo vijana wa mjini hupenda kuita, “funga kazi.” Tatizo la vijana hao ni kwamba hawaoni kuwa kazi haijafanyika. Ukweli ni kwamba hizo ni kauli za mwisho wa mwanzo wa kukata tamaa.

Tujadili. Kisiasa, kauli ya rais ilitolewa muda na mahali pasipofaa. Ilitolewa katika kijiji cha Olbalbal wilayani Ngorongoro. Taarifa za awali zilikuwa zimeeleza kuwa rais yuko likizo ndogo katika mbuga za wanyama za Ngorongoro.

Ngorongoro ni moja ya wilaya ambazo zimekumbwa na ukame wa aina yake. Mifugo inakufa. Mizoga imetapakaa huku na kule. Wafugaji hawana maji. Niliwahi kuandika kuwa hata wao wanaweza kuitwa “mizoga inayotembea.”

Ni huko rais alikwenda kufanya mapumziko. Nasema siyo sahihi kisiasa kwa kuwa rais kaenda “kujinyolosa” baada ya mahangaiko; pale – jirani tu – hata kama kwa umbali wa kilometa 80; lakini ndani ya wilaya hiyohiyo ambamo maafa ndiyo maisha.

Kama siyo kwa diplomasia – ule unafiki wa kicheko na mgonganisho wa bilauri za mvinyo huku watu wakiteketea – na hilo hufunzwa vyuoni – basi rais angekemewa.

Sasa rais amewahi. Amewaambia wananchi wanaoishi katika wilaya ambamo uoza wa Loliondo umefunika harufu kali ya ubani, kuwa hana la kufanya kuhusu ukame na vifo vya mifugo yao.

Kwamba wafuge kisasa; kwamba yeye ana ng’ombe 600 lakini hahitaji kuzungukazunguka nao kutafuta malisho; kwamba wajifunze kutoka wafugaji wa Uganda; kwamba hata serikali inaomba mvua zije.

Ukitaka waweza kuita hayo kuwa ni kejeli. Ukitaka waweza kuita kauli za kutojali kilio cha wafugaji. Ukitaka pia waweza kuita mizaha kwenye msiba. Mkuu wa nchi akisema hayo, wanasiasa wa viwango vya Yusuph Makamba watasema nini?

Uko wapi mpango wa serikali wa kushirikisha wananchi – wafugaji – katika kutatua matatizo yao? Kwa mfano, uongozi wa wilaya au mkoa kukaa na wafugaji; kujadili jinsi ya kuchanga ng’ombe, kuwauza, kupata fedha za kununulia mabomba ili kuvuta maji kutoka mbali. Uko wapi?

Uko wapi mpango wa serikali wa kutafuta vilipo vyanzo vya maji wilaya nzima; kuvilea, kuvihifadhi na kujenga malambo yenye uwezo mkubwa wa kulinda maisha ya mifugo na wafugaji?

Kama kuna mfano mzuri Uganda, wafugaji wa huko walianza vipi? Walitoka usingizini wakajikuta wameanza kufuga kisasa; au kuna waelekezaji – wataalam wenye moyo wa kutumikia jamii – ambao waliacha umangimeza; wakajitosha kwenye maeneo ya wafugaji na kuanza kushawishi, kufundisha na kuonyesha mifano?

Wafugaji wa wilaya ya Ngorongoro siyo ombaomba. Hutozwa kodi, yao na ya mifugo. Wanahitaji utaalam wa wale wanaojali na wasiosingizia Mungu kwa kila janga, pamoja na janga la ukame. Wanahitaji uongozi wenye akili na unaowathamini.

Umbali uliopo kutoka yalipo maji hadi walipo wafugaji na mifugo yao inayokufa, hauzidi kilometa 80. Pengine ni kilometa tano. Pengine kilometa 15. pengine kilometa 40.

Vilevile kuna maji yaliyofungiwa na wanaoitwa wawekezaji – wale waliojipa uwezo wa ki-Mungu wa kuamua huyu na mifugo yake hata wafe, potelea mbali, lakini hawawezi kuchota maji kwenye kisima kilichoko wilaya ya Ngorongoro, mkoa wa Arusha, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ushenzi uliopitiliza.

Wanaoitwa viongozi wa wilaya wamefumba au wamefumbwa midomo. Viongozi wa mikoa yenye ukame wamejikinga nyuma ya pazia la “sheria.” Waziri wa mifugo anahangaika kukanusha ukweli usiokanushika. Leo rais anasema hana la kufanya labda kumwomba Mungu.

Picha za mizoga ya mifugo – ng’ombe, mbuzi na kondoo, ni ushahidi wa serikali isiyotenda. Sauti za wafugaji, zinazotetereka na kupotelea mbugani bila kusikilizwa na watawala, ni ushahidi wa ukatili unaoendeshwa na wale wanaoishia kutukana, kukejeli na kufukuza wafugaji kutoka makazi yao.

Rais ana ardhi. Ana maji. Ana fedha za kutunzia bustani za vyakula vya mifugo. Ana fedha za kununulia dawa. Ana maji ya kunywesha mifugo na kumwagilia bustani za vyakula vyake. Ana madaraka – maji hayakatiki. Yakikatika akikohoa yanarudishwa. Haombi Mungu mvua inyeshe ili mifugo isife.

Rais alipewa ushauri na wataalam. Anakofugia paliandaliwa na wataalam. Panakaguliwa na wataalam; na ng’ombe ni ng’ombe tu; awe wa rais au wa Masaai.

Lakini mfugaji, mwenye elimu ya asili tu ya kujishughulisha na mifugo; kwa mfano kujua dawa za miti shamba za kuiponya na mahali pa kuilaza; anahitaji kufikiwa na mbinu za kisasa ili afuge kama rais au kama Jakaya Kikwete.

Wafugaji wengine, pamoja na kuishi mbali na miji, na hiyo ni faida kwao, wana ng’ombe wengi kuliko rais. Wengine wana hata zaidi ya 2,000. Kuwapa wananchi hawa wazo la kuchangia kupatikana kwa maji katika maeneo yao, hakuwezi kuwa mzigo. Watahiari. Lakini hakuna uongozi wa kufanya hivyo.

Hili ni la kuwashirikisha – wao na utajiri wao wa mifugo. Haliwaondolei haki yao ya kufaidi matunda ya kodi walipazo. Hapa ndipo tungetaka kuona watawala wakiwajibika kwa walipakodi na siyo kuwaambia wamwombe Mungu ili mvua inyeshe.

Dunia nzima inatambua kazi ya kodi na mapato ya nchi kwa ujumla. Mfano wa Libya huwa unanijia mara kwa mara. Ni Kanali Muamar Ghadaffi, kiongozi wa nchi hiyo aliyesukuma maji kwa njia ya mabomba kwa umbali wa zaidi ya kilometa 1,700 ndani ya jangwa la nchi hiyo.

Watu wakanywa maji. Wakaonga. Wakafua. Wakatunza bustani ndani ya jangwa. Jangwa likakoma kuwa jangwa pale maji yalipotiririkia. Tanzania hakuna jangwa.

Rais Kikwete amekoleza kilio cha wananchi wafugaji wa wilaya ya Ngorongoro. Alikwenda kupumzikia kwao wakati wao hawana mapumziko. Wengi wanalala nje. Wamechomewa nyumba na maboma ya mifugo.

Rais alikwenda kupumzikia kwa wale ambao wanaswagwa na watawala wilayani kwa msaada wa “wageni” waliokabidhiwa vipande vya ardhi ya nchi hii kwa ajili ya kuua raslimali wanyama.

Kubwa kuliko yote ni kwamba rais amewaambia wakazi wa Ngorongoro kuwa wachague Chama Cha Mapinduzi (CCM), katika uchaguzi wa serikali za mitaa, kwa kuwa ndicho chenye “uhakika wa kuwaletea maendeleo.”

Uko wapi uwezo alioahidi rais? Uuliyeyuka palepale aliposema hana uwezo wa kumaliza ukame na kusitisha vifo vya mifugo katika nchi yenye mito mikubwa isiyokauka; maziwa makubwa, marefu, yenye kina kirefu; na maeneo mengi yenye unyevu kunakoweza kuchimbwa mabwawa na malambo kwa ajili ya huduma kwa watu na mifugo yao.
(Makala hii ilichapishwa katika gazeti la MwanaHALISI toleo Na. 160 la 28 October 2009)

Saturday, October 17, 2009

KUENZI NYERERE KWA ULEVI, USINGIZI



WANANCHI WANAAMBIWA WALALE NA HUKO WATAMSAHAU

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI kumkumbuka Mwalimu Julius Nyerere kwa njia ambayo haifanani kabisa na matendo na fikra zake pale alipokuwa kiongozi wa nchi hii.

Sitaki kushiriki uchovu wa watawala unaoelekeza taifa kuwa kumkumbuka Mwalimu ni kuwa na siku ya mapumziko; siku ya kulala na kukoroma. Wengine wanaongeza hapo: kula na kuvimbiwa na kunywa na kulewa.

Nyerere aliyemaliza zaidi ya wiki mbili akichimba mtaro wa mabomba ya maji wa Ntomoko, mkoani Dodoma, hawezi kukumbukwa kwa usingizi wa pono unaotokana na ulevi wa siku nzima isiyo na shughuli ya maana.

Hapa kuna Nyerere aliyemaliza wiki nzima katika kijiji cha Muyama, wilayani Kasulu, mkoa wa Kigoma akijenga nyumba za wanakijiji. Tulikamilisha nyumba 15. Huwezi kukumbuka kiongozi wa aina hii kwa kile watawala wa sasa wanaita “mapumziko.”

Mwenyekiti wa kijiji atakwenda kwa Nyerere na kumwambia, “Mwalimu, unaona jua limekwenda; afadhali upumzike.” Nyerere atamwangalia kwa sekunde kadhaa, kumtolea macho na hatimaye kumwambia huku akicheka; kile kicheko chake cha mpasuko:

“Hah, ha, ha! Mwenyekiti, hayo si maneno yako. Umetumwa na wale paleee. Watu wa mjini wale. Naona vitambi vyao vinaanza kuporomoka. Hapana. Siyo maneno yako. Mwenyekiti, siyo maneno yako. Njoo tufanye kazi.” Ataendelea kufanya kazi.

Nyerere mchapakazi; aliye karibu na wananchi, hastahili kukumbukwa kwa kulala, kuamka, kula, kunywa, kulewa na kulala. Hapana. Nyerere asiyepumzika anaenziwa kwa mapumziko; tena ya nchi nzima? Kama siyo kejeli ni kashfa.

Kuanzia saa 12 au saa moja asubuhi, Nyerere anakata mbuga na viongozi akikagua “miradi ya maendeleo,” ya kweli na uwongo. Hapa anakuta usiku wa kuamkia siku anayofika, ndipo wamesimika miche ya kabichi udongoni. Wanamwambia, “Mzee tunajitahidi kutekeleza siasa ya kujitegemea.”

Tunazunguka bustani. Anaona. Hatimaye anachukua kifimbo chake na kusukuma mche mmoja, unaanguka. Anasukuma wa pili, unaanguka. Anasukuma wa tatu, unaanguka. Anasonya na kuondoka. Ataongea na viongozi wa wilaya au mkoa baadaye.

Ni mwenye kutambua haraka. Ni mwenye kutonywa haraka na wale wanaomwamini. Ni mwepesi wa kusikia kilichonong’onwa na kuuliza, “Kuna nini? Maana yake nini?” Huyo ndiye taifa linaongozwa kukumbuka kwa usingizi?

Twende kwenye chumba cha mkutano. Harufu. Ni harufu ya rangi iliyopakwa jana. Mwalimu anashika pua. Anaifinyanga. Anatoa kitambaa mfukoni; anaipangusapangusa kama anayetaka kupiga chafya. Anarudisha kitambaa mfukoni na kusema, “Hata kupiga rangi ni mpaka niwe ninakuja hapa?” Meseji delivadi.

Anafundisha kila aendapo. Anasema mkoa wa Shinyanga umezidi kwa ukame; sasa unageuka jangwa. Anaagiza wapande miti. Mkuu wa mkoa katika mkutano wa viongozi anasimama na kusema, “Mheshimiwa rais, tunaomba mradi wa kupanda miti uwe wa kitaifa.”

Nyerere anag’aka, “Nasema Shinyanga inageuka jangwa. Panda miti.” Lakini angalia Nyerere katika kijiji cha Mwamihanza ambako anaambiwa kuwa mzeee mmoja analima bangi. “Mimi, mimi sina tatizo kana hafanyi biashara. Wengine wanatumia majani hayo kwa dawa.”

Anawafikia wananchi wengi. Anatumia muda mwingi ndani ya nchi yake. Anasikiliza na kusikia matatizo mengi. Mwaka 2005, baadhi ya wafugaji waliokutwa Msata, mkoani Pwani, walipoulizwa wanataka kumpigia nani kura, kila mmoja alisema, “Nyerere.”

Nyerere huyo bado amegota vichwani mwao. Hakuwaibia wala kuwaswaga kama mifugo kutoka kwenye makazi yao. Leo wanahitaji njia bora ya kumuenzi mchapakazi. Siyo kupumzika. Siyo kulala.

Nyerere mwenye ujasiri wa kutunga maadili ya uongozi kwa viongozi – watu wazima na siyo watoto wa shule, akilenga uadilifu katika utawala; kiongozi wa kutangaza Azimio la Arusha na kutaifisha mashamba, majumba na mabenki, kwa nia njema kwa kadri ya uelewa wake na nia yake; leo anakumbukwa kwa kupiga usingizi? Ama ni mzaha au kashfa.

Rais aliyepeleka nchi vitani na ikarudi na ushindi – kwa sababu zozote zile za kuwepo kwa vita dhidi ya dikiteta Idi Amin Dada wa Uganda; aliyekuwa jemedari wa vita vya ukombozi Kusini mwa Afrika akifundisha wananchi kujitolea damu na uhai wao; akumbukwe kwa kula, kunywa na kulala?

Kiongozi wa nchi ambaye wakati wake elimu ya watu wazima ilifikia kiwango cha asilimia 90; aliyethamini elimu na aliyesoma wakati wote hata baada ya siku nzima ya kuongea na wakulima, kufokoeana na wataalamu wa kilimo, wakuu wa wilaya na mikoa, aenziwe kwa “mapumziko,” tena ya nchi nzima?

Mwalimu Nyerere – kile “kitabu” cha rejea juu ya fikra na maoni mbalimbali duniani; mpambanishaji hoja hadi kuitwa kaidi; aliyeandika vitabu vingi akiwa madarakani na aliyethamini elimu; sasa anakumbukwa kwa mapumziko. Ili iweje?

Kiongozi wa nchi ambaye hakupora fedha wala mali ya taifa; hakujilimbikizia mali wala kutumia vibaya kile alichopangiwa; yule ambaye alilinda utajiri wa ardhini, misitu na wanyama hadi anatoka madarakani; anakumbukwa kwa kulala usingizi wa pono.

Nyerere alikuwa binadamu. Alitokeza kwa wakati wake na kufanya mengi ya wakati wake, hasa taifa lilipokuwa linamea na kukua kuelekea tulipo sasa. Alisisitiza uzalendo – mapenzi kwa nchi, watu wake na raslimali zake.

Hili lina maana kubwa katika maisha ya taifa. Lina maana ya kutaka matumizi ya raslimali za nchi kwa manufaa ya wengi, kama siyo wote; lina maana ya kutumia raslimali za nchi kwa kiwango kikubwa ili kuepuka kuwa tegemezi. Kiini cha kujitegemea.

Taarifa zitaandikwa. Makala zitaandikwa. Vitabu vitaandikwa juu ya Nyerere na mijadala juu yake haitaisha leo wala kesho. Kiongozi aliyetetea na kuishi maisha ya aina anayofundisha – ya uadilifu; hakustahili kuenziwa kwa mapumziko, bali kazi.

Kama hili halieleweki kwa watawala ambao aliwaacha madarakani, wanataka nani aje kuwafundisha kuwa hata kama alikuwa TANU na CCM, Nyerere alikuwa mtu kabla ya kuwa mwansiasa na mtawala.

Siku ya kumkumbuka Nyerere watawala wanatutangazia mapumziko ili tule na kuvimbiwa, tunywe na kulewa na kulala usingizi wa pono ili kujisahaulisha aliyotenda au kumzika na mema aliyoyatenda? Naomba kutoa hoja: Mapumziko haya yafutwe.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
(Makala hii itachapishwa katika Tanzania Daima Jumapili, toleo la 18 Oktoba 2009 katika safu ya SITAKI)

Sunday, October 11, 2009

WATU NA MIFUGO YAO WATAKUFA




SERIKALI IMEKWENDA WAPI LOLIONDO?

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI kuambiwa kuwa kuna serikali. Haipo. Kama ipo imelala, tena usingizi wa pono? Imezimia? Waliolala hawaamki? Waliozimia hawazinduki? Haipo!

Wafugaji wilayani Ngorongoro wanasema, tena kwa sauti kubwa kuwa kuna ukame. Kuwa mifugo yao – ng’ombe, mbuzi na kondoo haina chakula. Hakuna malisho. Hakuna maji. Mifugo inakufa. Serikali haipo.

Mwandishi kutoka Loliondo anapaza sauti, kwa simulizi na takwimu: Hakuna maji. Hakuna nyasi. Mifugo inakufa. Ng’ombe sasa anauzwa kwa Sh. 2,000 hadi 20,000. Serikali kimya.

Mfugaji anapaza sauti. Anadhani serikali haijasikia. Anasema maji yapo; wamekuwa wakiyatumia. Lakini maeneo yenye maji yamefungiwa kwenye mipaka ya vitalu vya uwindaji ambavyo serikali imegawa kwa watu wa nje – “wawekezwaji” – wale waliowekezwa badala ya kuwekeza. Serikali tebilimu!

Kuna vilio, kwamba ng’ombe wawili wameuzwa kwa debe moja la mahindi. Kwamba bei ya debe la mahindi ni kati ya Sh. 8,000 na 10,000/=. Kwamba lazima ng’ombe auzwe haraka, hata kama ni kwa hasara, kabla hajafa. Serikali haipo.

Sikilizeni sauti zao, hao wafugaji. Kwangu ng’ombe wamekufa watano. Kwangu wamekufa 20. Kwangu wamekufa 50. Elias Kagili wa kitongoji cha Kirtalo anasema: Kwangu wamekufa 100. Ni hatari tupu. Vifo. Vifo. Mwandishi kaona. Kasikiliza waathirika. Kaona na kupiga picha za mizoga. Serikali haipo.

Sikilizeni kilio cha Ole Taki Saile wa kitongoji cha Ilichooroi. Ng’ombe wake 60 wamekufa. Wengine walio karibu kuwa taabani kawauza kwa bei ya kati ya Sh. 2,000 na 5,000. Naye Lekaneti Shekuti wa kitongoji cha Sekunya anasema karibu kila siku wanakufa ng’ombe wake 10. Serikali kimya.

Kauli ya Shekuti hii hapa. “Maji yapo pale. Nyasi zipo pale, lakini ng’ombe wetu wanakufa. Kampuni ya Thomson Safari inatuzuia kunywesha mifugo yetu pale,” anaonyesha sehemu husika kwa fimbo.

Maji yako Ngorika – mwekezwaji hataki. Maji yako Polelete; mwekezwaji hataki. Maji yako Sukenya, mwekezwaji hataki. Maji yako Olkimbai, mwekezwaji hataki. Maji yako Walaasaye, nako mwekezwaji hataki yanywewe. Kote huko ni visima na vijito vilivyoko katika ardhi waliyopewa wawekezwaji ili wafanyie “utalii wa uwindaji,” au ujangili ulioruhusiwa kisheria, ndani ya nchi ya wafugaji wanaotaabika.

Teremka kijitoni au kisimani wakukute; utakiona cha moto. Sukuma mifugo yako kijitoni na wakukute; ndipo utajuta kwa nini ulizaliwa. Huu ndio ukatili unaosababisha vifo vya mifugo. Serikali haipo.

Katika mazingira ya Ngorongoro na Loliondo, vifo vya ng’ombe, mbuzi na kondoo maana yake ni vifo vya watu. Wanaohangaika kutafuta chakula na maji kwa ajili ya mifugo, wao hawana chakula. Ni mizoga inayotembea; inahangaikia mifugo yake. Siku moja itadondoka njiani. Serikali tebilimu!

Serikali imetoa ardhi ya wananchi kwa makampuni kutoka nchi za nje, iwe sehemu ya kuwindia kwa ajili ya kujifurahisha. Katika mazingira ya sasa, nyasi na maji vinapatikana katika maeneo ambako wawekezwaji hawaruhusu mifugo kuingia.

Hata hivyo, kuanzia Aprili mwaka huu, nyumba na maboma ya wafugaji yamekuwa yakichomwa moto kwa nia ya kuwafukuza wafugaji kutoka makazi yao ili wawindaji wa wanyamapori wapate kustarehe. Ni starehe ya wawekezwaji na adha kwa wananchi.

Ni ukatili. Ni unyama usiomithilika. Haustahili kusimamiwa au kuvumiliwa na wanaojigamba asubuhi, mchana na jioni kuwa wao ni walinda haki na watetezi wa demokrasi na haki za binadamu. Haiwezekani. Ni kwa kuwa serikali haipo. Serikali tebilimu!

Kama serikali ipo inasubiri nini? Inasubiri mifugo ife na kumalizika? Ili iweje? Ili wafugaji wawe masikini? Ili wawe ombaomba? Au ili wafe kama mifugo yao, huku wawekezwaji kutoka nje wakimeremeta; wakitweta kwa shibe na kunenepeana kwa faida na ziada ya uwindaji Loliondo?

Wawekezaji hutegemewa kuleta fedha. Wawekezaji hutegemewa kuongeza ajira. Je, wawekezwaji wanaleta nini kama siyo adha; wanaongeza shida na dhiki. Wanasababisha roho mbaya. Wanafungia maji na nyasi “kabatini;” ili mifugo ife; ili wenye mifugo wafe au wahame.

Sitaki kuamini kuwa kuna serikali. Ipo? Inamlinda nani? Inalinda wawekezwaji ili watanue, huku ng’ombe wa wafugaji wakifa? Huku mbuzi na kondoo wanakufa? Huku wafugaji wakisubiri kufa pia?

Kungekuwa na serikali ingeona mahangaiko ya wafugaji wa Kimaasai. Tuseme ipo lakini haioni? Ingekuwepo ingesikia kilio cha wafugaji, waandishi wa habari, wanaharakati na wafanyabiashara wanaonunua ng’ombe mmoja kwa Sh. 2,000. Tuseme haina masikio au yameziba?

Kungekuwa na serikali, kwa maana ya watawala, ingekumbuka kuwa iliapa kutumikia watu, kuwalinda na kuwatendea haki; na iliapa kwa Mungu kuwa aisaidie kuyatenda kwa ukamilifu. Tuseme imesahau kiapo? Au wafugaji na maeneo yao siyo sehemu ya Tanzania? Au kiapo kimelainika? Nani amelainisha kiapo cha serikali?

Hata kama mambo haya yangekuwa yanatendeka Nigeria au Kongo; huwezi kukaa kimya juu ya unyama wanaotendewa binadamu wa Ngorongoro. Risasi za moto zinatafuta nini katika makazi ya Wamaasai na mifugo yao?

Alikuwa Desmond Tutu aliyesema, “Ukiona mguu mnene wa tembo umekanyaga mkia wa panya, na ukaangalia pembeni na kusema hayakuhusu na wewe huna upande; panya hataelewa msimamo wako wa kutokuwa na upande katika ukatili huu.”

Kuna kila sababu ya kuwa na upande katika kutetea haki. Na haki ya wananchi kuishi kwao na kufurahia matunda ya ardhi yao, haiwezi kupitwa na ujanjaujanja wa wawekezwaji hata kama wanamwaga mabilioni ya shilingi kwa yeyote yule.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
(Makala hii ilichapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili, toleo la tarehe 11 Oktoba 2009 chini ya safu ya SITAKI)

Saturday, September 26, 2009

ADHABU YA KIFO IMEPITWA NA WAKATI



Kunyonga siyo adhabu, ni kuua tu


Na Ndimara Tegambwage


SITAKI kuona wananchi na watawala wakishabikia hukumu ya kunyonga, hata kama kuna sheria ya nchi inayoruhusu mtu “kunyongwa hadi kufa.”

Sheria iliyopo ni katili, chovu, inayopaliliwa na kuendelea kurutubishwa na mfumo unaoendeshwa na watu ambao wamekuwa wagumu kuelewa mantiki ya thamani ya maisha na umuhimu wa adhabu.

Iwapo hawatakata rufaa, au wakikata rufaa na kushindwa, Masumbuko Madata, Emmanuel Masangwa na Charles Kalamuji, waweza kuuawa kutokana na hukumu iliyotolewa na Jaji Gabriel Rwakibalila.

Jumatano iliyopita, mjini Kahama, Jaji Rwakibalila aliwakuta vijana hao watatu na hatia ya jinai ya kuua Masumbuko Dunia, mtoto wa shule, umri wa miaka 13 na mwenye ulemavu wa ngozi (albino). Sasa kuna wanaoshangilia hukumu ya kifo.

Kifo cha Masumbuko kiliuma na kuumiza wengi, hata kama hawakuwa na uhusiano wowote naye. Umri wake mdogo; nafasi yake katika jamii iliyosababisha kuitwa majina ya kumtelekeza; utu wake ambao ulikuwa na bado ni sehemu ya utu wa kila mtu; ni sehemu tu ya chimbuko la uchungu.

Uchungu unakuwa mkubwa pale jamii inaposhuhudia mauaji yakilenga watu wenye ulemavu wa ngozi; wadogo kwa wakubwa, kwa sababu dhaifu, za kijinga na potofu – eti kupata viungo vya kuwawezesha “kuwa matajiri.”

Uchungu huu usio na udhibiti, unapokutana na sheria ambayo hata Jaji Mkuu Augustino Ramadhani amewahi kusema kuwa hafurahii kuitumia, ndipo unazaliwa ukatili mpya; ule wa kuondoa uhai wa aliyepatikana na hatia ya kuua.

Mahakama Kuu nchini Tanzania iliishawahi kutamka kuwa adhabu ya kifo ni ya kikatili na ya kudhalilisha na kutaka ifutwe. Pamoja na maeneo mengine, maneno “katili” na “kudhalilisha” ni ya msingi sana katika kuchambua hukumu ya kifo.

Katiba ya Jamhuri ya Muungano inakataza ukatili na udhalilishaji. Kwa hiyo kuwepo sheria inayoruhusu kuua; hivyo kuendesha “ukatili” na “udhalilishaji,” ni kuvunja katiba ya nchi. Lakini Mahakama ya Rufaa haikuafiki.

Hakuna ubishi kwamba vijana watatu wa Kahama, kwa kupatikana na hatia ya kumuua Masumbuko, walivunja haki za binadamu. Bali “haki za binadamu” haziwekwi na watu; zipo na zinahusu kila mmoja.

Watawala, sheria na hata Katiba za nchi, haziweki haki za binadamu. Ngazi zote hizo hazina uwezo wa “kugawia” watu haki za binadamu. Kinachofanyika ni kwa watawala, sheria na Katiba kutambua kuwepo kwa haki hizo na kutafuta jinsi ya kuzilinda na kuziendeleza.

Kwa hiyo, hapa siyo mahali pa hoja za jino kwa jino. Hoja ni kutovunja haki za binadamu. Kutoua. Kutofanya ukatili. Kutodhalilisha.

Hoja hii inaleta maana zaidi pale tunapojadili “thamani” ya adhabu anayopewa mkosaji. Watatu wa Kahama wamepatikana na hatia. Wamevunja haki za binadamu kwa kumuua Masumbuko. Wanastahili adhabu na ikiwezekana iwe adhabu kali.

Tujiulize. Je, hukumu inayoruhusu kifo ni adhabu? Je, kifo kinaweza kuwa adhabu? Je, adhabu hufanywa na aliyekufa? Kama sababu ya kuadhibu ni kutaka mtu ajirudi na kurejea katika utu wa jamii yake je, aliyeuawa anajirudi vipi, lini na wapi?

Hizi zinaonekana hoja ndogo kwa waliovimba vichwa na vifua, kwa hasira na uchungu wa kweli wa kupoteza watoto, ndugu, jamaa, rafiki au wenzao katika tabaka au kundi tambulishi kama walivyo albino.

Bali hasira zilizokaba koo za wafiwa; chuki zilizotunisha misuli ya shingo za ndugu wa aliyeuawa; na woga uliokumba nyoyo za wahusika; vyote vinaziba mifereji ya fikra kuhusu uhai wa mtu mwingine na nafasi ya muuaji mpya.

Vijana watatu wamepatikana na hatia ya kuua. Sheria inaruhusu wauaji kuuawa. Jaji, kwa mujibu wa sheria hajakosea kutamka hukumu hiyo kwa shabaha ya kulinda sheria na kazi yake. Bali Jaji aweza kuwa anaasi “shangazi wa mtima” wake.

Majaji wengi duniani wameeleza jinsi wanavyosutwa na dhamira zao pale wanapotamka hukumu ya kifo. Wameeleza jinsi kunavyokuwa na mapambano makali “rohoni” mwao na hatimaye kuanguka na kuwa mateka wa sheria na mfumo.

Leo kuna vijana watatu wa Kahama. Wanakabiliwa na mauti na siyo adhabu. Atakayeua vijana hao ni nani kama siyo muuaji?

Kuna tofauti gani kati ya aliyeua albino kwa panga na anayeua muuaji wa albino kwa kamba ya shingoni? Haipo. Wote ni wauaji. Mmoja anakanwa na sheria na mwingine anaruhusiwa na sheria. Wote wanatoa uhai wa watu wenye thamani ileile.

Ninaelewa ugumu wa wafiwa kuzingatia hoja hii haraka. Lakini malezi ya jamii hayawezi kwenda kwa misingi ya walioko madarakani kujipa fursa ya kuua na kujikinga na sheria walizotunga wenyewe.

Niliishawahi kuuliza katika safu hii wakati wa kujadili somo hilihili: “Kama serikali inaua, nani ataua serikali – ambayo sasa ni muuaji?” Sikupewa majibu.

Kuna haja ya kufikiri upya kuhusu sheria inayoruhusu kunyonga watu. Kunyonga ni kuangamiza maisha; siyo adhabu ya kurejesha mtu kwenye mstari wa maandili na utu wa wote.

Kunyonga ni kunyima aliyepatikana na hatia fursa ya mabadiliko katika maisha. Ni mabadiliko haya ambayo huweza kuwa mfano mkuu kwa jamii na kufanya watu wengi kukiri udhaifu wao na kuwa wanyoofu maishani.

Kuua hakuleti nafuu kwa mfiwa. Hakuna mafao kwa serikali. Hakuleti faida kwa jamii. Kunaendeleza vilio. Kunasimika hasira na chuki mpya. Kunafanya jamii ishindwe kuelewa nani anaweza kuikinga na ukatili huu.

Sheria zinazoruhusu mauaji kwa njia ya kunyonga ni za kuviziana; za kumalizana na mara nyingi, kama siyo mara zote, zinawaelemea wa tabaka la chini katika jamii. “Wakubwa” wana kila njia ya kuzipinda na hata kuzikatakata.

Sheria za kunyonga zinafanya jamii ianze kuona kuwa maisha hayana thamani. Zinafundisha usugu na kutothamini uhai binafsi na ule wa mtu mwingine. Zinazaa tabia ya “nitakuua hata kama wataniua.”

Sheria zinazoruhusu mauaji zinakomaza chuki na ghadhabu na zinafuta msamaha na tabia ya kujirudi ambayo ni nguzo kuu katika kupata suluhisho na muwafaka. Zinainyang’anya jamii ujasiri wa kufunza waliopogoka na kuikosesha jukumu la kufunza vizazi na vizazi.

Adhabu ilenge kurekebisha muhusika; kumfanya ajutie tendo lake na kutamani kurejea katika utu wake wa asili. Aliyekufa hajutii makosa yake; harekebiki pia.

Natamani kuona hukumu ya kifo ikifutwa na nafasi yake kwa sasa kichukuliwa na adhabu ya kifungo cha maisha. Aliyeua akiuawa, aliyeua muuaji anakuwa amekamilisha ukoo wa wauaji.

Katika ukoo huu, mauaji hayataisha. Hayataogopwa. Hayatapingwa kwa kuwa hayatachukiwa. Natamani yaishe. Jamii ivunje kimya.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
(Makala hii itachapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili toleo la 26 Septemba 2009 chini ya safu ya SITAKI)

Saturday, September 19, 2009

NGUVU ZA UNAFIKI NA SIASA ZA NJIAPANDA



Yusuf Makamba: Mara joto, mara baridi…

Na Ndimara Tegambwage
SITAKI tabia ya Yusuf Makamba, Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya kuwa mara baridi, mara joto, mara vuguvugu na mara baridi, tena katika muda mfupi.

Kwa mbunge, mteule wa rais, kiongozi mkuu wa utendaji katika chama kinachopanga ikulu, kuwa na tabia ya kubadilika kila kukicha au pale kipenga kinapopulizwa; siyo ishara ya kuwa makini.

Joto lilipokuja – kwa msukumo wa chama au makundi au mtu binafsi – Makamba alifura kwa hasira na kutangaza ubabe. Alifanya hivyo baada ya vikao vya CCM vya Kamati Kuu na Halmashauri Kuu jijini Dodoma hivi karibuni.

Alimwakia spika Samuel Sitta na wajumbe wa chama chake kumkaripia, kumtishia, kumpa onyo na kutaka kumlegeza. Ni Makamba aliyesimama na kusema, “Kama siyo CCM, Samwel Sitta ahojiwe na nani?”

Ndani ya vikao vya CCM, Samwel Sitta alikuwa anakabiliwa na tuhuma nyingi zilizopelekwa kwa njia ya mjadala juu ya hali ya hewa ndani ya chama na serikali.

Kwamba spika amejitwisha jukumu lisilo lake la “kupambana na mafisadi.” Kwamba ana upendeleo – anatoa nafasi mara nyingi kwa wenye “kupinga serikali” na hata wapinzani, kuhutubia bunge kuliko wale wanaotetea chama na serikali.

Ofisa mdogo katika ofisi ya Makamba, John Chilligati, kwa ushirikiano na Makamba au kwa kutumwa na chama chake, aliwawakia wale ambao wanadaiwa kupewa muda mwingi na spika “kukemea ufisadi,” akihoji nani aliwapa wajibu huo.

Ikaja asubuhi, ikaja jioni, siku zikapita. Makamba yuleyule, wiki iliyopita, akaenda jimbo la Urambo, mkoani Tabora. Huko ndiko nyumbani kwa spika Samwel Sitta. Akachukua sura ileile ya kuumbika na kuumbuka.

Aliwaambia viongozi wa chama chake vikaoni na wananchi kwenye mkutano wa hadhara, kwamba CCM inatambua kuwa Spika Samwel Sitta anafanya “kazi yake vizuri” na hasa anafanya kazi ya chama.

Makamba wa leo siyo wa jana, wa kesho wala keshokutwa. Anaumbika na kuumbuka au kuumbuliwa. Anafura kwa hasira, lakini dakika chache zifuatazo, anatoa kicheko – cha kweli au cha unafiki.

Vyombo vya habari vimemnukuu Makamba akisema kuwa Sitta ni mbunge wao imara na kazi anayofanya bungeni ni kazi nzuri ya chama chake; na kuwataka wamuunge mkono hata katika uchaguzi ujao. Hata walokole hawafikii hatua hii.

Joto la ndani ya vikao vya CCM ndilo lilifanya Makamba awe mkali, jeuri na aongee kwa kujiamini. Wajumbe walioongea kwa kukandia Sitta, tena mbele ya mwenyekiti wa chama na rais wa Jamhuri, Jakaya Kikwete, huku wakipendekeza afukuzwe uanachama, ndio walikuwa msukumo wa Makamba.

Msukumo mwingine ulikuwa “Kamati ya Mwinyi” iliyoundwa rasmi kuchunguza “msuguano” kati na baina ya spika, bunge na serikali. Kamati iliundwa katika kikao cha Halmashauri Kuu.

Kwa maandalizi ya vikao hivyo vya Dodoma; kwa taarifa kwamba wajumbe kutoka Zanzibar walikuwa wameandaliwa rasmi kumkabili Sitta na hivyo ndivyo ilivyojitokeza; na kwa wingi wa wajumbe walioongea kutaka “Sitta amalizwe,” hakika Makamba asingekuwa na mtu wa kutembelea Urambo anayeitwa Samwel Sitta – spika.

Tabia ya Makamba ya kubadilika haraka – kutoka joto sana hadi baridi na huenda kesho atakuwa vuguvugu – huenda ndiyo inamfaa yeyote anayetaka kuwa katibu mkuu wa CCM ya sasa.

Akiombwa na kundi moja linalopingana na lingine kuwa aandae mazingira ya uhasama na mashambulizi, basi afanye hivyo. Akiambiwa sasa apoe, ananyamaza kama aliyekwenda safari.

Lakini akitekenywa kwamba amwakie fulani, kwa sababu zozote zile, atafanya hivyo. Vilevile akiambiwa kurejesha amani, atawaangukia aliokorofishana nao na kukumbuka walivyopeana pipi wakiwa darasa la pili.

Makamba anakuwa mkuu wa maabara isiyofuzu – CCM. Hawaamini kuwa waliishamaliza utafiti juu ya utengenezaji hewa ya oksijeni. Kwao utafiti ni utafiti tu usioisha hata kama waliishapata matokeo; ili mradi waonekana wako kazini, wanalipwa na wanatumiwa na waajiri wao.

Safari ya Makamba nyumbani kwa Sitta imekuja baada ya Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara, Pius Msekwa kubanwa na wananchi na balozi za nchi za kigeni zilizoko Dar es Salaam, kuhusu vitisho alivyofanyiwa spika na nia mbaya ya kumdhoofisha.

Kama kwamba Rais Kikwete alijua kuwa hali hiyo ingedhoofisha uhusiano kati ya serikali yake na wananchi, asasi za kijamii zinazopigania haki za binadamu na hata nchi wahisani, akatafuta jinsi ya kulegeza msimamo kwa kutoa “maelezo ya nyongeza” kwa yale yaliyotolewa na Makamba na Chilligati.

Rais Kikwete alisema wiki iliyopita, katika kujibu “maswali ya wananchi ya papo kwa papo” katika televisheni kwamba, halmashauri kuu iliyokemea wabunge “wenye msimamo mkali,” ililenga tu kuleta nidhamu na siyo kuwatishia.

Alisema wabunge walikuwa wanatakiwa kujadili mambo ya chama chao ndani ya vikao vya chama na siyo hadharani; na kwamba kwa hatua hiyo, chama kamwe hakikulenga kuwanyamazisha.

Kama kauli ya Kikwete ilikuwa ndiyo kauli ya halmashauri kuu ya CCM, basi Makamba na Chilligati hawajui kuripoti na kuwasilisha taarifa za chama chao kwa wananchama, wananchi na dunia.

Lakini kama taarifa zao, na hasa Makamba, ziliwakilisha yaliyojiri ndani ya vikao vya chama chake; na kauli za Kikwete ni tofauti na zilizolenga kupoza wanachama na kurejesha “amani” ndani ya CCM, basi kuna mgogoro ndani ya chama hiki.

Bali kinacholeta nuru juu ya yaliyotendeka ndani ya vikao na iwapo yalilengwa; ni kwamba hakuna hatua yoyote waliyochukuliwa Makamba na Chilligati kwa kutoa taarifa tofauti na zile za chama na tofauti na kauli za mkuu wa kaya.

Dunia ya nje isiyotafiti wala kuchokonoa, yaweza kuamini kuwa aliyosema Kikwete ni sahihi na yale ya Makamba na Chilligati ni kauli binafsi au taarifa za chama zilizotiwa hamila. Kumbe sivyo.

Makamba ni mchekeshaji wa kweli. Aweza kutumika kwenye sherehe na kwenye misiba. Si yumo katika vikao vya kumsulubu Sitta? Leo kapewa ngwe ya kumpaka mafuta kwa mgongo wa chupa.

Hadithi zatufundisha: Lini sungura anakuwa rafiki wa simba? Ni pale tu simba anapokuwa ameshiba au anapokuwa na swala upandeni. Bali ni urafiki wa muda.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
(Makala hii haikuchapishwa katika toleo la Tanzania Daima Jumapili, 20 Septemba 2009 katika safu ya SITAKI kwa sababu ambazo mhariri aliniambia kwa simu kuwa ni "matatizo ya kiufundi.) Badala yake makala ilichapishwa katika gazeti la MwanaHALISI toleo la Jumatano 23 Septemba 2009).

Sunday, September 13, 2009

DC AKISHINDWA SERIKALI IMESHINDWA

DC Tarime anapokiri kushindwa

Na Ndimara Tegambwage


SITAKI kauli na mipango ya mkuu wa wilaya (DC) ya Tarime, Frank Uhahula aliyoitoa hivi karibuni. Inatishia maisha ya wananchi.

Gazeti hili lilichapisha habari kuwa mkuu huyo ametishia “kufuta shughuli za ufugaji wa ng’ombe mkoani Mara, endapo wenyeji wa mkoa huo wataendelea kuibiana mifugo, hali ambayo inachangia vitendo vya mauaji.”

Kwa kuwa hakuna taarifa zozote za kukanusha taarifa hiyo tangu ichapishwe, 7 Septemba mwaka huu, inaweza kuchukuliwa kuwa ni kweli alitoa kauli hiyo.

Katika hali ya kawaida, kauli hiyo haiwezi kutolewa na mkuu wa wilaya aliyepata mafunzo ya uongozi; aliyekulia katika mfumo wa uongozi au mwenye maarifa juu ya taaluma ya uongozi.

Ni muhimu kurudia, kurudia na kurudia kusema kuwa uongozi ni menejimenti na menejimenti haiji tu kwa kuteuliwa kuwa mkuu wa mahali fulani.

Ama umesomea shuleni, umepata mafunzo kwa njia mbalimbali, umeelekezwa ukiwa kazini na umetenda kwa kutumia misingi husika.

Katika baadhi ya nchi, ukuu wa wilaya na mkoa ni vyeo vinavyojazwa na watumishi ambao wamefikia ngazi fulani katika mpangilio wa madaraka serikalini. Hachomolewi mtu kutoka popote kule na kufanywa DC.

Mahali pengine vyeo hivi hupewa wale waliopata mafunzo na wenye maarifa ya uongozi na wamethibitika kuelewa jinsi ya kutumia taaluma hiyo ya menejimenti ya watu na raslimali zao.

Haikutarajiwa basi, kusikia mkuu wa wilaya ya Tarime akitishia “kufuta ufugaji” ng’ombe mkoani Mara. Amekerwa sana? Hana njia ya kukabili tatizo la wizi? Ameshindwa kazi? Anakiri kwa niaba ya serikali kwamba utawala wa nchi umeshindwa kudhibiti wizi wa mifugo Tarime?

Kama mkuu wa wilaya ameshindwa kazi, si amwambie aliyemteua, tena kimyakimya, “Mzee hapa sipawezi,” ili atafutiwe pengine au aachwe njiapanda? Si kauli ya DC inadhalilisha hata serikali nzima? Na serikali ikishindwa, wananchi wafanyeje?

Hata hiyo kauli ya DC ilitolewa mahali pabaya. Ni pale alipokuwa anazindua kikundi cha ulinzi shirikishi wa wananchi na polisi katika kijiji cha Kitenga. Je, kwa kauli hiyo alitaka kusema kuwa hata uzinduzi wa ulinzi aliokuwa anafanya haukuwa wa maana yoyote?

Kauli ya DC iligongana na kauli ya Polisi Jamii wa Mkoa Maalum wa Tarime-Rorya aliyesema ndani ya polisi kuna askari “wachache” wanaosaidiana na wezi wa mifugo. Alitaka wafichuliwe.

Kumbe tatizo siyo mifugo. Tatizo siyo wafugaji. Tatizo ni wizi. Wizi ni uhalifu endelevu unaoweza kukabiliwa na njia endelevu. Kama hakuna njia hizo endelevu, basi akili za watawala zitakwama; watalia, watalalamika na kujawa ghadhabu; watashindwa kazi.

Kwa kauli ya DC, ambayo ni kauli ya serikali, wizi wa ng’ombe ukiendelea, serikali “itafuta” ufugaji huo. Wizi wa mbuzi ukianza na kupanuka, serikali itafuta ufugaji wa mbuzi. Wizi wa kondoo ukianza na kuenea, serikali itafuta ufugaji wa kondoo; na wizi wa kuku ukishamiri, serikali itafuta ufugaji wa kuku!

Fanya mwendelezo hapa. Kila kinachoshindikana kipigwe marufuku. Watu wakiibiana mno nguo, serikali ifute uvaaji nguo. Wakiibiana mno chakula, serikali ifute kilimo cha mazao ya chakula. Wakiibiana mno fedha, serikali izuie watu kuwa na fedha!

Hii ndiyo dhana ya “Uhahulism” inayotokana na fikra za Uhahula wa Tarime. Huku ndiko kukiri kushindwa.

Uhahula anapendekeza kufuta mifugo. Maana yake ni kwamba hajui uhusiano kati ya wananchi na mifugo yao. Inaonekana hajajitahidi kujifunza mazingira ya watu aliokabidhiwa kuongoza na hana ujuzi na maarifa ya kutawala.

Mifugo ni uhai wa wafugaji. Mifugo ni mali. Mifugo ni fedha. Mifugo ni benki. Mingi au michache kama ilivyo, mifugo ndio utajiri wa pili kwa wafugaji. Kwanza ni watu – ndugu na marafiki ulionao; na pli ni mifugo.

Kwa hiyo kutenganisha wafugaji na mifugo ni kuwaondolea uhai – chakula – lishe ya nyama na maziwa. Ni kuwaondolea usalama wa maisha – watakosa kinga na kimbilio pale watakapokuwa na matatizo ya kiuchumi.

Kufuta mifugo ni kupora mali za wafugaji; ni kuwaibia fedha; ni kubomoa mabenki yao; ni kuua udugu, urafiki na uwezo wa jamii wa kujilisha, kujitunza na kuweka misingi kwa jamii zao za baadaye.

Hili ndilo linadhihirisha hatari iliyopo pale viongozi wanapokuwa hawakutokana na mkondo wa ngazi za utawala; wanapokuwa wa kuotesha tu, na hasa wanapokuwa wanaamini kuwa kila kitu huenda kwa amri na siyo fikra na ushawishi.

Kinachosikitisha zaidi ni kwamba mkutano alikohutubia DC haukuwa wa wezi wa ng’ombe. Ulikuwa wa wafugaji na wananchi wengine, hata kama ndani yake kulikuwa na watuhumiwa wawili au watatu.

Kwa hiyo vitisho vya DC, kama vililenga wezi, basi havikuwafikia au viliwachochea. Kilichofika kwa wengi ni hatua za uonevu ambazo serikali wilayani ilikuwa inaahidi kwa watu na mali zao. Huu siyo uongozi. Siyo utawala.

Kuna haja ya kurudia kuuliza: Serikali ikishindwa kazi ya ulinzi wa watu na mali zao, na ikakiri hivyo, wananchi wafanyeje? Labda wananchi na viongozi wao wa kweli wanajua. Tuwasikilize.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
(Makala hii imechapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili, toleo ya 13 Septemba 2009)

Saturday, September 5, 2009

UJANGILI ULIORUHUSIWA NA SERIKALI

Uwindaji wa leseni ni ‘ujangili’ pia
• Maliasili ya Tanzania, dunia itaisha

WAFUGAJI wanaofukuzwa kwenye makazi yao katika mbuga wana mengi ya kusema. Wengi hawana elimu ya darasani lakini ni wajuzi wa mazingira yao na wepesi wa kutambua mabadiliko. Hapa wanasema wanachoona ambacho serikali inaweza kufuatilia ili kuokoa maliasili wanyamapori.


Na Ndimara Tegambwage

WAMECHOMEWA makazi. Wakapigwa na wengine kuswekwa rumande kwa madai kuwa wamekaidi amri ya kuhama mbuga ambamo wameishi kwa miaka nendarudi. Lakini bado wana uchungu na nchi yao.

Wana uchungu na maliasili za Tanzania. Wanapendekeza kuwa uwindaji katika mbuga ungesimamishwa ili kuruhusu wanyamapori kuongezeka na kurejesha utajiri mkubwa wa taifa na dunia.

Wafugaji wa ng’ombe, mbuzi na kondoo ambao wameishi kwa kuingiliana sana na wanyamapori, wanasema serikali ingeweka sheria kali, kama hazipo, au kusimamia zilizopo ili kuokoa maisha ya wanyamapori.

“Sisi ndio walinzi wa wanyama hawa, usione wanatufukuza. Tungewabughudhi wasingekuwa hapa. Wala hatuwali. Sisi tunakula mifugo yetu. Lakini kwa mtindo wa sasa, wanyama watatoweka,” anaeleza mkazi wa kijiji cha Ololosokwan.

Kuna masimulizi mengi na marefu juu ya wanyamapori wanavyouawa kwa wingi. Mwanaume wa umri wa kati kijijini hapa anasema, “Kwa mfano, simba ni simba tu. Hawana mbadala. Kama simba watamalizika, hakuna tunachoweza kuona katika nafasi yake kiitwacho simba.”

“Tumeona mengi humu Loliondo. Hata wenzetu kutoka mbali wamekuja na kusimulia kuwa hali ni hiyohiyo. Wawindaji kutoka nje ya nchi wanaua hata watoto wa simba,” anaeleza.

Kijana wa umri upatao miaka 25 wa kijiji cha Magaiduru-Lorien anadakia na kusema, “Nimewahi kuona watalii wamebeba watoto wa simba na puma ndani ya gari lao.”

Kijana mwingine anaingilia kati, “Unasema simba tu? Mwaka jana wanamgambo wanaohudumia jumba la mfalme wa Umoja wa Nchi za Kiarabu (UAE) pale kilimani, walipita wakitangaza kuwa atakayepata chatu akiwa hai atalipwa shilingi milioni moja (1,000,000/=).”

Swali: Kwa hiyo na wewe uliingia vichakani kuwinda chatu?
Jibu: Hapana. Mimi nina shughuli zangu. Angalia ng’ombe wote hawa (kama 1,200).
Swali: Si ungemwambia mdogo wako akachangamkia hilo?
Jibu: Tuliacha wengine wanaohitaji fedha za haraka watafute.
Swali: Sasa chatu alipatikana?
Jibu: Alipatikana. Tulisikia walipatikana sita, wakubwa kwa wadogo. Waliwachukua wakiwa hai.
Swali: Kwani wewe umewahi kuona wanyama wakisafirishwa wakiwa hai?
Jibu: Si unaona uwanja wa ndege ule pale (ndani ya Loliondo)? Madege makubwa yanatua hapo hata yenye uwezo wa kubeba magari makubwa. Nendeni ukaulize maeneo yale utapewa taarifa. Hata simba na chui wachanga wanasemekana kuchukuliwa…lakini usinifanye shahidi wako.

Ni madai makubwa na mazito. Yanahitaji kuthibitishwa. Wafugaji wanasema walichoona. Huenda wanyama wanaodaiwa kuchukuliwa kutoka mbugani wakiwa hai ndio tunawakuta katika “hifadhi za wanyama” mijini (mazuu) katika baadhi ya nchi za nje.

Maelezo ya aina hii yanafanya wafugaji wakazi wa mbuga za Loliondo wachukiwe na watu kutoka nje ambao walipewa mbuga kufanyia biashara ya utalii na bila shaka baadhi ya maofisa wa maliasili wanaoshirikiana nao.

Mbuga za Loliondo ziko chini ya kampuni ya Ortelo Business Corporation (OBC) ya Umoja wa Falme za Kiarabu ambayo imekuwa ikiendesha biashara ya utalii wa uwindaji wanyama na upigaji picha kwa karibu miaka 17 sasa.

Wafugaji wanachukiwa kwa kuwa “wanasema uongo.” Kusema uongo, katika hali hii ni kusema ulichoona; kwamba wanaoitwa watalii wanafanya zaidi ya kile walichotarajiwa kufanya.

Kuna masimulizi kuwa “watalii” – ambao wananchi hapa wanapenda kuwaita “majangili wenye leseni” – wanaua hata wanyamapori ambao hawapo kwenye orodha ya kuwindwa na kuchukua hata wanyama hai.

“Uwongo” wa aina hii ni aghali. Vijana wengi wanasema wakijulikana kuwa wametoa taarifa kwa watu wa nje, huenda wakakamatwa na “kuwekwa ndani.”

“Kweli, mfano tukijulikana kuwa tuliongea nanyi kuhusu mambo haya, wanaweza kutupoteza au kututupa rumande kwa muda mrefu mpaka tukakuta mifugo yetu yote (ng’ombe 210, mbuzi 90 na kondoo 45) vimeibwa,” anaeleza kijana akitupa macho huku na kule.

“Sisi tunawajua wanyamapori. Wakiongezeka tunajua; wakipungua tunajua,” anasema Mzee Ngirimba mwenye umri wa miaka 59 kutoka kijiji cha Arash ambaye alikutwa Ololosokwan.

Bali kama ambavyo hakuna mbadala wa simba, vivyo hivyo hakuna mbadala wa swala, tembo wala digidigi.

Kwa mfano, taarifa kuhusu idadi ya wanyamapori zinaeleza kuwa swala-twiga wamepungua sana katika mbuga nyingi nchini. Tandala wadogo na tandala wakubwa – wote wamepungua kwa kiasi kikubwa.

Wanyama wengine ambao wakazi wa mbugani na baadhi ya maofisa wanyamapori wanakiri wamepungua ni digidigi wadogo ambao hutembea wawili-wawili na palahala.

Lakini wazee sita waliohojiwa juu ya wingi wa simba katika maeneo yao, walisema hata simba, chui, duma na mbwamwitu wamepungua.

“Hatuna elimu juu ya taratibu za wanyamapori na uwindaji, lakini tunajua kuwa siyo wanyama wote wanaowindwa. Lakini huku kwetu huwa tunaona wanapiga tu kila mnyama,” ameeleza mmoja wa wazee wa Olorien.

“Kwa mfano tumeona walioua twiga na siku zote tunaambiwa kuwa twiga siyo mnyama wa kuwinda,” anaeleza.

Anasema amesikia kuwa hata simba, duma na chui hawastahili kuwindwa lakini wameona wawindaji wa kitalii wakiburuta mizoga ya wanyama hao.

Masimulizi juu ya uwindaji shelabela – unaoua wanyama wakubwa na “watoto wao;” ukamataji wanyama hai na usafirishaji wake nchi za nje, ni mambo ambayo wafugaji katika mbuga wanasimulia kwa uwazi.

Wauaji wakuu wa maliasili wanyamapori ni wale wenye leseni za kuwinda. Wanadaiwa kuua wanyama wengi kuliko idadi ya waliopangiwa na wanaua hata wale wasio kwenye orodha ya kuwindwa, wenye mimba na wachanga.

Wawindaji wa aina hii basi, hata kama wana leseni, ni wahujumu ambao tunaweza kukubaliana na wananchi wa eneo hili wanaowaita “majangili wenye leseni.”

Uwindaji wa aina hii unateketeza wanyamapori; unaua vizazi vya maliasili hii adimu duniani. Walinzi wa mbuga na wanyama waliomo wana mapendekezo, kama anavyosema mmojawao katikamahojiano:

Swali: Kwa hiyo unaona afadhali utalii wa kuwinda wanyamapori upigwe marufuku?
Jibu: Wewe! Nani atakubali hilo? Hawa wazungu na waarabu wanaokuja wanataka kujiburudisha na serikali yetu inataka fedha. Unadhani nani atakubali hilo?
Swali: Kwa hiyo waendelee kuwinda?
Jibu: Hapana. Sisi tunaona wakisimamisha uwindaji kwa miaka kumi (10) wanyama watazaana na kuongezeka. Kuanzia hapo uwekwe utaratibu wa kuzuia kuangamiza wanyamapori.
Swali: Unadhani uuaji wanyama bila kujali nani ana mimba, nani ana umri mdogo na nani hastahili kuwindwa unatokana na nini?
Jibu: Sisi hayo hatuyajui. Hatuna majibu. Tunaona ni ukatili tu. Labda pia hawana mtu wa kuwaongoza ili kuwaambia ‘huyu msiue.’ Lakini tunaambiwa kuna masharti wanayopewa kabla ya kuingia kwenye mbuga kuwinda.
Swali: Na hili la kubeba wanyamya hai?
Jibu: Kwanza hilo hatukulikubali haraka. Tulidhani vijana wanasema hovyo. Jinsi siku zinavyokwenda ndipo tukapata ukweli. Inaonekana hakuna usimamizi. Hilo halipo hapa Loliondo peke yake. Tunasikia hata Serengeti katika eneo la Gumeti (Grumet).

Mzee huyu anasema hawajui iwapo wawindaji wa kitalii wanaruhusiwa kubeba nyama na kupeleka kwao

Wafugaji ndio wamekuwa walinzi wa mbuga. Wanyama wote waliomo wamekusanyika, kuzaana na kuishi bila bughudha kwa kuwa wafugaji hawakuwawinda.

Dunia nzima inayokusanyika katika mbuga za Tanzania inakuja kushuhudia, bahati mbaya bila kujua, utashi, ujasiri na mapenzi ya wafugaji kwa wanyamapori. Bali leo hii wafugaji na mifugo yao wanaswagwa nje ya makazi yao na mali zao kuharibiwa.

Laiti wanyama wangekuwa na uwezo wa kutambua kuwa marafiki wao wa karibu, wa miaka mingi, wanatendewa ukatili. Wangepinga kwa maandamano na kauli kali.

Tetesi hizi ni muhimu kwa serikali na dunia nzima. Wanaopenda wanyama na mapato kutokana na wanyamapori, sharti wachukue baadhi ya hatua zifuatazo:

Kwanza, kufanya uchunguzi juu ya madai ya walinzi wa miaka mingi wa wanyamapori. Hawa ni wafugaji ambao wamekuwa karibu na wanyama kiasi cha kujua hata tabia zao.

Pili, uchunguzi uongoze katika kuchukua hatua madhubuti za kusimamisha uwindaji wa kiharamia katika mbuga zote nchini. Hii ni kuzuia uteketezaji maliasili ya dunia.

Hatua hizi zitazuia pia ukamataji na usafirishaji wanyama hai nchi za nje, kama utakuwa umegundulika na kuthibitika; na au kusitisha uwindaji kwa kipindi kirefu ili kuruhusu wanyamapori kuongezeka.

Tatu, kuangalia jinsi ya kusimamisha uwindaji wa aina fulani ya wanyamapori na kuweka usimamizi wa kutosha wa mamlaka ya wanyamapori katika hatua zote za uwindaji.

Nne, kubadili masharti ya miliki au ukodishaji wa mbuga ili kuondoa ukiritimba wa wamilikishwaji au wenye leseni.

Wamiliki au wenye leseni za kukodi wanapokuwa na mamlaka kama yale ya nchi, waweza kufanya wapendalo ikiwa ni pamoja na kuua kishelabela na hata kuhamishia wanyama nchi za nje.

Tano, kuacha kuchoma makazi ya wafugaji na kusitisha hatua za sasa za kuwafukuza, wao na mifugo yao, kutoka kwenye mbuga. Badala yake watengewe maeneo ya kilimo na mifugo pale walipo.

Mashamba madogo ya mahindi ya wafugaji, chini ya kilima ambacho kilele chake ndiko liliko “kasri” la mfalme wa UAE, yanaonyesha mabadiliko muwafaka katika maisha ya wafugaji.

Wafugaji hawa, wanaoanza kuwa wakulima pia, wanaendelea kuwa walinzi wa wanyamapori na chanzo cha taarifa muhimu za kunusuru maliasili ya Tanzania na dunia. Huu nao ni ulinzi wa aina yake. Serikali yaweza kuanzia hapa.

Wako wapi akina Luteni mstaafu, mfugaji na mkulima, Lepillal ole Molloimet, ili wajiunge na jumuia ya kimataifa katika kusemea wasio na sauti na kupigania maliasili za taifa na dunia?

0713 614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com

(MAKALA HII ILICHAPISHWA KATIKA GAZETI LA MwanaHALISI TOLEO LA 19 AGOSTI 2009)

ASKOFU KAKOBE ATAMANI UDIKITETA



KUZIMA MAWAZO KWAWEZA KULETA VURUGU;
KUKUBALI YATOKE KWAWEZA KUZIEPUSHA


Na Ndimara Tegambwage

SITAKI Askofu Zakaria Kakobe wa kanisa la Full Gospel Bible Fellowship (FGBF) ajiingize katika mjadala ambao hauwezi na hautaleta manufaa kwa kanisa wala waumini wake.

Mapema wiki iliyopita alinukuliwa akiwaambia waandishi wa habari kuwa Rais Jakaya Kikwete amezidi kwa upole kwa vile hajakemea kanisa Katoliki kwa kutoa “Waraka” wa elimu ya uraia kwa wananchi kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.

Kakobe alisema pia rais amekuwa mpole mno kwa kutokemea Shura ya Maimamu kwa kutoa “Muongozo” wa waislamu ambao maimamu wanasema unalenga kumwelimisha mwislamu juu ya nafasi yake katika siasa za nchi hii.

Askofu wa kanisa la FGBF anasema maandishi haya yanaweza kuleta utata mkubwa na hata mifarakano katika jamii. Alimpongeza Kingunge Ngombale-Mwiru, mbunge mteule wa rais, kwa kukemea Waraka na kufikia hatua ya kusema “wauondoe” na kwamba Ngombale-Mwiru “aliona mbali.”

Lakini ukali wa rais unahitajika kwa lipi hapa? Katoliki wanasihi wananchi kujadili aina ya viongozi wanaowahitaji na ndio hao wawapigie kura. Wametoa andishi la kusaidia kuendesha mijadala miongoni mwa waamini na jamii kwa jumla.

Shura ya Maimamu imetoa andishi la kukumbushia lawama zao kwa utawala; malalamiko kuhusu kubaguliwa; nafasi ya mwislamu katika siasa za awali katika kutafuta uhuru na kuhimiza waislamu kuwachagua waislamu au wale wanaoona wataendeleza maslahi yao.

Kwanza, tujadili ukali wa rais. Huyu ni mtawala mkuu wa nchi. Ametokana na mfumo wa utawala ambao analazimika kuulinda, kuutetea na kuuendeleza. Ni mfumo huo ambao unatoa viongozi wanaolalamikiwa kwa kutokuwa makini.

Rais awe na ukali upi zaidi; wa kiasi gani kuliko huu alionao sasa; anaoutumia na kuusimamia na unaosababisha kupatikana kwa viongozi wanaolalamikiwa?

Askofu Kakobe anasema Rais Kikwete anatembeza tabasamu tu. Lakini tabasamu la rais ni ishara ya utulivu wake moyoni; kwamba hana presha; kila kitu kinakwenda kama anavyotaka na kwa mujibu wa mfumo anaosimamia.

Laiti Kakombe angejua kuwa mfumo wa jana na leo, ambao rais anasimamia, ni wa kibaguzi; unanyima fursa ya kuwa kiongozi wa siasa mpaka uwe mwanachama wa chama cha siasa.

Ni mfumo katili unaokufungia katika “mahabusu” ya chama hichochicho kiasi kwamba ukihama unakuwa umejifukuza kazi uliyopewa na umma kwa njia ya sanduku la kura.

Vilevile ukiwa na maoni tofauti, hata yanayolenga kuimarisha chama chako, kama yanaelemea baadhi ya wazito ndani ya vikao vya juu vya chama hicho kilichoko ikulu, basi utakuwa unajipalia mkaa; tena wa moto. Utawindwa. Unaweza kuuawa kisiasa. Huo ndio mfumo ambao rais anasimamia huku akiwa anatabasamu.

Katika mfumo huu ndimo aliyeiba mabilioni ya shilingi anasamehewa kwa kurejesha kiasi, lakini aliyeiba chungwa anafungwa miaka mitatu. Ubaguzi mzito.

Ni humuhumu ambamo kuna makubwa ya kukamua utajiri wa taifa hili. Mikataba ya kinyonyaji; wizi wa waziwazi kabisa wa fedha za umma; uporaji raslimali hata wanyama, magogo na mchanga.

Yote haya, hata kama hayakuanzishwa na viongozi wa utawala wa sasa, yako chini ya utawala wa rais anayeambiwa na Kakobe kuwa anunie barua ya kanisa kwa waamini na malalamiko ya waslamu.

Pili, katika mfumo huu ndimo kuna waandishi wa Waraka na Muongozo. Machapisho haya yanaeleza ama jinsi ya kujikwamua kutoka katika mazingira tuliyomo kwa kuwa na viongozi wakweli na thabiti; au yanawasilisha maoni ya makundi na watu binafsi katika mustakabali wa siasa za nchi yao.

Sasa Kakobe anataka rais awe mkali katika kuzuia maoni ya makundi, asasi na taasisi za wananchi? Akifanya hivyo atajuaje maoni yao? Atajuaje kuwa anapingwa katika hatua hii au ile? Atajuaje malalamiko na lawama ambazo serikali yake inabebeshwa?

Askofu Kakobe atakuwa ameona kuwa baadhi ya madhehebu duniani yameingia katika mageuzi ya fikra. Yanakiri kuwa hayawezi kuhudumia “roho za waamini na na waumini bila kufikiria hali zao kidunia.”

Roho za wafuasi wa madhehebu hayo zinakaa katika makasha yaitwayo “miili.” Kama miili itakuwa imedhoofika kwa njaa, maradhi na ujinga, hata kile wanachohubiriwa ili kukidhi matakwa ya roho hakitaingia.

Kunahitajika maandalizi ya roho. Haya yanaanza kwa kutambua kuwa kuna mwili. Kwamba mtu yupo; tunamwona na anashikika; siyo wa kufikirika. Kwamba ana mahitaji ambayo sharti ayapate ili aweze kuwa na uwezo wa kupokea mahubiri.

Maandishi makuu kwamba binadamu haishi kwa mkate (chakula) peke yake yana makali ya pili; kwamba binadamu haishi kwa kuhubiriwa tu, bali kwa chakula pia na mahitaji mengine ya mwili.

Ukamilifu wa mwili unahitajika ili kupata ukamilifu wa roho. Mbingu siyo kwa watu masikini na hohehahe peke yao, bali hata matajiri kwa njia ya halali ambao wamepondeka mitima.

Hii ndiyo maana hata kama rais hataki Waraka au Muongozo, sharti ajitahidi kuvisoma, kupata maoni ya wengine, kuyachambua na hata kuyatumia kutekeleza yale ambayo maandishi yanasema hata kulalamikia.

Bali kuna tabia ya serikali kuhusudu ukimya wa watu, ujinga na umasikini wao. Hii ni mitaji mikubwa ya serikali nyingi duniani. Vilevile ni mitaji mikuu ya baadhi ya madhehebu ambayo yanataka “kupakia” wananchi mahubiri kama anayepakia gunia.

Wanaohubiriwa ni watu wenye akili timamu na wana uwezo wa kufikiri. Wakipata fursa ya kujadili na kufanya maamuzi, wanaitumia vilivyo kuliko kutaka rais awanunie, awazibe mdomo na hivyo kuziba akili zao ili wasifikiri. Hapa Kakobe amekwama.

Fikra za Kakobe zinafanana na za serikali ya Zanzibar ambayo juzi ilitangaza kupiga marufuku Waraka na Muongozo. Bali hii siyo mara ya kwanza kwa serikali ya Zanzibar kufanya viroja.

Kuna wakati ilizuia ufundishaji wa historia (na fasihi?) mashuleni kwa madai kuwa historia inaibua chuki na uhasama. Haya ni maamuzi ya woga, ya kidikiteta; yenye shababa ya kudhibiti akili za watu na utashi wao.

Mbona nchi hii inahitaji nyaraka nyingi tu zenye maoni mbalimbali, tena ya mirengo tofauti. Zinaweka wazi maoni ya waandishi na wananchi. Zinasaidia watawala kuona walikofika au walikoshindwa kufika.

Kuziba maoni ni kujifungia katika kiza cha ujinga na ubabe wa kidikiteta. Ni kuhalalisha juhudi za wananchi, kupitia asasi mbalimbali, kuandaa mikakati halali ya kuondoa watawala madarakani.

Hata katika ukimya wa uzao wa udikiteta, mawasiliano hupenya na mikakati huundwa. Kipi bora: Kupata maoni ya wananchi au kusubiri hasira zao zijae vifuani na utokee mlipuko?

0713 614872
ndimara@yahoo.com

(Makala hii itachapishwa katika safu ya SITAKI ya gazeti la Tanzania Daima Jumapili toleo la 6 Septemba 2009)

Saturday, August 22, 2009

MAANDALIZI YA VURUGU UNGUJA NA PEMBA




Mategemeo, subira bila mafao Pemba


Na Ndimara Tegambwage

SITAKI mtu mzima, nyumbani kwake na familia yake, aambiwe na mgeni jinsi ya kuvaa vizuri, kulea watoto, kuweka nyumba yake katika hali ya usafi, kutafuna polepole na kutoacha mdomo wazi wakati anapopiga miayo.

Mtu mzima atang’aka na kuuliza iwapo ni wewe umekuwa ukimwelekeza kwa miaka yote hadi kufikia umri huu wa miaka 50. Atakushangaa. Aweza kukujibu kwa hamaki na hasira.

Ndivyo ilivyokuwa mwishoni mwa wiki. Marafiki wa serikali za Muungano wa Tanzania na Baraza la Mapinduzi Zanzibar (BMZ), waliona serikali hizi zinataka kupiga miayo bila kuweka kiganja mdomoni. Wakazibonyeza: Tahadhari!

Mabalozi wa nchi za Jumuiya ya Ulaya, Marekani, Japan na Canada wamezitaka serikali za Muungano na BMZ kuwa makini na demokrasi. Hii inafuatia hatua ya kusimamisha zoezi la kuhakiki daftari la wapigakura kisiwani Pemba, wiki mbili zilizopita, baada ya milipuko miwili ya mabomu katika makazi ya wananchi.

Katiba ya Zanzibar inazingatia kuwa kila raia ana haki ya kupiga na kupigiwa kura. Vigezo vya raia vipo. Lakini sheria ya uchaguzi inaongeza matakwa mengine, kuwa kila anayetaka kujiandikisha kupiga kura sharti awe na hati ya ukazi Zanzibar.

Kwa wiki mbili sasa kumekuwepo migongano kisiwani Pemba. Siyo kwamba wote wanapinga kuwepo matakwa ya hati ya ukazi, bali hata wenye hati wanadai kuwa wamekuwa hawaandikishwi au kuhakikiwa.

Ukazi umekuwa ukazi. Hivi kitambulisho kuwa ulipiga kura uchaguzi uliopita hakitoshi? Hivi kuwa na kitambulisho cha uraia kwa misingi ya ulipozaliwa, kukulia na bado unaishi hapo hakutoshi? Hivi ilikuwa lazima vitambulisho vya ukazi vitakiwe hivi sasa wakati wa uhakiki wa daftari; kwa nini kazi hiyo haikufanywa mapema?

Tayari kuna madai ya wananchi kwamba wamekwenda kwenye vituo wakiwa na hati ya ukazi, hati ya kupigia kura uchaguzi uliopita na vyeti vya kuzaliwa, lakini wakakataliwa kuhakikiwa. Hapa ndipo penye utata.

Madai mengine ni kwamba kuna waliokwenda vituoni, bila hati ya ukazi, bila hati ya kuzaliwa, bila hati ya kupiga kura katika uchaguzi wowote uliopita, lakini wakapokewa na kuhakikiwa. Wananchi wanajiuliza: Huu ni mradi maalum wa serikali, upendeleo maalum na wa makusudi au ngekewa?

Kwa hiyo, kabla serikali haijasimamisha uhakiki katika daftari la kupiga kura, tayari kulikuwa na makundi hapa na pale; yakijadili hali hii. Utata unazidi inapokuwa Pemba ni ngome ya chama kikuu cha upinzani Visiwani – Chama cha Wananchi (CUF).

Kwa kuzingatia ushindi wa asilimia 100 wa CUF katika uchaguzi mkuu uliopita kisiwani Pemba, kila sehemu ya kisiwa hicho ni ngome ya chama hicho. Hatua yoyote ile basi, ya kuweka taratibu ngumu au zenye utata katika kuhakiki majina ya wapigakura, itafikiriwa kuwa inalenga kuhujumu CUF.

Katika mazingira ambamo hakuna maelezo ya serikali yanayoeleweka juu ya chanzo cha milipuko ya mabomu; na kutokana na milipuko hiyo kuwa ndani ya ngome ya chama cha upinzani, tayari kuna madai kuwa milipuko ililenga kutishia wapigakura wa upande wa upinzani.

Kwa kuwa milipuko ya mabomu imefanya watu watawanyike na kukimbilia mafichoni; yawezekana wengi wasirudi kujiandikisha kupiga kura. Inawezekana wengine wakaja wakati wa kujiandikisha umeisha au wakachukia na kukata tamaa kwa kuwa siasa imeingiliwa na tishio kwa maisha yao.

Yote haya yakifanyika, haitakuwa kwa manufaa ya chama kikuu cha upinzani au hata vyama vidogo. Yaweza kuwa faida kuu kwa chama kilichoko ikulu ya Zanzibar. Kwa ufupi, inaweza kueleweka kuwa kura za wananchi tayari zimepigwa mabomu.

Katikati ya hali hii mabalozi wa Ulaya, Marekani, Canada na Japan wamesema kuwa hawafurahishwwi na hali kama ilivyo Kisiwani Pemba. Hilo tu, kwamba “Ndugu yangu, ziba kidogo mdomo wakati wa kupiga miayo.”

Kauli ya mabalozi tayari imeleta kizaazaa. Serikali ya Muungano imejibu kwa kusema iliishawaonya mabalozi wasiingilie mambo ya ndani ya nchi; huku Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ikisema mabalozi wamevuka mpaka.

Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UV-CCM) nao umekuja juu, mwenyekiti wake Hamad Masauni Yusuf Masauni akisema kuwa Tanzania iliishatoka kwenye ukoloni na kwamba “mabalozi wafanye kazi zilizowaleta nchini.”

Ni kauli kali zisizojibu hoja ya mikingamo katika uhakiki wa daftari la wapigakura kisiwani Pemba. Ni kali lakini ambazo sharti zitolewe ili kujikakamua ingawa wote waliosema wanajua kuwa mataifa hayo ni wabia wa serikali, tena kwa muda mrefu.

Vyovyote itakavyokuwa, tayari zoezi la kupiga kura katika uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka huu na uchaguzi mkuu mwaka kesho, limeingia doa. Kwa mtindo huu, inawezekana madoa mengi yataingia hata kabla siku ya kudondosha karatasi katika sanduku la kura.

Bali jambo moja ni muhimu hapa. Serikali, pamoja na ukali wake na kauli nyingine ambazo zinaweza kuwa zinakiuka itifaki, zinaelewana vema na wafadhili. Ukiangalia kwa undani utaona vema kwamba wanasikika kupingana lakini hawatupani.

Kinachofanyika ni kutaka kuonekana kuwa waliona jambo likifanyika; walihisi siyo sahihi; walilitolea kauli kwamba hawakufurahishwa; lakini mambo yanakwenda kama wanaoyafanya wanavyopenda. Hiyo ndiyo “itifaki.” Hakuna malumbano zaidi wala kukabana shingo.

Kama kuna aliyetegemea kauli za mabalozi kutikisa lolote katika mazingira ya sasa Pemba na huenda Unguja na Bara, anashauriwa avute pumzi. Kile ambacho mataifa haya wabia wa serikali wanaonekana wanaweza kufanya, huwa hakifanywi au kinafanywa kwa njia isiyofikia kubadilisha maamuzi.

Kwani ni mataifa haya ambayo utasikia yamekwishaahidi au tayari yametoa mabilioni ya shilingi kwa ajili ya shughuli za uchaguzi nchini – katika hali yoyote ile ambamo utakuwa umeandaliwa na watawala. Hatimaye watatangaza uchaguzi kuwa huru na wa haki.

Imekuwa hivyo siku zote. Itakuwa hivyo mwaka huu na mwaka kesho. Anayetaka mabadiliko katika msimamo wa mataifa ya nje kuhusu suala hili, atasubiri sana. Na kunakucha, kunakuchwa.

Sharti nguvu ya mabadiliko itoke kwa wanaoumia pindi wanapoweka mguu chini. Kuna mwiba. Kama unachoma, basi uondoe. Wanaoona unachechemea huenda wakadhani siku hizi una mikogo. Chukua hatua.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com
(Makala hii ilichapishwa katika Tanzania Daima Jumapili, toleo la 16 Agosti 2009)

UDIKITEA MBAYA SASA WAJA



CCM na ukandamizaji wa fikra

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI Chama Cha Mapinduzi (CCM) kiwe nguzo ya nne ya dola. Nilitarajia kikae uwani, kijirembe kwa vipodozi na mavazi ya kila aina, kisubiri harusi, lakini kisikoromee nguzo yoyote ya dola.

Jijini Dodoma, kupitia kwa mjumbe wa NEC ambaye pia ni spika wa bunge la Jamhuri ya Muungano, CCM ilitoa onyo kwa wawakilishi wa wananchi kwamba wamepanua mno midomo yao; wamekijeruhi chama na serikali; sasa wachunge sauti na kauli zao.

Wabunge wameambiwa, kupitia kwa Spika Samwel Sitta kuwa wasijadili masuala yahusuyo “ufisadi” ndani ya bunge bali ndani ya vikao vya chama, kikiwemo kikao cha wabunge wa CCM. Wameamriwa. Kutofanya hivyo ni “kukiumiza” chama na serikali na kuneemesha upinzani.

Amri hizo kutoka Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, hakika zinakwenda kinyume cha matarajio. Kinyume cha utaratibu. Kinyume cha mwenendo wa “klabu” za kisiasa. Kinyume cha Katiba.

Leo CCM inakaripia spika wa bunge; eti ametoa mwanya mkubwa kwa wabunge kuisakama serikali. Eti ameruhusu serikali idhalilishwe. Eti ameacha mwanya mkubwa unaotumiwa na baadhi ya wabunge kukaripia viongozi wa chama, serikali na hata viongozi wastaafu.

CCM inataka spika wa bunge awanyamazishe wabunge. Awakemee na kuwakoromea pindi wanapokuwa wakali kwa serikali. Kwani sasa inadaiwa wabunge “wamekuwa huru kupita kiasi” na kwamba wanastahili kudhibitiwa.

Hatua ya CCM inalenga kufanya bunge kuwa kamati ya chama. Inalenga kufanya spika kuwa mhamasishaji wa shughuli za chama na serikali ndani ya bunge. Inalenga kugeuza bunge – kutoka msimamizi na mshauri wa serikali – kuwa sekretarieti ya chama na serikali.

Hiyo ndiyo maana ya kukemea spika kwa madai kuwa “ameruhusu uhuru zaidi.” CCM inataka bunge lililopigwa pasi; lile la “Chama Kushika Hatamu” – magereza ya siasa yaliyoandaliwa na Pius Msekwa kutukuza mfumo wa chama kimoja. Watawala wanataka bunge liimbalo sifa na utukufu wa chama kimoja na kiongozi mmoja mwenye fikra ngumu na “zinazodumu.”

Kupitia kwa spika aliyenyamazishwa, wabunge wanyamaze. Kupitia kwa wabunge walionyamaza, wananchi nao “wafyate mkia.” Kuwepo na sauti moja, kauli moja – ile ya klabu moja siasa – CCM na serikali yake.

Hapa ndipo panakuza ukinzani. Wananchi hawakuchagua wabunge ili wabunge waitetee serikali. Mbona serikali ina watetezi wengi bungeni? Dhana ya uwakilishi ina maana ya jicho, sikio na mdomo wa nyongeza wa wananchi; vilivyopewa jukumu la kusimamia na kushauri serikali na kutetea maslahi yao.

Kwa chama na serikali kutafuta kunyamazisha wananchi kupitia vijembe, vitisho na tuhuma dhidi ya spika, ni kutaka kuwa na taifa la mazezeta; linalosikia bila kuelewa; lisilofikiri na lisiloongea kwa kuwa limekatwa ulimi; lisilotoa hata mgumio wala mguno kwa kuwa limetumbukizwa katika woga usiomithilika.

Kesho CCM yaweza kukemea Jaji Mkuu kwa madai kuwa hukumu zake zinakuwa kali kwa viongozi wa chama, serikali na viongozi wastaafu. Jaji mkuu aweza kusutwa kwa kutoa uhuru zaidi kwa mahakimu na majaji wenzake na kwamba uhuru huo “unadhoofisha serikali.”

Ikifikia hapo, siyo tu uhuru wa kufikiri utakuwa umeingiliwa sana na hata kunyongwa; uhuru wa watu wa kuishi utakuwa mashakani. Hii ndiyo hatari kubwa zaidi. Kwa chama kilichoko ikulu kutamani taifa lililokimya, ni sawa na kutamani kutawala miti, mawe na wanyamapori. Siyo watu.

Hoja kuu inayowagawa wabunge hivi sasa na ambayo CCM na serikali hawataki kusikia wabunge wakiijadili hadharani, ni juu ya “ufisadi.” Chama hiki na serikali yake vinataka hoja hii ijadiliwe kimyakimya kwenye vikao na siyo kweupe.

Hii ni hoja inayoeleweka kwa urahisi. Inayopenya katika vichwa vya wengi. Inayojadilika. Inayoweza kuhusishwa na maisha ya kila mmoja popote alipo. Inayofanya watu wafikiri, waulize maswali na watake majibu. Inahusu uhai wao – kufa au kupona.

Kwa upande wa watawala, hoja hii ni mbaya. Inaingiza watu wengi kwenye mjadala ambao serikali haiwezi kudhibiti. Ni mjadala huu mpana unaoweza kuathiri maamuzi ya wananchi wakati wa uchaguzi wa viongozi. Unaleta vidonda mwilini mwa serikali na CCM na unatonesha daima.

Mjadala huu ungehusu vyama vya upinzani, usingetafutiwa mbinu za kuuzima. Ungekuwa kipenzi cha watawala na ungekuzwa na kuenezwa nchini kote ili penye uoza paonekane. Yote yangefanywa “kwa jina la demokrasi na uhuru wa maoni.”

Bali mjadala unapolalia watawala, basi hakuna suala la demokrasi wala haki na uhuru wa maoni. Unakuwa mchungu. Unatishia walioko kileleni. Unatishia uhalali wa utawala wa serikali. Matokeo yake, serikali inatafuta kuuzima kwa njia yoyote ile.

Vitisho vilivyoelekezwa kwa spika vinakwenda mithili ya hadhithi ya Karumakenge – maji yanatishia kuzima moto; moto unatishia kuchoma fimbo; fimbo inatishia kupiga Karumakenge; na Karumakenga anakubali kwenda shule. Bali hii ni hadithi ya kimaendeleo na endelevu.

Sasa NEC ya CCM inatishia kufukuza Spika Sitta; Sitta atishie kuadhibu wabunge; wabunge watishie kugomea wananchi wanaowatuma; na wananchi wanyamaze – kama maiti. Kunahitajika ukimya ambamo kishindo cha mende kitasikika kama tsunami. Hii si hadithi; ni hali halisi inayopingana na maendeleo. Ni ujima mchafu.

Ukame wa fikra na mijadala ambao CCM inataka utawale bunge na jamii kwa ujumla, ni msiba mkubwa kwa taifa. Hii ni sababu ya kutosha kupinga kuendelea kuwepo utawala wa serikali ya CCM.

CCM, kama vilivyo vyama vingine, ni klabu ya kisiasa – moja ya asasi za kijamii za kuragbishia raia kushiriki katika siasa na utawala wa nchi zao. Kama klabu hii imeshindwa kutambua umuhimu wa uhuru na haki ya kuwa na maoni; na inatafuta njia za kuvihujumu; basi heri klabu ife kuliko uhuru wa watu na watu wenyewe.

0713 614872
ndimara@yahooo.com
(Makala hii itachapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili, toleo la Jumapili tarehe 23 Agosti 2009)

Tuesday, August 11, 2009

WAFUGAJI 'WAKIRUDI KWAO' ITAKUWAJE?


Yatatokea maafa makubwa ya kuangamiza mali na maisha

Na Ndimara Tegambwage


SERIKALI haiwezi kukimbia wajibu wake wa kurejesha amani kwa jamii za wafugaji nchini, kusitisha uvamizi na uporaji ardhi yao ambao umewafanya wakose mahali pa kuishi na kulishia mifugo yao.

Kile ambacho serikali inatakiwa kufanya sasa, ni kupanga na kutangaza maeneo maalum ya makazi ya wafugaji na maeneo ya kufugia na kuchungia mifugo yao.

Kumbukumbu zinaonyesha uzoefu wa serikali kutangaza mbuga za wanyama; mbuga za kuwindia kwa kuua wanyama au kuwinda kwa kutumia kamera (kupiga picha). Ni nadra kusikia serikali ikipanga, kutenga na kutangaza maeneo ya wafugaji na mifugo yao.

Kwani kinachoendelea hivi sasa, katika mbuga za Loliondo, wilayani Ngorongoro, katika mkoa wa Arusha, ni mwendelezo wa ukatili usiomithilika unaoendeshwa kwa baraka na mipango ya serikali, kuwang’oa wafugaji kama magugu na kuwaacha juani wakauke.

Baada ya miaka mingi ya uporaji, uliopangwa, kutekelezwa na kuratibiwa na serikali – ya kikoloni na ile ya uhuru – au matendo ya watu binafsi ambayo hayakukemewa na mamlaka, watawala sasa wanageuza kibao na kusema wafugaji ni wavamizi. Wanasema warudi walikotoka.

Chukua mfano wa Kilimanjaro Magharibi (West Kilimanjaro). Wakazi wa maeneo haya, wengi wao wakiwa Wamasai, walifukuzwa katika maeneo ya Enduimet na kuswagwa hadi chini ya mlima Kilimanjaro.

Madai yalikuwa kwamba wafugaji wanaharibu mazingira kwa “kuchezea vyanzo vya mito ya asili.” Baada ya wafugaji kuondolewa, wakulima wa kizungu na baadhi ya Waafrika walivamia maeneo ya mlimani na kuharibu vyanzo vya maji ambavyo wafugaji walitunza kwa miaka nendarudi.

Leo hii, vyanzo vya maji vya Olmorog, Lelanwa, Kamwanga na Engare-Nairobi, vimepungukiwa maji na vingine kukauka kabisa.

Katika hali hii, nani ameharibu mazingira: Wafugaji walioyalinda miaka yote au wavamizi, wakiwemo wazungu wa Kiholanzi waliodai kuyalinda lakini wakayakausha kwa kilimo na ukosefu wa mipango endelevu?

Madai hayohayo yalitumiwa kufukuza wafugaji kutoka eneo lote la Monduli. Wananchi katika eneo lenye rutuba la Lorkisalie waliswagwa nje kwa madai kuwa wazungu wanataka kuanzisha kilimo cha mbegu za maharage.

Kilimo hakikudumu. Ardhi ikawa tayari imechafuliwa kwa wingi wa mbolea za kisasa na kupoteza uasili wake. Wafugaji wakawa wemeswagwa kama mifugo, kwenda “kokote kule” bila kutengewa sehemu maalum iliyopangwa na serikali kwa ajili ya kuishi na machungio.

Naberera katika Simanjiro, lilikuwa eneo zuri la wafugaji. Ardhi nzuri iliyokuwa ikinawirisha watu na mifugo yao ilinyakuliwa na wazungu na Waafrika, wakiwemo viongozi wa siasa na serikali. Wafugaji wakatupwa nje.

Twende Kiteto. Sehemu kubwa ya ardhi iliyokuwa makazi ya wafugaji na malisho ya mifugo, ilivamiwa na baadhi ya viongozi wa siasa, serikali na matajiri wengine. Wafugaji wengi wakaswagwa nje na wakuja wakaanzisha kilimo cha mahindi.

Katika eneo hili, wakulima wamefanya kufuru. Wameparamia hata vilima vya kijani vilivyotunzwa na wafugaji. Wameingilia vyanzo vya maji vilivyoneemesha mifugo. Sikiliza sauti ya mfugaji:

“Sisi wachache tuliokuwa timesalia, tukawa kama ulimi katikati ya meno,” anaeleza mmoja wa wafugaji wa Kiteto. Wafungwa. Huu ukawa mwanzo wa mapigano kati ya wakulima na wafugaji katika eneo hili.

Uporaji ardhi ya wafugaji ulienea na bado unaendelea katika maeneo mbalimbali. Angalia Serengeti ambako wafugaji wengi waliswagwa kama mifugo yao, nje ya makazi yao na malisho ya mifugo, kwa madai ya kuhifadhi wanyamapori.

Serengeti ambayo imekuwa makazi ya wanyamapori ainaaina; kutambuliwa na kutangazwa dunia nzima kuwa kivutio cha aina ya pekee kwa watalii na labda “boma” la mwisho la viumbe wa porini, imelindwa na kuhifadhiwa na wafugaji ambao mifugo yao ilifanya urafiki na wanyamapori.

Njama za kutawanya, kutelekeza na labda hata kuteketeza wafugaji katika Serengeti ni njama za ngazi ya kimataifa. Vimeandikwa vitabu vingi juu ya maajabu ya Serengeti lakini nafasi ya mfugaji kama mhifadhi wa wanyama hao haijazingatiwa. Itaonekana picha ya mfugaji kwenye jalada tu.

Leo hii, ndani ya mbuga za Serengeti, ambamo wafugaji waliishi, kufugia ng’ombe, mbuzi na kondoo na kuchunga mbuga na wanyamapori, ndimo kumejaa wanaoitwa wawekezaji.

Wawekezaji hawa hawataki hata kuona mtoto wa mfugaji akikatiza, wala ng’ombe akinusa maji ya mto ambao wafugaji wametunza kwa maisha yao yote. Kutoka ng’ambo moja ya mto hadi nyingine limekuwa kosa kubwa la kusababisha vifungo kwa walinzi wa Serengeti na watoto wao.

Mwekezaji ndani ya Serengeti hataki kuona mwananchi; anataka kuona watalii kutoka nje. Anataka kuona shilingi tu itokanayo na wanyamapori ambao wananchi wametunza na kuhifadhi kwa kipindi chote cha maisha yao.

Hapa pia wafugaji waliswagwa nje ya maeneo yao walikoishi, kufuga na kulinda wanyamapori. Wafugaji walilinda wanyamapori kwa kuwa hawawali; wao hula mifugo yao tu.

Hivi sasa wafugaji waliobaki Serengeti wanaishi kwa mfano uleule wa “ulimi katikati ya meno.” Wamefungwa. Wamebanwa mithili ya watumwa; katika nchi yao iliyopata uhuru wa kisiasa yapata miaka 50 iliyopita.

Yaliyotokea West Kilimanjaro, Monduli, Simanjiro, Kiteto na Serengeti, ndiyo hayohayo yaliyotokea Ngorongoro: Kuvamiwa kwa ardhi na kufukuzwa kwa wakazi wa miaka yote ili kuanzisha “Jamuhuri za Wanyamapori.”

Maeneo yote tuliyojadili yamekuwa yakiitwa Masailand – kuanzia Kilimanjaro Magharibi hadi Lobo – kwenye mpaka wa Kenya. Haya ndiyo yalikuwa makazi ya Wamasai.

Historia inasema Wamasai ni taifa linalotembea. Linalohamahama. Lina mifugo na linafuata maji na malisho. Lakini ukweli ni kwamba taifa hili lilikuwa limetua na kuridhika katika maeneo yaliyojadiliwa.

Kama ambavyo hakuna mwenye asili ya mahali alipo, kwamba vizazi vilivyotangulia viliumbiwa hapo (imani) au viligeukia hapo kutoka nyani wangurumao (sayansi), Wanilotiki kutoka milima ya Golani sasa walikuwa wametua na “ardhi” yao kupewa jina na wakoloni kuwa Masailand.

Jirani na Wamasai walikuwa Wabarbaig ambao pia katika miaka ya hivi karibuni walitendewa unyama huohuo wa kuporwa ardhi na kufukuzwa kwenye makazi yao na kuanza kutangantanga.

Mradi wa Basotu, Arusha wa kilimo kikubwa kilichoitwa “mashamba ya ngano ya Basotu” yaliyoendeshwa na Wakanada, uliwaacha Wabarbaig bila makazi.

Leo hii hakuna mashamba. Kilimo kimeshindikana. Yalikuwa mazingaombwe. Ardhi imechoka. Limebaki vumbi tupu. Wabarbaig waliishatupwa nje; wanatangatanga na mifugo yao.

Kwa mtindo huu, jamii za wafugaji zimefanywa za wakimbizi wasiotakiwa popote pale ndani ya nchi yao.

Soma majina haya: Lomnyak Siololo, Kayiok Leitura, Ngiliyayi Ndoinyo, Ngirimba Ndoinyo, Sepekita Kaura na Tokore Siololo. Hawa ni miongoni mwa waathirika wakuu wa mipango ya serikali iliyofukarisha wananchi na kuneemesha watu kutoka nje ya nchi.

Wananchi hawa, kutoka kijiji cha Ololosokwan, wamechomewa nyumba, mazizi ya ng’ombe na wanaswagwa, wao na ng’ombe wao, kutoka walikoishi kwenda kusikojulikana.

Ni kutokana na mfumo huu wa uvamizi na uporaji makazi, wafugaji wametafuta makazi na malisho katika maeneo mengine ya nchi hii. Ni nchi yao. Ni kwao kama kulivyo kwa wengine.

Tatizo hapa ni kwamba serikali, iliyoshiriki kuwafanya wafugaji kuwa watu wa kutangatanga kuliko asili yao, ndiyo inatangaza kuwa wafugaji “warudi kwao.”

Sasa wafugaji wanauliza” “Kwetu ni wapi?” Swali kubwa hapa ni hili: Wafugaji wakirudi kwao, itakuwaje?

Jibu: Vitatokea vita vikubwa vya kuangamiza watu na mali zao; kile kilichoimbwa kwa miaka mingi kuwa ni amani na utulivu wa nchi, kitatoweka kama ukungu wa asubuhi.

Kutatokea vita kwa kuwa maeneo walikofukuzwa wafugaji sasa ni mbuga za wanyama zilizomo mikononi mwa waporaji wakubwa wa maliasili wanaopewa upendeleo kwa kuitwa “wawekezaji.”

Unawekeza nini katika mbuga yenye wanyama waliolindwa na kuhifadhiwa na wafugaji kwa karne na karne? Hapana. Hapa unachuma usipopanda. Vita vya wafugaji kujaribu kurudi walikotoka vitakuwa vikubwa na huenda endelevu na kwa gharama kubwa ya maisha.

Wafugaji wakirudi walikotoka – Kilimanjaro Mashariki, Lorkisalie, Simanjiro, Kiteto na Basotu (Barbaig), kutakuwa na vita ambavyo vitaharibu mashamba ya “wakubwa,” majumba ya kifahari, mifumo ya maisha ambayo tayari imejengwa na kuangamiza uhai wa watu na viumbe vingine.

Bali amani pia haiwezi kuwepo kwa kuendelea kuwa na watu wanaofukuzwa kila waendapo kwa kuambiwa “rudi kwenu.”

Wakati umefika kwa serikali kufanya mambo yafuatayo, yakiwa hatua za haraka na za mwanzo ili kusitisha uonevu na udhalilishaji wa wafugaji na kuepusha migongano na hata vita:

Kwanza, kusimamisha na kuacha kabisa mipango ya kufukuza wafugaji kutoka makazi yao ya sasa. Hili litahusisha kuacha kuchoma moto makazi yao. Nchi hii ni yao.

Pili, kurejesha wafugaji mahali pao katika sehemu ambako walifukuzwa hivi karibuni na kupanga, kuunda na kutangaza makazi ya wafugaji na malisho ya mifugo yao.

Tatu, serikali isitishe na izuie uchochezi wa wanasiasa na baadhi ya watendaji wake kwa wafugaji waliohamishwa zamani, kwa kuwaambia kurejea walikotoka, kwani hilo litazua vita ya maangamizi makubwa.

Nne, wafugaji wakaribishwe pale walipo; waelezwe kuwa safari yao imefika mwisho; watengewe ardhi kwa makazi na malisho bila kujali walikotoka.

Tano, maeneo yaliyopangwa kwa ajili ya ufugaji yatengwe rasmi kwa alama zinazoonekana. Wafugaji wenye mifungo mingi, washirikishwe katika kugharimia miundombinu muwafaka katika mpangilio mpya.

Sita, serikali ijenge mahusiano mapya kati yake na wakulima badala ya kuwakemea na kuwalaani kwa madai dhaifu kuwa mifugo mingi “inaharibu mazingira.”

Saba, serikali iondokane na dharau na kutojali; badala yake itambue kuwa mifugo – mamilioni ya ng’ombe, mbuzi na kondoo wa wafugaji wanaotangatanga katika nchi yao – ni mali na kwamba kwa kuweka mazingira bora, itakuwa ya manufaa zaidi kwa wafugaji na taifa kwa jumla.

Nane, wafugaji washawishiwe na asasi za kijamii na serikali, “kusimama” na kubaki walipo sasa na kufanya makazi hayo kuwa ya kudumu.

Tisa, wafugaji washirikishwe katika kuandaa makazi, malisho na miundombinu. Kwa mfano, malisho yawe ya maeneo makubwa ambamo mifugo itahama kutoka sehemu moja kwenda nyingine, ndani ya eneo husika, ili kuruhusu upatikanaji wa chakula katika maeneo walikochungiwa kwanza.

Umuhimu wa kushirikisha wafugaji katika kuandaa miundombinu unatokana na kuwepo kwa baadhi yao wenye uwezo kifedha kutokana na kuwa na mifugo mingi.

Ni hao ambao wana uwezo wa kuchangia ujenzi wa mipaka ya kutenganisha makazi na malisho, kujenga mabwawa wakati serikali inasaidia katika ujenzi wa miundombinu mingine kama ile ya maji, elimu, barabara na afya.

Kumi, ndani ya mipaka ya maeneo ya malisho, na wafugaji wakiwa sehemu ya jamii ya wakulima katika maeneo husika, ndimo inaweza kuendeshwa elimu juu ya upunguzaji wa mifugo kwa ufugaji wa kisasa.

Hatua hii itakayoendana na wafugaji kukataa kuendelea kusukumwa nje ya mahali walipo, itajenga mshikamano mkubwa kati ya wakulima na wafugaji na kufanya uhasama kuwa historia.

Nilipata fursa ya kuongea na Luteni mstaafu Lepilall ole Molloimet (60) kuhusu suala hili. Aliwahi kuwa mbunge kwa miaka tisa, mkuu wa wilaya kwa miaka 12 katika wilaya za Kiteto, Babati, Korogwe, Musona na Rombo.

Molloimet ambaye sasa ni mfanyabiashara, anasema wakati umefika kwa Wamasai na wafugaji wengine kukataa kuhama kutoka walipo sasa.

Anasema, “Wamasai wabaki pale walipo. Wakatae kuondoka. Washiriki elimu lakini wabaki na mila na desturi zao nzuri; wachague viongozi wao wazuri, wajiamini, wawe jasiri na wakatae kuonewa; wawe tayari kukosoa na kukosolewa.”

Molloimet anasema anawashangaa wabunge katika maeneo ambako wananchi wanaswagwa kama mifugo kutoka kwenye makazi yao ya miaka mingi. Anasema wabunge hao, kwa kukaa kimya, ina maana wanaunga mkono unyama ambao wananchi wanatendewa.

“Kwa ufupi, wabunge hawa wanastahili kujiuzulu maana wameshindwa kazi ya kuwakilisha na kutetea waliowachagua,” anasema Molloimet.

Akiongea kwa sauti ya uchungu, Molloimet anaungana na baadhi ya wananchi wa Olorien, Soitsambu na Magaiduru-Lorien huko Ngorongoro.

Amasema, “Dunia haituelewi. Tunafukuza Wamasai katika maeneo yao; lakini tunakaribisha Wazungu na Waarabu! Nani atatuelewa. Mimi nasema tu kwamba wafugaji wanataka amani.”

Taarifa zinasema juzi Jumatatu, ulifanyika mkutano juu ya hali ya wafugaji na hifadhi ya Loliondo. Miongoni mwa waliohudhuria mkutano huo katika kijiji cha Ololosokwan ni wawakilishi wa Chama cha Wanasheria wa Mazingira (LEAT).

Wengine ni asasi ya kimataifa ya utetezi wa wafugaji tawi la Tanzania (PINGOs), maofisa wa Idara ya Wanyamapori, Ortelo Business Corporation Limited ya Nchi za Falme za Kiarabu (OBC) walioshikilia eneo kubwa ya mbuga ya Loliondo na wajumbe wa kijiji cha Ololosokwan.

Haijafahamika waliongelea nini. Lakini taarifa zinasema watakuwa walijadili hatua ya serikali ya kuchoma makazi na maboma ya mifugo wakilazimisha wananchi kutoka kwenye makazi yao na katika vijiji vilivyoandikishwa kisheria.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com

(Makala hii itachapishwa katika gazeti la MwanaHALISI toleo la 12 Agosti 2009)

Saturday, August 1, 2009

KUSAJILI SIMU ZA MKONONI NI UHALIFU



BADALA YA KUVUMBUA WANADIDIMIZA TEKNOLOJIA



Na Ndimara Tegambwage

SITAKI mpango wa kusajili wamiliki wa simu za mkononi na namba zao kama serikali inavyotaka na kama inavyoshinikiza.

Hii ni kwa kuwa sababu zilizotolewa na serikali; na kusisitizwa na Mamlaka ya Udhibiti ya Mawasiliano Tanzania (TCRA); zile ambazo zinatumiwa kuhalalisha usajili; siyo za msingi na hazina mashiko.

Serikali ina maoni kuwa simu za mkononi zinatumiwa vibaya. Inadai zinatumiwa kufanya uhalifu. Kwamba zinarahisisha mawasiliano ya wale wanaopanga uhalifu.

Uhalifu unaotajwa ni pamoja na kutukana, kupanga wizi na, au hujuma; kutoa vitisho kwa watu mbalimbali; kutoa taarifa za upotoshaji na wakati wote huo bila muhusika kufahamika.

Inadaiwa kuwa namba na wamiliki wakisajiliwa, itakuwa rahisi kujua nani ametoa taarifa, uzushi, vitisho; na kupitia namba ipi ya simu. Serikali inafikiri kwa njia hii, kazi yake ya “ulinzi wa amani” itakuwa imerahisishwa.

Hii ina maana kwamba serikali na wenye makampuni ya kutoa huduma za simu za mkononi, wamekula njama. Wamekubaliana kuingilia mawasiliano ya wananchi na labda wamekuwa wakifanya hivyo, tena kwa kiwango kikubwa.

Uhalifu hauletwi na simu. Uhalifu hauletwi na siri katika mawasiliano. Vyombo vya mawasiliano ni mifereji ya kupitishia taarifa. Unahitaji mawasiliano mapana kukabili uhalifu.

Katika mazingira ambamo waliopewa jukumu la kuzuia uhalifu ndio wenyewe wanaofanya uhalifu; unahitaji vyanzo vya siri vya kuibua uhalifu. Pale penye uhalifu unaofanywa na watawala na wateule wao, unahitaji mifereji isiyo bayana.

Katika mazingira ambamo aliyeibua uhalifu anatendewa kama mhalifu; na wakati mwingine jina lake kuwekwa wazi kwa wahalifu – wawe wakwapuzi wa mabilioni benki, wauza dawa za kulevya au majambazi yaliyokubuhu – unahitaji mifereji ya mawasiliano isiyo bayana.

Tujenge hoja kuwa mtu asiyejulikana, ambaye amekupelekea simu ya vitisho kupitia namba ya simu isiyojulikana ya nani, basi ameshindwa kutekeleza anachotaka. Tumuone kama anayetishia tu.

Bali inawezekana akawa anatishia kweli. Hapo atakuwa ametoa onyo; amekupa muda wa kujipekua na kujiandaa. Simu hiyo pia yaweza kukupa fursa ya kuacha kile ulichokuwa ukifanya na ambacho tayari wengine wameona hakifai au kinawadhuru.

Katika mazingira ya Tanzania, taarifa juu ya kifo cha mahabusu ambaye maofisa wa magereza hawataki kijulikane, inapatikana kwa mfereji wa siri wa mawasiliano – simu isiyoweza kutambulika.

Orodha za wahalifu walioko serikalini, karibu sana na watawala wakuu, inafikia vyombo vya habari kwa njia ya simu ya siri. Maagizo ya siri ya kuumba au kuua, yanapatikana kwa njia ya namba ya simu isiyosajiliwa.

Kilio cha wananchi wakazi wa Kilosa, mkoani Morogoro na Ololosakwani, mkoani Arusha juu ya unyama wanaotendewa, kinafikia vyombo vya habari, watawala na dunia nje ya nchi, kwa njia ya simu isiyopekuliwa.

Dereva wa mbunge ambaye hajalipwa mshahara wake kwa miezi sita, anatumia namba isiyosajiliwa kuwasiliana na vyombo vya habari na hata spika wa bunge ili angalau kilio chake kiweze kusikika na yeye apate kushughulikiwa.

Hayo ndiyo matakwa ya mazingira ya sasa. Dereva akijulikana kuwa analalamika, basi anafukuzwa kazi. Karani akifahamika kuwa “amevujisha” majina ya wezi idarani, anafukuzwa kazi palepale.

Ofisa Utumishi akijulikana kuwa hakushirikishwa katika ajira ya watoto wa bosi wake, siyo tu atafukuzwa kazi; aweza kuundiwa kosa kubwa hata la kufikishwa mahakamani.

Mfugaji wa Kilosa na Ololosakwani akijulikana kuwa ni yeye aliyepeleka taarifa za askari wa FFU kuchoma nyumba zao na kutesa wananchi, huenda “akapotezwa” katika mazingira ya kutatanisha.

Tetesi nyingi kwa vyombo vya habari, watumishi makini na waaminifu ndani ya serikali, taasisi zake na hata makampuni na mashirika binafsi; zinapatikana kwa mifereji ya siri, kwa kuwa “uwazi” limekuwa neno tupu la wanasiasa na halimo katika utendaji.

Tetesi hizi zimekuwa muhimu kwa hatua za kwanza za uchunguzi. Wakati aliye karibu aweza kukuona na kuongea nawe, aliye mbali anapata fursa ya kukupa taarifa bila wasiwasi wa kuchukuliwa hatua na wale wanaodaiwa kutenda uhalifu.

Aidha, wakati baadhi ya waandishi wa habari wamesahau au wamedharau msingi muhimu wa “kutunza chanzo cha taarifa,” baadhi wametaja majina ya waliowapa taarifa na kuwaweka hatarini.

Simu ambazo haziwezi kuingiliwa ni nyenzo kuu ya wananchi na wafanyakazi waliomo katika karakati za kupigania uhuru na haki zao. Watapanga jinsi ya kukutana hadi jinsi ya kufanya walichopanga.

Asasi za kijamii zilizomo katika ushawishi ainaaina, huweza kutumia njia hii ya simu isiyo wazi ili taarifa zisivuje, hadi hatua ya mwisho iliyolengwa na kufanya hoja zao kuibuka kwa kishindo na labda kupatikana kwa mafanikio yaliyotarajiwa.

Uhalifu hauletwi na simu za mkononi ambazo namba zake na wamiliki hawajulikani kwa watawala. Nyenzo hii ya mawasiliano ya teknolojia ya kisasa inaweza kutumiwa na mkweli au mwongo; mtiifu au mwasi; mwaminifu au mkora, “mungu” au “shetani.”

Aliwahi kusema Karl Marx, kuwa uhalifu ni tasnia pana inayoajiri kuanzia mtu wa kada ya chini kabisa kama mesenja hadi profesa wa masuala ya jinai. Hapa kuna hoja ya “uendelevu.”

Kadri jamii zinavyopita katika nyakati tofauti za maendeleo na kuingia na kutoka katika ustaarabu tofauti, ndivyo zinavyokumbana na matatizo mapya na changamoto mbalimbali.

Mlango wa kusumumiza hautoshi kuziua mwizi. Chomeko siyo tena chombo cha ulinzi. Kofuli haifai tena kulinda nyumba. Magrili yanatawanywa kwa moto wa gesi.

Kukua kwa maarifa ya kuhudumia jamii kunaenda sambamba na uvumbuzi katika tasnia ya uhalifu. Huwezi kuzuia hili. Lakini serikali inakwenda mbali. Inafikiri kuwa simu ambazo haijui ni za nani, zinaleta au zinachochea uhalifu(!?) Huu ni udhaifu mbaya.

Badala ya kutafuta mbinu za kisasa za kukabiliana na kile wanachoona ni tatizo, serikali na makampuni ya simu wanatafuta kufanya teknolojia na matumizi yake kuwa butu. Huu ni mkasa.

Serikali inaziba mifereji ya taarifa za siri kuhusu utendaji wake. Hasa kuziba kasi ya kuenea kwa taarifa juu ya mambo inayofanya lakini hayakustahili kufanywa na waliopewa madaraka ya utawala.

Hapa serikali imeingilia uhuru wa mawasiliano wa mtu binafsi. Inakana maendeleo ya teknolojia. Inaziba upenyo wa kupitishia kilio na tetesi. Serikali inatenda uhalifu.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
(Makala hii iichapishwa katika gazeti la Tanzania daima Jumapili, toleo la 22 Julai 2009)

KASHFA YA MEREMETA YAWEZA KUZAMISHA SERIKALI



MAWE YAKISEMA, SERIKALI ITAUMBUKA


Na Ndimara Tegambwage


SITAKI waziri Jeremiah Sumari achokoze Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), kwa kutumwa au kwa sababu zake binafsi.

Majeshi ni mawe makubwa. Majabali. Miamba. Majeshi ni wagumba. Majeshi yakitaka kuzaa sharti yakubali kufa polepole; kwa maana kwamba atokee wa kuyapasua ili yatoke mengi kwenye mawe makubwa au miamba. Hapo hayabaki mojamoja na imara tena.

Na kawaida majeshi ya nchi hayachokozwi na mtu wa ndani wala wa nje. Wachokozi huchokoza nchi na watawala wa nchi zilizochokozwa huagiza majeshi yake kwenda mstari wa mbele na kukunja uchokozi kama jamvi la wageni.

Lakini uchokozi uliofanywa na waziri Sumari ni wa ndani na unaweza kufanya mawe makubwa, miamba kutamani kutoa sauti na kusema hayataki kupasuliwa; yaachwe kama yalivyo.

Akijibu swali la Dk. Willibrod Slaa juu ya ufisadi ndani ya mradi wa Meremeta, Sumari alitoa majibu ya vitisho. Alimwambia mwakilishi wa Karatu (CHADEMA) aachane na hoja ya ufisadi ndani ya Meremeta.

Kiasi kinachodaiwa kupitia Meremeta kwenda mifuko isiyojulikana si haba. Ni zaidi ya Sh. 155 bilioni. Waziri anamwambia mbunge aachane na hoja ya Meremeta kwa madai kuwa mradi huo ulikuwa wa jeshi; kwamba ni suala nyeti na labda ni kuingilia suala la usalama wa taifa.

Waziri anataka kulazimisha mawe kusema. Mawe yatabaki kimya juu ya ahadi zao; juu ya mipango yao na silaha zao; juu ya mikakati ya sasa na baadaye; juu ya mbinu mpya walizopata katika medani ya vita; juu ya wanachopanga kufanya hivi sasa.

Ukimya huu ni kama jua, mvua na upepo vipigapo kwenye mwamba na mwamba ukavumilia. Zaidi ya hapo, miamba husema. Miamba mingi imeota juu ya mizimu ya kale iongeayo wakati wa jua kali.

Inawezekana, siku moja unapita karibu na miamba hiyo, wakati wa jua kali, ukasikia mtu akikuita kwa sauti ya juu sana – mara mbili au mara tatu – na usimwone.

Wale dhaifu wa moyo huweza kuanguka chini na kuzimia; wengine humudu kukimbia hadi nyumbani kwao, wakitweta na kulowa jasho mwili mzima huku wakiishiwa na kauli. Mawe, majabali, miamba imeamua kusema!

Wakati huo hujawahi kuichokoza. Hujailalamikia wala kuituhumu. Hujaisingizia wala kuihusisha katika miradi bubu ya watawala. Inasema tu. Inabubujika. Sembuse utakapoihusisha na wizi, uporaji, ukwapuaji, au kwa ujumla – ufisadi!

Ikae kimya? Sitaki waziri Sumari achokoze miamba na yenyewe iseme kwamba haijui Meremeta ni nini na ya nani. Kwamba haijawahi kunufaika na kampuni hiyo. Kwamba mafao yaliyotokana na Meremeta hayafahamiki jeshini. Kwamba hayakuingia jeshini.

Sitaki waziri achokoze miamba ianze kukohoa na kunong’ona na hatimaye kulipuka. Miamba hii inajua kuwa fedha za kuendesha jeshi hutoka kwenye bajeti ya serikali inayosomwa na kupitishwa bungeni.

Miamba hii inaelewa vema kwamba wakati Meremeta wanaanzisha mradi walihamisha wananchi kutoka makazi yao. Walihamisha hata kambi ya Jeshi la Kujenga Taifa na kutawanya askari katika vijiji kwa kutumia mikokoteni.

Si wananchi – raia, wala askari walionufaika na mafao ya Maremeta baada ya kuanza kuvuna kutokana na mgodi. Shule na zahanati vilivyong’olewa havijarudishwa. Bwawa kubwa la maji lililokuwa sehemu ya uhai wa watu na viumbe anuwai, halijarejeshewa hadhi yake.

Sitaki watawala jeshini wajitokeze na kuiumbua serikali juu ya matumizi haya. Sitaki wapatikane watumishi wa Wizara ya Ulinzi na kuthibitisha kuwa hawajawahi kupanga fedha za Meremeta au sehemu yake katika matumizi ya wizara.

Sitaki maofisa wa ngazi za kati jeshi waanze kufurukuta na kusema hawataki kusingiziwa katika suala la ukwapuaji na hivyo kujitokeza na ukweli utakaoangamniza hadhi ndogo ya watawala iliyosalia.

Sitaki askari wa vyeo vya chini ambao wanajua vema kilichokuwa kinaendelea waanze kujitokeza na kusema walichoona na nani hasa walikuwa wavunaji wakuu wa Meremeta na siyo jeshi.

Wala sitaki askari wakumbushe serikali kwamba Tume ya Jaji Bomani iliishasema kuwa Meremeta si mali ya serikali bali ni ya binafsi. Labda likisemwa na wao ndipo serikali itasikia na waziri Sumari ataelewa.

Nani anataka azibuliwe masikio kuliko alivyofanya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali. Aliiambia Kamati ya Bunge kuwa Meremeta haimo katika orodha ya mashirika ya umma na kwamba ofisi yake haijawahi kuikagua.

Mei mwaka jana tulipeleka baruapepe kwa benki ya Nedcor Trade Services ya Afrika Kusini kuhusiana na suala hili. Hatukujibiwa. Tuliwaandikia Deutsche Bank AG ya Uingereza. Hawakujibu.

Lakini kwa kufuatilia kinachoendelea ni kwamba serikali haifanyi lolote. Imetafuta mahali pa kuegesha na kusahau hoja za wananchi wanaotaka kujua huyu Meremeta ni nani na fedha alizochota alizitumia wapi.

Matumizi ya visingizio vya jeshi, kama anavyosema Sumari, hayana uzito tena. Hayamtishi yeyote. Wananchi, wachunguzi na wengine wanaotafuta ukweli wangestuka na hata kuogopa kama wangekuwa wameingilia undani wa shughuli za jeshi.

Lakini hili la kikampuni cha Meremeta halimtishi mtu. Badala yake linaweza kuiweka serikali pabaya, kwani inaendelea kujichanganya; kuficha ukweli na hatimaye kusema uwongo.

Hatari kubwa inaweza kuzuka pale mawe, majabali na miamba itakaoamua kuvunja kimya; siyo lazima kwa mikutano ya hadhara bali kwa mn’ong’ono tu ambao hatimaye utavuma kama upepo wa kimbunga.

Na askari – hiyo miamba – ni watoto wa watu masikini na wao ni masikini pia. Hawana cha kupoteza kwa kusema ukweli wanaoujua. Hapo ndipo serikali itaumbuka zaidi.

Nani anaweza kuiondolea aibu serikali kwa kusema ukweli na kuijengea heshima na uhalali? Kama siyo mawaziri wake, nani hasa? Tusubiri majabali yaite wakati wa jua kali na kwa mzizimo wahusika wazimie?

Uwezekano wa aliyezimia kupitiliza hadi dunia nyingine ni mkubwa kuliko aliyesimama. Kwa nini serikali ijiingize kwenye majaribu tata? Ukimya unaidhalilisha serikali na kuiondolewa uhalali. Itoboe kilichomo ndani ya Meremeta.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
(Makala hii ilichapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili Juni 2009)