Saturday, August 22, 2009

MAANDALIZI YA VURUGU UNGUJA NA PEMBA




Mategemeo, subira bila mafao Pemba


Na Ndimara Tegambwage

SITAKI mtu mzima, nyumbani kwake na familia yake, aambiwe na mgeni jinsi ya kuvaa vizuri, kulea watoto, kuweka nyumba yake katika hali ya usafi, kutafuna polepole na kutoacha mdomo wazi wakati anapopiga miayo.

Mtu mzima atang’aka na kuuliza iwapo ni wewe umekuwa ukimwelekeza kwa miaka yote hadi kufikia umri huu wa miaka 50. Atakushangaa. Aweza kukujibu kwa hamaki na hasira.

Ndivyo ilivyokuwa mwishoni mwa wiki. Marafiki wa serikali za Muungano wa Tanzania na Baraza la Mapinduzi Zanzibar (BMZ), waliona serikali hizi zinataka kupiga miayo bila kuweka kiganja mdomoni. Wakazibonyeza: Tahadhari!

Mabalozi wa nchi za Jumuiya ya Ulaya, Marekani, Japan na Canada wamezitaka serikali za Muungano na BMZ kuwa makini na demokrasi. Hii inafuatia hatua ya kusimamisha zoezi la kuhakiki daftari la wapigakura kisiwani Pemba, wiki mbili zilizopita, baada ya milipuko miwili ya mabomu katika makazi ya wananchi.

Katiba ya Zanzibar inazingatia kuwa kila raia ana haki ya kupiga na kupigiwa kura. Vigezo vya raia vipo. Lakini sheria ya uchaguzi inaongeza matakwa mengine, kuwa kila anayetaka kujiandikisha kupiga kura sharti awe na hati ya ukazi Zanzibar.

Kwa wiki mbili sasa kumekuwepo migongano kisiwani Pemba. Siyo kwamba wote wanapinga kuwepo matakwa ya hati ya ukazi, bali hata wenye hati wanadai kuwa wamekuwa hawaandikishwi au kuhakikiwa.

Ukazi umekuwa ukazi. Hivi kitambulisho kuwa ulipiga kura uchaguzi uliopita hakitoshi? Hivi kuwa na kitambulisho cha uraia kwa misingi ya ulipozaliwa, kukulia na bado unaishi hapo hakutoshi? Hivi ilikuwa lazima vitambulisho vya ukazi vitakiwe hivi sasa wakati wa uhakiki wa daftari; kwa nini kazi hiyo haikufanywa mapema?

Tayari kuna madai ya wananchi kwamba wamekwenda kwenye vituo wakiwa na hati ya ukazi, hati ya kupigia kura uchaguzi uliopita na vyeti vya kuzaliwa, lakini wakakataliwa kuhakikiwa. Hapa ndipo penye utata.

Madai mengine ni kwamba kuna waliokwenda vituoni, bila hati ya ukazi, bila hati ya kuzaliwa, bila hati ya kupiga kura katika uchaguzi wowote uliopita, lakini wakapokewa na kuhakikiwa. Wananchi wanajiuliza: Huu ni mradi maalum wa serikali, upendeleo maalum na wa makusudi au ngekewa?

Kwa hiyo, kabla serikali haijasimamisha uhakiki katika daftari la kupiga kura, tayari kulikuwa na makundi hapa na pale; yakijadili hali hii. Utata unazidi inapokuwa Pemba ni ngome ya chama kikuu cha upinzani Visiwani – Chama cha Wananchi (CUF).

Kwa kuzingatia ushindi wa asilimia 100 wa CUF katika uchaguzi mkuu uliopita kisiwani Pemba, kila sehemu ya kisiwa hicho ni ngome ya chama hicho. Hatua yoyote ile basi, ya kuweka taratibu ngumu au zenye utata katika kuhakiki majina ya wapigakura, itafikiriwa kuwa inalenga kuhujumu CUF.

Katika mazingira ambamo hakuna maelezo ya serikali yanayoeleweka juu ya chanzo cha milipuko ya mabomu; na kutokana na milipuko hiyo kuwa ndani ya ngome ya chama cha upinzani, tayari kuna madai kuwa milipuko ililenga kutishia wapigakura wa upande wa upinzani.

Kwa kuwa milipuko ya mabomu imefanya watu watawanyike na kukimbilia mafichoni; yawezekana wengi wasirudi kujiandikisha kupiga kura. Inawezekana wengine wakaja wakati wa kujiandikisha umeisha au wakachukia na kukata tamaa kwa kuwa siasa imeingiliwa na tishio kwa maisha yao.

Yote haya yakifanyika, haitakuwa kwa manufaa ya chama kikuu cha upinzani au hata vyama vidogo. Yaweza kuwa faida kuu kwa chama kilichoko ikulu ya Zanzibar. Kwa ufupi, inaweza kueleweka kuwa kura za wananchi tayari zimepigwa mabomu.

Katikati ya hali hii mabalozi wa Ulaya, Marekani, Canada na Japan wamesema kuwa hawafurahishwwi na hali kama ilivyo Kisiwani Pemba. Hilo tu, kwamba “Ndugu yangu, ziba kidogo mdomo wakati wa kupiga miayo.”

Kauli ya mabalozi tayari imeleta kizaazaa. Serikali ya Muungano imejibu kwa kusema iliishawaonya mabalozi wasiingilie mambo ya ndani ya nchi; huku Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ikisema mabalozi wamevuka mpaka.

Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UV-CCM) nao umekuja juu, mwenyekiti wake Hamad Masauni Yusuf Masauni akisema kuwa Tanzania iliishatoka kwenye ukoloni na kwamba “mabalozi wafanye kazi zilizowaleta nchini.”

Ni kauli kali zisizojibu hoja ya mikingamo katika uhakiki wa daftari la wapigakura kisiwani Pemba. Ni kali lakini ambazo sharti zitolewe ili kujikakamua ingawa wote waliosema wanajua kuwa mataifa hayo ni wabia wa serikali, tena kwa muda mrefu.

Vyovyote itakavyokuwa, tayari zoezi la kupiga kura katika uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka huu na uchaguzi mkuu mwaka kesho, limeingia doa. Kwa mtindo huu, inawezekana madoa mengi yataingia hata kabla siku ya kudondosha karatasi katika sanduku la kura.

Bali jambo moja ni muhimu hapa. Serikali, pamoja na ukali wake na kauli nyingine ambazo zinaweza kuwa zinakiuka itifaki, zinaelewana vema na wafadhili. Ukiangalia kwa undani utaona vema kwamba wanasikika kupingana lakini hawatupani.

Kinachofanyika ni kutaka kuonekana kuwa waliona jambo likifanyika; walihisi siyo sahihi; walilitolea kauli kwamba hawakufurahishwa; lakini mambo yanakwenda kama wanaoyafanya wanavyopenda. Hiyo ndiyo “itifaki.” Hakuna malumbano zaidi wala kukabana shingo.

Kama kuna aliyetegemea kauli za mabalozi kutikisa lolote katika mazingira ya sasa Pemba na huenda Unguja na Bara, anashauriwa avute pumzi. Kile ambacho mataifa haya wabia wa serikali wanaonekana wanaweza kufanya, huwa hakifanywi au kinafanywa kwa njia isiyofikia kubadilisha maamuzi.

Kwani ni mataifa haya ambayo utasikia yamekwishaahidi au tayari yametoa mabilioni ya shilingi kwa ajili ya shughuli za uchaguzi nchini – katika hali yoyote ile ambamo utakuwa umeandaliwa na watawala. Hatimaye watatangaza uchaguzi kuwa huru na wa haki.

Imekuwa hivyo siku zote. Itakuwa hivyo mwaka huu na mwaka kesho. Anayetaka mabadiliko katika msimamo wa mataifa ya nje kuhusu suala hili, atasubiri sana. Na kunakucha, kunakuchwa.

Sharti nguvu ya mabadiliko itoke kwa wanaoumia pindi wanapoweka mguu chini. Kuna mwiba. Kama unachoma, basi uondoe. Wanaoona unachechemea huenda wakadhani siku hizi una mikogo. Chukua hatua.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com
(Makala hii ilichapishwa katika Tanzania Daima Jumapili, toleo la 16 Agosti 2009)

UDIKITEA MBAYA SASA WAJA



CCM na ukandamizaji wa fikra

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI Chama Cha Mapinduzi (CCM) kiwe nguzo ya nne ya dola. Nilitarajia kikae uwani, kijirembe kwa vipodozi na mavazi ya kila aina, kisubiri harusi, lakini kisikoromee nguzo yoyote ya dola.

Jijini Dodoma, kupitia kwa mjumbe wa NEC ambaye pia ni spika wa bunge la Jamhuri ya Muungano, CCM ilitoa onyo kwa wawakilishi wa wananchi kwamba wamepanua mno midomo yao; wamekijeruhi chama na serikali; sasa wachunge sauti na kauli zao.

Wabunge wameambiwa, kupitia kwa Spika Samwel Sitta kuwa wasijadili masuala yahusuyo “ufisadi” ndani ya bunge bali ndani ya vikao vya chama, kikiwemo kikao cha wabunge wa CCM. Wameamriwa. Kutofanya hivyo ni “kukiumiza” chama na serikali na kuneemesha upinzani.

Amri hizo kutoka Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, hakika zinakwenda kinyume cha matarajio. Kinyume cha utaratibu. Kinyume cha mwenendo wa “klabu” za kisiasa. Kinyume cha Katiba.

Leo CCM inakaripia spika wa bunge; eti ametoa mwanya mkubwa kwa wabunge kuisakama serikali. Eti ameruhusu serikali idhalilishwe. Eti ameacha mwanya mkubwa unaotumiwa na baadhi ya wabunge kukaripia viongozi wa chama, serikali na hata viongozi wastaafu.

CCM inataka spika wa bunge awanyamazishe wabunge. Awakemee na kuwakoromea pindi wanapokuwa wakali kwa serikali. Kwani sasa inadaiwa wabunge “wamekuwa huru kupita kiasi” na kwamba wanastahili kudhibitiwa.

Hatua ya CCM inalenga kufanya bunge kuwa kamati ya chama. Inalenga kufanya spika kuwa mhamasishaji wa shughuli za chama na serikali ndani ya bunge. Inalenga kugeuza bunge – kutoka msimamizi na mshauri wa serikali – kuwa sekretarieti ya chama na serikali.

Hiyo ndiyo maana ya kukemea spika kwa madai kuwa “ameruhusu uhuru zaidi.” CCM inataka bunge lililopigwa pasi; lile la “Chama Kushika Hatamu” – magereza ya siasa yaliyoandaliwa na Pius Msekwa kutukuza mfumo wa chama kimoja. Watawala wanataka bunge liimbalo sifa na utukufu wa chama kimoja na kiongozi mmoja mwenye fikra ngumu na “zinazodumu.”

Kupitia kwa spika aliyenyamazishwa, wabunge wanyamaze. Kupitia kwa wabunge walionyamaza, wananchi nao “wafyate mkia.” Kuwepo na sauti moja, kauli moja – ile ya klabu moja siasa – CCM na serikali yake.

Hapa ndipo panakuza ukinzani. Wananchi hawakuchagua wabunge ili wabunge waitetee serikali. Mbona serikali ina watetezi wengi bungeni? Dhana ya uwakilishi ina maana ya jicho, sikio na mdomo wa nyongeza wa wananchi; vilivyopewa jukumu la kusimamia na kushauri serikali na kutetea maslahi yao.

Kwa chama na serikali kutafuta kunyamazisha wananchi kupitia vijembe, vitisho na tuhuma dhidi ya spika, ni kutaka kuwa na taifa la mazezeta; linalosikia bila kuelewa; lisilofikiri na lisiloongea kwa kuwa limekatwa ulimi; lisilotoa hata mgumio wala mguno kwa kuwa limetumbukizwa katika woga usiomithilika.

Kesho CCM yaweza kukemea Jaji Mkuu kwa madai kuwa hukumu zake zinakuwa kali kwa viongozi wa chama, serikali na viongozi wastaafu. Jaji mkuu aweza kusutwa kwa kutoa uhuru zaidi kwa mahakimu na majaji wenzake na kwamba uhuru huo “unadhoofisha serikali.”

Ikifikia hapo, siyo tu uhuru wa kufikiri utakuwa umeingiliwa sana na hata kunyongwa; uhuru wa watu wa kuishi utakuwa mashakani. Hii ndiyo hatari kubwa zaidi. Kwa chama kilichoko ikulu kutamani taifa lililokimya, ni sawa na kutamani kutawala miti, mawe na wanyamapori. Siyo watu.

Hoja kuu inayowagawa wabunge hivi sasa na ambayo CCM na serikali hawataki kusikia wabunge wakiijadili hadharani, ni juu ya “ufisadi.” Chama hiki na serikali yake vinataka hoja hii ijadiliwe kimyakimya kwenye vikao na siyo kweupe.

Hii ni hoja inayoeleweka kwa urahisi. Inayopenya katika vichwa vya wengi. Inayojadilika. Inayoweza kuhusishwa na maisha ya kila mmoja popote alipo. Inayofanya watu wafikiri, waulize maswali na watake majibu. Inahusu uhai wao – kufa au kupona.

Kwa upande wa watawala, hoja hii ni mbaya. Inaingiza watu wengi kwenye mjadala ambao serikali haiwezi kudhibiti. Ni mjadala huu mpana unaoweza kuathiri maamuzi ya wananchi wakati wa uchaguzi wa viongozi. Unaleta vidonda mwilini mwa serikali na CCM na unatonesha daima.

Mjadala huu ungehusu vyama vya upinzani, usingetafutiwa mbinu za kuuzima. Ungekuwa kipenzi cha watawala na ungekuzwa na kuenezwa nchini kote ili penye uoza paonekane. Yote yangefanywa “kwa jina la demokrasi na uhuru wa maoni.”

Bali mjadala unapolalia watawala, basi hakuna suala la demokrasi wala haki na uhuru wa maoni. Unakuwa mchungu. Unatishia walioko kileleni. Unatishia uhalali wa utawala wa serikali. Matokeo yake, serikali inatafuta kuuzima kwa njia yoyote ile.

Vitisho vilivyoelekezwa kwa spika vinakwenda mithili ya hadhithi ya Karumakenge – maji yanatishia kuzima moto; moto unatishia kuchoma fimbo; fimbo inatishia kupiga Karumakenge; na Karumakenga anakubali kwenda shule. Bali hii ni hadithi ya kimaendeleo na endelevu.

Sasa NEC ya CCM inatishia kufukuza Spika Sitta; Sitta atishie kuadhibu wabunge; wabunge watishie kugomea wananchi wanaowatuma; na wananchi wanyamaze – kama maiti. Kunahitajika ukimya ambamo kishindo cha mende kitasikika kama tsunami. Hii si hadithi; ni hali halisi inayopingana na maendeleo. Ni ujima mchafu.

Ukame wa fikra na mijadala ambao CCM inataka utawale bunge na jamii kwa ujumla, ni msiba mkubwa kwa taifa. Hii ni sababu ya kutosha kupinga kuendelea kuwepo utawala wa serikali ya CCM.

CCM, kama vilivyo vyama vingine, ni klabu ya kisiasa – moja ya asasi za kijamii za kuragbishia raia kushiriki katika siasa na utawala wa nchi zao. Kama klabu hii imeshindwa kutambua umuhimu wa uhuru na haki ya kuwa na maoni; na inatafuta njia za kuvihujumu; basi heri klabu ife kuliko uhuru wa watu na watu wenyewe.

0713 614872
ndimara@yahooo.com
(Makala hii itachapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili, toleo la Jumapili tarehe 23 Agosti 2009)

Tuesday, August 11, 2009

WAFUGAJI 'WAKIRUDI KWAO' ITAKUWAJE?


Yatatokea maafa makubwa ya kuangamiza mali na maisha

Na Ndimara Tegambwage


SERIKALI haiwezi kukimbia wajibu wake wa kurejesha amani kwa jamii za wafugaji nchini, kusitisha uvamizi na uporaji ardhi yao ambao umewafanya wakose mahali pa kuishi na kulishia mifugo yao.

Kile ambacho serikali inatakiwa kufanya sasa, ni kupanga na kutangaza maeneo maalum ya makazi ya wafugaji na maeneo ya kufugia na kuchungia mifugo yao.

Kumbukumbu zinaonyesha uzoefu wa serikali kutangaza mbuga za wanyama; mbuga za kuwindia kwa kuua wanyama au kuwinda kwa kutumia kamera (kupiga picha). Ni nadra kusikia serikali ikipanga, kutenga na kutangaza maeneo ya wafugaji na mifugo yao.

Kwani kinachoendelea hivi sasa, katika mbuga za Loliondo, wilayani Ngorongoro, katika mkoa wa Arusha, ni mwendelezo wa ukatili usiomithilika unaoendeshwa kwa baraka na mipango ya serikali, kuwang’oa wafugaji kama magugu na kuwaacha juani wakauke.

Baada ya miaka mingi ya uporaji, uliopangwa, kutekelezwa na kuratibiwa na serikali – ya kikoloni na ile ya uhuru – au matendo ya watu binafsi ambayo hayakukemewa na mamlaka, watawala sasa wanageuza kibao na kusema wafugaji ni wavamizi. Wanasema warudi walikotoka.

Chukua mfano wa Kilimanjaro Magharibi (West Kilimanjaro). Wakazi wa maeneo haya, wengi wao wakiwa Wamasai, walifukuzwa katika maeneo ya Enduimet na kuswagwa hadi chini ya mlima Kilimanjaro.

Madai yalikuwa kwamba wafugaji wanaharibu mazingira kwa “kuchezea vyanzo vya mito ya asili.” Baada ya wafugaji kuondolewa, wakulima wa kizungu na baadhi ya Waafrika walivamia maeneo ya mlimani na kuharibu vyanzo vya maji ambavyo wafugaji walitunza kwa miaka nendarudi.

Leo hii, vyanzo vya maji vya Olmorog, Lelanwa, Kamwanga na Engare-Nairobi, vimepungukiwa maji na vingine kukauka kabisa.

Katika hali hii, nani ameharibu mazingira: Wafugaji walioyalinda miaka yote au wavamizi, wakiwemo wazungu wa Kiholanzi waliodai kuyalinda lakini wakayakausha kwa kilimo na ukosefu wa mipango endelevu?

Madai hayohayo yalitumiwa kufukuza wafugaji kutoka eneo lote la Monduli. Wananchi katika eneo lenye rutuba la Lorkisalie waliswagwa nje kwa madai kuwa wazungu wanataka kuanzisha kilimo cha mbegu za maharage.

Kilimo hakikudumu. Ardhi ikawa tayari imechafuliwa kwa wingi wa mbolea za kisasa na kupoteza uasili wake. Wafugaji wakawa wemeswagwa kama mifugo, kwenda “kokote kule” bila kutengewa sehemu maalum iliyopangwa na serikali kwa ajili ya kuishi na machungio.

Naberera katika Simanjiro, lilikuwa eneo zuri la wafugaji. Ardhi nzuri iliyokuwa ikinawirisha watu na mifugo yao ilinyakuliwa na wazungu na Waafrika, wakiwemo viongozi wa siasa na serikali. Wafugaji wakatupwa nje.

Twende Kiteto. Sehemu kubwa ya ardhi iliyokuwa makazi ya wafugaji na malisho ya mifugo, ilivamiwa na baadhi ya viongozi wa siasa, serikali na matajiri wengine. Wafugaji wengi wakaswagwa nje na wakuja wakaanzisha kilimo cha mahindi.

Katika eneo hili, wakulima wamefanya kufuru. Wameparamia hata vilima vya kijani vilivyotunzwa na wafugaji. Wameingilia vyanzo vya maji vilivyoneemesha mifugo. Sikiliza sauti ya mfugaji:

“Sisi wachache tuliokuwa timesalia, tukawa kama ulimi katikati ya meno,” anaeleza mmoja wa wafugaji wa Kiteto. Wafungwa. Huu ukawa mwanzo wa mapigano kati ya wakulima na wafugaji katika eneo hili.

Uporaji ardhi ya wafugaji ulienea na bado unaendelea katika maeneo mbalimbali. Angalia Serengeti ambako wafugaji wengi waliswagwa kama mifugo yao, nje ya makazi yao na malisho ya mifugo, kwa madai ya kuhifadhi wanyamapori.

Serengeti ambayo imekuwa makazi ya wanyamapori ainaaina; kutambuliwa na kutangazwa dunia nzima kuwa kivutio cha aina ya pekee kwa watalii na labda “boma” la mwisho la viumbe wa porini, imelindwa na kuhifadhiwa na wafugaji ambao mifugo yao ilifanya urafiki na wanyamapori.

Njama za kutawanya, kutelekeza na labda hata kuteketeza wafugaji katika Serengeti ni njama za ngazi ya kimataifa. Vimeandikwa vitabu vingi juu ya maajabu ya Serengeti lakini nafasi ya mfugaji kama mhifadhi wa wanyama hao haijazingatiwa. Itaonekana picha ya mfugaji kwenye jalada tu.

Leo hii, ndani ya mbuga za Serengeti, ambamo wafugaji waliishi, kufugia ng’ombe, mbuzi na kondoo na kuchunga mbuga na wanyamapori, ndimo kumejaa wanaoitwa wawekezaji.

Wawekezaji hawa hawataki hata kuona mtoto wa mfugaji akikatiza, wala ng’ombe akinusa maji ya mto ambao wafugaji wametunza kwa maisha yao yote. Kutoka ng’ambo moja ya mto hadi nyingine limekuwa kosa kubwa la kusababisha vifungo kwa walinzi wa Serengeti na watoto wao.

Mwekezaji ndani ya Serengeti hataki kuona mwananchi; anataka kuona watalii kutoka nje. Anataka kuona shilingi tu itokanayo na wanyamapori ambao wananchi wametunza na kuhifadhi kwa kipindi chote cha maisha yao.

Hapa pia wafugaji waliswagwa nje ya maeneo yao walikoishi, kufuga na kulinda wanyamapori. Wafugaji walilinda wanyamapori kwa kuwa hawawali; wao hula mifugo yao tu.

Hivi sasa wafugaji waliobaki Serengeti wanaishi kwa mfano uleule wa “ulimi katikati ya meno.” Wamefungwa. Wamebanwa mithili ya watumwa; katika nchi yao iliyopata uhuru wa kisiasa yapata miaka 50 iliyopita.

Yaliyotokea West Kilimanjaro, Monduli, Simanjiro, Kiteto na Serengeti, ndiyo hayohayo yaliyotokea Ngorongoro: Kuvamiwa kwa ardhi na kufukuzwa kwa wakazi wa miaka yote ili kuanzisha “Jamuhuri za Wanyamapori.”

Maeneo yote tuliyojadili yamekuwa yakiitwa Masailand – kuanzia Kilimanjaro Magharibi hadi Lobo – kwenye mpaka wa Kenya. Haya ndiyo yalikuwa makazi ya Wamasai.

Historia inasema Wamasai ni taifa linalotembea. Linalohamahama. Lina mifugo na linafuata maji na malisho. Lakini ukweli ni kwamba taifa hili lilikuwa limetua na kuridhika katika maeneo yaliyojadiliwa.

Kama ambavyo hakuna mwenye asili ya mahali alipo, kwamba vizazi vilivyotangulia viliumbiwa hapo (imani) au viligeukia hapo kutoka nyani wangurumao (sayansi), Wanilotiki kutoka milima ya Golani sasa walikuwa wametua na “ardhi” yao kupewa jina na wakoloni kuwa Masailand.

Jirani na Wamasai walikuwa Wabarbaig ambao pia katika miaka ya hivi karibuni walitendewa unyama huohuo wa kuporwa ardhi na kufukuzwa kwenye makazi yao na kuanza kutangantanga.

Mradi wa Basotu, Arusha wa kilimo kikubwa kilichoitwa “mashamba ya ngano ya Basotu” yaliyoendeshwa na Wakanada, uliwaacha Wabarbaig bila makazi.

Leo hii hakuna mashamba. Kilimo kimeshindikana. Yalikuwa mazingaombwe. Ardhi imechoka. Limebaki vumbi tupu. Wabarbaig waliishatupwa nje; wanatangatanga na mifugo yao.

Kwa mtindo huu, jamii za wafugaji zimefanywa za wakimbizi wasiotakiwa popote pale ndani ya nchi yao.

Soma majina haya: Lomnyak Siololo, Kayiok Leitura, Ngiliyayi Ndoinyo, Ngirimba Ndoinyo, Sepekita Kaura na Tokore Siololo. Hawa ni miongoni mwa waathirika wakuu wa mipango ya serikali iliyofukarisha wananchi na kuneemesha watu kutoka nje ya nchi.

Wananchi hawa, kutoka kijiji cha Ololosokwan, wamechomewa nyumba, mazizi ya ng’ombe na wanaswagwa, wao na ng’ombe wao, kutoka walikoishi kwenda kusikojulikana.

Ni kutokana na mfumo huu wa uvamizi na uporaji makazi, wafugaji wametafuta makazi na malisho katika maeneo mengine ya nchi hii. Ni nchi yao. Ni kwao kama kulivyo kwa wengine.

Tatizo hapa ni kwamba serikali, iliyoshiriki kuwafanya wafugaji kuwa watu wa kutangatanga kuliko asili yao, ndiyo inatangaza kuwa wafugaji “warudi kwao.”

Sasa wafugaji wanauliza” “Kwetu ni wapi?” Swali kubwa hapa ni hili: Wafugaji wakirudi kwao, itakuwaje?

Jibu: Vitatokea vita vikubwa vya kuangamiza watu na mali zao; kile kilichoimbwa kwa miaka mingi kuwa ni amani na utulivu wa nchi, kitatoweka kama ukungu wa asubuhi.

Kutatokea vita kwa kuwa maeneo walikofukuzwa wafugaji sasa ni mbuga za wanyama zilizomo mikononi mwa waporaji wakubwa wa maliasili wanaopewa upendeleo kwa kuitwa “wawekezaji.”

Unawekeza nini katika mbuga yenye wanyama waliolindwa na kuhifadhiwa na wafugaji kwa karne na karne? Hapana. Hapa unachuma usipopanda. Vita vya wafugaji kujaribu kurudi walikotoka vitakuwa vikubwa na huenda endelevu na kwa gharama kubwa ya maisha.

Wafugaji wakirudi walikotoka – Kilimanjaro Mashariki, Lorkisalie, Simanjiro, Kiteto na Basotu (Barbaig), kutakuwa na vita ambavyo vitaharibu mashamba ya “wakubwa,” majumba ya kifahari, mifumo ya maisha ambayo tayari imejengwa na kuangamiza uhai wa watu na viumbe vingine.

Bali amani pia haiwezi kuwepo kwa kuendelea kuwa na watu wanaofukuzwa kila waendapo kwa kuambiwa “rudi kwenu.”

Wakati umefika kwa serikali kufanya mambo yafuatayo, yakiwa hatua za haraka na za mwanzo ili kusitisha uonevu na udhalilishaji wa wafugaji na kuepusha migongano na hata vita:

Kwanza, kusimamisha na kuacha kabisa mipango ya kufukuza wafugaji kutoka makazi yao ya sasa. Hili litahusisha kuacha kuchoma moto makazi yao. Nchi hii ni yao.

Pili, kurejesha wafugaji mahali pao katika sehemu ambako walifukuzwa hivi karibuni na kupanga, kuunda na kutangaza makazi ya wafugaji na malisho ya mifugo yao.

Tatu, serikali isitishe na izuie uchochezi wa wanasiasa na baadhi ya watendaji wake kwa wafugaji waliohamishwa zamani, kwa kuwaambia kurejea walikotoka, kwani hilo litazua vita ya maangamizi makubwa.

Nne, wafugaji wakaribishwe pale walipo; waelezwe kuwa safari yao imefika mwisho; watengewe ardhi kwa makazi na malisho bila kujali walikotoka.

Tano, maeneo yaliyopangwa kwa ajili ya ufugaji yatengwe rasmi kwa alama zinazoonekana. Wafugaji wenye mifungo mingi, washirikishwe katika kugharimia miundombinu muwafaka katika mpangilio mpya.

Sita, serikali ijenge mahusiano mapya kati yake na wakulima badala ya kuwakemea na kuwalaani kwa madai dhaifu kuwa mifugo mingi “inaharibu mazingira.”

Saba, serikali iondokane na dharau na kutojali; badala yake itambue kuwa mifugo – mamilioni ya ng’ombe, mbuzi na kondoo wa wafugaji wanaotangatanga katika nchi yao – ni mali na kwamba kwa kuweka mazingira bora, itakuwa ya manufaa zaidi kwa wafugaji na taifa kwa jumla.

Nane, wafugaji washawishiwe na asasi za kijamii na serikali, “kusimama” na kubaki walipo sasa na kufanya makazi hayo kuwa ya kudumu.

Tisa, wafugaji washirikishwe katika kuandaa makazi, malisho na miundombinu. Kwa mfano, malisho yawe ya maeneo makubwa ambamo mifugo itahama kutoka sehemu moja kwenda nyingine, ndani ya eneo husika, ili kuruhusu upatikanaji wa chakula katika maeneo walikochungiwa kwanza.

Umuhimu wa kushirikisha wafugaji katika kuandaa miundombinu unatokana na kuwepo kwa baadhi yao wenye uwezo kifedha kutokana na kuwa na mifugo mingi.

Ni hao ambao wana uwezo wa kuchangia ujenzi wa mipaka ya kutenganisha makazi na malisho, kujenga mabwawa wakati serikali inasaidia katika ujenzi wa miundombinu mingine kama ile ya maji, elimu, barabara na afya.

Kumi, ndani ya mipaka ya maeneo ya malisho, na wafugaji wakiwa sehemu ya jamii ya wakulima katika maeneo husika, ndimo inaweza kuendeshwa elimu juu ya upunguzaji wa mifugo kwa ufugaji wa kisasa.

Hatua hii itakayoendana na wafugaji kukataa kuendelea kusukumwa nje ya mahali walipo, itajenga mshikamano mkubwa kati ya wakulima na wafugaji na kufanya uhasama kuwa historia.

Nilipata fursa ya kuongea na Luteni mstaafu Lepilall ole Molloimet (60) kuhusu suala hili. Aliwahi kuwa mbunge kwa miaka tisa, mkuu wa wilaya kwa miaka 12 katika wilaya za Kiteto, Babati, Korogwe, Musona na Rombo.

Molloimet ambaye sasa ni mfanyabiashara, anasema wakati umefika kwa Wamasai na wafugaji wengine kukataa kuhama kutoka walipo sasa.

Anasema, “Wamasai wabaki pale walipo. Wakatae kuondoka. Washiriki elimu lakini wabaki na mila na desturi zao nzuri; wachague viongozi wao wazuri, wajiamini, wawe jasiri na wakatae kuonewa; wawe tayari kukosoa na kukosolewa.”

Molloimet anasema anawashangaa wabunge katika maeneo ambako wananchi wanaswagwa kama mifugo kutoka kwenye makazi yao ya miaka mingi. Anasema wabunge hao, kwa kukaa kimya, ina maana wanaunga mkono unyama ambao wananchi wanatendewa.

“Kwa ufupi, wabunge hawa wanastahili kujiuzulu maana wameshindwa kazi ya kuwakilisha na kutetea waliowachagua,” anasema Molloimet.

Akiongea kwa sauti ya uchungu, Molloimet anaungana na baadhi ya wananchi wa Olorien, Soitsambu na Magaiduru-Lorien huko Ngorongoro.

Amasema, “Dunia haituelewi. Tunafukuza Wamasai katika maeneo yao; lakini tunakaribisha Wazungu na Waarabu! Nani atatuelewa. Mimi nasema tu kwamba wafugaji wanataka amani.”

Taarifa zinasema juzi Jumatatu, ulifanyika mkutano juu ya hali ya wafugaji na hifadhi ya Loliondo. Miongoni mwa waliohudhuria mkutano huo katika kijiji cha Ololosokwan ni wawakilishi wa Chama cha Wanasheria wa Mazingira (LEAT).

Wengine ni asasi ya kimataifa ya utetezi wa wafugaji tawi la Tanzania (PINGOs), maofisa wa Idara ya Wanyamapori, Ortelo Business Corporation Limited ya Nchi za Falme za Kiarabu (OBC) walioshikilia eneo kubwa ya mbuga ya Loliondo na wajumbe wa kijiji cha Ololosokwan.

Haijafahamika waliongelea nini. Lakini taarifa zinasema watakuwa walijadili hatua ya serikali ya kuchoma makazi na maboma ya mifugo wakilazimisha wananchi kutoka kwenye makazi yao na katika vijiji vilivyoandikishwa kisheria.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com

(Makala hii itachapishwa katika gazeti la MwanaHALISI toleo la 12 Agosti 2009)

Saturday, August 1, 2009

KUSAJILI SIMU ZA MKONONI NI UHALIFU



BADALA YA KUVUMBUA WANADIDIMIZA TEKNOLOJIA



Na Ndimara Tegambwage

SITAKI mpango wa kusajili wamiliki wa simu za mkononi na namba zao kama serikali inavyotaka na kama inavyoshinikiza.

Hii ni kwa kuwa sababu zilizotolewa na serikali; na kusisitizwa na Mamlaka ya Udhibiti ya Mawasiliano Tanzania (TCRA); zile ambazo zinatumiwa kuhalalisha usajili; siyo za msingi na hazina mashiko.

Serikali ina maoni kuwa simu za mkononi zinatumiwa vibaya. Inadai zinatumiwa kufanya uhalifu. Kwamba zinarahisisha mawasiliano ya wale wanaopanga uhalifu.

Uhalifu unaotajwa ni pamoja na kutukana, kupanga wizi na, au hujuma; kutoa vitisho kwa watu mbalimbali; kutoa taarifa za upotoshaji na wakati wote huo bila muhusika kufahamika.

Inadaiwa kuwa namba na wamiliki wakisajiliwa, itakuwa rahisi kujua nani ametoa taarifa, uzushi, vitisho; na kupitia namba ipi ya simu. Serikali inafikiri kwa njia hii, kazi yake ya “ulinzi wa amani” itakuwa imerahisishwa.

Hii ina maana kwamba serikali na wenye makampuni ya kutoa huduma za simu za mkononi, wamekula njama. Wamekubaliana kuingilia mawasiliano ya wananchi na labda wamekuwa wakifanya hivyo, tena kwa kiwango kikubwa.

Uhalifu hauletwi na simu. Uhalifu hauletwi na siri katika mawasiliano. Vyombo vya mawasiliano ni mifereji ya kupitishia taarifa. Unahitaji mawasiliano mapana kukabili uhalifu.

Katika mazingira ambamo waliopewa jukumu la kuzuia uhalifu ndio wenyewe wanaofanya uhalifu; unahitaji vyanzo vya siri vya kuibua uhalifu. Pale penye uhalifu unaofanywa na watawala na wateule wao, unahitaji mifereji isiyo bayana.

Katika mazingira ambamo aliyeibua uhalifu anatendewa kama mhalifu; na wakati mwingine jina lake kuwekwa wazi kwa wahalifu – wawe wakwapuzi wa mabilioni benki, wauza dawa za kulevya au majambazi yaliyokubuhu – unahitaji mifereji ya mawasiliano isiyo bayana.

Tujenge hoja kuwa mtu asiyejulikana, ambaye amekupelekea simu ya vitisho kupitia namba ya simu isiyojulikana ya nani, basi ameshindwa kutekeleza anachotaka. Tumuone kama anayetishia tu.

Bali inawezekana akawa anatishia kweli. Hapo atakuwa ametoa onyo; amekupa muda wa kujipekua na kujiandaa. Simu hiyo pia yaweza kukupa fursa ya kuacha kile ulichokuwa ukifanya na ambacho tayari wengine wameona hakifai au kinawadhuru.

Katika mazingira ya Tanzania, taarifa juu ya kifo cha mahabusu ambaye maofisa wa magereza hawataki kijulikane, inapatikana kwa mfereji wa siri wa mawasiliano – simu isiyoweza kutambulika.

Orodha za wahalifu walioko serikalini, karibu sana na watawala wakuu, inafikia vyombo vya habari kwa njia ya simu ya siri. Maagizo ya siri ya kuumba au kuua, yanapatikana kwa njia ya namba ya simu isiyosajiliwa.

Kilio cha wananchi wakazi wa Kilosa, mkoani Morogoro na Ololosakwani, mkoani Arusha juu ya unyama wanaotendewa, kinafikia vyombo vya habari, watawala na dunia nje ya nchi, kwa njia ya simu isiyopekuliwa.

Dereva wa mbunge ambaye hajalipwa mshahara wake kwa miezi sita, anatumia namba isiyosajiliwa kuwasiliana na vyombo vya habari na hata spika wa bunge ili angalau kilio chake kiweze kusikika na yeye apate kushughulikiwa.

Hayo ndiyo matakwa ya mazingira ya sasa. Dereva akijulikana kuwa analalamika, basi anafukuzwa kazi. Karani akifahamika kuwa “amevujisha” majina ya wezi idarani, anafukuzwa kazi palepale.

Ofisa Utumishi akijulikana kuwa hakushirikishwa katika ajira ya watoto wa bosi wake, siyo tu atafukuzwa kazi; aweza kuundiwa kosa kubwa hata la kufikishwa mahakamani.

Mfugaji wa Kilosa na Ololosakwani akijulikana kuwa ni yeye aliyepeleka taarifa za askari wa FFU kuchoma nyumba zao na kutesa wananchi, huenda “akapotezwa” katika mazingira ya kutatanisha.

Tetesi nyingi kwa vyombo vya habari, watumishi makini na waaminifu ndani ya serikali, taasisi zake na hata makampuni na mashirika binafsi; zinapatikana kwa mifereji ya siri, kwa kuwa “uwazi” limekuwa neno tupu la wanasiasa na halimo katika utendaji.

Tetesi hizi zimekuwa muhimu kwa hatua za kwanza za uchunguzi. Wakati aliye karibu aweza kukuona na kuongea nawe, aliye mbali anapata fursa ya kukupa taarifa bila wasiwasi wa kuchukuliwa hatua na wale wanaodaiwa kutenda uhalifu.

Aidha, wakati baadhi ya waandishi wa habari wamesahau au wamedharau msingi muhimu wa “kutunza chanzo cha taarifa,” baadhi wametaja majina ya waliowapa taarifa na kuwaweka hatarini.

Simu ambazo haziwezi kuingiliwa ni nyenzo kuu ya wananchi na wafanyakazi waliomo katika karakati za kupigania uhuru na haki zao. Watapanga jinsi ya kukutana hadi jinsi ya kufanya walichopanga.

Asasi za kijamii zilizomo katika ushawishi ainaaina, huweza kutumia njia hii ya simu isiyo wazi ili taarifa zisivuje, hadi hatua ya mwisho iliyolengwa na kufanya hoja zao kuibuka kwa kishindo na labda kupatikana kwa mafanikio yaliyotarajiwa.

Uhalifu hauletwi na simu za mkononi ambazo namba zake na wamiliki hawajulikani kwa watawala. Nyenzo hii ya mawasiliano ya teknolojia ya kisasa inaweza kutumiwa na mkweli au mwongo; mtiifu au mwasi; mwaminifu au mkora, “mungu” au “shetani.”

Aliwahi kusema Karl Marx, kuwa uhalifu ni tasnia pana inayoajiri kuanzia mtu wa kada ya chini kabisa kama mesenja hadi profesa wa masuala ya jinai. Hapa kuna hoja ya “uendelevu.”

Kadri jamii zinavyopita katika nyakati tofauti za maendeleo na kuingia na kutoka katika ustaarabu tofauti, ndivyo zinavyokumbana na matatizo mapya na changamoto mbalimbali.

Mlango wa kusumumiza hautoshi kuziua mwizi. Chomeko siyo tena chombo cha ulinzi. Kofuli haifai tena kulinda nyumba. Magrili yanatawanywa kwa moto wa gesi.

Kukua kwa maarifa ya kuhudumia jamii kunaenda sambamba na uvumbuzi katika tasnia ya uhalifu. Huwezi kuzuia hili. Lakini serikali inakwenda mbali. Inafikiri kuwa simu ambazo haijui ni za nani, zinaleta au zinachochea uhalifu(!?) Huu ni udhaifu mbaya.

Badala ya kutafuta mbinu za kisasa za kukabiliana na kile wanachoona ni tatizo, serikali na makampuni ya simu wanatafuta kufanya teknolojia na matumizi yake kuwa butu. Huu ni mkasa.

Serikali inaziba mifereji ya taarifa za siri kuhusu utendaji wake. Hasa kuziba kasi ya kuenea kwa taarifa juu ya mambo inayofanya lakini hayakustahili kufanywa na waliopewa madaraka ya utawala.

Hapa serikali imeingilia uhuru wa mawasiliano wa mtu binafsi. Inakana maendeleo ya teknolojia. Inaziba upenyo wa kupitishia kilio na tetesi. Serikali inatenda uhalifu.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
(Makala hii iichapishwa katika gazeti la Tanzania daima Jumapili, toleo la 22 Julai 2009)

KASHFA YA MEREMETA YAWEZA KUZAMISHA SERIKALI



MAWE YAKISEMA, SERIKALI ITAUMBUKA


Na Ndimara Tegambwage


SITAKI waziri Jeremiah Sumari achokoze Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), kwa kutumwa au kwa sababu zake binafsi.

Majeshi ni mawe makubwa. Majabali. Miamba. Majeshi ni wagumba. Majeshi yakitaka kuzaa sharti yakubali kufa polepole; kwa maana kwamba atokee wa kuyapasua ili yatoke mengi kwenye mawe makubwa au miamba. Hapo hayabaki mojamoja na imara tena.

Na kawaida majeshi ya nchi hayachokozwi na mtu wa ndani wala wa nje. Wachokozi huchokoza nchi na watawala wa nchi zilizochokozwa huagiza majeshi yake kwenda mstari wa mbele na kukunja uchokozi kama jamvi la wageni.

Lakini uchokozi uliofanywa na waziri Sumari ni wa ndani na unaweza kufanya mawe makubwa, miamba kutamani kutoa sauti na kusema hayataki kupasuliwa; yaachwe kama yalivyo.

Akijibu swali la Dk. Willibrod Slaa juu ya ufisadi ndani ya mradi wa Meremeta, Sumari alitoa majibu ya vitisho. Alimwambia mwakilishi wa Karatu (CHADEMA) aachane na hoja ya ufisadi ndani ya Meremeta.

Kiasi kinachodaiwa kupitia Meremeta kwenda mifuko isiyojulikana si haba. Ni zaidi ya Sh. 155 bilioni. Waziri anamwambia mbunge aachane na hoja ya Meremeta kwa madai kuwa mradi huo ulikuwa wa jeshi; kwamba ni suala nyeti na labda ni kuingilia suala la usalama wa taifa.

Waziri anataka kulazimisha mawe kusema. Mawe yatabaki kimya juu ya ahadi zao; juu ya mipango yao na silaha zao; juu ya mikakati ya sasa na baadaye; juu ya mbinu mpya walizopata katika medani ya vita; juu ya wanachopanga kufanya hivi sasa.

Ukimya huu ni kama jua, mvua na upepo vipigapo kwenye mwamba na mwamba ukavumilia. Zaidi ya hapo, miamba husema. Miamba mingi imeota juu ya mizimu ya kale iongeayo wakati wa jua kali.

Inawezekana, siku moja unapita karibu na miamba hiyo, wakati wa jua kali, ukasikia mtu akikuita kwa sauti ya juu sana – mara mbili au mara tatu – na usimwone.

Wale dhaifu wa moyo huweza kuanguka chini na kuzimia; wengine humudu kukimbia hadi nyumbani kwao, wakitweta na kulowa jasho mwili mzima huku wakiishiwa na kauli. Mawe, majabali, miamba imeamua kusema!

Wakati huo hujawahi kuichokoza. Hujailalamikia wala kuituhumu. Hujaisingizia wala kuihusisha katika miradi bubu ya watawala. Inasema tu. Inabubujika. Sembuse utakapoihusisha na wizi, uporaji, ukwapuaji, au kwa ujumla – ufisadi!

Ikae kimya? Sitaki waziri Sumari achokoze miamba na yenyewe iseme kwamba haijui Meremeta ni nini na ya nani. Kwamba haijawahi kunufaika na kampuni hiyo. Kwamba mafao yaliyotokana na Meremeta hayafahamiki jeshini. Kwamba hayakuingia jeshini.

Sitaki waziri achokoze miamba ianze kukohoa na kunong’ona na hatimaye kulipuka. Miamba hii inajua kuwa fedha za kuendesha jeshi hutoka kwenye bajeti ya serikali inayosomwa na kupitishwa bungeni.

Miamba hii inaelewa vema kwamba wakati Meremeta wanaanzisha mradi walihamisha wananchi kutoka makazi yao. Walihamisha hata kambi ya Jeshi la Kujenga Taifa na kutawanya askari katika vijiji kwa kutumia mikokoteni.

Si wananchi – raia, wala askari walionufaika na mafao ya Maremeta baada ya kuanza kuvuna kutokana na mgodi. Shule na zahanati vilivyong’olewa havijarudishwa. Bwawa kubwa la maji lililokuwa sehemu ya uhai wa watu na viumbe anuwai, halijarejeshewa hadhi yake.

Sitaki watawala jeshini wajitokeze na kuiumbua serikali juu ya matumizi haya. Sitaki wapatikane watumishi wa Wizara ya Ulinzi na kuthibitisha kuwa hawajawahi kupanga fedha za Meremeta au sehemu yake katika matumizi ya wizara.

Sitaki maofisa wa ngazi za kati jeshi waanze kufurukuta na kusema hawataki kusingiziwa katika suala la ukwapuaji na hivyo kujitokeza na ukweli utakaoangamniza hadhi ndogo ya watawala iliyosalia.

Sitaki askari wa vyeo vya chini ambao wanajua vema kilichokuwa kinaendelea waanze kujitokeza na kusema walichoona na nani hasa walikuwa wavunaji wakuu wa Meremeta na siyo jeshi.

Wala sitaki askari wakumbushe serikali kwamba Tume ya Jaji Bomani iliishasema kuwa Meremeta si mali ya serikali bali ni ya binafsi. Labda likisemwa na wao ndipo serikali itasikia na waziri Sumari ataelewa.

Nani anataka azibuliwe masikio kuliko alivyofanya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali. Aliiambia Kamati ya Bunge kuwa Meremeta haimo katika orodha ya mashirika ya umma na kwamba ofisi yake haijawahi kuikagua.

Mei mwaka jana tulipeleka baruapepe kwa benki ya Nedcor Trade Services ya Afrika Kusini kuhusiana na suala hili. Hatukujibiwa. Tuliwaandikia Deutsche Bank AG ya Uingereza. Hawakujibu.

Lakini kwa kufuatilia kinachoendelea ni kwamba serikali haifanyi lolote. Imetafuta mahali pa kuegesha na kusahau hoja za wananchi wanaotaka kujua huyu Meremeta ni nani na fedha alizochota alizitumia wapi.

Matumizi ya visingizio vya jeshi, kama anavyosema Sumari, hayana uzito tena. Hayamtishi yeyote. Wananchi, wachunguzi na wengine wanaotafuta ukweli wangestuka na hata kuogopa kama wangekuwa wameingilia undani wa shughuli za jeshi.

Lakini hili la kikampuni cha Meremeta halimtishi mtu. Badala yake linaweza kuiweka serikali pabaya, kwani inaendelea kujichanganya; kuficha ukweli na hatimaye kusema uwongo.

Hatari kubwa inaweza kuzuka pale mawe, majabali na miamba itakaoamua kuvunja kimya; siyo lazima kwa mikutano ya hadhara bali kwa mn’ong’ono tu ambao hatimaye utavuma kama upepo wa kimbunga.

Na askari – hiyo miamba – ni watoto wa watu masikini na wao ni masikini pia. Hawana cha kupoteza kwa kusema ukweli wanaoujua. Hapo ndipo serikali itaumbuka zaidi.

Nani anaweza kuiondolea aibu serikali kwa kusema ukweli na kuijengea heshima na uhalali? Kama siyo mawaziri wake, nani hasa? Tusubiri majabali yaite wakati wa jua kali na kwa mzizimo wahusika wazimie?

Uwezekano wa aliyezimia kupitiliza hadi dunia nyingine ni mkubwa kuliko aliyesimama. Kwa nini serikali ijiingize kwenye majaribu tata? Ukimya unaidhalilisha serikali na kuiondolewa uhalali. Itoboe kilichomo ndani ya Meremeta.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
(Makala hii ilichapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili Juni 2009)

WOGA WA SERIKALI SASA WAPINDUKIA



Serikali inapotishia uhuru wa mijadala



Na Ndimara Tegambwage

SITAKI watawala wakatae Waraka wa Kanisa Katoliki ambao hasa ni elimu ya uraia ambayo ni mhimu kwa maisha ya kiroho, kijamii, kisiasa na kiuchumi kwa wananchi na taifa lao.

Kwa upande wa watawala, kukataa elimu kunaweza kuonekana kuwa jambo la kawaida; kwani kwao, elimu ambayo haikutolewa na watawala, siku zote huonekana ama yenye kasoro au isiyofaa kabisa.

Kitu kibaya zaidi ni kwa watawala kutaka kuzuia raia kusambaza elimu ya uraia kwa jamii kupitia asasi zao. Ni kama inavyodhihirika sasa kwa baadhi ya walioko kwenye utawala kupinga Waraka wa madhehebu ya Katoliki unaochokoza mawazo tu juu ya kupata viongozi bora nchini.

Nimesoma waraka husika. Maudhui ni yaleyale ambayo tumezoea kuyasikia kanisani, misikitini na katika maoni ya watu wanaojali maslahi ya taifa. Lakini mara hii yameandikwa. Yamewekwa kwenye hali ya kudumu kwa muda mrefu na yataweza kufanyiwa rejea.

Kwa ufupi waraka ni wito kwa wananchi kukaa chini, kujadili na kuamua nani wanastahili kuchaguliwa kuwaongoza; wawe watu wa mwenendo na tabia gani. Sikuona zaidi.

Waraka unafanya jambo moja kubwa ambalo watawala hawataki kusikia. Unawapa wananchi fursa, uwezo na ujasiri wa kujadili na kuamua nani wawachague kuwa viongozi wao. Basi.

Waraka unahimiza utekelezaji wa haki ya kila raia katika kupata uongozi; unahimiza wajibu wa kushiriki katika kuchagua viongozi na uongozi, kuanzia ngazi ya chini kabisa hadi ya taifa.

Ni waraka huu unaohimiza njia ya kukaa pamoja, kufanya uchambuzi na ikiwezekana kukubaliana juu ya vigezo vya kijamii mahali husika katika kupata viongozi.

Lakini hata baada ya majadiliano ya pamoja, bado kila raia ana uwezo na haki ya kupima nani, kati ya wagombea, anazidi wengine na anaweza kuwa kiongozi bora.

Waraka unasaidia kuchokoza mbongo za washiriki katika mjadala kwa kueleza kiongozi bora ni nani. Huu ni uchokozi tu. Katika mjadala, wahusika waweza kutanua wigo wa waraka na kugusa hata hoja ambazo hazijafukuliwa na kuweka vigezo vyao. Hawafungwi.

Kupatikana kwa mwafaka wa vikundi, makundi au jumuia pana juu ya nani wanafaa kuongoza, kunawatwisha wapigakura wajibu wa kipekee wa kufuatilia viongozi na utendaji wao.

Labda ni hapa ambapo watawala wanapata shida kuelewa au wanaelewa lakini wanaogopa. Wanafikiri kuwa zinaweza kupatikana kura za makundi na wao kuenguliwa kwa njia ya sanduku la kura.

Bali ni ukweli usiopingika kuwa ujinga na umasikini ni mitaji mikubwa ya watawala. Kadri raia wengi wanavyobaki katika ujinga ndindindi, ndivyo watawala wanavyozidi kujichimbia ikulu mwaka baada ya mwaka.

Kama kuna kitu kinaitwa elimu ya uraia ambayo hutolewa na watawala, basi ni ile ya kueleza uwezo wa serikali, majukumu yake, mafanikio yake, utii na heshima ya raia kwa mamlaka. Ni vitisho vitupu vinavyopora ujasiri wa wananchi na kuzidisha upofu na ujinga.

Woga mkubwa wa serikali ni kwamba wananchi wakijua kinachoendelea ndani ya utawala, wataasi kimyakimya au watalipuka na kudai mabadiliko.

Katika hali hii, ikipatikana elimu ya kufanya watu wafikiri, wajadili kwa pamoja hoja kuu zinazowahusu; zinazohusu uhusiano wao na watawala na jinsi ya kufanya maamuzi; basi serikali hujawa na woga.

Ujasiri uliolengwa kupatikana kwa njia ya waraka wa kanisa unatishia “elimu” ya watawala; unabomoa kuta za siri, unaandaa jamii kuachana na ujinga na kuasisi mabadiliko ya fikra, bila kujali rangi, mahali mtu alipozaliwa wala imani.

Kanisa lisipofanya haya, na hasa leo, litabaki asasi kama asasi nyingine zisizo na uhai. Asasi zote, yakiwemo madhehebu, hazina budi kutambua kuwa haziwezi kuhudumia kiroho wale ambao ni dhaifu kimwili. Sharti zisimame nao na kuwapa ujasiri wa kufikiri na kutenda.

Mahali pengine, kuhubiri dini kwa watu masikini kumeongeza ukandamizaji. Wakati watawala wameishi katika uhondo, wametumia ghiliba ya kisiasa na mahubiri ya dini kufanya raia wawe butu zaidi na kulazimishwa kukiri kuwa hali waliyomo ndio matakwa ya Mwenyezi Mungu.

Hatua ya baadhi ya madhehebu kufundisha umuhimu wa kuwa na jamii inayofikiri, inayoelewa kinachotendwa na watawala, inayodai haki na inayojadili jinsi ya kuwa na viongozi na uongozi bora, ni ya kukaribisha na siyo kusuta.

Walioingia katika uongozi kwa njia ya wizi, ghiliba, upendeleo na hujuma kwa wengine, ndio wanaweza kutilia mashaka fursa mwanana ya wapigakura kukaa pamoja na kujadili jinsi ya kupata viongozi bora.

Kuna swali: Kila madhehebu yakitoa waraka wa uchaguzi itakuwaje? Jibu: Kwa kuzingatia maudhui ya waraka wa kanisa Katoliki, madhehebu mengine yatasema mambo hayohayo lakini kwa maneno tofauti.

Hoja ya kuwa na kiongozi bora haina sura ya madhehebu. Hoja ya kukaa chini na kujadili nani katika jamii yenu anaweza kuwa kiongozi, haina hata harufu ya madhehebu.

Hoja ya uongozi bora ina misingi katika utu wa mtu na haki ya kila raia bila kulalia imani za dini – za asili na za kuja – isipokuwa pale imani hizo zinapokuwa zinakiri kwelikweli kile tunachotaka: Haki.

Kwa hiyo, katika mazingira ya uhuru wa maoni, siyo madhehebu tu yenye haki ya kutoa elimu ya uraia kwa kutumia waraka; bali mashirika na asasi zote za kiraia na watu binafsi.

Kinachohitajika siyo madhehebu au imani ya mtu au asasi, bali hoja ya kiongozi bora kutoka katika jamii na bila kujali ni wa madhehebu yapi.

Elimu ya uraia inayopendekezwa na waraka wa sasa, haifuti wala kudhoofisha sifa za mgombea uongozi au mpiga kura ambazo zinatajwa na Katiba ya nchi.

Hivyo ndivyo zinaweza kuwa nyaraka nyingine za madhehebu mengine, asasi nyingine, mashirika mengine na watu binafsi. Zitakuwa zinaimarisha sifa na misingi ya Katiba kwa kuwezesha raia kushiriki vya kutosha na kutumia utashi wao kupata viongozi bora.

Waraka uwe mwanzo tu. Tunatamani pamoja na viongozi wa dini kuombea amani na utulivu, waanze kufikiria kuacha kuombea watawala na kuwafanya sehemu ya utukufu wa Mungu.

Ni maombi ya viongozi wa madhehebu mbalimbali ambayo yamesimika madikiteta; kuwadumisha kwenye tawala na kuwaaminisha wananchi kuwa mamlaka waliyonayo (madikiteta) inatoka kwa Mungu.

Sharti wanaoogopa waraka wa kanisa Katoliki waanze kuogopa kutoombewa na kubarikiwa. Labda huu ndio utakuwa mwisho wa mwanzo wa kutenda mema.

0713 614872
ndimara@yahoo.com
(Makala hii itachapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili toleo la 2 Julai 2009)