Serikali isiyojali maisha ya ‘Masalia’
Na Ndimara Tegambwage
SITAKI serikali ichukue nafasi ya mtazamaji tu pale maisha ya watu yanapokuwa hatarini; hata kwa madai kuwa huo ni utashi wa waliomo hatarini.
Hili linahusu wale wanaojiita Wasabato Masalia. Hii ni klabu ya wanaojiita waumini katika imani fulani wanayoona inaweza kuwafikisha kwa Mungu au kuwaweka katika njia ielekeayo kwake.
Waumini hawa wanajiita “masalia.” Kwa jina hilo tu, utaona kuwa wao ni “mabaki.” Yaweza kuwa mabaki baada ya wenzao kuangamia au kupotea. Yaweza kuwa mabaki baada ya kuchekecha na wao kubaki makapi. Yaweza kuwa mabaki kwa uamuzi wao kuwa watabaki walivyo na hawataki kubadilishwa.
Katika hali ya kawaida, masalia ni masazo; yale yaliyoachwa, siyo kwa utashi wa masazo bali kwa utashi wa waliokuwa na uamuzi. Hatua ya kijiita masalia au masazo ni hatua ya kukata tamaa. Hatua ya kuwekwa pembeni na hata kutengwa.
Wasabato Masalia walitoka mikoa mbalimbali nchini na kwenda Dar es Salam kwa shabaha moja: Kutumia uwanja wa ndege wa kimataifa – Julius Nyerere Airport (JNA) kwenda sehemu mbalimbali za dunia kuhubiri “Neno la Bwana.”
Kilichowakwamisha hakina uhusiano na masuala ya jinsia; kwamba walitaka kuhubiri “Neno la Bwana” bila kuhubiri “Neno la Bibi.” Walikwamishwa na sheria, kanuni na taratibu za safari.
Walitaka kukaa uwanja wa ndege JNA, hadi hapo “Bwana” atakapoamua kuwachukua, tena kwa ndege, bila wao kuwa na pasipoti; bila vibali vya kusafiria kwenda nchi za nje (viza) na bila tiketi.
Hiyo ni miezi tisa iliyopita. Walikuwa 52; sasa wamebaki 30. Kuna madai kuwa hao pungufu (12) wameachana na imani isiyotekelezeka. Hilo laweza kuwa kweli au si kweli. Bali hao 30 bado wanakaa Tabata-Segerea, kwenye viunga vya Dar es Salaam wakisubiri “meli ya angani” iwapeleke kuhubiri nchi za nje.
Kwa kipindi chote, serikali imekaa kimya, ikiangalia mabaki ya wasabato yakilazimisha pumzi kutoka ndani ya miili yao, lakini bila mafanikio. Na kwa kuwa wameachwa bila ukaguzi, uangalizi na ufuatiliaji wa karibu, yawezekana hata hao 20 wanaosemekena kukana imani, siyo kwamba wamehama kambi, bali wamekufa.
Usiri uliowaweka pamoja katika kuamini kisichoaminika wala kuaminiwa; ni usiri huohuo unaoweza kuwafanya wasitoe taarifa juu ya wagonjwa na waliokufa.
Kushindikana kwa utekelezaji wa mpango wao; au tuseme ile hatua ya Mungu ya kukataa kuwapelekea ndege isiyodai pasipoti, nauli na tiketi wala viza; mawili haya yanawafanya waone aibu na hivyo kushindwa kurejea kwenye jamii za awali.
Ving’ang’anizi au masalia waliosalia kati ya 50 wa awali, waweza kuitwa wenye “imani kali.” Maana ya imani kali (entuhi), ni ukaidi usio na mipaka; usiojali hoja, fikra wala hekima. Katika hili mambo kadhaa yaweza kujitokeza.
Kwanza, masalia waweza kuendelea kuishi Segerea; wakiugua na hata kufa mmojammoja na kimyakimya, hadi pasiwepo na masalia wa masalia.
Pili, masalia waliosalia au watakaokuwa wamesalia hapo baadaye, waweza kuamua kutorudi makwao; wakatawanyika miongoni mwa jamii wanamoishi na kuwa mzigo kwa jamii hiyo ambako watakuwa ombaomba hadi mwisho wa uhai wao.
Tatu, masalia wa masalia waweza, hasa baada ya kuona Mungu amekataa au amedharau au ameshindwa kuwapelekea ndege, kuamua kuondoa maisha yao, tena kwa pamoja, ili kukwepa kimbunga cha aibu na hasira ya wanafamilia wao.
Nne, masalia wa masalia waweza kuanzisha ushawishi mpya; tena kwa nguvu zaidi; kupata wafuasi wengine wanaojifikiria kuwa wameachwa na kwa pamoja kuunda jamii ya waliosazwa – wasiolima, wasiochuuza wala kufanya kazi yoyote, bali kuwa waumini wa kisichoaminiwa na kubaki ombaomba.
Tano, masalia wa masalia wanaendelea kujamiiana na kuzaa watoto masalia wa masalia wa masalia. Kizazi hiki ni bomu kubwa na hatari kwa maisha yao wenyewe na taifa kwa ujumla.
Sita, masalia waliofikia hatua ya kujiaminisha kuwa Mungu atawapelekea ndege ili wasafiri bwerere kwenda watakako duniani kote, tayati ni watu hatari kwao wenyewe na jamii wanamoishi. Mbegu yao yaweza kuzaa gugu lenye uwezo wa kuangamiza bustani za fikra na hekima.
Lakini serikali imekaa kimya juu ya maisha ya hatari ya wasabato masalia. Na hapa hatuongelei imani. Hakuna imani hapa! Kuna kuemewa kwa akili ambako kuna msingi katika mambo mengi yakiwemo, umasikini uliokithiri na ujinga uliowazonga na kuwafanya kujifungia na kufanya kazi moja tu maishani: Kuomba.
Alikuwa Mama Theresa wa Calcutta (mzaliwa wa Albania); mtumishi wa watu aliyejizolea heshima na utukufu kwa njia ya kutumikia watu. Siku moja alikuta masista aliokuwa akifanya nao kazi wametoka kwenda “kusali.” Aliwashangaa sana.
Katikati ya kitongoji cha Calcutta; jiji linalochukuliwa kuwa chafu zaidi na lililojaa masikini wa viwango vya kufa nchini India, Mama Theresa alikemea mtindo wa kusali, kusali, kusali!
Aliwaambia masista, walipokuwa wamerejea kutoka kusali, kwamba kamwe wasithubutu tena kuweka muda maalum wa kusali.
Alisema, kwa kila tendo jema wanalofanya – iwe kuosha vidonda vya masikini, vya waliopata ajali, kulisha walio taabani na hata kusikiliza matatizo ya wanyonge – wanakuwa wamesali. Kusali kwa njia ya vitendo. Kusali kwa njia ya utumishi. Kusali na kutukuza Mungu kwa njia ya kutumikia wengine na kujitumikia.
Leo, katika viunga vya jiji la Dar es Salaam, wasabato masalia wanajiua polepole – kwa kukaa na kuomba; kusubiri kisichopo; kutokuwa hata na kazi ndogo ya kujilisha, wao na familia zao; wanatenda jinai ya kujaribu kuondoa uhai wao kwa kisingizio cha kuomba Mungu na kusubiri maajabu.
Hakuna mwenye busara ambaye atapendekeza serikali itumie nguvu kukamata na kuondosha masalia. Wala hakuna mwenye busara atakayependekeza serikali iache masalia wafe kwa kisingizio cha “demokrasi na uhuru wa kuabudu.”
Kuwaacha wafe mmojammoja au hata kwa makundi, ni kukiri kushindwa wajibu wa kulinda watu/raia na mali zao – jukumu kuu la serikali. Na masalia hawajaisha kabisa. Bado wana uhai na walichonacho ndiyo mali iliyosalia.
Serikali inayojali yaweza kuokoa maisha ya Wasabato Masalia. Na itende.
0713 614872
ndimara@yahoo.com
(Makala hii itachapishwa katika Toleo la Tanzania Daima Jumapili la 22 Machi 2009 katika safu ya SITAKI)
Saturday, March 21, 2009
Friday, March 6, 2009
Uwongo wa Butiku, Kitine na Warioba
Na Ndimara Tegambwage
Uwongo wa Butiku, Kitine na Warioba
SITAKI kusikia vilio vya wasioambilika. Hapa Joseph Butiku. Kule Joseph Warioba. Huku Hassy Kitine. Sitaki!
Sasa imekuwa nongwa. Tumsikilize nani? Mara Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimepoteza dira. Mara nchi inaendeshwa kienyeji. Mara CCM inatapatapa. Tumsikilize nani na nani hasa mkweli.
Wewe ni mwanachama wa chama kikongwe. Kilichokupa madaraka hadi ukayachoka au hadi kikakunyang’anya. Bado umo tu – CCM ndiyo baba, CCM ndiyo mama! Halafu unalalama kila kukicha: CCM mbaya! Hawana uongozi. Hawana dira.
Hivi nani hasa atakuamini? Unatafuta nini wewe mwenye dira mahali ambako hakuna dira? Nani kakushikia huko? Utamu upi usioweza kuutema?
Imetokea vipi ukawa na dira katikati ya wasio na dira? Au dira ipo na wewe umeanza kushindwa kuisoma. Au dira imepotea kweli na wewe unasema, “potelea mbali” tutakufa wengi huko anga za mbali au maji marefu. Hutaki kuachana na chombo ingawa una mwavuli; ingawa una chombo cha kuelea. Unataka kuponea humohumo au kufia humohumo.
Eh! Hata baada ya kujua kuwa chombo chako hakina dira; waongozaji wanatapatapa na chombo chenyewe kinaendeshwa kienyeji; bado hutoki? Hivi wewe ukoje? Ni kauli za dhati au za kufurahisha baraza?
Hivi ni kweli dira ya CCM imetoweka au wajanja wameipoteza, kwa hiyo haipo? Nani alikuwa ameishikilia mara ya mwisho? Ameiweka wapi? Yeye anasemaje? Amehojiwa? Au dira ipo lakini “wazee” hawa hawawezi tena kusoma; hawawezi tena kuelewa hata wakisoma?
Sikiliza. Kitine anasema hali iliyopo inahatarisha “usalama wa taifa.” Anasema nchi inaendeshwa kienyeji; uchumi na maliasili za taifa vimeshikwa na wageni wakati wazalendo wakifangia barabara na kufanya kazi za uboi.
Anajua hayo yanafanyika chini ya utawala wa CCM. Bado ni mwanachama wa CCM na bado hataki kutoka katika chama hicho. Anataka kulalama, kusikika na kurudi ukimyani. Basi. Huyu mkweli, mwongo?
Anayotaja Kitine yameanza kuwa hivyo tangu lini? Si yalikuwepo alipokuwa mkuu wa mashushushu nchini? Si yalishamiri wakati akiwa waziri, Ofisi ya rais, anayeshughulikia “Utawala bora?” Je, wakati huo hayakuonekana katika dira ya chama chake?
Butiku na Warioba wamekuwa wakilalamikia CCM na serikali kukosa mwelekeo katika mambo mbalimbali. Niliwahi kushikana mashati na Warioba katika safu hii hadi akanipigia simu na kuniuliza, “Wewe…ulikuwa umelewa wakati unaandika makala hii?” Tulicheka. Yaliisha.
Mara hii Butiku anatumia mkutano wa uchaguzi wa Chama cha Wananchi (CUF) kupeleka ujumbe kuwa chama chake “kinatapatapa” na kwamba hakina uongozi thabiti.
Joseph Butiku ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere. Alikuwa msaidizi maalum wa Mwalimu kwa zaidi ya miaka ishirini. Warioba alikuwa Waziri Mkuu, Waziri na sasa wakili; lakini mtu mwenye uzito wa aina yake katika jamii na kauli yake inasikika na kuheshimika.
Ukitaka kuwatendea haki Butiku, Kitine na Warioba, sharti kwanza ukubali kuwa ni watu, raia wa Tanzania , wenye haki ya kuwa na maoni juu ya mambo yanayowahusu wao na nchi yao . Wana haki ya kuona kama wanavyoona.
Pili, sharti ukubali kuwa wana haki ya kushawishi wengine kuona kama wenyewe wanavyoona. Hili hasa ndilo linafanya watoe kauli zao hadharani; bila woga wala kificho. Sasa tatizo liko wapi?
Tatizo liko katika kulalamika. Tuanze hivi: Kulalamika kunatokana na kutokubaliana jinsi mambo yanavyoendeshwa – utawala, miliki ya raslimali za taifa na mengine. Kunatokana na wao kutokuwa kwenye nafasi ya kuweza kuleta mabadiliko wanayoona ni muwafaka.
Kwa nyakati tofauti, hawa walikuwa kwenye nafasi za madaraka. Hawakulalamika. Labda hawakuona au waliona lakini wakazidiwa nguvu; au waliona ni mambo ya kawaida. Jana na leo ni tofauti; kila siku inayokuja na kupita, ni mwalimu na wakati huohuo ni maarifa.
Lakini siku zimepita nyingi. Walimu, tena walimu bora, wamekuwa wengi na maarifa yanapaswa kuwa yameongezeka. Bahati mbaya kwa Butiku, Warioba na Kitine, maarifa hayaongezeki na wingi wa walimu bora si hoja.
Inafikia wakati unalazimika kufikiri kuwa watu hawa ni waongo; tena waongo sana . Kuna tatizo; wanasema linawauma na kuwasumbua. Linawakera. Wanaelewa kiini chake. Lakini mbona hawachukii, na badala yake wanabakia kulalamika tu?
Siyo hoja mpya, kwamba ukichukia unachukua hatua. Hakika hatua haiwezi kuwa malalamiko katika vyombo vya habari au mikutanoni. Kuchukia siyo kuendelea kujiviringisha kwenye tope; kulialia huku ukiendelea kujizamisha miongoni mwa unaolalamikia.
Katika mazingira ya sasa nchini, kuchukia siyo tena kuendelea kuimba wimbo uleule wa kusubiri Mwenyezi Mungu alete fikra mpya na kupitia kwa kiongozi mkuu wa chama au serikali. Hapana!
Ni ukweli usiopingika kuwa Warioba, Butiku na Kitine wamepoteza muda mwingi kupiga porojo badala ya kuwaelekeza Watanzania nini kifanyike ili kuondoa kile ambacho wanaona hakifai.
Naye aliyeko madarakani, chukua mfano wa Rais Jakaya Kikwete, ambaye pia ni mwenyekiti wa CCM, wala hana papara. Amewapa kamba ndefu ili kila mmoja ajinyonge kwa wakati wake.
Ijumaa wiki hii aliwaambia waliostaafu uongozi wakae kimya kama Mzee Rashid Mfaume Kawawa na siyo kuwa “kilomolomo” wakati wao walishindwa yao walipokuwa kwenye uongozi. Amewachoka!
Kama Butiku, Kitine na Warioba wamesikia hayo na wangekuwa makini, wasingebakia CCM na kulalama kila kukicha. Kwa mfano, jinsi Butiku na Kitine walivyoongelea utawala na CCM, hawana sababu ya kubaki kwenye chama hicho “hatari.”
Wana kila sababu, pamoja na Warioba na wengine, kuhama chama hatari wanachosema kinatapatapa, kinauza nchi, kinaongoza kwa njia ya ubabaishaji; na kuanzisha chama kipya au kujiunga na kilichopo kwa ajili ya kuleta mabadiliko wanayotaka.
Kutofanya hivyo na badala yake kubakia kulalama, ni kupoteza muda na fursa mwanana ya kufanya jambo la maana katika maisha yao na maisha ya taifa lao. Ukichukia sharti uchukue hatua na hatua sahihi ni kuhama na kuelekeza umma wapi pa kuweka nguvu ili kukamilisha matumaini yao .
Hadi hapa, ningeombwa kutaja mafanikio ya CCM, nisingeacha kutaja “uwezo” wake wa kufyonza nguvu za mwili, roho na akili za viongozi na wanachama wake wengi, kiasi kwamba hata wanapokuwa hawakubaliani nacho, hubaki makasha yasiyoweza kufanya maasi.
Hiyo nayo ni sababu tosha ya kukataa mikatale ya CCM. Warioba, Butiku na Kitine, mpooo? Kuendelea kulalamikia CCM na utawala wake, na wakati huohuo kubaki kwapani mwake, ni kudhihirisha udhaifu, uwongo na unafiki.
(Makala hii ilichapishwa katika safu ya SITAKI katika toleo la Tanzania Daima Jumapili la 1 Machi 2009)
0713 614872
ndimara@yahoo.com
Uwongo wa Butiku, Kitine na Warioba
SITAKI kusikia vilio vya wasioambilika. Hapa Joseph Butiku. Kule Joseph Warioba. Huku Hassy Kitine. Sitaki!
Sasa imekuwa nongwa. Tumsikilize nani? Mara Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimepoteza dira. Mara nchi inaendeshwa kienyeji. Mara CCM inatapatapa. Tumsikilize nani na nani hasa mkweli.
Wewe ni mwanachama wa chama kikongwe. Kilichokupa madaraka hadi ukayachoka au hadi kikakunyang’anya. Bado umo tu – CCM ndiyo baba, CCM ndiyo mama! Halafu unalalama kila kukicha: CCM mbaya! Hawana uongozi. Hawana dira.
Hivi nani hasa atakuamini? Unatafuta nini wewe mwenye dira mahali ambako hakuna dira? Nani kakushikia huko? Utamu upi usioweza kuutema?
Imetokea vipi ukawa na dira katikati ya wasio na dira? Au dira ipo na wewe umeanza kushindwa kuisoma. Au dira imepotea kweli na wewe unasema, “potelea mbali” tutakufa wengi huko anga za mbali au maji marefu. Hutaki kuachana na chombo ingawa una mwavuli; ingawa una chombo cha kuelea. Unataka kuponea humohumo au kufia humohumo.
Eh! Hata baada ya kujua kuwa chombo chako hakina dira; waongozaji wanatapatapa na chombo chenyewe kinaendeshwa kienyeji; bado hutoki? Hivi wewe ukoje? Ni kauli za dhati au za kufurahisha baraza?
Hivi ni kweli dira ya CCM imetoweka au wajanja wameipoteza, kwa hiyo haipo? Nani alikuwa ameishikilia mara ya mwisho? Ameiweka wapi? Yeye anasemaje? Amehojiwa? Au dira ipo lakini “wazee” hawa hawawezi tena kusoma; hawawezi tena kuelewa hata wakisoma?
Sikiliza. Kitine anasema hali iliyopo inahatarisha “usalama wa taifa.” Anasema nchi inaendeshwa kienyeji; uchumi na maliasili za taifa vimeshikwa na wageni wakati wazalendo wakifangia barabara na kufanya kazi za uboi.
Anajua hayo yanafanyika chini ya utawala wa CCM. Bado ni mwanachama wa CCM na bado hataki kutoka katika chama hicho. Anataka kulalama, kusikika na kurudi ukimyani. Basi. Huyu mkweli, mwongo?
Anayotaja Kitine yameanza kuwa hivyo tangu lini? Si yalikuwepo alipokuwa mkuu wa mashushushu nchini? Si yalishamiri wakati akiwa waziri, Ofisi ya rais, anayeshughulikia “Utawala bora?” Je, wakati huo hayakuonekana katika dira ya chama chake?
Butiku na Warioba wamekuwa wakilalamikia CCM na serikali kukosa mwelekeo katika mambo mbalimbali. Niliwahi kushikana mashati na Warioba katika safu hii hadi akanipigia simu na kuniuliza, “Wewe…ulikuwa umelewa wakati unaandika makala hii?” Tulicheka. Yaliisha.
Mara hii Butiku anatumia mkutano wa uchaguzi wa Chama cha Wananchi (CUF) kupeleka ujumbe kuwa chama chake “kinatapatapa” na kwamba hakina uongozi thabiti.
Joseph Butiku ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere. Alikuwa msaidizi maalum wa Mwalimu kwa zaidi ya miaka ishirini. Warioba alikuwa Waziri Mkuu, Waziri na sasa wakili; lakini mtu mwenye uzito wa aina yake katika jamii na kauli yake inasikika na kuheshimika.
Ukitaka kuwatendea haki Butiku, Kitine na Warioba, sharti kwanza ukubali kuwa ni watu, raia wa Tanzania , wenye haki ya kuwa na maoni juu ya mambo yanayowahusu wao na nchi yao . Wana haki ya kuona kama wanavyoona.
Pili, sharti ukubali kuwa wana haki ya kushawishi wengine kuona kama wenyewe wanavyoona. Hili hasa ndilo linafanya watoe kauli zao hadharani; bila woga wala kificho. Sasa tatizo liko wapi?
Tatizo liko katika kulalamika. Tuanze hivi: Kulalamika kunatokana na kutokubaliana jinsi mambo yanavyoendeshwa – utawala, miliki ya raslimali za taifa na mengine. Kunatokana na wao kutokuwa kwenye nafasi ya kuweza kuleta mabadiliko wanayoona ni muwafaka.
Kwa nyakati tofauti, hawa walikuwa kwenye nafasi za madaraka. Hawakulalamika. Labda hawakuona au waliona lakini wakazidiwa nguvu; au waliona ni mambo ya kawaida. Jana na leo ni tofauti; kila siku inayokuja na kupita, ni mwalimu na wakati huohuo ni maarifa.
Lakini siku zimepita nyingi. Walimu, tena walimu bora, wamekuwa wengi na maarifa yanapaswa kuwa yameongezeka. Bahati mbaya kwa Butiku, Warioba na Kitine, maarifa hayaongezeki na wingi wa walimu bora si hoja.
Inafikia wakati unalazimika kufikiri kuwa watu hawa ni waongo; tena waongo sana . Kuna tatizo; wanasema linawauma na kuwasumbua. Linawakera. Wanaelewa kiini chake. Lakini mbona hawachukii, na badala yake wanabakia kulalamika tu?
Siyo hoja mpya, kwamba ukichukia unachukua hatua. Hakika hatua haiwezi kuwa malalamiko katika vyombo vya habari au mikutanoni. Kuchukia siyo kuendelea kujiviringisha kwenye tope; kulialia huku ukiendelea kujizamisha miongoni mwa unaolalamikia.
Katika mazingira ya sasa nchini, kuchukia siyo tena kuendelea kuimba wimbo uleule wa kusubiri Mwenyezi Mungu alete fikra mpya na kupitia kwa kiongozi mkuu wa chama au serikali. Hapana!
Ni ukweli usiopingika kuwa Warioba, Butiku na Kitine wamepoteza muda mwingi kupiga porojo badala ya kuwaelekeza Watanzania nini kifanyike ili kuondoa kile ambacho wanaona hakifai.
Naye aliyeko madarakani, chukua mfano wa Rais Jakaya Kikwete, ambaye pia ni mwenyekiti wa CCM, wala hana papara. Amewapa kamba ndefu ili kila mmoja ajinyonge kwa wakati wake.
Ijumaa wiki hii aliwaambia waliostaafu uongozi wakae kimya kama Mzee Rashid Mfaume Kawawa na siyo kuwa “kilomolomo” wakati wao walishindwa yao walipokuwa kwenye uongozi. Amewachoka!
Kama Butiku, Kitine na Warioba wamesikia hayo na wangekuwa makini, wasingebakia CCM na kulalama kila kukicha. Kwa mfano, jinsi Butiku na Kitine walivyoongelea utawala na CCM, hawana sababu ya kubaki kwenye chama hicho “hatari.”
Wana kila sababu, pamoja na Warioba na wengine, kuhama chama hatari wanachosema kinatapatapa, kinauza nchi, kinaongoza kwa njia ya ubabaishaji; na kuanzisha chama kipya au kujiunga na kilichopo kwa ajili ya kuleta mabadiliko wanayotaka.
Kutofanya hivyo na badala yake kubakia kulalama, ni kupoteza muda na fursa mwanana ya kufanya jambo la maana katika maisha yao na maisha ya taifa lao. Ukichukia sharti uchukue hatua na hatua sahihi ni kuhama na kuelekeza umma wapi pa kuweka nguvu ili kukamilisha matumaini yao .
Hadi hapa, ningeombwa kutaja mafanikio ya CCM, nisingeacha kutaja “uwezo” wake wa kufyonza nguvu za mwili, roho na akili za viongozi na wanachama wake wengi, kiasi kwamba hata wanapokuwa hawakubaliani nacho, hubaki makasha yasiyoweza kufanya maasi.
Hiyo nayo ni sababu tosha ya kukataa mikatale ya CCM. Warioba, Butiku na Kitine, mpooo? Kuendelea kulalamikia CCM na utawala wake, na wakati huohuo kubaki kwapani mwake, ni kudhihirisha udhaifu, uwongo na unafiki.
(Makala hii ilichapishwa katika safu ya SITAKI katika toleo la Tanzania Daima Jumapili la 1 Machi 2009)
0713 614872
ndimara@yahoo.com
SERIKALI IONJESHWE UANDISHI WENYEWE
WAANDISHI WA HABARI WASIOHITIMU
Na Ndimara Tegambwage
SITAKI waandishi wa habari wafundishwe jinsi ya kuandika habari kwa muda wote wa maisha yao. Ifike mahali wajue kuandika na waanze kuwafundisha wenzao wanaoingia katika kazi hii.
Kasheshe iliyozuka wiki hii kati ya ikulu na gazeti la Mwananchi inatokana na kutokomaa kwa waandishi katika taaluma yao. Hili linawahusu waandishi walioko kwenye magazeti, redio, televisheni, mashirika ya umma, makampuni binafsi na hata ikulu.
Mwananchi waliandika kichwa cha habari (3 Machi 2008), “Kikwete ajitosa sakata la umeme.” Maelezo yakasema Kikwete amesema Sheria ya Manunuzi ya Umma “isiwe kikwazo” katika miradi mikubwa ya umeme.
Gazeti likaongeza kuwa hilo limetokea wakati “suala la ununuzi wa mitambo ya ufuaji umeme wa dharura ya Dowans Tanzania Limited limekuwa gumzo kubwa.”
Kesho yake, Mkurugenzi wa mawasiliano ikulu, Salva Rweyemamu akasema gazeti hilo limeonyesha “Rais Kikwete amejiingiza kwenye suala la ununuzi wa mitambo ya umeme ya Dowans.”
Kwa idhini yenu wasomaji, naomba turudi darasani. Tutumie vifungu sita vya taarifa ya ikulu (a, b, c, d, e na f). Shabaha iwe kuonyesha kwanza, jinsi ikulu isivyokuwa na sababu ya kulalamika; na pili jinsi Mwananchi lilivyowanyima wananchi uhondo wote katika taarifa ya ikulu.
Kifungu (a): “Kwamba sekta ya madini isimamiwe kikamilifu kwa kuhakikisha kuwa wenye leseni za kutafuta na kuchimba mafuta wanazitumia kwa masharti yaliyoombewa na kuwa wasiozitumia leseni hizo kwa kuzingatia masharti ya leseni hizo wanyang’anywe leseni hizo badala ya kuzitumia kuendesha ulanguzi tu.”
Kumbe gazeti lingeandika kwamba mkutano wa tathmini ya utendaji wa serikali umegundua kuwa:
(i) Sekta ya madini haisimamiwi kikamilifu
(ii) Wenye leseni za kutafuta na kuchimba madini wanazitumia kuendesha ulanguzi tu.
Ujumla wa yote haya ni kwamba waziri muhusika na watendaji hawafanyi kazi yao na kwa hiyo hawastahili kuwepo. Rais aliyekuwa kwenye kikao ni shahidi.
Kifungu (b): “Kwamba zichukuliwe hatua za haraka kukomesha kabisa wizi wa mafuta ya transfoma ambao umesababisha hasara kubwa kwa taifa na kuvuruga mtandao wa kusambaza umeme kwa wananchi.”
Kumbe gazeti lingeandika kuwa tathmini ya utendaji wa serikali imegundua kuwa:
(i) Wizara na polisi wameshindwa kudhibiti wizi wa mafuta ya transfoma, tena kwa muda mrefu
(ii) Uzembe huo umesababishia hasara kubwa kwa taifa (hapa wangetafuta takwimu)
(iii) Uzembe huo au kutotenda kumevuruga mtandao wa kusambaza umeme nchini nzima.
Ujumla wa yote haya ni kwamba waziri muhusika na watendaji hawafanyi kazi yao na kwa hiyo hawastahili kuwa kwenye nafasi hizo. Rais aliyekuwa kwenye kikao ni shahidi.
Kifungu (c): “Kwamba Kamishna wa Madini Nchini, kwa kutumia madaraka na mamlaka yake kisheria, achukue hatua mara moja kukomesha uchimbaji wa kokoto katika maeneo yasiyostahili, na hasa katika eneo la Kunduchi/Tegeta, Dar es Salaam ambako serikali ilikwishakupiga marufuku uchimbaji wa kokoto, lakini baadhi ya wachimbaji wamerudi katika eneo hilo kuendesha uchimbaji.”
Kumbe gazeti lingeandika kuwa tathmini ya utendaji wa serikali imegundua kuwa:
(i) Kamishna wa Madini hajui au ameshindwa kutumia madaraka yake kisheria na hivyo ameshindwa kazi
(ii) Amri ya serikali haina uzito au inapuuzwa katika eneo la kuchimba kokoto la Kunduchi/Tegeta
(iii) Au amri inapindwa na baadhi ya watendaji serikalini kwa manufaa binafsi.
Ujumla wa yote haya ni kwamba watendaji wizarani wameshindwa kazi, kwa hiyo waondolewe; au serikali imekosa nguvu, hivyo iweje? Rais aliyekuwa kwenye kikao ni shahidi.
Kifungu (d): “Kwamba ziongezwe juhudi katika uzalishaji wa umeme nchini kwa sababu programu ya taifa ya uzalishaji umeme bado iko nyuma na liko pengo kubwa kati ya mahitaji halisi ya umeme nchini na umeme unaozalishwa kwa sasa.”
Kumbe gazeti lingeandika kuwa tathmini ya utendaji wa serikali imegundua kuwa:
(i) Watawala hawakuwa na taarifa, hadi wiki hii, kuwa programu ya taifa ya uzalishaji umeme bado iko nyuma
(ii) Wizara na serikali kwa ujumla haikujua, hadi leo, kuwa kuna pengo kubwa kati ya mahitaji halisi ya umeme na umeme unaozalishwa
(iii) Wahusika katika kufanya utafiti/kutoa taarifa watakuwa wamezembea.
Ujumla wa yote haya ni kwamba watawala na watendaji, kwa miaka yote, wanafanya wasichojua; kwamba hawastahili kuwa madarakani. Rais aliyekuwa kwenye kikao ni shahidi.
Kifungu (e): “Kwamba dhana ya tenda na Sheria ya Manunuzi isiruhusiwe kuwa kikwazo katika miradi mikubwa mikubwa ya miundombinu ya nishati hasa ile ambako wawekezaji wamejitokeza katika maeneo ambako taifa linahitaji uwekezaji mkubwa na wa haraka na ambako nchi inaonekana ilichelewa kuwekeza.”
Kumbe gazeti lingeandika kuwa tathmini ya utendaji wa serikali imegundua kuwa:
(i) Serikali imedhamiria kuvunja sheria za nchi kwa maslahi ya wawekezaji
(ii) Utaratibu mzima wa kuitisha tenda sasa ni upuuzi mtupu pale wawekezaji watakapokuwa wamejitokeza
(iii) Sasa ni mwendo holela kwa wawekezaji – wakiishajitokeza na kuwa nchini, basi sheria ya manunuzi iende likizo
(iv) Nchi sasa itavamiwa na kuwa “uwanja wa fujo”
Ujumla wa yote haya ni kwamba Sheria ya Manunuzi ya Umma haina maana tena na kwamba kitakachotumika ni “ujanja kuwahi” kwa upande wa wenye miradi mikubwa na hasa ya umeme. Aidha, huu waweza kuwa mwanzo wa “uwanja wa fujo” katika kila sekta ya uwekezaji. Rais aliyekuwa kwenye kikao ni shahidi.
Kifungu (e): “Kwamba kasi iongezwe katika kuhakikisha kuwa maeneo yaliyoahidiwa umeme yanapatiwa umeme bila ucheleweshaji usiokuwa na sababu.”
Kumbe gazeti lingeandika kuwa tathmini ya utendaji wa serikali imegundua kuwa:
(i) Wizara husika imeshindwa kwenda kwa kasi inayohitajika katika kusambaza umeme
(ii) Maeneo yaliyoahidiwa umeme yanacheleweshwa kupata umeme
(iii) Hakuna sababu zozote za msingi za kuchelewesha usambazaji umeme.
Ujumla wa yote haya ni kwamba uzembe umekithiri; waliopewa madaraka wameshindwa kazi na kwamba wakati ukifika serikali itaumbuka kwa kushindwa kutekeleza ahadi zake. Rais aliyekuwa kwenye kikao ni shahidi.
Kwa usahihi zaidi, gazeti lingeandika kuwa wajumbe wa mkutano wa tathmini, walijiumbua mbele ya Rais Jakaya Kikwete kwa kujadili mambo ambayo walipaswa kuwa wameyafanya.
Au, rais atakuwa alishangazwa sana na kauli za wajumbe katika kikao cha kujadili utekelezaji katika Wizara ya Nishati na Madini ambako imedhihirika, kwa mujibu wa taarifa ya ikulu, “karibu hakuna kinachoendelea.”
Huo ndio ungekuwa uandishi wa kuhitimu. Hata kama gazeti lingekabwa koo, kungekuwa na sababu kuwa limefikisha ujumbe kwa wananchi. Kwamba siri ya uzembe ndani ya ofisi za serikali, sasa imefichuka.
Huu ndio uandishi wa aina ya “uchambuzi fafanuzi,” ambao ni muhimu sana katika vyombo vya habari ambavyo vinatumikia wananchi katika kada zao nyingi.
Walichofanya Mwananchi ni kuripoti moja kwa moja kilichosemwa kwa kuongeza kidogo tu, mazingira ambamo hayo yametendeka. Halijakosea. Hata hivyo, hii haitoshi kukomea ambapo gazeti hilo lilikomea – kwa gharama yoyote ile.
Nenda mbele. Nenda ndani zaidi. Chukua mifano ya fafanuzi zilizowekwa kwa kila kipengee cha ikulu. Ikulu na serikali kwa ujumla, watazoea. Wataheshimu. Watavumilia. Tuwazoeshe wao na waandishi wao. Tuhitimu nao. Inawezekana.
(Makala hii itachapishwa katika safu ya SITAKI ya gazeti la Tanzania Daima Jumapili toleo la 8 Machi 2009)
0713 614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com
Na Ndimara Tegambwage
SITAKI waandishi wa habari wafundishwe jinsi ya kuandika habari kwa muda wote wa maisha yao. Ifike mahali wajue kuandika na waanze kuwafundisha wenzao wanaoingia katika kazi hii.
Kasheshe iliyozuka wiki hii kati ya ikulu na gazeti la Mwananchi inatokana na kutokomaa kwa waandishi katika taaluma yao. Hili linawahusu waandishi walioko kwenye magazeti, redio, televisheni, mashirika ya umma, makampuni binafsi na hata ikulu.
Mwananchi waliandika kichwa cha habari (3 Machi 2008), “Kikwete ajitosa sakata la umeme.” Maelezo yakasema Kikwete amesema Sheria ya Manunuzi ya Umma “isiwe kikwazo” katika miradi mikubwa ya umeme.
Gazeti likaongeza kuwa hilo limetokea wakati “suala la ununuzi wa mitambo ya ufuaji umeme wa dharura ya Dowans Tanzania Limited limekuwa gumzo kubwa.”
Kesho yake, Mkurugenzi wa mawasiliano ikulu, Salva Rweyemamu akasema gazeti hilo limeonyesha “Rais Kikwete amejiingiza kwenye suala la ununuzi wa mitambo ya umeme ya Dowans.”
Kwa idhini yenu wasomaji, naomba turudi darasani. Tutumie vifungu sita vya taarifa ya ikulu (a, b, c, d, e na f). Shabaha iwe kuonyesha kwanza, jinsi ikulu isivyokuwa na sababu ya kulalamika; na pili jinsi Mwananchi lilivyowanyima wananchi uhondo wote katika taarifa ya ikulu.
Kifungu (a): “Kwamba sekta ya madini isimamiwe kikamilifu kwa kuhakikisha kuwa wenye leseni za kutafuta na kuchimba mafuta wanazitumia kwa masharti yaliyoombewa na kuwa wasiozitumia leseni hizo kwa kuzingatia masharti ya leseni hizo wanyang’anywe leseni hizo badala ya kuzitumia kuendesha ulanguzi tu.”
Kumbe gazeti lingeandika kwamba mkutano wa tathmini ya utendaji wa serikali umegundua kuwa:
(i) Sekta ya madini haisimamiwi kikamilifu
(ii) Wenye leseni za kutafuta na kuchimba madini wanazitumia kuendesha ulanguzi tu.
Ujumla wa yote haya ni kwamba waziri muhusika na watendaji hawafanyi kazi yao na kwa hiyo hawastahili kuwepo. Rais aliyekuwa kwenye kikao ni shahidi.
Kifungu (b): “Kwamba zichukuliwe hatua za haraka kukomesha kabisa wizi wa mafuta ya transfoma ambao umesababisha hasara kubwa kwa taifa na kuvuruga mtandao wa kusambaza umeme kwa wananchi.”
Kumbe gazeti lingeandika kuwa tathmini ya utendaji wa serikali imegundua kuwa:
(i) Wizara na polisi wameshindwa kudhibiti wizi wa mafuta ya transfoma, tena kwa muda mrefu
(ii) Uzembe huo umesababishia hasara kubwa kwa taifa (hapa wangetafuta takwimu)
(iii) Uzembe huo au kutotenda kumevuruga mtandao wa kusambaza umeme nchini nzima.
Ujumla wa yote haya ni kwamba waziri muhusika na watendaji hawafanyi kazi yao na kwa hiyo hawastahili kuwa kwenye nafasi hizo. Rais aliyekuwa kwenye kikao ni shahidi.
Kifungu (c): “Kwamba Kamishna wa Madini Nchini, kwa kutumia madaraka na mamlaka yake kisheria, achukue hatua mara moja kukomesha uchimbaji wa kokoto katika maeneo yasiyostahili, na hasa katika eneo la Kunduchi/Tegeta, Dar es Salaam ambako serikali ilikwishakupiga marufuku uchimbaji wa kokoto, lakini baadhi ya wachimbaji wamerudi katika eneo hilo kuendesha uchimbaji.”
Kumbe gazeti lingeandika kuwa tathmini ya utendaji wa serikali imegundua kuwa:
(i) Kamishna wa Madini hajui au ameshindwa kutumia madaraka yake kisheria na hivyo ameshindwa kazi
(ii) Amri ya serikali haina uzito au inapuuzwa katika eneo la kuchimba kokoto la Kunduchi/Tegeta
(iii) Au amri inapindwa na baadhi ya watendaji serikalini kwa manufaa binafsi.
Ujumla wa yote haya ni kwamba watendaji wizarani wameshindwa kazi, kwa hiyo waondolewe; au serikali imekosa nguvu, hivyo iweje? Rais aliyekuwa kwenye kikao ni shahidi.
Kifungu (d): “Kwamba ziongezwe juhudi katika uzalishaji wa umeme nchini kwa sababu programu ya taifa ya uzalishaji umeme bado iko nyuma na liko pengo kubwa kati ya mahitaji halisi ya umeme nchini na umeme unaozalishwa kwa sasa.”
Kumbe gazeti lingeandika kuwa tathmini ya utendaji wa serikali imegundua kuwa:
(i) Watawala hawakuwa na taarifa, hadi wiki hii, kuwa programu ya taifa ya uzalishaji umeme bado iko nyuma
(ii) Wizara na serikali kwa ujumla haikujua, hadi leo, kuwa kuna pengo kubwa kati ya mahitaji halisi ya umeme na umeme unaozalishwa
(iii) Wahusika katika kufanya utafiti/kutoa taarifa watakuwa wamezembea.
Ujumla wa yote haya ni kwamba watawala na watendaji, kwa miaka yote, wanafanya wasichojua; kwamba hawastahili kuwa madarakani. Rais aliyekuwa kwenye kikao ni shahidi.
Kifungu (e): “Kwamba dhana ya tenda na Sheria ya Manunuzi isiruhusiwe kuwa kikwazo katika miradi mikubwa mikubwa ya miundombinu ya nishati hasa ile ambako wawekezaji wamejitokeza katika maeneo ambako taifa linahitaji uwekezaji mkubwa na wa haraka na ambako nchi inaonekana ilichelewa kuwekeza.”
Kumbe gazeti lingeandika kuwa tathmini ya utendaji wa serikali imegundua kuwa:
(i) Serikali imedhamiria kuvunja sheria za nchi kwa maslahi ya wawekezaji
(ii) Utaratibu mzima wa kuitisha tenda sasa ni upuuzi mtupu pale wawekezaji watakapokuwa wamejitokeza
(iii) Sasa ni mwendo holela kwa wawekezaji – wakiishajitokeza na kuwa nchini, basi sheria ya manunuzi iende likizo
(iv) Nchi sasa itavamiwa na kuwa “uwanja wa fujo”
Ujumla wa yote haya ni kwamba Sheria ya Manunuzi ya Umma haina maana tena na kwamba kitakachotumika ni “ujanja kuwahi” kwa upande wa wenye miradi mikubwa na hasa ya umeme. Aidha, huu waweza kuwa mwanzo wa “uwanja wa fujo” katika kila sekta ya uwekezaji. Rais aliyekuwa kwenye kikao ni shahidi.
Kifungu (e): “Kwamba kasi iongezwe katika kuhakikisha kuwa maeneo yaliyoahidiwa umeme yanapatiwa umeme bila ucheleweshaji usiokuwa na sababu.”
Kumbe gazeti lingeandika kuwa tathmini ya utendaji wa serikali imegundua kuwa:
(i) Wizara husika imeshindwa kwenda kwa kasi inayohitajika katika kusambaza umeme
(ii) Maeneo yaliyoahidiwa umeme yanacheleweshwa kupata umeme
(iii) Hakuna sababu zozote za msingi za kuchelewesha usambazaji umeme.
Ujumla wa yote haya ni kwamba uzembe umekithiri; waliopewa madaraka wameshindwa kazi na kwamba wakati ukifika serikali itaumbuka kwa kushindwa kutekeleza ahadi zake. Rais aliyekuwa kwenye kikao ni shahidi.
Kwa usahihi zaidi, gazeti lingeandika kuwa wajumbe wa mkutano wa tathmini, walijiumbua mbele ya Rais Jakaya Kikwete kwa kujadili mambo ambayo walipaswa kuwa wameyafanya.
Au, rais atakuwa alishangazwa sana na kauli za wajumbe katika kikao cha kujadili utekelezaji katika Wizara ya Nishati na Madini ambako imedhihirika, kwa mujibu wa taarifa ya ikulu, “karibu hakuna kinachoendelea.”
Huo ndio ungekuwa uandishi wa kuhitimu. Hata kama gazeti lingekabwa koo, kungekuwa na sababu kuwa limefikisha ujumbe kwa wananchi. Kwamba siri ya uzembe ndani ya ofisi za serikali, sasa imefichuka.
Huu ndio uandishi wa aina ya “uchambuzi fafanuzi,” ambao ni muhimu sana katika vyombo vya habari ambavyo vinatumikia wananchi katika kada zao nyingi.
Walichofanya Mwananchi ni kuripoti moja kwa moja kilichosemwa kwa kuongeza kidogo tu, mazingira ambamo hayo yametendeka. Halijakosea. Hata hivyo, hii haitoshi kukomea ambapo gazeti hilo lilikomea – kwa gharama yoyote ile.
Nenda mbele. Nenda ndani zaidi. Chukua mifano ya fafanuzi zilizowekwa kwa kila kipengee cha ikulu. Ikulu na serikali kwa ujumla, watazoea. Wataheshimu. Watavumilia. Tuwazoeshe wao na waandishi wao. Tuhitimu nao. Inawezekana.
(Makala hii itachapishwa katika safu ya SITAKI ya gazeti la Tanzania Daima Jumapili toleo la 8 Machi 2009)
0713 614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com