Friday, December 26, 2008

MTIHANI MWINGINE KWA CHAMA CHA MAPINDUZI

Uchaguzi na bundi wa Mbeya Vijijini

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI mashujaa wa Tarime washindwe kudhihirisha ushujaa huo katika jimbo la uchaguzi la Mbeya Vijijini. Kwani mazingira yanaonyesha wana kila sababu ya kufanya vizuri.

Lakini mara hii, uwanja una milima mikubwa na mabonde ya kina kirefu, huku bundi wakiwa wamelaliana matawini mwa miti ya mirefu ya kisiasa.

Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinampeleka rais mstaafu, Ali Hassan Mwinyi kufungua kampeni zake. Kwa mujibu wa habari za ndani ya CCM, kiongozi wa kampeni ni Naibu Katibu Mkuu wa CCM ambaye pia ni Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo.

Mtaalam wa kampeni na ambaye hana rekodi ya kupoteza jimbo katika chaguzi ndogo ni John Samwel Malecela, makamu mwenyekiti mstaafu na mmoja wa washindani 11 ndani ya CCM waliowania tiketi ya kugombea urais mwaka 2005.

Kiongozi mwingine muhimu kwa upande wa CCM ni kijana Nape Nnauye ambaye tayari ameonya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kwa kutishia “kumlipulia” kashfa Ali Hassan Mwinyi.

Kinachofurahisha katika kampeni za kupata mbunge atakayerithi ofisi ya Richard Nyaulawa, mbunge aliyefariki mwezi mmoja uliopita, ni kwamba viongozi wakuu wanne wa kampeni ya CCM wana mgogoro, ama ndani au nje ya chama chao.

Hao ni Malecela, Nape, Waziri wa Habari ambaye jina lake liko kifungoni na William Ngeleja, waziri wa nishati na madini. Tutaangalia kwa ufupi tu jinsi watakavyojilazimisha kufanya kampeni ya kupata mbunge na kurejeshea CCM kiti cha Mbeya Vijijini.

Tuanze na aliyetajwa mwisho, William Ngeleja. Ikitokea akakanyaga uwanjani Mbeya, atakuwa na kazi ngumu ya kueleza kile alichonukuliwa akisema.

Mara baada ya kifo cha Nyaulawa, Ngeleja alidakwa na vyombo vya habari akisema kwamba serikali itapeleka umeme katika jimbo la Mbeya Vijijini ikiwa njia bora ya “kumuenzi” mbunge aliyefariki.

Wapiga kura watataka kujua kwa nini serikali ilisubiri kifo cha mbunge wao ndipo itangaze kuwa itawapelekea umeme wakazi wa jimbo hilo. Hata hivyo watataka kujua iwapo hiyo ni ahadi ya kweli au kauli za kukidhi haja iliyopo.

Bila shaka Ngeleja atajiuma midomo. Atadai waandishi wa habari walimnukuu vibaya au kwamba aliishasahihisha usemi wake. Vyovote itakavyokuwa, kuna mgogoro kati ya chama kinachoongoza serikali na wakazi wa Mbeya Vijijini juu ya suala hilo na mengine mengi.

Kuna mzee “Tingatinga.” Huyu ni John Malecela. Asiwepo wa kudai kuwa mzee huyu hasahau au huweka kinyongo; au kwamba amesahau na amesamehe. Huyu ni mhanga wa siasa za “shingo-kwa-shingo” kuelekea uchaguzi mkuu wa 2005.

Ni Malecela huyuhuyu aliyesema wakati wa kugombea nafasi ya mgombea urais ndani ya CCM kwamba amekuwa “tingatinga” linalotengeneza barabara lakini likishamaliza kazi, basi haliruhusiwi huitumia.

Alikuwa anajenga hoja ya kulea na kuimarisha chama chake; kupigania na kuleta ushindi katika chaguzi za marudio na kutafuta muwafaka penye mifarakano. Lakini lilipokuja suala la kugombea urais, yakaja madai kuwa “huyo ni mzee.”

Katika kuleta ushindi kwa chama wakati wa chaguzi, Malecela alikuwa kijana; tena mbichi kabisa. Katika kutafuta urais, akaonekana mzee asiyeweza. Alisononeka. Alibubujikwa machozi ya ndani kwa ndani. Hatimaye akasema amesamehe. Leo anakwenda Mbeya Vijijini kutafuta mbunge.

Hakuna ushahidi kwamba Malecela aliwahi kugombana na Katibu Mkuu wa CCM, Yusuf Makamba; lakini kuna tetesi kwamba asingependa kufanya naye kazi huko Mbeya.

Taarifa zilizopo ni kwamba kutoiva huko ndiko kumefanya vikao vya CCM kumteua Malecela kwenda Mbeya na pia kutompa jukumu kubwa Makamba katika kampeni hata kama atakwenda uwanjani.

Kiongozi mwingine anayekwenda Mbeya ni Nape Nnauye. Huyu anafahamika kwa kauli kali ndani ya chama. Ni majuzi tu viongozi wa Umoja wa Vijana wa CCM walipendekeza avuliwe uanachama kutokana na kushambulia baadhi yao kwa kushiriki ufisadi.

Kana kwamba hiyo haitoshi, ni Nape aliyenukuliwa hivi karibuni akisema katibu mkuu wa chama chake, Yusufu Makamba “anakumbatia mafisadi” ndani ya chama.

Inaambukiza hamu kutaka kuona Nape amekaa jukwaa moja na Makamba wakitafuta mbunge wa Mbeya Vijijini. Ni shauku ya wapiga kura kujua iwapo wanaotetea mafisadi hakika wanastahili kushinda katika uwanja huu.

Jukwaa lilelile la CCM lina waziri wa habari, utamaduni na michezo ambaye vyombo huru vya habari vilifungia jina lake kuandikwa kutokana na hatua yake kufungia gazeti la MwanaHALISI kwa siku 90.

Jina lake na kazi zake vitaandikwa katika magazeti ya CCM, serikali na baadhi ya magazeti ya wamiliki binafsi walio maswahiba wa CCM.

Kifungo cha waziri kinafahamika nchi nzima. Ilikuwa baada ya kufungia gazeti, wahariri wa vyombo huru vya habari – katika jukwaa lao – waliamua kumwadhibu waziri kwa kususia kuandika habari zake na inapotokea zikaandikwa, basi jina lake lisiandikwe.

Waziri aliye “kifungoni,” na wakati huohuo ndiye naibu katibu mkuu wa CCM, anapoteza uzito na hadhi mbele ya wananchi. Hatua tu ya kulipua taarifa kuhusu alivyoua chombo cha habari cha wananchi, inatosha kumwambukiza kizunguzungu na kuleta kizaazaa mikutanoni na hata kusababisha kukosekana kwa kura.

Mbeya Vijijini ni mtihani mgumu kwa CCM hata bila kutaja ahadi lukuki ambazo viongozi wametoa lakini hawajatekeleza na uwezekano wa kufanya hivyo ni finyu.

Hata hivyo, Mbeya ni milima na mabonde yenye rutuba kisiasa. Kila mwenye ufundi wa kutumia milima na mabonde hayo aweza kuvuna. Lakini bundi walioko mitini wakikwekweza vicheko, waweza kuelekeza kilio nyumbani mwa yeyote.

Kilio kitakuwa kwa nani? Mashujaa wa Tarime? Chama kikongwe? Vyama vingine? Tusubiri msimu mpya wa siasa za njiapanda.
0713 614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com

(Makala hii itachapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili, 28 Desemba 2008)

Saturday, December 20, 2008

UDANGANYIFU KARIBU NA KRISMASI

SITAKI
Usafiri mbaya wa ‘Air Buffalo’



Na Ndimara Tegambwage


SITAKI wasafiri wanaokwenda kazini, matembezini au makwao kwa kutumia usafiri wa mabasi, watapeliwe, wasumbuliwe na waghadhabishwe na wamiliki wa mabasi.

Mfano mbaya ambao haustahili kufanywa na kampuni yeyote inayotoa huduma ya usafiri wa mabasi, na ambao haustahili kurudiwa ni ule wa kampuni inayomiliki mabasi ya Air Buffalo.

Nifuateni. Kuna wasafiri. Hawa wanakwenda Bukoba. Wengine wanakwenda miji mingine ya njiani. Wana tiketi kwa ajili ya safari. Siku ya safari ni Ijumaa. Tarehe 19 Desemba 2008. Saa 12.30 asubuhi.

Ninamsindikiza ndugu yangu. Niko kituo kikuu cha mabasi ya mikoani, Ubungo, jijini Dar es Salaam. Nimefika hapa saa 11 alfajiri. Saa 12 kasoro robo wamiliki wa basi la Air Buffalo wanatangaza, “Basi la Air Boffalo la njia ya kati halitaondoka saa 12.30. Litaondoka saa moja kamili. Tunasikitika kwa usumbufu wowote utakaojitokeza.”

Kwa tangazo hilo nilihisi aina ya utapeli. Tangazo lilisema “njia ya kati” na siyo kituo/mji wa mwisho - Bukoba. Nadadisi. Naambiwa katika basi hilo kutakuwa na abiria wanne wanaokwenda Kigoma. Kwa hiyo tangazo limechukua mtindo wa “Reli ya Kati.”

Ni saa moja kamili asubuhi. Hakuna basi. Hakuna ofisa wa kampuni kueleza kilichotokea. Hakuna tangazo jingine. Napiga simu ofisi za Air Buffalo – Simu:0755555575. Naambiwa gari litakuwa kituoni katika muda wa dakika 30.

Ni saa 2.30. Hakuna gari. Napiga tena simu ofisini. Namba zipo kwenye tiketi za abiria. Najibiwa gari litakuwa kituoni “wakati wowote.” Saa tatu. Saa nne. Kila abiria anasema, “Tumetapeliwa.” Nikaita Buffalo. Simu inalia. Hakuna anayepokea.

Kila mmoja alianza kukumbuka”Bijampola” – wale vijana waliokuwa na kampuni hewa na basi hewa lakini wakaandikisha majina mengi ya wasafiri kutoka Dar es Salaam kwenda Bukoba na kuyeyukia mitaani siku na tarehe ya kusafiri.

Ndipo nikaamua kushirikisha polisi. Yule polisi niliyeita akanambia siku hizi ni wakili. Akanipa mamba ya polisi mwingine. Polisi huyo akasema hahusiki sana lakini pale ofisini kwake kulikuwa na kamanda wa usalama barabarani kanda ya Dar es Salaam aliyetaja jina lake kuwa ni Sanga.

Nikamweleza Sanga kisanga kilichoko Ubungo. Akasikiliza kwa hamu. Akanambia, “Nipe dakika 30 niandae vijana wangu.”

Katika dakika 30 hadi 40 hivi, polisi, wakiandamana na maofisa wa Mamlaka ya Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (SUMATRA), walikuwa ndani ya kituo cha mabasi Ubungo wakiongea na wasafiri waliokuwa wakionekana kuchoka na kuwa na karaha.

“Tumekwishawaona wenye basi. Endelea kusubiri hapa,” alieleza ofisa wa Sumatra. “Gari linaletwa. Wale ambao hawataki tena kuendelea na safari watarudishiwa fedha zao; wanaotaka kuendelea wataondoka na basi,”

Kwa mujibu wa Sumatra, nauli ya basi kutoka Dar es Salaam kwenda Bukoba ni Sh. 55,000. Wasafiri wa Ijumaa kwenye basi la Buffalo walikata tiketi kwa Sh. 65,000 au zaidi.

Muda si muda basi liliingizwa kituoni. Lilionekana la zamani sana, ukilinganisha na mabasi mapya na ya kisasa yanayokwenda Bukoba na sehemu nyingine ndani na nje ya nchi. Abiria waliingia kwa msongamano. Sumatra wakaamuru abiria warudishiwe fedha zinazozidi kiwango cha Sh. 55,000 na basi likaondoka. Ilikuwa kama saa tano na nusu na siyo saa 12.30 asubuhi kama abiria walivyokuwa wameahidiwa.

Kama dakika 50 hivi tangu basi litoke Ubungo, nikapata simu ya ndugu yangu niliyekuwa nasindikiza. Alisema hivi, “ Bado tuko Kiluvya. Dereva na kondakta wametuacha hapa; wakapanda basi na kurudi Dar es Salam.”

Wale ambao hawakuanza safari saa 12.30 asubuhi. Wale ambao wamekuwa juani kituoni kwa zaidi ya saa nne na nusu. Wametelekezwa nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam.

Nilianza upya mawasiliano. Ni kama nilivyofanya asubuhi. Polisi. Sumatra. Abiria. Polisi. Sumatra. Abiria. Polisi…Saa 12 jioni, ofisa wa Sumatra akanieleza kwamba wamewalazimisha wakodishe gari kutoka kampuni yoyote na “kusafirisha abiria wao.”

Huku abiria wakiwa wanajiandaa kurejea Dar es Salaam, kwani pale walipoachwa kulikuwa ni vichaka vitupu, ofisa wa Sumatra akanambia kuwa yuko kituo cha mafuta Ubungo akisimamia waweke mafuta kwenye basi linalokwenda kuwachukua abiria waliotelekezwa Kiluvya.

Saa moja na nusu usiku, abiria walikuwa wanaanza kuingia katika basi. Lakini waliambiwa pia kuwa basi hilo lingewafikisha tu Kahama. Kutoka hapo wangepata “usafiri mwingine.”

Nikarudi kwa ofisa wa Sumatra. Akanithibitishia kuwa ni kweli Buffalo wamekodisha gari la kupeleka abiria hadi Kahama na kwamba Buffalo wamethibitishia mamlaka kuwa wameandaa usafiri kutoka hapo hadi Bukoba. Nami nikawa nimechoka kama abiria.

Kama wamiliki wa Buffalo wasingefuatwa na kung’ang’anizwa, hakika wasingekwenda hata kwenye kituo cha mabasi cha Ubungo. Walikuwa waoga wa kusema iwapo gari ni bovu au wafanyakazi walikuwa hawajalipwa posho au kulikuwa na kitu kingine kilichokuwa kinawakwaza.

Hiyo ndiyo Air Buffalo. Nauli juu ya kiwango. Kukimbia abiria na kutotaka kuwaambia kinachoendelea. Kuwatelekeza porini kwa zaidi ya saa tano. Kuweka maisha yao hatarini, kwani wangeweza kuvamiwa na kuporwa kila walichokuwa nacho.

Hilo ni Air Buffalo lenya namba ya usajili T 155 ADU iliyoandikwa kwenye tiketi za wasafiri lakini lenyewe likionekana kuzeeka sana; kuchoka sana na hatimaye kuishia Kiluvya, nje kidogo ya Dar es Salaam.

Sumatra walifanya kazi yao. Polisi walifanya kazi yao pia. Nami nilitenda wajibu wangu wa kuwakutanisha; kuwakumbusha na labda kuwasumbua kwa kuwapa ripoti za abiria mara kwa mara.

Lakini kwa upande wa Air Buffalo, hakika hivi sivyo jinsi ya kuwa kampuni ya usafirishaji abiria. Usafirishaji wa abiria unapaswa kuwa mwepesi, wa kicheko na furaha wakati wote – tangu kukata tiketi, kupanda basi, kusafiri hadi kuteremka.

Lakini nani anaweza kujitokeza na kutetea Air Buffalo pale atakapokuta abiria waliokuwa wasafari kwa gari T 155 ADU wakisema “hawa bwana ni matapeli?” Yupooo?

0713 614875
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com

(Makala hii itachapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapaili, 21 Oktoba 2008)

Wednesday, December 10, 2008

MUGABE ANATAKA KUFIA IKULU

SITAKI

Mugabe anavyoisha kama sabuni

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI Afrika iendelee kukumbatia Robert Mugabe, rais wa sasa wa Zimbabwe ambaye hakika amechoka, amechakaa na hana jipya la kufaa nchi yake na bara hili.

Katika Zimbabwe hivi sasa, aliyebakia mtu wa karibu sana na Mugabe na mshauri pekee mwandani ni mke wake. Ukiona askari wa jeshi la ulinzi wanaanza kushiriki maandamano, ujue jamii imepokea mlio wa bundi. Ishara mbaya kwa Mugabe.

Ukiona askari polisi wameanza kushiriki uporaji katika maduka ya biashara jijini Harare badala ya kulinda amani; na wengine wakigoma kuwapiga wananchi wasiokuwa na hatia, ujue harufu ya bundi imepita. Ishara mbaya kwa Mugabe.

Angalia walimu – nguzo kuu katika Afrika ya wanasiasa na serikali wakati wa mapambano na shida kuu. Ona walivyoanza kuikaba koo serikali wakidai kulipwa mishahara katika fedha za kigeni, kwani thamani ya dola ya nchi imeporomoka kupindukia. Jua basi, huu ni mbomoko.

Ukiona wanasiasa wenza wa Mugabe wanaanza kumkatalia, kumkana, kumpinga; na wengine kwa woga wakiamua kuacha kazi za kisiasa ili isionekane wanapinga “komredi,” ujue Mugabe kabakiwa na mvumo wa sauti na si mantiki ya kauli. Mlio wa bundi.

Mgabe alichuja. Wananchi wakasema sasa basi. Akakataa. Ili abaki madarakani akaanzisha uvamizi wa mashamba ya wazungu ili kupata sifa za wakati huo. Yakavamiwa. Yakachukuliwa na mawaziri wake, maofisa wake, marafiki zake na vijana wa mijini waliojiita “wapigania uhuru” lakini ambao walikuwa hawajazaliwa wakati wa vita vya ukombozi.

Mugabe aliona anakwenda na mkondo wa maji. Ni pale wanajeshi walipotaka kustaafu akiwa hana hata senti ya kuwalipa. Mungu bariki, vikaingia vita Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo. Akaahirisha malipo ya wastaafu; akapeleka majeshi vitani na kuahirisha kasheshe. Bundi huyo.

Kilimo kikadorora. Chakula kikapungua na hatimaye kukosekana. Mugabe hakuona tatizo. Aliona kuwa ni wafanyabiashara waliokuwa wakificha vyakula. Akavamia wachuuzi wa Harare. Akawapiga. Akawapora. Njaa haikuisha. Ndio hasa imeota ndevu. Sauti ya bundi.

Hakuna atakayesahau operesheni ya kuwaswaga wakazi wa Harare nje ya jiji hilo ili wakakae shamba na wasiwe vichaka vya “wapinzani” mjini. Nyumba na vibanda walimoishi vilivunjwa. Walikosa makazi. Walikosa chakula. Walipoteza mali zao – ndogo, chache au nyingi – kila mmoja na kiwango chake.

Busara zikavuma dunia nzima. Mugabe umechoka. Akajibu: Hapana. Kilimo kikafifia. Uchumi ukadorora zaidi. Amani ikapungua na kubakia kwenye makazi ya walioko kwenye utawala. Hasira na chuki vikatawala. Sauti ya bundi.

Naye Mugabe hakukaa kimya. Kila tatizo akalihusisha na wakoloni wa zamani wa Uingereza. Akavurumisha maneno makali kwa Uingerza na Marekani. Akasema matatizo yanaletwa na ubeberu. Akataka wananchi waelewe hivyo. Wananchi wakaelewa tofauti na alivyotaka. Sauti ya bundi.

Bado anataka kutawala. Nyenzo yake pekee ya kisiasa ikiwa bado ileile; kwamba Waingereza hawakutoa fedha za kufidia wazungu walioshika mashamba makubwa aliyoamua kuwanyang’anya.

Suala la umilikishaji ardhi lilihitaji kushughulikiwa miaka kumi baada ya uhuru; kwa mujibu wa Katiba ya uhuru iliyoandikiwa Uingereza. Baada ya miaka hiyo Mugabe alikuwa “bize” na uhondo wa ikulu. Ujenzi wa kasri. Ulimbikizaji ainaaina na majigambo ya kupambana na ubeberu.

Mugabe alisahau kuwa aliingia mjini akiwa na wapiganaji; ambao hawakuwa na jembe, panga, koleo, nyumba wala shamba; bali bunduki. Badala ya kutumia miaka kumi ya kwanza ya uhuru kujenga misingi ya kuwapa makazi, anawaambia washindane na wengine katika kuvamia mashamba ya wazungu.

Kutwaa mashamba ya wazungu na wengine wenye ardhi kubwa katikati ya wananchiwasiokuwa na ardhi, ni suala linalokubalika lakini lililohitaji mipango na utaratibu katika kugawana raslimali za taifa. Mugabe alijisahau. Hadi bundi alipolia na yeye kuamuru, “Kamata!”

Chunga haya: Uhaba wa chakula na njaa. Kukosekana kwa fedha za ndani zitokanazo na kodi na kutokuwepo fedha za kigeni kutokana na kutokuwa na bidhaa za kutosha zilizouzwa nje. Ukame. Mafuriko. Mipango mibovu isiyokidhi matakwa ya nchi. Kupungua kwa misaada kutoka nje kulikotokana na wafadhili kutilia mashaka utawala wa Mugabe.

Ongeza haya: Kujitokeza kwa chama cha upinzani chenye nguvu. Migomo ya vyama vya wafanyakazi. Mwamko wa wananchi kuhusu haki zao. Tishio la jeshi kuasi, isipokuwa askari wachache walio karibu na rais. Kauli za viongozi wa mataifa mbalimbali juu ya mwenendo wa uchumi na utawala nchini Zimbabwe.

Yote haya na mengine, yalifanya Mugabe akose pumzi. Kukosekana kwa pumzi kunatokana na kukosekana kwa majibu kwa maswali mengi aliyoulizwa na wananchi, walimu, vyama vya wafanyakazi, askari na wanasiasa wenzake.

Matokeo ya kukosea majibu, ni kutumia mkono wa chuma. Mugabe akawa mbogo; dikiteta. Akamwaga chumvi kwenye kidonda. Akavunja haki za msingi za binadamu kwa kuziba mifereji ya mawasiliano – kupokonya uhuru wa maoni – na kujenga woga katika jamii kwa shabaha ya kuinyamazisha. Bundi hilooo!

Ni uchaguzi mkuu wa mwisho nchini humo uliompa Mugabe hali halisi ya utashi wa wananchi. Akabwagwa katika kinyang’anyiro cha ubunge na urais. Hakupata kura za kutosha kutamkwa kuwa rais moja kwa moja.

Marudio ya uchaguzi wa rais ndiyo yalionyesha sura yake kamili. Akatishia kuita jeshi lake kuchukua nchi. Akatangaza, kupitia askari wake watiifu sana au waoga, kwamba yuko tayari kuanzisha upya vita vya kukomboa nchi kwa njia ya silaha. Akatoa macho. Akafoka dunia nzima ikasikia.

Katika hali isiyo ya kawaida, Mugabe akarudia kutamka kuwa chama cha upinzani kinatumiwa na wazungu na mabeberu na kwamba hawezi kutawaliwa na wakoloni. Kauli za kijasiri katika mazingira magumu na tata.

Polisi wa Mugabe wakawaandama wapinzani. Wakawakamata. Wakawapiga. Wakawafunga. Wakawazuia kufanya mikutano. Mugabe na ZANU-PF wakawa pekee walioingia kwenye raudi ya pili ya uchaguzi wa rais. Sasa nchi haitawaliki na yeye, pamoja na kujiita rais, ameshindwa kuunda serikali.

Nani, miongoni mwa viongozi wa Afrika ambaye hajui yote haya? Mugabe anaendelea kubebembelezwa kwa lipi; hadi lini na kwa faida ipi na ya nani?

Mugabe ametoka kuwa mpigania uhuru shupavu wa Zimbabwe huru, kuwa rais na sasa dondandugu la Afrika lisilotamanika nchini mwake na bara zima. Ameonyesha kutoshaurika. Acha Mugabe aende na maji.

(Makala hii ilichapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili, 7 Desemba 2008) Mwandishi anapatikana kwa:
Simu:0713 614872
imeili: ndimara@yahoo.com