Kigeugeu cha serikali kuhusu AZAKi
Na Ndimara Tegambwage
SITAKI serikali ibadili msimamo wake wa kutambua na kuthamini asasi za kiraia nchini (AZAKi) uliosisitizwa na mawaziri wawili wiki hii.
Katika Tamasha la Sita na Maonyesho ya Asasi za Kiraia yaliyomalizika Ijumaa, serikali imetamka kuwa inatambua na kuthamini kazi za AZAKi na kwamba iko tayari kushirikiana nazo.
Wa kwanza kutoa kauli hiyo alikuwa Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia na Watoto, Margaret Sitta pale alipofungua maonyesho kwenye viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam.
Mwingine alikuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais, Batilda Buriani aliyefungua jukwaa la kila mwaka la asasi hizo katika hoteli ya Blue Pearl, Ubungo Plaza, Dar es Salaam.
Kwa miaka mingi sasa baadhi ya viongozi wa serikali wamekuwa wakielekeza shutuma na kejeli kwa AZAKi. Wamedai kuwa asasi hizi “ni za mfukoni” wakiwa na maana kuwa ni za wababaishaji; wamedai ni za mtu mmojammoja; zinafuja fedha tu; hazina manufaa kwa jamii na kwamba zinatumiwa na wafadhili.
Katika msafara wa mamba na kenge wamo. Lakini siyo msafara wa kenge na siyo siku zote. Ndio maana methali zinabadilika: Samaki mmoja akioza katika furushi, usitupe wote; bwaga furushi chini na changua ambao hawajaoza. Siyo wote waliooza.
Hili linathibitishwa na asasi mwavuli ya Foundation for Civil Society. Kwa miaka mitano sasa Foundation imesimamia asasi hizi kwa maana ya kuzipa uwezo. Imetafiti kuwepo kwake, mahali zilipo, kazi zake, mafanikio na changamoto zake.
Wakati kazi hiyo inaendelea, Foundation imejikita katika jukumu la kuzipa uwezo; ili ziweze kujipa sura, taswira na mwelekeo unaoendelea. Ni uwezo huo ambao unazipa AZAKi heshima na thamani mbele ya jamii. Aliyeona kazi za asasi Mnazi Mmoja au kuhudhuria jukwaa, hawezi tena kubeza.
AZAKi huanzishwa na wananchi katika maeneo yao. Ni matunda ya akili zao. Ni matokeo ya mahusiano na mfumo wa maisha na mazingira pale wanapoishi. Nyingine zaweza kuanzishwa kwa ushauri na ushawishi mwanana uliolenga kuinua hadhi ya wahusika.
Asasi hizi zinatokana na utashi binafsi wa wanaoziunda. Malengo yake yameelekezwa katika kukabiliana na changamoto za mahali walipo na ushirikiano miongoni mwa asasi mbalimbali (mitandao) zenye malengo yaleyale au yanayoshabihiana katika Kata, wilaya, mkoa na taifa.
Kwa hiyo, hata ziwe asasi zenye kazi moja au zinazohusika na shughuli nyingi, shabaha imekuwa moja: Kubadili mazingira wanapoishi ili yawe bora zaidi kwao na jamii. Hapo ndipo kuna umuhimu wa AZAKi.
Raia wanapounda chombo chao kwa madhumuni ya kukabiliana na changamoto katika mazingira yao, wanakuwa wametambua jukumu lao katika maendeleo yao wenyewe. Wanakuwa waelewa kuwa hawawezi kusubiri serikali ya mtaa au kuu kuwafanyia kila kitu.
Lakini muhimu zaidi, wanakuwa wametambua umuhimu wa kujiunga pamoja, kufikiri pamoja na kutenda pamoja. Wanakuwa wamejifunza kujitegemea kwa njia ya vitendo.
Kwenye moyo huo, ukiongeza uwezeshaji kwa njia ya raslimali watu, uelewa katika kupanga na kutekeleza, ufundi katika asasi zinazohusiana na uzalishaji na kiwango fulani cha fedha, raia watafanya shughuli zao bila kusubiri kuhubiriwa na wanasiasa au warasimu kutoka serikalini.
Kwa hiyo AZAKi ni hatua muhimu katika kujitegemea. Kwanza, kujitegemea kifikra na kuweza kufanya maamuzi sahihi miongoni mwa wanachama wa asasi na jamii kwa ujumla.
Pili, kujitegemea kwa uzalishaji wa mawazo na mazao ambavyo vinanufaisha jamii ya karibu na mbali kama ilivyodhihirika jijini Dar es Salaam wiki hii.
AZAKi zilizokutana Dar es Salaam katika tamasha la sita ni chemchemi ya mwamko wa jamii nzima. Wakati waliokuwa hawajaunda asasi watakuwa wamechocheka kuanzisha haraka; wale waliomo wamepata fursa ya kupeana uzoefu na fikra mpya.
Kupanuka kwa shughuli za AZAKi na kuongezeka kwa asasi nyingine, kuna maana ya kupatikana kwa fursa zaidi za wananchi kuwa pamoja, kufikiri pamoja na kutenda pamoja.
Hii ndiyo nguvu ya jamii ya kiraia. Ndiyo chimbuko la heshima na thamani ya asasi. Jamii iliyoungana kwa njia ya AZAKi ina nguvu ya kufikiri, kutambua mazingira na matakwa yake, uelewa na uwezo wa kusema “ndiyo” au “hapana.”
Hata katika nchi zilizoendelea, AZAKi zina nafasi kubwa katika kuamua mwelekeo wa nchi, kwa kuwa zinachangia fikra na ni kiwakilishi cha matakwa ya jamii pana. Hujafaulu kisiasa au kiuchumi kwa kuacha AZAKi nje ya duara la fikra na utendaji.
Na hapa wengi tunafikiria asasi zilizojiunga na Foundation. Lakini kuna nyingine nyingi ambazo hazijasajiliwa kisheria. Zina nguvu kuu katika maamuzi pale zilipo na zinapata ushawishi kutoka kwa zile ambazo zimepiga hatua katika kuzalisha mawazo na mazao.
Kwa hiyo kazi hii ya kukuza uwezo wa AZAKi, ambayo inafanywa na Foundation for Civil Society, hainabudi kuendelezwa, kukuzwa na kutetewa kwa viwango vyote. Hainabudi kupanuliwa kufikia wengine ambao wana hamu ya kuwa asasi inayotambulika kimuundo.
Ni kwa msingi huo sitaki kuona au kusikia serikali inarudi nyuma na kuanza kubeza AZAKi, hata kama itatokea mara moja au mara kadhaa serikali kutofautiana kimawazo na moja au baadhi ya asasi katika utekelezaji wake.
Jamii ambamo AZAKi zimeenea kuna uhuru mpana wa kufikiri na kutoa maoni; jamii nzima inaongea bila woga wala aibu na inatenda kwa uhakika. Foundation itakuwa imefanikiwa iwapo itafikisha Tanzania katika kiwango hicho. Na ifike huko!
0713 614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com
(Makala hii itachapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili, Toleo la kesho 30 Novemba 2008)
Saturday, November 29, 2008
Friday, November 21, 2008
IGP HAWEZI KUCHUNGUZA SERIKALI

Migomo inasababishwa na serikali,
Polisi watachunguzaje mwajiri wao?
Na Ndimara Tegambwage
SITAKI Inspekta Jenerali wa Polisi, Said Mwema apoteze muda kuchunguza kiini cha migomo vyuoni au popote pale nchini. Kwani kiini kinajulikana.
Tuanzie kwenye kitongoji. Wenyeviti wa vitongoji katika Halmashauri ya Wilaya ya Tandahimba wamegoma kuanzia Novemba 10 mwaka huu. Wanadai malimbikizo ya posho zao za miaka miwili. Wanadai haki yao.
Wanafunzi wa shule za msingi za serikali – Tabata na Mbagala jijini Dar es Salaam na baadhi ya shule mikoani – wameandamana kudai haki yao ya kufundishwa. Hii ni baada ya mgomo baridi na mgomo wa wazi wa walimu. Wanadai haki yao.
Walimu wameandamana na kugoma kufundisha. Wanadai malimbikizo ya mishahara yao, posho za kujikimu pale walipopewa uhamisho, malipo ya likizo, nyongeza za mishahara ambazo zimekwama kwa kipindi kirefu na marupurupu yao mengine. Wanadai haki yao.
Wanafunzi katika vyuo vikuu vya serikali wameandamana vyuoni kwao na kugoma kuingia madarasani wakitaka serikali iondoe utaratibu wa uchangiaji karo wanaosema unaumiza wanafunzi ambao wazazi wao ni masikini.
Zimwi la uchangiaji linatishia vyuo kubaki vya wenye fedha ambao siyo lazima wawe na uwezo. Pindi waliochaguliwa kuingia vyuoni kwa utaratibu wa alama maalum za kinachoitwa “kushinda” watakapoondolewa, vyuo vitafurika wenye fedha hata kama ni kugeuza makazi hayo kuwa mapango ya wavuta bangi.
Wanafunzi wanapinga ubaguzi katika mfumo mzima wa uchangiaji, lakini pia wanadai haki ya kunufaika na raslimali za nchi hii – nyasi, miti, misitu, mito, maziwa, bahari, madini, ardhi na nyingine – ambazo zimeneemesha watu wa nje kuliko wazawa wa Mama Tanzania.
Kusoma ni haki yao. Kusomeshwa na raslimali za nchi yao ni haki yao pia. Kugoma na kuandamana kusisitiza haki, maoni na msimamao wao ni haki yao katika kukumbusha viongozi wanaokaa kimya wakijifariji, “acha waseme watachoka!”
Vyama vya wafanyakazi vinaandaa migomo. Vinataka kima cha chini cha mshahara kipandishwe. Vinasema mishahara ya sasa halingani na hali halisi ya maisha nchini. Vinadai haki ya kuishi ya wanachama wake.
Wafanyakazi wa benki (National Microfinance Bank) ya Dar es Salaam wanagoma. Wanataka mkataba wao na mwajiri utiwe saini na wao wapate hisa zao katika benki. Wanadai haki yao.
Wastaafu hawana wa kugomea. Wanaandamana. Wanaziba barabara. Wanapanga kuweka kambi ikulu ingawa wanatishwa. Mama ntilie waliokuwa wakiwapa chakula, pale karibu na kituo cha garimoshi jijini Dar es Salaam, wameacha kutoa mkopo wa chakula.
Wastaafu wanapinga kufa. Wanadai kulipwa. Wakataa kauli za baadhi ya viongozi kuwa waliishalipwa zamani. Wanataka kusikilizwa.
Hakuna haja ya kuendelea kuorodhesha wanaogoma na wanaoandamana katika Tanzania leo. Hakuna haja ya kurodhesha sababu zinazofanya wagome na kuandamana. Ziko wazi.
Ni bahati mbaya kwamba Saidi Mwema hawezi kuchunguza wale wanaochelewesha na wanaonyima haki wenyeviti wa vitongoji Tandahimba, wanafunzi shule za msingi, walimu nchi nzima, wanafunzi vyuoni na wafanyakazi mahali pao pa kazi. Hawezi.
Mwema hawezi kwa kuwa waliomwajiri ndio chanzo cha malalamiko, migomo na maandamano. Labda ataelewa hili vizuri pale polisi wakigoma au wakiandamana.
Mwema hawezi na wala hana haja ya kufanya uchunguzi. Wanaoleta na wanaochochea migomo wanafahamika. Ni wale waliokabidhiwa madaraka katika maeneo mbalimbali ya utawala na hawafanyi kazi yao.
Ni wale wanaoona watendaji hawatendi lakini wanawaacha kwenye madaraka hadi malalamiko, migomo na maandamano. Ni serikali ambayo inakaa kimya huku wananchi wakilia na kusaga meno; lakini pia wakiigeukia na kuilaani vikali. Mwema hawezi kuchunguza serikali.
Pamoja na kwamba kugoma ni haki ya mtu kusisitiza madai yake, leo hii ondoa malalamiko ya wanaogoma kwa kuwapa haki zao; nani atasikia sauti zao, migomo wala maandamano? Mwema hahitaji kuchunguza.
(Makala hii itachapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili, 23 Oktoba 2008 chini ya safu ya SITAKI).
0713 614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com
SIKU 90 ZA KIFUNGO CHA MwanaHALISI
Friday, November 14, 2008
MAISHA YA WATOTO YANAPOHARIBIWA ASUBUHI
Serikali inayochekea wabakaji Liwale
Na Ndimara Tegambwage
SITAKI serikali ishindwe kuelewa umuhimu wa haraka wa kupambana na unyama unaofanywa na wabakaji katika wilaya ya Liwale, mkoani Lindi.
Taarifa za wiki hii kutoka wilayani Liwale zinasema “Watoto 255 wajifungua Liwale.” Lugha laini kama vile inatoka kwa mama mzazi anayesema mwanae aliyeolewa sasa amejifungua.
Sivyo ilivyo. Tufuatane na taarifa: “Idadi hiyo ni ya watoto kuanzia miaka 12, 13, 14 na wachache wa umri wa miaka 15…Hao ni wale wanaokuja hospitali. Wengine wakiishapima na kuona wana ujauzito hawaji tena…”
Maelezo hayo yanafafanua kuwa “watoto” hawa hawajaolewa. Kwanza hawajafikia umri wa kufanya maamuzi juu ya kuwa na familia. Hawajapewa ushauri na wazazi au walinzi wao. Ni watoto waliokumbwa na jinai.
Hao ni watoto waliobakwa na wanaume wa rika mbalimbali na kuwasababishia ujauzito. Ni watoto wa umri wa kwenda shule ambao wamenyimwa na, au wamekoseshwa haki ya kupata elimu. Wametupwa mitaani.
Hao ni watoto ambao utamu wa utoto wao umekatishwa. Ambao ung’avu wa ujana wao umeingizwa doa hata kabla hawajaweza kujua jinsi ya kujihudumia. Ambao ukubwa wao huko waendako umepata kilema. Ambao maisha yao yamewekwa njiapanda.
Kitendo cha watoto wa umri mdogo tena wajawazito wapatao 255 kuhudumiwa katika hospitali moja, kina kishindo kisicho cha kawaida katika jamii husika.
Kishindo kinatokana na ukweli kwamba kwa kipindi hicho cha 2007 – 2008, idadi ya watoto waliopata ujauzito wilayani Liwale inaweza kuwa hata zaidi ya mara nne au tano ya idadi iliyopatikana.
Kwa nini? Kwa sababu takwimu zilizopo ni kutoka hospitali moja. Kuna hospitali nyingine, vituo vya afya na zahanati wilayani. Kuna wakunga wa asili vijijini au familia ambamo “watoto” wamejifungua salama na bila msaada wa kitaalam. Idai yaweza kuwa kubwa zaidi.
Tufuatane na taarifa ya mwandishi kutoka Liwale ambaye ananukuu muuguzi mkuu: “…Wanaenda kutoa mimba kienyeji …kwa kujichokonoa na vijiti. (Wazazi) wanawaleta hospitali wakiwa wanavuja damu nyingi lakini tunajitahidi kuokoa maisha yao.”
“Wanaookolewa” ni wale waliofika hospitalini. Ni wangapi walijichokonoa kwa vijiti, wakavuja sana, wakapoteza damu nyingi na kufia kwa waganga vijijini?
Ni wangapi wamefia nyumbani kwa wazazi wao wakiwa wanajifungua kutokana na wazazi, ama kuwa mbali na hospitali, au kutoamini hospitali, au kufikiria kuwa watatozwa fedha wakati wao hawana chochote?
Wangapi wamekufa wakiwa wanatoa mimba au kutokana na matatizo mbalimbali ya ujauzito lakini hawajaripotiwa kufa? Wangapi wametelekezwa na wazazi wao kwa madai ya “kuwaaibisha” na sasa hawajulikani iwapo wako hai au wamekufa?
Wangapi wamepata matatizo ya ukosefu wa chakula (achana na chakula bora), mahali pa kuishi na kukosekana utulivu wa moyo hadi ujauzito kuharibika na hivyo afya zao kutetereka na wengine kupoteza maisha?
Watoto hawa wa umri mdogo hawajaolewa. Wamevamiwa na kubakwa na wanaume nyumbani kwao, njiani, vichakani, shuleni, kwenye nyumba za kulala wageni na kokote walikopelekwa kwa tendo la ngono.
Ni huzuni iliyoje kusikia kuwa kati ya watoto wajawazito 130 waliopelekwa hospitalini Liwale mwaka jana, ni 13 tu ambao walijifungua kwa njia ya kawaida.
Wengine, kutokana na viungo vyao kuwa vichanga na hivyo kushindwa kuhimili kazi kubwa ya kujifungua, ilibidi wapewe msaada wa nyongeza ikiwa ni pamoja na upasuaji mdogo.
Hilo ni janga la Liwale. Lakini ni janga la taifa zima. Halihitaji kufumbiwa macho. Linaambatana na janga jingine la ubakaji. Wabakaji wamevuka mipaka. Wanabaka watoto na kuwaingiza katika hali ya familia wakiwa bado hawajajitambua.
Ukiangalia umri uliotajwa wa kati ya miaka 12 na 15, utakuta ni umri wa kwenda shule. Hapa, ama kuna ukatili mkubwa wa kuwabaka watoto kwa nguvu au hakuna mazingira muwafaka – shuleni na nyumbani – kiasi kwamba ubakaji unafanywa kwa njia ya vishawishi.
Mathalani, shule zisizo na walimu au zenye walimu wachache; zisizo na madawati, vitabu na vifaa mbalimbali vya kufundishia na kujifunzia; zisizo na mafunzo ya nyongeza kwa yale ya darasani; zinaweza kuwa mahabusi ambamo watoto wengi watapenda kuasi au kushawishiwa kuasi.
Shuleni ambako hakuna shughuli za kuimba, midahalo, kucheza michezo mbalimbali kama mpira, kikapu, tenesi, kukimbia, kuruka, kuvuta kamba na michezo mingine ya riadha, ni mahali pa kuchosha pasipokuza akili na pasipo vishawishi vya kusoma.
Mahali ambako ufundishaji ni ule wa kukaririsha na siyo kufikirisha kwa njia ya kushirikisha wanafunzi kutafuta majibu na ufumbuzi, panaweza pia kuzaa tabia ya kukata tamaa na kuogopa kwenda shule; hivyo kunufaisha wabakaji.
Aidha, umasikini uliokithiri katika kaya, ambako wazazi wanamwambia mtoto wa kike asiwaulize kitoweo “kwa kuwa amekua,” unaweza kuchochea mazingira ya kubakwa wakiwa na umri mdogo.
Lakini ubakaji pia unaweza kushamiri kutokana na ujinga wa wazazi na wanafuzi. Ni kwa kiwango gani elimu ya uzazi imetolewa kwa wazazi na watoto tangu wakiwa na umri mdogo?
Kinachotendeka Liwale kipo kila wilaya nchini. Watoto wa kike wanaingizwa katika maisha ya familia kabla ya muda wao – “mtoto amezaa mtoto.” Katika hali hii, maisha ya kichanga na “mtoto-mama” yanabaki mashakani.
Serikali ina jukumu la kuwahakikishia watoto wa kike ulinzi wa haki zao zote za msingi kuanzia uhai na elimu.
Serikali haina budi kutafuta kiini cha tatizo hili – mazingira ya kiuchumi na kijamii ambamo ukatili huu unafanyika – na kutafuta ufumbuzi wa kudumu Liwale na nchini nzima. Kusubiri ni kuongeza tatizo na hata vifo.
(Makala hii itachapishwa katika safu ya SITAKI ya Tanzania Daima Jumapili, 16 Novemba 2008)
0713 614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com
Na Ndimara Tegambwage
SITAKI serikali ishindwe kuelewa umuhimu wa haraka wa kupambana na unyama unaofanywa na wabakaji katika wilaya ya Liwale, mkoani Lindi.
Taarifa za wiki hii kutoka wilayani Liwale zinasema “Watoto 255 wajifungua Liwale.” Lugha laini kama vile inatoka kwa mama mzazi anayesema mwanae aliyeolewa sasa amejifungua.
Sivyo ilivyo. Tufuatane na taarifa: “Idadi hiyo ni ya watoto kuanzia miaka 12, 13, 14 na wachache wa umri wa miaka 15…Hao ni wale wanaokuja hospitali. Wengine wakiishapima na kuona wana ujauzito hawaji tena…”
Maelezo hayo yanafafanua kuwa “watoto” hawa hawajaolewa. Kwanza hawajafikia umri wa kufanya maamuzi juu ya kuwa na familia. Hawajapewa ushauri na wazazi au walinzi wao. Ni watoto waliokumbwa na jinai.
Hao ni watoto waliobakwa na wanaume wa rika mbalimbali na kuwasababishia ujauzito. Ni watoto wa umri wa kwenda shule ambao wamenyimwa na, au wamekoseshwa haki ya kupata elimu. Wametupwa mitaani.
Hao ni watoto ambao utamu wa utoto wao umekatishwa. Ambao ung’avu wa ujana wao umeingizwa doa hata kabla hawajaweza kujua jinsi ya kujihudumia. Ambao ukubwa wao huko waendako umepata kilema. Ambao maisha yao yamewekwa njiapanda.
Kitendo cha watoto wa umri mdogo tena wajawazito wapatao 255 kuhudumiwa katika hospitali moja, kina kishindo kisicho cha kawaida katika jamii husika.
Kishindo kinatokana na ukweli kwamba kwa kipindi hicho cha 2007 – 2008, idadi ya watoto waliopata ujauzito wilayani Liwale inaweza kuwa hata zaidi ya mara nne au tano ya idadi iliyopatikana.
Kwa nini? Kwa sababu takwimu zilizopo ni kutoka hospitali moja. Kuna hospitali nyingine, vituo vya afya na zahanati wilayani. Kuna wakunga wa asili vijijini au familia ambamo “watoto” wamejifungua salama na bila msaada wa kitaalam. Idai yaweza kuwa kubwa zaidi.
Tufuatane na taarifa ya mwandishi kutoka Liwale ambaye ananukuu muuguzi mkuu: “…Wanaenda kutoa mimba kienyeji …kwa kujichokonoa na vijiti. (Wazazi) wanawaleta hospitali wakiwa wanavuja damu nyingi lakini tunajitahidi kuokoa maisha yao.”
“Wanaookolewa” ni wale waliofika hospitalini. Ni wangapi walijichokonoa kwa vijiti, wakavuja sana, wakapoteza damu nyingi na kufia kwa waganga vijijini?
Ni wangapi wamefia nyumbani kwa wazazi wao wakiwa wanajifungua kutokana na wazazi, ama kuwa mbali na hospitali, au kutoamini hospitali, au kufikiria kuwa watatozwa fedha wakati wao hawana chochote?
Wangapi wamekufa wakiwa wanatoa mimba au kutokana na matatizo mbalimbali ya ujauzito lakini hawajaripotiwa kufa? Wangapi wametelekezwa na wazazi wao kwa madai ya “kuwaaibisha” na sasa hawajulikani iwapo wako hai au wamekufa?
Wangapi wamepata matatizo ya ukosefu wa chakula (achana na chakula bora), mahali pa kuishi na kukosekana utulivu wa moyo hadi ujauzito kuharibika na hivyo afya zao kutetereka na wengine kupoteza maisha?
Watoto hawa wa umri mdogo hawajaolewa. Wamevamiwa na kubakwa na wanaume nyumbani kwao, njiani, vichakani, shuleni, kwenye nyumba za kulala wageni na kokote walikopelekwa kwa tendo la ngono.
Ni huzuni iliyoje kusikia kuwa kati ya watoto wajawazito 130 waliopelekwa hospitalini Liwale mwaka jana, ni 13 tu ambao walijifungua kwa njia ya kawaida.
Wengine, kutokana na viungo vyao kuwa vichanga na hivyo kushindwa kuhimili kazi kubwa ya kujifungua, ilibidi wapewe msaada wa nyongeza ikiwa ni pamoja na upasuaji mdogo.
Hilo ni janga la Liwale. Lakini ni janga la taifa zima. Halihitaji kufumbiwa macho. Linaambatana na janga jingine la ubakaji. Wabakaji wamevuka mipaka. Wanabaka watoto na kuwaingiza katika hali ya familia wakiwa bado hawajajitambua.
Ukiangalia umri uliotajwa wa kati ya miaka 12 na 15, utakuta ni umri wa kwenda shule. Hapa, ama kuna ukatili mkubwa wa kuwabaka watoto kwa nguvu au hakuna mazingira muwafaka – shuleni na nyumbani – kiasi kwamba ubakaji unafanywa kwa njia ya vishawishi.
Mathalani, shule zisizo na walimu au zenye walimu wachache; zisizo na madawati, vitabu na vifaa mbalimbali vya kufundishia na kujifunzia; zisizo na mafunzo ya nyongeza kwa yale ya darasani; zinaweza kuwa mahabusi ambamo watoto wengi watapenda kuasi au kushawishiwa kuasi.
Shuleni ambako hakuna shughuli za kuimba, midahalo, kucheza michezo mbalimbali kama mpira, kikapu, tenesi, kukimbia, kuruka, kuvuta kamba na michezo mingine ya riadha, ni mahali pa kuchosha pasipokuza akili na pasipo vishawishi vya kusoma.
Mahali ambako ufundishaji ni ule wa kukaririsha na siyo kufikirisha kwa njia ya kushirikisha wanafunzi kutafuta majibu na ufumbuzi, panaweza pia kuzaa tabia ya kukata tamaa na kuogopa kwenda shule; hivyo kunufaisha wabakaji.
Aidha, umasikini uliokithiri katika kaya, ambako wazazi wanamwambia mtoto wa kike asiwaulize kitoweo “kwa kuwa amekua,” unaweza kuchochea mazingira ya kubakwa wakiwa na umri mdogo.
Lakini ubakaji pia unaweza kushamiri kutokana na ujinga wa wazazi na wanafuzi. Ni kwa kiwango gani elimu ya uzazi imetolewa kwa wazazi na watoto tangu wakiwa na umri mdogo?
Kinachotendeka Liwale kipo kila wilaya nchini. Watoto wa kike wanaingizwa katika maisha ya familia kabla ya muda wao – “mtoto amezaa mtoto.” Katika hali hii, maisha ya kichanga na “mtoto-mama” yanabaki mashakani.
Serikali ina jukumu la kuwahakikishia watoto wa kike ulinzi wa haki zao zote za msingi kuanzia uhai na elimu.
Serikali haina budi kutafuta kiini cha tatizo hili – mazingira ya kiuchumi na kijamii ambamo ukatili huu unafanyika – na kutafuta ufumbuzi wa kudumu Liwale na nchini nzima. Kusubiri ni kuongeza tatizo na hata vifo.
(Makala hii itachapishwa katika safu ya SITAKI ya Tanzania Daima Jumapili, 16 Novemba 2008)
0713 614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com
Thursday, November 6, 2008
TUMPONGEZE OBAMA LAKINI NI MMAREKANI

Wanaotarajia Obama kuwaokoa
Na Ndimara Tegambwage
SITAKI Watanzania na Waafrika wakae wakisubiri Barack Obama, rais wa 44 wa Marekani awaletee unafuu wa maisha au asababishe mabadiliko ya kisiasa, kiuchumi na kijamii katika mataifa yao.
Kila mmoja, popote alipo, hana budi kueleza hisia zake kuhusiana na ushindi wa Obama lakini baada ya hapo arejee kwenye nafasi yake ya awali na kupambana na changamoto za maisha katika nchi na bara lake.
Kwa mantiki hii kusiwepo wa kusema kwamba kupanda kwa Obama kwenye kiti cha urais kutaiokoa Tanzania au Afrika.
Obama ana nchi yake. Ni Marekani. Obama ana wananchi wake. Ni Wamarekani. Obama ana majukumu yake mazito ambayo ameahidi kuyakabili. Ni majukumu ya Marekani na Wamarekani.
Majukumu ya Obama na wananchi wake ndiyo Na. 1 kwa rais wa 44 wa taifa kubwa kiuchumi na kijeshi na ambalo kwa takribani miaka 60 sasa limeitwa taifa la kibeberu duniani.
Kama ubeberu wa Marekani ungalipo leo – na hatuhitaji wa kutushawishi kuwa umeisha – basi ni Obama atakayeusimamia. Chembechembe za Uafrika ndani ya Obama haziondoi ubabe wala ubeberu wa Marekani.
Kuna mafunzo hapa. Barack Hussein Obama, mwenye damu mchanganyiko, ni raia wa Marekani. Ni uzao wa wananchi wa Marekani wenye historia ndefu ya kupigania haki na usawa wa watu wote ndani ya nchi yao.
Kuingia kwake madarakani kunampa fursa ya kujenga hoja zaidi na sahihi kwamba Waafrika-Wamarekani, kama walivyo raia wengine nchini humo, “wanaweza” na wataweza.
Ushindi wa Obama ni mwendelezo tu wa harakati za kijamii nchini Marekani za kuthibitisha kuwa weupe au weusi – jambo ambalo limekuwa msingi wa ubaguzi wa rangi nchini humo – ni mbinu chafu, ya kale, ya kishenzi, isiyo na maana tena na isiyokubalika.
Lakini siyo kwamba jambo hilo lilikuwa halijaeleweka hadi Novemba 4, bali ukurutu katika vichwa vya baadhi ya wabaguzi, ambao hutumia rangi kunyonya jasho na damu ya jamii na kunyima haki za msingi na fursa mbalimbali, huwa hauishi mara moja.
Kwamba Obama mwenye mzazi wa Kenya na mzazi wa Marekani amepanda hadi ofisi kuu ya utawala nchini humo, unaweza kuwa ushahidi mwingine kuwa Wamarekani wanaendelea kukata minyororo iliyowafunga akili kwa tarkriban karne tano; na wanachopaswa kujali sasa ni “tunda” la nchi yao na si rangi ya mwili.
Bali jambo moja ni wazi kabisa. Obama amedhihirisha kujitambua – yeye ni nani katika jamii yake – na anaweza kufanya nini kwa jamii hiyo. Alichoomba ndicho amepata.
Pamoja na urais, aliomba kuvunja zaidi nguvu za fikra dhalili zinazojali rangi kuliko utu. Ameongoza Marekani kushinda.
Obama asingechaguliwa kuwa rais wa Marekani kama siyo Mmarekani. Hivyo, jukumu lake ni kutumikia Wamarekani, kusimamia na kuendeleza mipango ya Wamarekani, kulinda taifa na Katiba ya nchi yake na kwa ujumla, kushirikiana na mataifa mengine kukabiliana na changamoto za dunia.
Tunaloweza kujifunza kutoka kwa Obama ni jinsi alivyokua, kujilea, kuingia katika jamii yake na kukubalika; kuingia katika moja ya vyama vikubwa nchini, kukubali kulelewa na kujiimarisha hadi kuwa mahiri katika siasa za chama chake; kupata uongozi kama seneta na sasa kuchaguliwa kuwa rais.
Obama ni rais kama rais mwingine wa Marekani. Chembechembe za weusi hazimfanyi awe na huruma kwa Afrika. Atakwenda kwa kufuata misingi na sera za nchi yake. Hatua yoyote ya kutaka upendeleo kwa Afrika au hata Kenya, ambayo haimo katika sera zao za mambo ya nje, yaweza hata kuhatarisha upangaji wake ikulu.
Lakini hata akitaka kuwa laini kwa Afrika, bara hili, Tanzania ikiwemo, halina sababu ya kutarajia au kusubiri fadhila za mkuu wa nchi wa Marekani.
Hakuna sababu ya kutarajia huruma na misaada kutoka Marekani wakati watawala wa nchi zetu wamejenga au wanalinda mifumo inayofuja kodi za wananchi, misaada na hata mikopo kutoka nje.
Hakuna sababu ya kutarajia Obama awe karimu wakati watawala wetu wanauza nyasi, miti, misitu, wanyama na madini kwa bei ya kutupa. Ni matumizi ya raslimali hizi ambayo yangefanya mkuu wa nchi Tanzania awe na jeuri sawa na rais wa nchi kubwa, kwani nchi yake itakuwa inajitegemea na kutembea kifua mbele.
Acha vijana wajifunze na kuiga uwezo wa Obama wa kujieleza na kujenga hoja kwa uthabiti. Acha wajifunze ujasiri wake wa kutosubiri kupewa bali wa kujitafutia. Acha wajifunze umuhimu wa elimu kama silaha muhimu maishani.
Tuwaache wakubwa na wadogo wajifunze kutokata tamaa na badala yake kuwa king’ang’anizi katika kupigania haki na fursa sawa za kijamii na kisiasa.
Baada ya hapo tumwache Obama atumikie taifa lake kama marais wengine wa Marekeni. Kama ni suala la maendeleo na mabadiliko katika maisha ya wananchi katika Afrika, tuwakabe wanaotutoza kodi, kupokea misaada na mikopo halafu wakatembeza bakuli la ombaomba.
Tanzania na Afrika, ina unyonge na umasikini wa kuletewa na watawala – ama kwa kutojali, kushiriki kuibia nchi, kuendeleza mifumo mibovu inayoendelea kufunga nchi hii kwenye bomba kuu la unyonyaji wa kimataifa au kwa ujinga.
Afrika haipaswi kutarajia Obama aingie jikoni na vyumbani mwetu kumaliza matatizo yetu. Tumpe hongera; kaandika historia. Basi! Kinachohitajika ni kuandaa mbinu za mabadiliko. Na uwezekano wa mafanikio katika kuleta mabadiliko ni mkubwa.
(Makala hii itachapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili, 9 Novemba 2008 chini ya safu ya SITAKI)
0713 614872
ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com
Monday, November 3, 2008
MAUAJI YA KISHIRIKINA YAUMBUA SERIKALI
Baada ya albino, nani?
• Mwito wa elimu, mabadiliko
Na Ndimara Tegambwage
SIYO siri tena. Katika Tanzania, baadhi ya wananchi wanawinda wananchi wenzao wenye ulemavu wa ngozi – Albino – na kuwaua.
Mauaji yanaenda sambamba na uvumi kwamba viungo vya albino ni mali na kwamba aliyenavyo aweza kupewa dawa ya kumwezesha kuwa tajiri.
Hivi sasa mbio za kupata utajiri zimechukua kasi ileile ya mauaji. Wengi wanatamani utajiri wa miujiza. Kadri fikra hizo zinavyozingatiwa, ndivyo albino wanavyoendelea kuangamia.
Wanawaua. Wanakata viungo vyao na kuvipeleka kwa watu masikini lakini wenye imani ya kuwapa utajiri watu wengine. Hata makaburi ya albino yanafukuliwa ili kupata viungo. Wazimu!
Mauaji ya albino ni mauaji sawa na yale ya mtu yeyote. Ni uhalifu usiosameheka. Ni msiba mkubwa na endelevu wa kitaifa.
Lakini madhara makuu ni kwamba mauaji haya yana tabia ya kuambukiza. Leo vinatakiwa viungo vya albino, kesho vitatakiwa vya nani?
Haitakuwa rahisi kujua albino wote waliouawa na waliosalia, kwani hakuna takwimu za idadi ya albino nchi nzima. Idadi ya waliouawa ni ya kuokoteza hapa na pale au ile iliyoripotiwa na waandishi wa habari za uchunguzi.
Hii ni kutokana na sababu zifuatazo:
Kwanza, kuna wanaoishi mbali na miji na taarifa juu yao hazipatikani kwa urahisi au hazipatikani kabisa.
Pili, kuna wale ambao wazazi wao walishiriki kuwaua kutokana na imani kwamba kuzaa albino ni “balaa.” Wazazi hawatasema au watasingizia sababu nyingine za kifo.
Tatu, kuna wanaoogopa kusema matukio hayo kutokana na kutishiwa au hata kuhongwa fedha au ahadi ili wakae kimya. Kimya hiki, katika maeneo haya, kinaweza kuwa kinaendeleza mauaji mengi zaidi ya albino.
Bali jambo moja ambalo limefahamika. Katika siku za karibuni, kila albino aliyeuawa imedaiwa ni kwa sababu ya kupata viungo vya mwili wake ili vipelekwe kwa “mganga” kutengenezea “dawa ya utajiri.”
Bila shaka idadi ya albino, haiwezi kutosheleza mahitaji ya wanaotaka utajiri au vyeo vya siasa. Hata hivyo, hakuna anayeua albino mmoja na kumweka nyumbani kusubiri mteja anayehitaji kiungo fulani.
Hata kama kuna mwenye ghala la waliouawa, hakuna anayejua ni kiungo kipi mganga fulani atahitaji na kama atataka kilichokauka au kibichi.
Kwa hiyo albino waweza kuisha. Lakini pia waganga waweza kusema albino “si mali tena;” wakataja mtu mwingine wa jinsia, cheo, umaarufu na nafasi fulani katika jamii.
Hapo ndipo itakuwa mshikemshike, na labda ndipo watawala watakurupushwa usingizini na kuonekana wamekuwa wakilea mauaji endelevu.
Kama awali mahitaji yalikuwa kiungo chochote cha albino yeyote; fikiria idadi ya watakaouawa pale waganga wakianza kusema wanataka kiganja cha mkono wa kulia wa kichanga cha siku 10. Vichanga vingapi vitauawa?
Mahitaji ya viungo vya binadamu yaweza kwenda yanapanuka kila siku. Chukua mfano wa waganga watakaotaka kichwa cha bibi kizee wa miaka 80; pua ya mtoto wa kike wa mwenyekiti wa mtaa; au magoti yote mawili ya mama yake diwani.
Kasheshe itaaanza kukomaa pale utakaposikia sasa waganga wanataka nyama ya katikati ya mgongo ya mama mkwe wa mkurugenzi wa halmashauri; huku wengine wakidai matiti yote mawili ya binti wa mkuu wa wilaya na wengine wakitaka visigino vyote vya mke wa mbunge.
Labda baada ya hapo serikali inaweza kustuka, kwamba hali inaanza kuwa mbaya na kukumbuka kuwa laiti ingechukua hatua wakati albino wanapiga yowe.
Hapo ndipo kimbunga cha aina yake kinaweza kutokea. Leo utasikia mganga anataka masikio mawili ya dada yake (wa kuzaliwa) mkuu wa mkoa. Kesho utasikia mganga mwingine anataka kiganja cha mkono wa kushoto cha mtoto wa kiume wa waziri.
Yote hayo ni nyongeza tu kwa taarifa za awali, kwamba mganga mwingine anataka titi la kushoto la mama mkwe wa waziri mkuu.
Wakati waziri mkuu wa zamani anaanza kuchekelea kuwa afadhali yeye hayuko tena kwenye uongozi, zinaingia zile motomoto kwamba mganga anataka utumbo mdogo wa aliyewahi kuwa waziri mkuu.
Waganga hawana simile. Kadri idadi ya wanaosaka utajiri na hata vyeo katika siasa inavyoongezeka, nao wanapanua wigo wa matakwa ya dawa.
Mara hii habari zitasambaa kuwa kwa utajiri mkubwa sharti upeleke figo za rais mstaafu. Uuuhwi! Hapa marais wastaafu watawindwa kama swala, wakati walioukosa wakichekea kiganjani.
Kwa utajiri wa juu zaidi ya hapo, sharti lipatikane taya zima la chini la rais aliyeko kitini. Ni kazi kubwa kulipata kutokana na ulinzi mkali alionao lakini nani anajua kiasi ambacho mganga anatarajia kutoza mteja wake?
Kama hatua ya kulegeza mahitaji, taarifa zitasambazwa kwamba kwa utajiri na vyeo vya kati, waganga wanataka shingo la waliowahi kuwa viongozi wakuu visiwani.
Baada ya miezi kadhaa taarifa zitaenea kuwa kwa biashara nzuri na nchi za nje, inahitajika ngozi ya waziri kiongozi au utumbo mkubwa wa mkurugenzi wa ikulu.
Sasa woga utakuwa umetanda. Wananchi watakuwa wanapumua mapigo nusunusu. Watawala watakuwa wamekuwa sehemu ya ushirikina katika kujaribu kujikinga.
Kama kwamba matakwa ya waganga yatakuwa yameanza kuzoeleka, ndipo utasikia sasa wanataka uti wa mgongo wa kiongozi wa chama cha kikuu cha upinzani.
Baada ya siku kadhaa utasikia wanataka ubongo wa kardinali na kabla wananchi hawajaanza kutafakari vema matakwa hayo, watasikia sasa waganga wanataka ulimi wa sheikh mkuu.
Huku hoja nzito zikiwa zimepamba moto bungeni, utasikia waganga sasa wanataka kilo mbili za nyama ya paja la kulia la wabunge machachari (na majina yao yanatajwa).
Ni hofu kuu. Spika wa bunge anajitahidi kuyeyusha kile anachoita uvumi lakini siku inayofuata taarifa zinafika kwamba waganga sasa wanataka ubavu mzima (kidali) wa spika.
Na bado watu wengi wanakwenda kwa waganga. Hapa ndipo wengi wanakumbana na kisiki. Waganga wanataka korodani za watuhumiwa wa ufisadi. Eh!
Utawala unayumba. Majeshi yanawekwa kwenye hali ya tahadhari. Lakini katikati ya maandalizi zinakuja taarifa kwamba waganga wanataka moyo wa mke wa mkuu wa majeshi.
Polisi wanapoanza doria, taarifa zinamiminika kuwa waganga sasa wanataka macho yote mawili ya binti mkubwa wa mkuu wa jeshi la polisi.
Huku upelelezi ukiwa unaendelea kujaribu kuona kilicholeta janga, taarifa zinaingia kwamba waganga sasa wanataka mikono yote miwili ya mkuu wa mashushushu.
Kana kwamba waganga sasa ndio wanatawala, taarifa zinaenea kote, bara na visiwani, kwamba waganga wanataka koromeo za waandishi wa habari “kaidi.”
Hivyo ndivyo itakavyokuwa, iwapo watawala hawatasitisha mauaji ya albino.
Vita vya kusitisha mauaji ya albino ni vita vya kuzuia maafa makubwa zaidi kwa jamii nzima.
Silaha kuu ni elimu. Darasani na mitaani; kwenye mikutano ya hadhara, vijiweni, maofisini na viwandani, ujumbe uwe mmoja:
“Albino ni mtu kama wewe na mimi. Ana haki ya kuishi. Hakuna mwenye viungo vya kuzalisha utajiri.”
Mauaji ya albino yafafanuliwe kuwa ni ukatili. Ni uhalifu mkuu. Ni ukiukwaji wa haki za binadamu. Kunyamazia haya, au kutoyakomesha ni kujiunga na wauaji.
Elimu inaweza kuimarishwa kwa sheria, taratibu, kanuni na ufuatiliaji usiokoma na kwa njia hii, mabadiliko yaweza kutokea. Bali sharti idadi ya albino nchini ifahamike; kuwepo utaratibu wa kudumu wa kujua wanaozaliwa, wanaofariki na kwa sababu zipi.
Ukatili, ujinga, ushirikina, uzembe na dharau si maadili ya jamii nyofu wala watawala. Kushindwa kulinda maisha ya albino mmoja ni kukiri kushindwa kulinda maisha ya jamii nzima. Albino wasiuawe.
(Imeandaliwa kuchapishwa katika gazeti la Tanzania Daima wiki ya 3 -9 Novemba 2008)
Simu:0713 614872
Imeili:ndimara@yahoo.com
• Mwito wa elimu, mabadiliko
Na Ndimara Tegambwage
SIYO siri tena. Katika Tanzania, baadhi ya wananchi wanawinda wananchi wenzao wenye ulemavu wa ngozi – Albino – na kuwaua.
Mauaji yanaenda sambamba na uvumi kwamba viungo vya albino ni mali na kwamba aliyenavyo aweza kupewa dawa ya kumwezesha kuwa tajiri.
Hivi sasa mbio za kupata utajiri zimechukua kasi ileile ya mauaji. Wengi wanatamani utajiri wa miujiza. Kadri fikra hizo zinavyozingatiwa, ndivyo albino wanavyoendelea kuangamia.
Wanawaua. Wanakata viungo vyao na kuvipeleka kwa watu masikini lakini wenye imani ya kuwapa utajiri watu wengine. Hata makaburi ya albino yanafukuliwa ili kupata viungo. Wazimu!
Mauaji ya albino ni mauaji sawa na yale ya mtu yeyote. Ni uhalifu usiosameheka. Ni msiba mkubwa na endelevu wa kitaifa.
Lakini madhara makuu ni kwamba mauaji haya yana tabia ya kuambukiza. Leo vinatakiwa viungo vya albino, kesho vitatakiwa vya nani?
Haitakuwa rahisi kujua albino wote waliouawa na waliosalia, kwani hakuna takwimu za idadi ya albino nchi nzima. Idadi ya waliouawa ni ya kuokoteza hapa na pale au ile iliyoripotiwa na waandishi wa habari za uchunguzi.
Hii ni kutokana na sababu zifuatazo:
Kwanza, kuna wanaoishi mbali na miji na taarifa juu yao hazipatikani kwa urahisi au hazipatikani kabisa.
Pili, kuna wale ambao wazazi wao walishiriki kuwaua kutokana na imani kwamba kuzaa albino ni “balaa.” Wazazi hawatasema au watasingizia sababu nyingine za kifo.
Tatu, kuna wanaoogopa kusema matukio hayo kutokana na kutishiwa au hata kuhongwa fedha au ahadi ili wakae kimya. Kimya hiki, katika maeneo haya, kinaweza kuwa kinaendeleza mauaji mengi zaidi ya albino.
Bali jambo moja ambalo limefahamika. Katika siku za karibuni, kila albino aliyeuawa imedaiwa ni kwa sababu ya kupata viungo vya mwili wake ili vipelekwe kwa “mganga” kutengenezea “dawa ya utajiri.”
Bila shaka idadi ya albino, haiwezi kutosheleza mahitaji ya wanaotaka utajiri au vyeo vya siasa. Hata hivyo, hakuna anayeua albino mmoja na kumweka nyumbani kusubiri mteja anayehitaji kiungo fulani.
Hata kama kuna mwenye ghala la waliouawa, hakuna anayejua ni kiungo kipi mganga fulani atahitaji na kama atataka kilichokauka au kibichi.
Kwa hiyo albino waweza kuisha. Lakini pia waganga waweza kusema albino “si mali tena;” wakataja mtu mwingine wa jinsia, cheo, umaarufu na nafasi fulani katika jamii.
Hapo ndipo itakuwa mshikemshike, na labda ndipo watawala watakurupushwa usingizini na kuonekana wamekuwa wakilea mauaji endelevu.
Kama awali mahitaji yalikuwa kiungo chochote cha albino yeyote; fikiria idadi ya watakaouawa pale waganga wakianza kusema wanataka kiganja cha mkono wa kulia wa kichanga cha siku 10. Vichanga vingapi vitauawa?
Mahitaji ya viungo vya binadamu yaweza kwenda yanapanuka kila siku. Chukua mfano wa waganga watakaotaka kichwa cha bibi kizee wa miaka 80; pua ya mtoto wa kike wa mwenyekiti wa mtaa; au magoti yote mawili ya mama yake diwani.
Kasheshe itaaanza kukomaa pale utakaposikia sasa waganga wanataka nyama ya katikati ya mgongo ya mama mkwe wa mkurugenzi wa halmashauri; huku wengine wakidai matiti yote mawili ya binti wa mkuu wa wilaya na wengine wakitaka visigino vyote vya mke wa mbunge.
Labda baada ya hapo serikali inaweza kustuka, kwamba hali inaanza kuwa mbaya na kukumbuka kuwa laiti ingechukua hatua wakati albino wanapiga yowe.
Hapo ndipo kimbunga cha aina yake kinaweza kutokea. Leo utasikia mganga anataka masikio mawili ya dada yake (wa kuzaliwa) mkuu wa mkoa. Kesho utasikia mganga mwingine anataka kiganja cha mkono wa kushoto cha mtoto wa kiume wa waziri.
Yote hayo ni nyongeza tu kwa taarifa za awali, kwamba mganga mwingine anataka titi la kushoto la mama mkwe wa waziri mkuu.
Wakati waziri mkuu wa zamani anaanza kuchekelea kuwa afadhali yeye hayuko tena kwenye uongozi, zinaingia zile motomoto kwamba mganga anataka utumbo mdogo wa aliyewahi kuwa waziri mkuu.
Waganga hawana simile. Kadri idadi ya wanaosaka utajiri na hata vyeo katika siasa inavyoongezeka, nao wanapanua wigo wa matakwa ya dawa.
Mara hii habari zitasambaa kuwa kwa utajiri mkubwa sharti upeleke figo za rais mstaafu. Uuuhwi! Hapa marais wastaafu watawindwa kama swala, wakati walioukosa wakichekea kiganjani.
Kwa utajiri wa juu zaidi ya hapo, sharti lipatikane taya zima la chini la rais aliyeko kitini. Ni kazi kubwa kulipata kutokana na ulinzi mkali alionao lakini nani anajua kiasi ambacho mganga anatarajia kutoza mteja wake?
Kama hatua ya kulegeza mahitaji, taarifa zitasambazwa kwamba kwa utajiri na vyeo vya kati, waganga wanataka shingo la waliowahi kuwa viongozi wakuu visiwani.
Baada ya miezi kadhaa taarifa zitaenea kuwa kwa biashara nzuri na nchi za nje, inahitajika ngozi ya waziri kiongozi au utumbo mkubwa wa mkurugenzi wa ikulu.
Sasa woga utakuwa umetanda. Wananchi watakuwa wanapumua mapigo nusunusu. Watawala watakuwa wamekuwa sehemu ya ushirikina katika kujaribu kujikinga.
Kama kwamba matakwa ya waganga yatakuwa yameanza kuzoeleka, ndipo utasikia sasa wanataka uti wa mgongo wa kiongozi wa chama cha kikuu cha upinzani.
Baada ya siku kadhaa utasikia wanataka ubongo wa kardinali na kabla wananchi hawajaanza kutafakari vema matakwa hayo, watasikia sasa waganga wanataka ulimi wa sheikh mkuu.
Huku hoja nzito zikiwa zimepamba moto bungeni, utasikia waganga sasa wanataka kilo mbili za nyama ya paja la kulia la wabunge machachari (na majina yao yanatajwa).
Ni hofu kuu. Spika wa bunge anajitahidi kuyeyusha kile anachoita uvumi lakini siku inayofuata taarifa zinafika kwamba waganga sasa wanataka ubavu mzima (kidali) wa spika.
Na bado watu wengi wanakwenda kwa waganga. Hapa ndipo wengi wanakumbana na kisiki. Waganga wanataka korodani za watuhumiwa wa ufisadi. Eh!
Utawala unayumba. Majeshi yanawekwa kwenye hali ya tahadhari. Lakini katikati ya maandalizi zinakuja taarifa kwamba waganga wanataka moyo wa mke wa mkuu wa majeshi.
Polisi wanapoanza doria, taarifa zinamiminika kuwa waganga sasa wanataka macho yote mawili ya binti mkubwa wa mkuu wa jeshi la polisi.
Huku upelelezi ukiwa unaendelea kujaribu kuona kilicholeta janga, taarifa zinaingia kwamba waganga sasa wanataka mikono yote miwili ya mkuu wa mashushushu.
Kana kwamba waganga sasa ndio wanatawala, taarifa zinaenea kote, bara na visiwani, kwamba waganga wanataka koromeo za waandishi wa habari “kaidi.”
Hivyo ndivyo itakavyokuwa, iwapo watawala hawatasitisha mauaji ya albino.
Vita vya kusitisha mauaji ya albino ni vita vya kuzuia maafa makubwa zaidi kwa jamii nzima.
Silaha kuu ni elimu. Darasani na mitaani; kwenye mikutano ya hadhara, vijiweni, maofisini na viwandani, ujumbe uwe mmoja:
“Albino ni mtu kama wewe na mimi. Ana haki ya kuishi. Hakuna mwenye viungo vya kuzalisha utajiri.”
Mauaji ya albino yafafanuliwe kuwa ni ukatili. Ni uhalifu mkuu. Ni ukiukwaji wa haki za binadamu. Kunyamazia haya, au kutoyakomesha ni kujiunga na wauaji.
Elimu inaweza kuimarishwa kwa sheria, taratibu, kanuni na ufuatiliaji usiokoma na kwa njia hii, mabadiliko yaweza kutokea. Bali sharti idadi ya albino nchini ifahamike; kuwepo utaratibu wa kudumu wa kujua wanaozaliwa, wanaofariki na kwa sababu zipi.
Ukatili, ujinga, ushirikina, uzembe na dharau si maadili ya jamii nyofu wala watawala. Kushindwa kulinda maisha ya albino mmoja ni kukiri kushindwa kulinda maisha ya jamii nzima. Albino wasiuawe.
(Imeandaliwa kuchapishwa katika gazeti la Tanzania Daima wiki ya 3 -9 Novemba 2008)
Simu:0713 614872
Imeili:ndimara@yahoo.com