CCM YATAKA MSAADA WA ASKARI
Na Ndimara Tegambwage
SITAKI Chama Cha Mapinduzi (CCM) kibaki katika jimbo la uchaguzi la Tarime wakati tayari kimekiri kushindwa. Tujenge mashaka: Kinabaki uwanjani hadi uchaguzi ili kifanye nini?
Mapema wiki hii, Makamu Mwenyekiti wa CCM, Pius Mekwa alikaririwa na vyombo vya habari akikiri kuzidiwa nguvu; akisema vurugu zimezidi na wafuasi wa chama chake wanamwagiwa pilipili.
Katika hali inayoonyesha kuwa ingekuwa kazi yake binafsi angebwaga manyanga na kuacha jimbo, Msekwa amekaririwa akisema kuwa atamweleza Rais Jakaya Kikwete apeleke askari wengi zaidi kukabiliana na kile alichoita “vurugu.”
Hapo ndipo CCM imefikia. Siyo siasa tena. Ni askari. Ni silaha. Ni vita. Rejea kauli za watawala wakati wa vuguvugu la kurejesha mfumo wa vyama vingi: Kuanzia kiongozi wa ngazi ya chini kabisa hadi mkuu wa nchi, wote walieneza hofu kuwa “vyama vingi vikija, vita vitakuja pia.”
Leo, tunajua nani angeleta vita. Watawala wakishindwa, au wakionekana kushindwa, au wakitikiswa; wanaweka siasa chini. Wanachukua kauli na vitendo vya ubabe. Wanakimbilia kwa rais kuomba askari na silaha. Wanatangaza vita. Wanaanzisha vita. Wanaingiza vita Tarime na nchini.
Hivyo ndivyo vita ambavyo wanasiasa waliokuwa madarakani kati ya 1985 na 1992 walikuwa wakitishia wananchi. Kwamba wao, watawala wakishindwa, au wakiona wanaanza kutetereka, hawatakubali. Wataanzisha vita.
Naomba kutoa hoja, kwamba kwa kushikilia utawala kwa karibu miaka 50; kwa mbwembwe za utukufu wa kisiasa na majigambo; kwa woga wa kushindwa na hisia tu kwamba watadhalilika iwapo watashindwa; hakika baadhi ya viongozi wa CCM wanaweza kuingiza nchi vitani.
Lakini hiyo ndiyo hali iliyoko jimboni Tarime. Kama makamu mwenyekiti wa chama kinachopanga ikulu anatamani matumizi ya “askari zaidi” na hivyo silaha zaidi, basi mambo ni magumu kwa chama hicho.
Na haya mapenzi ya CCM kwa askari na silaha ni mapenzi hatari. Silaha badala ya siasa? Askari badala ya raia wanaoimba nyimbo na ngonjera? Milio ya bunduki badala ya hotuba zilizosheheni ahadi zinazotekelezeka na kuambizana ukweli uwanjani? Hapana.
Naomba kutoa hoja, kwamba ikifikia hapo, askari wanaoitwa katika siasa wataanza kujiuliza: Hivi kumbe watu hawa (watawala) ni chui wa karatasi?
Mwandishi mmoja wa vitabu wa Afrika Magharibi aliwahi kusema kuwa, “Kama wanasiasa wanatumia mabavu, kwa nini basi wasiwaanchie nafasi hiyo askari ambao kutumia mabavu ndio kazi waliyosomea?”
Hatari! Askari wameweza kusema, katika nchi mbalimbali, tena kwa jeuri ya uhakika: Kama siasa zimeshindwa, si basi ziwekwe chini; tutawale sisi kuliko kuwa na mseto wa siasa na silaha? Uuuuhwi! Mungu apishe mbali. Lakini ndiko CCM inataka kuelekeza.
Kwa CCM kutaka askari zaidi uwajani Tarime wakati wa uchaguzi mdogo wa kutafuta diwani na mbunge, ni kujitia kitanzi mbele ya wapiga kura.
Ni wilayani Tarime ambako kumekuwa na ugomvi kati na baina ya koo; tena kwa muda mrefu. Serikali imeshindwa au imekataa au imedharau kuingilia kati kwa busara na kishindo ili kumaliza migogoro.
Iweje basi, serikali iombwe kupeleka kishindo cha askari na silaha wakati wa uchaguzi? Je, si atakayetangazwa kuwa mshindi kupitia askari na silaha atakuwa amewekwa kwa mabavu, badala ya ridhaa ya wananchi kwa kauli za kisiasa tu?
Je, atakayeshindwa au hata akishinda, baada ya kutumia askari wa taifa, silaha za nchi, muda na fedha nyingi za umma; atafidia vipi gharama hizo, tena kwa riba gani? Lakini kabla ya hapo, nani anaruhusu matumizi hayo?
Ushauri mzuri ungekuwa, kwamba anayeona ameemewa, ajiondoe taratibu na kimyakimya. Wachezaji katika uwanja wa Tarime ni vyama vya siasa na wanasiasa. Chama ambacho kinaona siasa zake zimeyeyuka, kisiite askari. Kijiondoe.
Kutumia nguvu ya nyongeza ya askari katika uchaguzi kutadhoofisha siasa za utashi. Kutajenga woga miongoni mwa wananchi. Kutafanya baadhi ya wananchi kupoteza fursa ya kupiga kura.
Matumizi ya askari kujaribu kuleta ushindi kwa chama kilichoko madarakani, kuna uwezekano wa kuleta mbunge legelege; aliyechoka kabla ya kuanza kazi na ambaye amezibwa mdomo kabla ya uchaguzi kufanyika. Huyu siye wanayemtaka wananchi wa Tarime.
Kutafuta mbunge kwa kusaidiwa na askari, ni kukana kanuni za kidemokrasia; ni kufuta utawala wa kiraia hatua kwa hatua na kuasisi kinyemera utawala wa kiaskari.
Hii ni njia ya kuonjesha askari asali. Wakinogewa asali wafanyeje? Bila shaka watachonga mzinga. Huko ndiko wanatupeleka Pius Msekwa na Yusuf Makamba.
Mkoa wa Mara una historia ya upinzani tangu kurejea kwa mfumo wa vyama vingi nchini. Kwa Msekwa ambaye hana uzoefu wa kukurukakara za kutafuta kura katika mazingira ya mshikemshike, bila shaka ataogopa.
Woga wa Msekwa unatokana na ukweli kwamba CCM inaweza kushindwa vibaya pale wananchi wa Tarime watakapoamua kuiadhibu kwa kutumia vitisho; ikiwa ni pamoja na kauli kwamba wasipochagua CCM “hawatapata maendeleo.”
Hivi sasa Halmashauri ya Tarime inaongozwa na upinzani. Ina mipango kabakaba ikiwa ni pamoja na kuwalipia karo baadhi ya wanafunzi. Hili ni moja ya mambo ambayo mgombea wa Chadema, Charles Mwera Nyanguru, ambaye pia ni Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, anajivunia sana.
Kutishiwa kunyimwa “maendeleo” ambako CCM imeshikia bango, kunaweza kuwa kichocheo kikubwa cha wananchi wa Tarime kufanya maamuzi ya busara ambayo ni kuchagua Chadema au chama kingine na siyo chama tawala.
Vyovyote itakavyokuwa, askari hawahitajiki katika uwanja wa siasa jimboni Tarime.
(Makala hii imeandikwa kwa ajili ya gazeti la Tanzania Daima Jumapili, 28 September 2008. Mwandishi anapatikana kwa simu: 0713 614872; imeili: ndimara@yahoo.com)
Friday, September 26, 2008
Monday, September 22, 2008
CCM YAENEZA UJINGA TARIME
PIGA NIKUPIGE NYUMBANI KWA WANGWE
Na Ndimara Tegambwage
MSIMU wa ujinga umewadia. Ujinga huu unaimarishwa na vitisho kwa njia ya kauli na silaha. Ukitaka uthibitisho nenda Tarime, mkoani Mara ambako unafanyika uchaguzi mdogo wa diwani na mbunge.
Viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wakiongozwa na Katibu Mkuu Yusuf Makamba, tayari wamefungulia mabomba ya kauli na vitisho kwa shabaha ya kupata ushindi katika uchaguzi huu.
Wanawaambia wakazi wa Tarime kuwa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), ambacho ni mshindani mkuu, siyo chama bali “kampuni binafsi ya mtu mmoja.”
Wanataka wapiga kura wa Tarime waamini kuwa mbunge wao aliyefariki, Chacha Wangwe, alikuwa kwenye kampuni. Wanataka kupendekeza kuwa Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa, ama amehongwa au ana ubia katika kampuni hiyo kwa kuwa hajafuta Chadema kwenye orodha ya vyama.
Msimu wa ujinga huu hapa. Waziri Stephen Wasira anaripotiwa akisema, hukohuko Tarime kuwa Chadema ni chama cha mtu mmoja; anamtaja Edwin Mtei.
Huyu anataka kusema kwamba Msajili wa Vyama vya Siasa, ama alihongwa kukiandikisha chama cha mtu mmoja, kwani kinapingana na sheria ya vyama; au ana maslahi nacho ndiyo maana hajakifuta.
Makamu Mwenyekiti wa CCM, Pius Msekwa ananukuliwa akisema Chadema ni chama cha wafanyabiashara wawili. Wanatajwa Mtei na Philemon Ndesamburo.
Msekwa anataka wananchi waamini kuwa mara hii, katika uchaguzi wa Tarime, kila mmoja anaingia tu – mwenye chama, kampuni au duka. Kwa maana kwamba sheria ya uchaguzi haitumiki! Msimu wa ujinga.
Ni Msekwa anayenukuliwa akisema “vyama vingi” vilikuja ili kutoa haki kwa watu wachache (asilimia 20) wakati wengi (asilimia 80) hawakutaka mfumo wa vyama vingi. Hapa anazungumzia Tume ya Nyalali juu ya vyama vingi.
Elimu ya Msekwa na uzoefu ndani ya chama kimoja havimuongozi kuelewa kuwa hodhi ya kisiasa ingeendelea, nchi ingeshindikana kutawalika.
Bali hatushangai. Ni Msekwa aliyetunga kitabu cha kushindilia ukiritimba wa kisiasa kiitwacho “Chama kushika hatamu.”
Haoni kuwa hata hadidu za rejea za Tume ya Nyalali zilikuwa na kasoro kubwa. Kuuliza wananchi kama wanataka chama kimoja au vingi ulikuwa msiba wa kihistoria; hata kama mkuu wa tume alikuwa jaji mkuu.
Tayari wananchi waliishaporwa haki ya kuunda vyama na asasi zao huru. Iweje wananchi waulizwe iwapo wanataka haki yao badala ya mwizi kujisalimisha kwao, akilamba mchanga na kuomba msamaha? Kilichohitajika ni kurejesha mfumo wa vyama bila kupoteza fedha za wananchi na kutubu.
Ni Wassira pia anayenukuliwa akisema Chacha Wangwe, aliyekuwa mbunge wa Tarime (sasa marehemu), alichaguliwa kwa kura nyingi, lakini chama chake cha Chadema hakikuteua mbunge wa viti maalum kutoka Tarime.
Huyu anataka wananchi waamini kuwa kila jimbo ambako CCM inapata mbunge kwa kura nyingi, inateua pia mbunge wa viti maalum. Huu siyo tu uwongo, bali pia uzushi mpevu.
Na huyo Peter Keba, ndugu yake Wangwe, anasema ndugu yake “aliuawa kutokana na kudai kujua matumizi ya ruzuku” ya chama chake.
Naye huyu anataka wananchi, wakazi wa Tarime, waamini kuwa mtu yeyote atakayetaka kujua matumizi ya ruzuku ya Chadema, atauawa au hata Msajili wa Vyama akitaka kujua matumizi ya chama hicho, naye atauawa.
Huo ndio uwanja wa ujinga. Si hayo tu. Viongozi na wapiga chapuo wa CCM wanadai kuwa vyama vya upinzani havina fedha za kuleta maendeleo; kwa hiyo kama wananchi wanataka maendeleo sharti wachague mgombea wa CCM.
Mbegu ya ujinga iko mikononi mwa Katibu Mkuu wa CCM, ambaye tayari amejipa jina la “Yohana Mbatizaji” ambaye anatengeneza “njia ya bwana” – Makamu Mwenyekiti, Pius Msekwa!
Yote haya ni kutafuta kiti cha ubunge na kiti cha udiwani katika jimbo la Tarime. Kila uwongo utasemwa; wakiwapakia wananchi kila sura ya kishawishi ili wapate “ushindi.”
Katika hali ya kawaida, kwa umri na huenda ukomavu uendao na uzoefu, CCM ingekuwa na hoja za maana na kuwa mfano kwa vyama vingine.
Haya yote yanayomwagwa usoni na vichwani mwa wananchi yanatokana na uelewa na imani, kwamba wananchi hawajui; hivyo wataamini tu chochote kile wanachoambiwa na hatimaye kuchagua CCM.
Uwongo na ujinga vinafinyangwa na kusokomezwa katika akili ya wananchi wenye kiu ya kujua. Kumbe ndio wananchi wanapotoshwa. Wanapigwa kafuti ya ujinga na ghiliba ili watawala waweze kuondoka na kiti cha ubunge na kile cha udiwani.
Wakati kuna kilio cha kutoa na kusambaza elimu muwafaka, watawala wanasambaza uwongo, uzushi na ujinga usiomithilika kwa madai ya kutafuta ushindi. Huu ni msiba.
Hakika, wanaoishi kwa tamaa ya kutawala kwa kutumia ujinga wa wananchi, hawawezi kuondoa ujinga. Kwao, ujinga ni mtaji wa kuchukulia madaraka. Ni silaha ya kuulia wapinzani na daraja la kuwapeleka kwenye utukufu wa kisiasa.
Kwa watawala wa aina hii, shule ni adui mkubwa. Elimu ya watu wazima ni kinyamkera ndani ya nyumba. Mijadala ya kutaka kushiriki katika uongozi wa nchi ni adui mtukutu.
Kwa umri huu, CCM wasingekuwa bado wanatamani ujinga. Wasingekuwa wanapenda umma ulioganda kwa propaganda na vitisho. Wasingekuwa wanataka kondoo au umma uliopigwa kafuti za uwongo, uliotishwa kwa silaha au unaogeuzwageuzwa mithili ya chapati.
Chama kikubwa, chenye uzoefu, sharti kiingie uwanjani kwa hoja ili kiwe mfano. Kisipofanya hivyo, basi kisubiri hatma: Nyumba iliyojengwa kwa uwongo, ujinga na vitisho, ni tofali la barafu. Itayeyuka.
(Makala hii imechapishwa katika gazeti la MwanaHALISI, toleo la Jumatano,24 Septemba 2008. Mwandishi anapatikana kwa simu: 0713 614872; imeili: ndimara@yahoo.com)
Saturday, September 20, 2008
SERIKALI ITABEBA TRL MPAKA LINI?
Mbeleko ya serikali TRL
Na Ndimara Tegambwage
SITAKI wananchi washindwe kujenga mashaka juu ya uhusiano wa serikali na waendeshaji wa Kampuni ya Reli Tanzania (TRL).
Machi mwaka huu waendeshaji, wawekezaji, wabia au “marafiki” wa serikali walishindwa kulipa kima cha chini cha mshahara kama walivyokuwa wamekubaliana na wafanyakazi – kutoka Sh. 80,000 hadi Sh. 160,000 kwa mwezi.
Ilikuwa baada ya vuta nikuvute, mgomo wa wafanyakazi uliokuwa umepangwa kufanyika mwezi huo ukasitishwa. Serikali iliingilia kati, kuwakingia kifua waendeshaji, wawekezaji, wabia au marafiki zao katika kampuni ya RITES kutoka India.
Kwa serikali kukingia kifua mtu wa nje dhidi ya wananchi wapatao 3,200 siyo kazi ndogo. Ni gharama kubwa iliyosababisha serikali kupokonya kodi ya wananchi kiasi cha Sh. 3.6 bilioni ili kulipa wafanyakazi. Ili kuzuia wasigome. Ili kuokoa menejimenti ya TRL.
Tangu Machi serikali imelipa kima cha chini TRL cha Sh. 160,000 kwa mwezi kwa ahadi kuwa ifikapo Agosti, menejimenti ya TRL itaanza kulipa Sh. 200,000 kwa mwezi kama ilivyoahidi. Imeshindwa. Kwa mara nyingine serikali imeingilia kulipa malimbikizo na mishahara kwa wafanyakazi wa TRL.
Kuna nini kati ya serikali na TRL? Kuna udugu gani kati ya serikali na kampuni inayoendesha menejimenti ya kampuni ya reli? Kuna uhusiano gani kati ya maofisa serikalini na maofisa wa kampuni ya RITES kutoka India?
Je, serikali iliyoibeba menejimenti ya TRL mapema mwaka huu kwa kodi za wananchi, inajua kinachoendelea ndani ya TRL? Inajua udhaifu wa menejimenti hiyo au inaendelea kuifungia dripu ya mabilioni ya shilingi huku kirusi kikiendelea kuitafuna mfupa?
Kama serikali ilitaka kujivua biashara ya usafirishaji kwa njia ya reli, inatafuta nini katika kubeba menejimenti dhaifu isiyoweza hata kulipa mishahara ya wafanyakazi?
Serikali inalipa mishahara TRL ili baadaye ipate nini? Au inalinda maslahi ya nani au inataka kumlinda nani asiumbuke kutokana na uamuzi iliochukua au mahusiano kati ya serikali, maofisa serikalini na kampuni ya RITES?
Maswali haya yanaulizwa kwa kuwa haiwezekani kuwa “bure tu.” Waziri Mkuu Mizengo Pinda aliwahi kusema Machi mwaka huu kuwa pande zote mbili – serikali na RITES hawakuwa wawazi wakati wa kutoa taarifa za kuandaa mkataba.
Ilinong’onwa kuwa kila upande haukueleza uwezo wake halisi, jambo ambalo linasababisha hata kushindwa kulipa mishahara. Kama hivyo ndivyo, kwa nini mkataba usivunjwe kwa vile umejengwa kwenye ulaghai?
Je, kutoweka wazi taarifa sahihi wakati wa kuandaa mkataba kulifanywa kwa makusudi? Ili iweje? Ili nani anufaike? Ilikuwa kwa makusudi au kupitiwa? Kama kupitiwa, kwanini serikali haijachukua hatua inayostahili?
Je, maofisa wa serikali waliosema uwongo au waliotoa taarifa zisizo za kweli, wamechukuliwa hatua gani? Kama kuna kasoro ya kutokuwepo taarifa sahihi, kwa nini serikali inaendelea kuneemesha mkataba wenye malengo tofauti?
Hapa kuna madai kwamba serikali inawakopesha na kwamba watarudisha fedha hizo. Kama ni kukopesha, kwa nini serikali haikukopesha wananchi ili waendeshe kampuni yao?
Kuna suala la kulipa wafanyakazi – wananchi – wasipate adha wakati serikali yao ipo. Lakini serikali inalipa mishahara ili mapato ya RITES yafanyiwe kazi gani?
Nani anajua RITES wanapata kiasi gani kwa saa, kwa mwezi na kipindi chote hicho tangu waingie mkataba na waanze kazi? Wao wanamlipa nani kama siyo mfanyakazi?
Inaonekana RITES walikuja na baadhi ya wafanyakazi wao, hata madereva wa treni. Kuna ushahidi wa kutosha kuwa wako wafanyakazi kutoka nje ya nchi.
Je, hata hawa wanalipwa kutoka kodi ya wananchi wakati wa kuepusha migomo? Serikali inafanya hayo ili iweje na kwa manufaa ya nani? Tulizo hilo linalofanywa na serikali kuipa afueni menejimenti na TRL, linalenga kumkinga nani hasa?
Hivi haiwezi kuwa kweli kwamba menejimenti ya TRL inafanya jeuri kwa makusudi kwa kuwa ina siri na baadhi ya viongozi serikalini? Kwamba wako pamoja na serikali haiwezi kufanya lolote? Kwamba serikali ikiwa kaidi basi watalipua bomu?
Kuna mambo mengi TRL ambayo yanastahili kujengewa mashaka. Mkataba wa menejimenti ya kampuni hiyo na uhusiano wa menejimenti na uongozi serikalini, ni moja ya mambo makuu ya kuchunguzwa (hili tutalijadili katika makala ifuatayo).
Kuna jinsi wafanyakazi wanavyoendeshwa, kama wao wanavyodai, “kama gari bovu.” Mfanyanyazi – fundi wa TRL wa miaka nendarudi, anawekwa benchi kwa miezi kadhaa kwa kuambiwa hajui kazi. Lini aliacha kujua kazi yake na kipi kilimsibu?
Kuna dereva wa treni anayechengwa na menejimenti kuwa hajui kazi yake wakati vichwa vyote vimezeekea mikononi mwake. Ujuzi wake umefyonzwa na nini?
Kwa ujumla kuna malalamiko kuwa menejimenti ya TRL inawaweka kando wafanyakazi wake wa siku nyingi na wenye ujuzi; badala yake inaingiza wafanyakazi kutoka nje ya nchi.
Kuna madai ya usafirishaji wa vichwa vya treni kwenda India. Kuna yanayohusu kuwepo vichwa visivyofanya kazi lakini vinalipiwa mamilioni ya shilingi kila mwezi.
Kuna mengine yanayohusu ugeuzaji vichwa vya zamani vya nchini kuwa spea kwa vichwa vinavyotoka India ambavyo inadaiwa ni vibovu.
Katikati ya madai haya, serikali inaendelea kulipa mishahara, kuipakata na kuibeba kwenye mbeleko menejimenti ya TRL. Serikali ina nini TRL na RITES? Hapa ndipo tunaanzia kujenga mashaka.
Bali kwa wafanyakazi, wembe uleule – kudai ujira unaolingana na kazi inayofanywa na kugoma kufanya kazi pindi nguvu na akili zao vinapodhalilishwa kwa ujira duni na nje ya mapatano na mwajiri.
(Makala hii itachapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili 21 Septemba 2008. Mwandishi wake anapatikana kwa simu: 0713-614872 na ndimara@yahoo.com)
Na Ndimara Tegambwage
SITAKI wananchi washindwe kujenga mashaka juu ya uhusiano wa serikali na waendeshaji wa Kampuni ya Reli Tanzania (TRL).
Machi mwaka huu waendeshaji, wawekezaji, wabia au “marafiki” wa serikali walishindwa kulipa kima cha chini cha mshahara kama walivyokuwa wamekubaliana na wafanyakazi – kutoka Sh. 80,000 hadi Sh. 160,000 kwa mwezi.
Ilikuwa baada ya vuta nikuvute, mgomo wa wafanyakazi uliokuwa umepangwa kufanyika mwezi huo ukasitishwa. Serikali iliingilia kati, kuwakingia kifua waendeshaji, wawekezaji, wabia au marafiki zao katika kampuni ya RITES kutoka India.
Kwa serikali kukingia kifua mtu wa nje dhidi ya wananchi wapatao 3,200 siyo kazi ndogo. Ni gharama kubwa iliyosababisha serikali kupokonya kodi ya wananchi kiasi cha Sh. 3.6 bilioni ili kulipa wafanyakazi. Ili kuzuia wasigome. Ili kuokoa menejimenti ya TRL.
Tangu Machi serikali imelipa kima cha chini TRL cha Sh. 160,000 kwa mwezi kwa ahadi kuwa ifikapo Agosti, menejimenti ya TRL itaanza kulipa Sh. 200,000 kwa mwezi kama ilivyoahidi. Imeshindwa. Kwa mara nyingine serikali imeingilia kulipa malimbikizo na mishahara kwa wafanyakazi wa TRL.
Kuna nini kati ya serikali na TRL? Kuna udugu gani kati ya serikali na kampuni inayoendesha menejimenti ya kampuni ya reli? Kuna uhusiano gani kati ya maofisa serikalini na maofisa wa kampuni ya RITES kutoka India?
Je, serikali iliyoibeba menejimenti ya TRL mapema mwaka huu kwa kodi za wananchi, inajua kinachoendelea ndani ya TRL? Inajua udhaifu wa menejimenti hiyo au inaendelea kuifungia dripu ya mabilioni ya shilingi huku kirusi kikiendelea kuitafuna mfupa?
Kama serikali ilitaka kujivua biashara ya usafirishaji kwa njia ya reli, inatafuta nini katika kubeba menejimenti dhaifu isiyoweza hata kulipa mishahara ya wafanyakazi?
Serikali inalipa mishahara TRL ili baadaye ipate nini? Au inalinda maslahi ya nani au inataka kumlinda nani asiumbuke kutokana na uamuzi iliochukua au mahusiano kati ya serikali, maofisa serikalini na kampuni ya RITES?
Maswali haya yanaulizwa kwa kuwa haiwezekani kuwa “bure tu.” Waziri Mkuu Mizengo Pinda aliwahi kusema Machi mwaka huu kuwa pande zote mbili – serikali na RITES hawakuwa wawazi wakati wa kutoa taarifa za kuandaa mkataba.
Ilinong’onwa kuwa kila upande haukueleza uwezo wake halisi, jambo ambalo linasababisha hata kushindwa kulipa mishahara. Kama hivyo ndivyo, kwa nini mkataba usivunjwe kwa vile umejengwa kwenye ulaghai?
Je, kutoweka wazi taarifa sahihi wakati wa kuandaa mkataba kulifanywa kwa makusudi? Ili iweje? Ili nani anufaike? Ilikuwa kwa makusudi au kupitiwa? Kama kupitiwa, kwanini serikali haijachukua hatua inayostahili?
Je, maofisa wa serikali waliosema uwongo au waliotoa taarifa zisizo za kweli, wamechukuliwa hatua gani? Kama kuna kasoro ya kutokuwepo taarifa sahihi, kwa nini serikali inaendelea kuneemesha mkataba wenye malengo tofauti?
Hapa kuna madai kwamba serikali inawakopesha na kwamba watarudisha fedha hizo. Kama ni kukopesha, kwa nini serikali haikukopesha wananchi ili waendeshe kampuni yao?
Kuna suala la kulipa wafanyakazi – wananchi – wasipate adha wakati serikali yao ipo. Lakini serikali inalipa mishahara ili mapato ya RITES yafanyiwe kazi gani?
Nani anajua RITES wanapata kiasi gani kwa saa, kwa mwezi na kipindi chote hicho tangu waingie mkataba na waanze kazi? Wao wanamlipa nani kama siyo mfanyakazi?
Inaonekana RITES walikuja na baadhi ya wafanyakazi wao, hata madereva wa treni. Kuna ushahidi wa kutosha kuwa wako wafanyakazi kutoka nje ya nchi.
Je, hata hawa wanalipwa kutoka kodi ya wananchi wakati wa kuepusha migomo? Serikali inafanya hayo ili iweje na kwa manufaa ya nani? Tulizo hilo linalofanywa na serikali kuipa afueni menejimenti na TRL, linalenga kumkinga nani hasa?
Hivi haiwezi kuwa kweli kwamba menejimenti ya TRL inafanya jeuri kwa makusudi kwa kuwa ina siri na baadhi ya viongozi serikalini? Kwamba wako pamoja na serikali haiwezi kufanya lolote? Kwamba serikali ikiwa kaidi basi watalipua bomu?
Kuna mambo mengi TRL ambayo yanastahili kujengewa mashaka. Mkataba wa menejimenti ya kampuni hiyo na uhusiano wa menejimenti na uongozi serikalini, ni moja ya mambo makuu ya kuchunguzwa (hili tutalijadili katika makala ifuatayo).
Kuna jinsi wafanyakazi wanavyoendeshwa, kama wao wanavyodai, “kama gari bovu.” Mfanyanyazi – fundi wa TRL wa miaka nendarudi, anawekwa benchi kwa miezi kadhaa kwa kuambiwa hajui kazi. Lini aliacha kujua kazi yake na kipi kilimsibu?
Kuna dereva wa treni anayechengwa na menejimenti kuwa hajui kazi yake wakati vichwa vyote vimezeekea mikononi mwake. Ujuzi wake umefyonzwa na nini?
Kwa ujumla kuna malalamiko kuwa menejimenti ya TRL inawaweka kando wafanyakazi wake wa siku nyingi na wenye ujuzi; badala yake inaingiza wafanyakazi kutoka nje ya nchi.
Kuna madai ya usafirishaji wa vichwa vya treni kwenda India. Kuna yanayohusu kuwepo vichwa visivyofanya kazi lakini vinalipiwa mamilioni ya shilingi kila mwezi.
Kuna mengine yanayohusu ugeuzaji vichwa vya zamani vya nchini kuwa spea kwa vichwa vinavyotoka India ambavyo inadaiwa ni vibovu.
Katikati ya madai haya, serikali inaendelea kulipa mishahara, kuipakata na kuibeba kwenye mbeleko menejimenti ya TRL. Serikali ina nini TRL na RITES? Hapa ndipo tunaanzia kujenga mashaka.
Bali kwa wafanyakazi, wembe uleule – kudai ujira unaolingana na kazi inayofanywa na kugoma kufanya kazi pindi nguvu na akili zao vinapodhalilishwa kwa ujira duni na nje ya mapatano na mwajiri.
(Makala hii itachapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili 21 Septemba 2008. Mwandishi wake anapatikana kwa simu: 0713-614872 na ndimara@yahoo.com)
Saturday, September 13, 2008
VITISHO KWA UHURU WA HABARI

Chenge anavyotishia waandishi
Na Ndimara Tegambwage
SITAKI mwanasiasa Andrew Chenge achoke kusemwa. Sitaki achoke kuandikwa. Hii ni kwa sababu, asipoandikwa atakufa kisiasa.
Kijijini kwa Chenge kuna watu wengi wa umri wake. Wanafahamika kwake na wanakijiji wenzake. Hawajaandikwa na huenda muda utafika watatoweka bila kuandikwa.
Vivyo hivyo kwa wananchi wengine wengi katika makabila na koo zao; katika nyadhifa mbalimbali; katika biashara na uchuuzi; na katika mahusiano ainaaina.
Chenge anaandikwa; lakini siyo kwa kuwa ni Chenge. Hapana. Ni kwa kuwa ni Mbunge. Kwa kuwa alikuwa Waziri wa Miundombinu. Kwa kuwa ni mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambacho kimepanga ikulu.
Chenge anaandikwa kwa kuwa ni mjumbe wa Kamati ya Madili ya CCM; alikuwa mserikali muhimu wakati akiwa Mwanasheria Mkuu. Lakini zaidi ya yote, Chenge anaandikwa kwa kuwa ni mwanasiasa.
Kuandikwa ni matokeo ya kuwa na nafasi maalum katika jamii. Mara hii, Chenge amepata nafasi maalum kwa kuwa yote yaliyotajwa hapo juu na hasa kwa kuwa mwanasiasa – kazi ambayo inamuhusisha moja kwa moja na maslahi ya nchi na watu wake.
Mjadala uliopo sasa ni juu ya Chenge kuwa mjumbe katika kamati ya CCM ya “kupitia upya” mkataba wa Umoja wa Vijana wa CCM na mwekezaji katika kuendeleza kitegauchumi cha umoja huo.
Mkataba huo ambao sasa inafahamika kuwa ulishughulikiwa na watu binafsi, na siyo vikao husika, na hivyo kuwepo harufu ya ufisadi, “unaangaliwa” na timu ya viongozi watatu akiwemo Chenge.
Kinachofanywa na vyombo vya habari hivi sasa ni kunukuu na kuchapisha maoni ya wananchi juu ya Chenge kuwa katika kamati ya CCM wakati yeye ni mtuhumiwa katika kashfa ya rada; kashfa iliyosababisha ajiuzulu uwaziri.
Utaona basi, kwamba kushika nafasi ya utumishi wa ngazi alizopitia Chenge, ni kukaa uchi mbele ya kamera na kalamu za waandishi; na kupitia kwa waandishi, ni kukaa utupu mbele ya umma uliomtuma kazi.
Hili ndilo somo kuu juu ya sababu za kuandika wanasiasa – kuanzia yule wa kijijini hadi mpangaji mkuu wa ikulu. Anayelalamika kwa kuandikwa, ama hajui nafasi yake katika jamii au anataka kuendeshea gizani shughuli za umma.
Vyombo vya habari haviundi habari. Habari inakuwepo au vinaichokonoa na vinaiandika, kuichapisha au kuitangaza. Chombo cha habari kinachobuni habari kinajitia kitanzi.
Chombo cha habari kikijiua kinakuwa kimewanyang’anya wasomaji, wasikilizaji au watazamaji wake, nafasi adimu ya kupata taarifa na habari za kuwasaidia kufurahia na kukamilisha uhuru wao wa maoni.
Na taarifa ambazo wananchi wanataka ni juu ya wanavyotawaliwa: haki zao, misingi na taratibu. Ni juu ya tabia na mwenendo wa wanaowatawala wakiwa katika ofisi za umma.
Wananchi wanataka, na vyombo vya habari vinawajibika kuwapa, taarifa juu ya mipango, uadilifu wa serikali, utawala wa sheria au utawala wa mwituni; umakini, uwazi, weledi au upendeleo, ukabila au ufisadi.
Katika kuripoti na kujadili, vyombo vya habari vinagusa wanasiasa na watawala kwa ujumla, siyo kwa majina yao, bali kwa nafasi zao katika kuvunja kiu ya wananchi ya kujua. Hapa, jina kama Chenge ni utambulisho tu wa mwajiriwa wa umma.
Kauli iliyoripotiwa kutolewa wiki iliyopita na utambulisho unaoitwa Chenge, kwamba waandishi wa habari wanamwandika sana na hawamweshimu; na kwamba atawafunza adabu, ni ya kusikitisha.
Kwa mujibu wa ufafanuzi juu ya kwa nini wanasiasa na viongozi wengine waandikwe, iwapo Chenge hataki kuchokonolewa na kuandikwa, sharti aachie ofisi zote za umma zinazomweka wazi kwa kila raia kumjadili na kumtathmini.
Vilevile akitaka kutoandikwa, basi asiingie katika biashara kubwa au ndogo. Kwani, wakati biashara kubwa inahusu maslahi ya nchi na umma kwa msingi wa mapato na kodi, biashara ndogo, hata ya kuuza vocha za simu, inamrejesha kwenye ulingo kuwa ameporomoka zaidi.
Hapa ataandikwa tu. Njia pekee ya kuandikwa na usiyumbe, usikasirike na kughadhabika, ni kutenda kazi yako bila uficho; kutenda haki na kuwa mwadilifu. Ukiwa hivyo na ukaandikwa, utachekelea maisha yako yote.
Kutishia “kufunza adabu” waandishi wa habari, ni kwenda mbali. Ni kukata tamaa. Ni kuloloma kusikoweza kuitikiwa kwa huruma. Ni kutishia kunyamazisha waandishi wa habari.
Aidha, vitisho hivyo vinaashiria kuvunja haki ya msingi ya binadamu – uhuru wa maoni; lakini pia vinaashiria kuvunja Katiba ya Jamhuri ya Muungano inayolinda uhuru wa kutafuta na kutawanya habari.
Kama kweli Chenge amesema aliyoripotiwa kusema, basi anashauriwa bure kufanya yafuatayo: Asifute usemi bali asitende alichokusudia kutenda. Hakina tija.
(Makala hii itachapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili 14 Septemba 2008. Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa simu: 0713-614872; imeili: ndimara@yahoo.com)
Wednesday, September 10, 2008
WAKO WAPI WALIO WAKALI SANA?
VIJANA WA TANZANIA WASIOKUA
Na Ndimara Tegambwage
WAKO wapi walio wakali sana, sisi twawataka…Huu ni wimbo. Tuliuimba tukiwa madarasa ya awali. Wakati unaimba, unapiga chini, tena kwa kishindo, mguu wako wa kulia na kuonyesha uso wa ukakamavu.
Ni enzi za ujana. Katika ubichi wa umri na kujituma; na kutumwa na wazazi. Acha siasa ziingie. Wanasiasa wa umri mkubwa wakaanza kutuma vijana.
Fanya hili, fanya lile. Ninyi ni taifa la kesho. Leo ni taifa letu – sisi kwa sisi. Na vijana wakakubali. Mgongoni wakapandwa mithili ya farasi; na vikongwe kuwavusha.
Lakini vijana hawa hawakui. Akibahatika mmoja akaona mwezi, anaudaka uwaziri au unaibu waziri. Mwingine anakuwa katibu ndani ya chama; lakini sharti wakubali kuendelea kunyonya na kuwekewa kiporo mafigani.
Vijana wakitaka kula sharti waombe ruksa. Sharti waombe ruksa kwenda matembezi. Sharti waombe ruksa kuimba nyimbo za vijana; na sharti wacheze ngoma za kale; za leo zina maasi.
Chini, ardhi haipenyeki. Ardhi imegandana. Juu, wamekaa vigogo kwa maana halisi ya vigogo. Vizito kwa umri. Kwa madaraka. Vizito kwa mamlaka. Kwa kauli nzito na kali. Kwa kutotaka kubishiwa au kujadiliwa hadharani. Vigogo.
Wako wapi walio wakali sana wa kuvunja ardhi; kutokomea na kutokezea kwingine? Kama hilo ni aghali, wako wapi basi walio wakali sana wa kupasua ufa katikati ya vigogo?
Wale wa kulenga na kunasa. Wale wa kutamani kupenyeza sauti na utashi wa vijana kwenye mwamba wa vigogo na ardhi ya ugumu wa kigumu.
Wako wapi walio wakali sana wa kujadili hoja kuu za vijana wanaokua; na siyo waliolemaa na wanaolamba nyonyo hata katika umri mkubwa?
Wako wapi wanaoona mbali na wasioteta? Wale wenye damu moto ya ujasiri wa kweli. Wako wapi waliojaa hekima lakini wakali kwa mali ya vijana na umma, pale inapogugunwa na fungo? Wako wapi?
Wako wapi wenye uwezo wa kuwaambia wale waliowakalia vichwani: Asante kwa malezi, lakini kwa hili baba, tuheshimiane? Wale waliotayari kuweka mitima yao wazi kwa kila mmoja kuona.
Wako wapi walio wakali sana wa kuona mbali; wale wa kukiri kukua na kukomaa na wasiotaka nyonyo tena? Wako wapi wenye bisibisi, tindo na sululu za kuvunja mwamba uliowakandamiza?
Wako wapi walio wakali sana – wasio na mapenzi ya minong’ono na kuumana sikio? Wale wasioteta bali wanaoweka wazi hoja zao; hoja za vijana na wa makamo; hoja za taifa na nchi. Wako wapi wasiojimung’unya kwa aibu na unafiki?
Wako wapi wa kuwaambia vikongwe kwamba sasa watulie wahudumiwe? Kwamba ni kweli, wamewatoa mbali, lakini leo hii wakubali kuwa wamechoka na wanahitaji kusaidiwa.
Wako wapi walio wakali sana; wale wa kuwaambia vigogo: Ahsante kwa malezi lakini kuendelea kuwa “kamanda wa dogodogo,” tena kwa umri huu, ni kejeli kama siyo matusi?
Wako wapi wa kuhoji ukamanda wa vijana kushikwa na vikongwe? Wale wa kuhoji utitiri wa nondo umwagwao vichwani mwa vijana kwa madai ya kuadabisha, kutiisha na kunidhamisha?
Wako wapi walio wakali sana – wa kuweza kunyoosha kidole na kusema, baba hapa umekosea? Kwamba baba hapa uko uchi? Wasionyenyekea ukali wa sauti bali hoja mwanana yenye tija kwao na kwa taifa?
Asije mtu na kusema hawapo. Asitokee wa kuamini kuwa wote bado ni vifaranga. Asiwepo wa kuamini kuwa vijana ni watoto wasiokua; wasioweza kufikiri na kutenda.
Nani anataka kuwa mtoto ukubwani? Isije kuwa hadithi ya Kabuyanga. Alinyonya. Miaka miwili. Akanyonya. Miaka minne. Akanyonya. Miaka mitano.
Kabuyanga akawa anamwambia mama yake: Mama ee, naona umevaa vizuri na unataka kuondoka. Naomba urudi mapema mama; nataka kunyonya!
Umri mkubwa. Nyonyo mdomoni. Mama analiendekeza lakini pia analinyima haki na uhuru wa kufikiri na hivyo linashindwa kujitegemea.
Kumbe ni mabavu ya Kabuyanga tangu udogo. Waliona mwili wake ule ungewaletea kasheshe kama angepewa mbawa. Akabakizwa kwenye mapakato ya mama. Akanyonya na kulewa maziwa. Akalelemaa.
Bali huyo ni mmoja. Ni mmoja peke yake. Hukaa na walomlemaza na kuteta vijana wenye nguvu, ukakamavu na nia ya kupasua ardhi na mbingu ya vigogo vikongwe.
Fumbua macho. Inua kichwa. Angalia juu na usiogope. Ni utando wa mwamba tikitiki. Kwa haraka, mwamba hauvunjiki. Haupasuki.
Bali kwa walio makini, ni ukungu mtupu. Panahitajika ujasiri mdogo kupenya hasira, chuki na gadhabu za baba na mama Kabuyanga.
Wako wapi walio wakali sana – wenye uwezo wa kuhimili vishindo vya matusi, kebehi na kejeli; ukali wa macho mekundu na mibubujiko ya midomo na mashavu yanayoanguka mithili ya embe la vuli?
Wako wapi walio wakali sana wa kuandaa mahusiano mapya na kukata mikatale iwawekao vijana utumwani? Wako wapi wa kuzima migegemo ya Kabuyanga ya kuendelea kuuma nyonyo ukubwani?
(Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa simu: 0713-614872 na imeili: ndimara@yahoo.com)
Na Ndimara Tegambwage
WAKO wapi walio wakali sana, sisi twawataka…Huu ni wimbo. Tuliuimba tukiwa madarasa ya awali. Wakati unaimba, unapiga chini, tena kwa kishindo, mguu wako wa kulia na kuonyesha uso wa ukakamavu.
Ni enzi za ujana. Katika ubichi wa umri na kujituma; na kutumwa na wazazi. Acha siasa ziingie. Wanasiasa wa umri mkubwa wakaanza kutuma vijana.
Fanya hili, fanya lile. Ninyi ni taifa la kesho. Leo ni taifa letu – sisi kwa sisi. Na vijana wakakubali. Mgongoni wakapandwa mithili ya farasi; na vikongwe kuwavusha.
Lakini vijana hawa hawakui. Akibahatika mmoja akaona mwezi, anaudaka uwaziri au unaibu waziri. Mwingine anakuwa katibu ndani ya chama; lakini sharti wakubali kuendelea kunyonya na kuwekewa kiporo mafigani.
Vijana wakitaka kula sharti waombe ruksa. Sharti waombe ruksa kwenda matembezi. Sharti waombe ruksa kuimba nyimbo za vijana; na sharti wacheze ngoma za kale; za leo zina maasi.
Chini, ardhi haipenyeki. Ardhi imegandana. Juu, wamekaa vigogo kwa maana halisi ya vigogo. Vizito kwa umri. Kwa madaraka. Vizito kwa mamlaka. Kwa kauli nzito na kali. Kwa kutotaka kubishiwa au kujadiliwa hadharani. Vigogo.
Wako wapi walio wakali sana wa kuvunja ardhi; kutokomea na kutokezea kwingine? Kama hilo ni aghali, wako wapi basi walio wakali sana wa kupasua ufa katikati ya vigogo?
Wale wa kulenga na kunasa. Wale wa kutamani kupenyeza sauti na utashi wa vijana kwenye mwamba wa vigogo na ardhi ya ugumu wa kigumu.
Wako wapi walio wakali sana wa kujadili hoja kuu za vijana wanaokua; na siyo waliolemaa na wanaolamba nyonyo hata katika umri mkubwa?
Wako wapi wanaoona mbali na wasioteta? Wale wenye damu moto ya ujasiri wa kweli. Wako wapi waliojaa hekima lakini wakali kwa mali ya vijana na umma, pale inapogugunwa na fungo? Wako wapi?
Wako wapi wenye uwezo wa kuwaambia wale waliowakalia vichwani: Asante kwa malezi, lakini kwa hili baba, tuheshimiane? Wale waliotayari kuweka mitima yao wazi kwa kila mmoja kuona.
Wako wapi walio wakali sana wa kuona mbali; wale wa kukiri kukua na kukomaa na wasiotaka nyonyo tena? Wako wapi wenye bisibisi, tindo na sululu za kuvunja mwamba uliowakandamiza?
Wako wapi walio wakali sana – wasio na mapenzi ya minong’ono na kuumana sikio? Wale wasioteta bali wanaoweka wazi hoja zao; hoja za vijana na wa makamo; hoja za taifa na nchi. Wako wapi wasiojimung’unya kwa aibu na unafiki?
Wako wapi wa kuwaambia vikongwe kwamba sasa watulie wahudumiwe? Kwamba ni kweli, wamewatoa mbali, lakini leo hii wakubali kuwa wamechoka na wanahitaji kusaidiwa.
Wako wapi walio wakali sana; wale wa kuwaambia vigogo: Ahsante kwa malezi lakini kuendelea kuwa “kamanda wa dogodogo,” tena kwa umri huu, ni kejeli kama siyo matusi?
Wako wapi wa kuhoji ukamanda wa vijana kushikwa na vikongwe? Wale wa kuhoji utitiri wa nondo umwagwao vichwani mwa vijana kwa madai ya kuadabisha, kutiisha na kunidhamisha?
Wako wapi walio wakali sana – wa kuweza kunyoosha kidole na kusema, baba hapa umekosea? Kwamba baba hapa uko uchi? Wasionyenyekea ukali wa sauti bali hoja mwanana yenye tija kwao na kwa taifa?
Asije mtu na kusema hawapo. Asitokee wa kuamini kuwa wote bado ni vifaranga. Asiwepo wa kuamini kuwa vijana ni watoto wasiokua; wasioweza kufikiri na kutenda.
Nani anataka kuwa mtoto ukubwani? Isije kuwa hadithi ya Kabuyanga. Alinyonya. Miaka miwili. Akanyonya. Miaka minne. Akanyonya. Miaka mitano.
Kabuyanga akawa anamwambia mama yake: Mama ee, naona umevaa vizuri na unataka kuondoka. Naomba urudi mapema mama; nataka kunyonya!
Umri mkubwa. Nyonyo mdomoni. Mama analiendekeza lakini pia analinyima haki na uhuru wa kufikiri na hivyo linashindwa kujitegemea.
Kumbe ni mabavu ya Kabuyanga tangu udogo. Waliona mwili wake ule ungewaletea kasheshe kama angepewa mbawa. Akabakizwa kwenye mapakato ya mama. Akanyonya na kulewa maziwa. Akalelemaa.
Bali huyo ni mmoja. Ni mmoja peke yake. Hukaa na walomlemaza na kuteta vijana wenye nguvu, ukakamavu na nia ya kupasua ardhi na mbingu ya vigogo vikongwe.
Fumbua macho. Inua kichwa. Angalia juu na usiogope. Ni utando wa mwamba tikitiki. Kwa haraka, mwamba hauvunjiki. Haupasuki.
Bali kwa walio makini, ni ukungu mtupu. Panahitajika ujasiri mdogo kupenya hasira, chuki na gadhabu za baba na mama Kabuyanga.
Wako wapi walio wakali sana – wenye uwezo wa kuhimili vishindo vya matusi, kebehi na kejeli; ukali wa macho mekundu na mibubujiko ya midomo na mashavu yanayoanguka mithili ya embe la vuli?
Wako wapi walio wakali sana wa kuandaa mahusiano mapya na kukata mikatale iwawekao vijana utumwani? Wako wapi wa kuzima migegemo ya Kabuyanga ya kuendelea kuuma nyonyo ukubwani?
(Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa simu: 0713-614872 na imeili: ndimara@yahoo.com)
Tuesday, September 2, 2008
MNC-LUMUMBA YAJIANDAA KWA UCHAGUZI
VIONGOZI WA MNC-L KIVU WAJIANDAA MAPEMA

Naibu Katibu Mkuu wa Mouvement National de Congolais (MNC-Lumumba), Venance W’ialango (katikati) akilakiwa na Mwenyekiti wa MNC-Lumumba mkoa wa Kivu, Ramadhani Lumumba Mulezi (kulia) mara baada ya kuwasili katika Jimbo la Fizi tarehe 20 Mei 2008. Kushoto ni Naibu Mwenyekiti Antoine Lulacha.

Naibu Katibu Mkuu wa Mouvement National de Congolais (MNC-Lumumba), Venance W'ialango akiwa na viongozi wa MNC-L mkoa wa Kivu hivi karibuni, Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo (DRC). Hapa ni katika jimbo la Fizi wakipanga mikakati ya maandalizi ya chaguzi za ubunge na urais nchini humo za mwaka 2010.
Kutoka kushoto ni Dieu-donne Kashindi (Katibu Mwenezi/uhamasishaji), Antoine Lulacha (Naibu Mwenyekiti wa mkoa wa Kivu, Venance W’ialango (Naibu Katibu Mkuu MNC-L Taifa), Ramadhani Lumumba Mulezi (Mwenyekiti wa Mkoa), Jean Pierre Ngeza (Katibu wa Mkoa), Kulenga Kambi (Mshauri Masuala ya Siasa), na Lukele Bakwela (Mshauri masuala ya Uchumi).

Naibu Katibu Mkuu wa Mouvement National de Congolais (MNC-Lumumba), Venance W’ialango (katikati) akilakiwa na Mwenyekiti wa MNC-Lumumba mkoa wa Kivu, Ramadhani Lumumba Mulezi (kulia) mara baada ya kuwasili katika Jimbo la Fizi tarehe 20 Mei 2008. Kushoto ni Naibu Mwenyekiti Antoine Lulacha.

Naibu Katibu Mkuu wa Mouvement National de Congolais (MNC-Lumumba), Venance W'ialango akiwa na viongozi wa MNC-L mkoa wa Kivu hivi karibuni, Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo (DRC). Hapa ni katika jimbo la Fizi wakipanga mikakati ya maandalizi ya chaguzi za ubunge na urais nchini humo za mwaka 2010.
Kutoka kushoto ni Dieu-donne Kashindi (Katibu Mwenezi/uhamasishaji), Antoine Lulacha (Naibu Mwenyekiti wa mkoa wa Kivu, Venance W’ialango (Naibu Katibu Mkuu MNC-L Taifa), Ramadhani Lumumba Mulezi (Mwenyekiti wa Mkoa), Jean Pierre Ngeza (Katibu wa Mkoa), Kulenga Kambi (Mshauri Masuala ya Siasa), na Lukele Bakwela (Mshauri masuala ya Uchumi).