Monday, August 25, 2008

KIKWETE AVURUGA UTAWALA BORA


Wezi walindwa, Rais awa msemaji wa Benki

Na Ndimara Tegambwage

HATUA ya Rais Jakaya Kikwete kuhusu fedha zilizochotwa kutoka Akaunti ya Madeni ya Nje katika Benki Kuu (BoT), inamwelekeza katika kuvunja misingi ya utawala bora.

Sasa rais amechukua nafasi ya wataalam wa mipango ya maendeleo na amejitwisha jukumu la bunge la kuamua juu ya matumizi ya fedha katika taasisi na asasi za umma.

Kwa hatua hii peke yake, rais ameingilia mamlaka ya bunge na ametia dosari msingi wa utawala bora kuhusu mgawano wa madaraka na majukumu na misingi na kanuni za matumizi ya fedha za umma.

Akihutubia Bunge Alhamisi iliyopita, Rais Kikwete aliliambia bunge mpango wake wa kutumia fedha zinazodaiwa kurejeshwa na watuhumiwa wa ufisadi katika akaunti maarufu kwa jina la EPA, ambapo alisema zitaingizwa katika Mfuko wa Ruzuku ya Mbolea.

Alisema fedha nyingine zitaingizwa katika Benki ya Raslimali ya Taifa (TIB) ili kuimarisha utoaji mikopo ya riba ndogo lakini ya muda mrefu kwa wakulima, jambo ambalo alisema alishindwa kulitekeleza akiwa waziri, “lakini sasa ni rais.”

Akiongea kama anayepanga matumizi ya kaya yake, rais alisema sehemu nyingine ya fedha hizo inaweza kusaidia katika kuanzisha Benki ya Kilimo.

Hatua ya rais inaibua maswali mengi. Mfuko wa Ruzuku ya Mbolea una bajeti? Je, bajeti inapungukiwa kiasi gani? Mfuko ulipanga vipi kukabiliana na nakisi hiyo? Ni kweli mfuko huo unahitaji fedha hizo hivi sasa; zilizopatikana kwa dharura?

Je, TIB inaendeshwa kama genge la nyanya, ambako unaweza kuongeza mtaji wakati wowote ukipata mfadhili? Hiyo ni benki, inayotegemea bahati nasibu?

Kuna suala la Benki ya Kilimo. Hivi nalo linasubiri fedha za bahati nasibu? Hakuna mipango ya muda mrefu ya kuanzisha benki? Sharti fedha za kuanzisha benki zitokane na zile zilizoibwa na nje ya mkondo wa kawaida wa idhini ya bunge?

Kwanza, rais alilieleza bunge kuwa fedha za EPA siyo za umma. Kwa kauli yake hiyo, kwa nini fedha zisizo za umma ziingizwe katika matumizi ya umma na kwa amri yake bila kupitia chombo cha umma – Bunge?

Rais alijitahidi sana kutafuta maneno yanayofaa kuelezea jinsi fedha hizo zilivyofika BoT. Lakini mwishoni akasema, “hajulikani mwenyewe.”

Pili, kwa nini serikali itumie fedha inazojua siyo zake? Uadilifu uko wapi hata juu ya mali isiyo yako? Kama serikali haiwezi kuzitaifisha moja kwa moja, kwa nini izitumie tena nje ya duara la mamlaka husika – Bunge?

Ni rais aliyeliambia bunge kuwa fedha zitumike lakini serikali “ianze kutenga fedha kwenye bajeti yake ya kila mwaka,” ili wenye fedha wakijitokeza, wachukue fedha zao.

Bila shaka uingizaji fedha katika mzunguko kwa njia hiyo – kwa amri ya rais – kunaingilia bajeti ya nchi ambayo tayari ilikuwa imepitishwa kama “sheria kuu ya mapato na matumizi” kwa mwaka husika.

Na rais hakusema ni kwa vigezo vipi ameamua kutoa fedha hizo kwa wale aliowataja; ufuatiliaji wake utafanywaje na nani. Lakini rais alisema wenye fedha wakija wapewe fedha zao. Hakusema wasipojitokeza fedha hizo zitawekwa wapi.

Tatu, uamuzi wa rais wa kutenga fedha kila mwaka kwa ajili ya kulinda “fedha zisizo na wenyewe,” unalitwisha taifa mzigo mkubwa na usio wa lazima.

Kwa utaratibu wa bajeti ya kila mwaka kutenga fedha za kusubiri “wenyewe,” wananchi watakuwa wameingizwa katika ulipaji madeni yatokanayo na ufisadi wa makampuni yaliyochota mabilioni ya shilingi za EPA.

Nne, haijulikani iwapo fedha hizo zinazosambazwa zitatumika vizuri kwa kuwa hazikuwa kwenye bajeti na wanaopewa hawakuwa wanazihitaji pale rais alipofanya maamuzi. Aidha, hazikupelekwa kwa utaratibu unaolazimisha uwajibikaji.

Tano, muda wa bajeti kuchangia watuhumiwa wasioonekana ili waweze kulipa wenye fedha wasiojulikana, unaweza kutegemea utashi wa aliyeanzisha mradi huu.

Hii ni kwa kuwa chombo kilichopaswa kupitisha maamuzi juu ya matumizi ya fedha katika vyombo vya umma, au vinavyopokea fedha za umma, ambacho ni Bunge, hakikushirikishwa.

Sita, fedha za EPA zilikuwa mikononi mwa chombo cha umma – BoT. Zikaibiwa. Wizi ni kosa la jinai. Bahati mbaya, katika suala la EPA, rais hajaona hilo; analifananisha na madai.

Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) na Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) watakuwa wanajua hivyo na wana kila nafasi ya kumshauri rais.

Inaonekana wamekataa kumshauri, au wamemshauri akakataa kwa kuwa katiba inasema rais halazimiki kufuata ushauri wa mtu yeyote.

Ile hatua tu ya kukubali kurejesha fedha zinazodaiwa kuibwa BoT, ni kukiri kuiba na huo ni ushahidi wa kutosha kumpeleka mtu mahakamani.

Vilevile ile hatua ya kugundulika kuwa muhusika ametumia nyaraka za kugushi, peke yake inamweka mtuhumiwa katika nafasi ya kushitakiwa.

Bali ile hatua ya kutumia nyaraka za kugushi na kuweza kuiba – vyote viwili – ni ushahidi wa kutosha kumfikisha mtu kizimbani.

Pamoja na yote hayo, rais na wasaidizi wake hawajaona kuwa watuhumiwa tayari wanastahili kushitakiwa. Rais anasema hawapeleki mahakamani labda kama watakuwa wameshindwa “kurejesha” fedha hizo ifikapo Oktoba 31 mwaka huu.

Hatua hii ya kukataa kuona kosa, na hata kubadili kosa kuwa sahihi, ni sehemu ya matumizi mabaya ya madaraka na ni kukiuka misingi ya utawala wa sheria na hivyo kukiuka utawala bora.

Kuruhusu walioiba kurejesha fedha kimyakimya na kukataa kuwafikisha mbele ya sheria, ni kufanya ubaguzi kwani wananchi wengine wanapelekwa mbele ya vyombo vya sheria.

Ubaguzi wa aina hii una maana ya kuvunja katiba ya nchi ambayo inakataza ubaguzi wa aina yoyote. Ubaguzi huu unakuwa mchafu zaidi unapohusisha rais.

Hapa rais angeweza kujinasua. Angeweza kuachia sheria ikachukua mkondo wake hadi watuhumiwa kuachiwa au kupewa adhabu na yeye akatumia madaraka aliyonayo kuwasamehe.

Kunyima fursa vyombo vya sheria kufanya kazi yake, na au kukatisha mkondo wa sheria, ni kuingia eneo la kutofuata utawala wa sheria na hivyo kukiuka utawala bora.

Kuna kila sababu ya kujiuliza ni utamaduni gani umeanzishwa na rais wa kutaka aliyeiba arejeshe alichoiba na “mambo yaishe.” Bila shaka ni matokeo ya matumizi ya madaraka makubwa yaliyopindukia.

Kitabu cha “Corrupt Cities” kilichochapishwa na Benki ya Dunia, kinafafanua rushwa kuwa ni: “hodhi ya madaraka, inayoambatana na uwezo wa kutoa maamuzi lakini bila uwajibikaji.”

Hata hivyo, rais anasema serikali imechukua mali za watuhumiwa. “Mali zao zote tumezikamata; mpaka magari…makampuni yote ‘assets’ zote tumezikamata…wako hoi,” aliliambia bunge.

Inaleta mashaka kama watu ambao tayari ni hoi; ambao mali zao zote zimekamatwa na hivyo kutokuwa na uwezo wa kuzalisha, wanaweza kutegemewa vipi kurejesha fedha zozote.

Ni kutokana na kauli hiyo, akili dadisi inajenga mashaka juu ya kuwepo fedha zozote zilizorejeshwa kutoka kwa wakwapuaji wa EPA.

Aidha, mashaka hayo yanazidishwa na rais kutotaja majina ya watuhumiwa; mahali walipo, kiasi gani walichukua, kiasi gani wamerejesha na kiasi gani wamebakiza; wanafanya biashara gani na ziliko mali ambazo serikali imekamata.

Mashaka pia yanajengeka kwenye ukimya juu ya akaunti inayodaiwa kuhifadhi fedha zinazodaiwa kurejeshwa. Haitoshi kwa rais kusema ameambiwa kuna akaunti “maalum” kwa fedha hizo.

Akaunti ya fedha za aina hiyo, ambazo haitarajiwi zitumike kwa manufaa ya watu binafsi, inastahili kuwa wazi kwa hata wananchi kujua tawi la benki ilipo na hata kuweza kuikagua.

Rais, kwa kukataa kutoa, au kwa kuficha, taarifa zote hizo muhimu, anaweza kueleweka au kujengewa mashaka kuwa, anawakingia kifua watuhumiwa na kujenga ukuta wa siri.

Kwa hatua hiyo, rais atakuwa ameshiriki kuweka wananchi gizani na hivyo kukiuka kanuni ya utawala bora inayozingatia uwazi katika shughuli zote za utawala na mahusiano ya umma.

Jambo jingine linaloleta kizunguzungu katika ukwapuaji wa mabilioni EPA ni kuwepo ndimi nyingi juu ya suala moja.

Rais anasema fedha zilizorejeshwa ni Sh. 53.7 bilioni. Waziri wa Fedha Mustafa Mkullo aliishawaambia wafadhili kuwa tayari zimekusanywa Sh. 60 bilioni wakati CCM iliishasema zimekusanywa Sh. 64 bilioni.

Nani mkweli kati ya watatu? Si wafadhili wakubali sasa kuwa “wameliwa” na kwamba hata ahadi za kushitaki watuhumiwa wa ufisadi wanazosubiri ili watoe misaada waliyoahidi ni upepo uvumao?

Lakini rais, katika maelezo yake, alisema uchotaji fedha za EPA usingefahamika kama siyo wahusika “kuchomeana utambi.”

Kuchomeana utambi ni kuchongeana, kushitakiana, kutoa taarifa za mwenzako ambaye mlikuwa pamoja katika mpango mbaya na huenda wa kifisadi.

Sikiliza asemavyo rais, “Hajulikani mwenyewe. Hakuna atakayekuuliza. Unasuka laini yako pale na wenzako mnazitoa; bahati mbaya anatokea mtu mmoja anachoma utambi…ndiyo siri ikafichika. Isingekuwa hivyo asingekuwepo wa kujua kuna mtu ananufaika nazo…”

Kwamba rais anajua kuwa watuhumiwa walichomeana utambi ni jambo linaloibua hisia kuwa rais anajua fika kile kilichokuwa kinaendelea.

Bali hapa muhimu ni kwamba mifumo ya utawala wa fedha ni dhaifu; inayoruhusu rushwa na ufisadi mpaka atokee wa “kuchoma utambi” – bila shaka aliyedhulumiwa au “mlokole!”

Bila shaka udhaifu huu haukuanza juzi au jana. Ni wa muda mrefu na wa makusudi; ulioshirikisha mkondo mrefu kati ya benki, wafanyabiashara na baadhi ya viongozi.

Rais anasema akaunti ya EPA ilikuwa na zaidi ya dola 600 milioni. Anasema kuna zilizolipwa kwa wahusika na nyingine ni zile zilizokwapuliwa watuhumiwa. Anasema hivi sasa kuna dola 260 milioni.

“Hela zinazagaazagaa…huko kuna mapesa mengi hayana mwenyewe halafu watu wananufaika nayo…” anasema rais katika kufafanua akaunti ya EPA.

Kinachoongeza mashaka katika igizo zima la EPA, BoT na Serikali ni kuona kazi ya benki inachukuliwa na rais. BoT imemgeuza rais kuwa msemaji wake, jambo ambalo halikubaliki.

Kilichotendeka BoT siyo siasa. Ni utovu wa nidhamu ya utawala wa fedha na wizi. Ni kazi ya Gavana wa sasa wa BoT kutoa maelezo ya kina jinsi mtangulizi wake na watumishi chini yake walivyoboronga na kurahisisha ukwapuaji.

Ni gavana awezaye kuandika hata kitabu juu ya sakata hili akielezea mkondo wake kiofisi na kufuatilia mwingiliano wa wafanyabiashara, wanasiasa na siasa kwa ujumla.

Kwani katika hali ya kawaida, mtu aweza kuuliza, “Rais unatafuta nini benki?” Kwa nini mwanataaluma anamwachia rais kueleza mambo ya kitaaluma ambayo yeye angefafanua vizuri zaidi? Au kuna kitu rais anataka au ametakiwa kukizima kabla hakijachomoza?

Ni mashaka hayo yanayoongoza katika kueleza nani mwenye fedha za EPA na kwamba hakika, na kwa kutofautiana na rais, fedha hizi zina wenyewe na wenyewe ni umma wa Tanzania.

Ni kweli fedha ziliingizwa benki na wafanyabiashara wa ndani kwa mpango wa kuagiza bidhaa kutoka nje. Wakati huo amana ilikuwa ikiitwa “110% Cash Cover.” Bidhaa zililetwa.

Ni kweli benki haikuwa na fedha za kigeni kwa kipindi kirefu ili kugeuza fedha za ndani kuwa za kulipia walioleta bidhaa. Kuna ushahidi kuwa baadhi ya waliostahili kulipwa waliishasamehe madeni na wengine madeni yao kulipwa na bima za nchi zao.

Hoja ni hii. Misamaha ya kutolipwa iliyotolewa na wenye mali zilizoletwa nchini; na mara nyingi kupitia serikali zao, mpaka fedha zikabaki Dar es Salaam, imetolewa kwa nchi – kwa umma wa Tanzania na siyo wafanyabiashara wachache.

Makampuni yaliyoanzishwa kwa kasi na kuchota mabilioni ya shilingi EPA, yalifanya hivyo kwa kutumia nyaraka za kugushi na kwa kujua kuwa wafanyabiashara wa nje tayari walishalipwa au waliishasamehe madeni.

Kwa hiyo fedha ni za umma. Katika chombo cha umma. Zikilindwa kwa akili, silaha na bima za nchi hii. Fedha hizi hazizagaizagai. Ziko mahali pake.

Fedha za EPA, zilizopo na zinazodaiwa kurejeshwa, sharti ziwe kwenye akaunti inayojulikana na ziingizwe kwenye mkondo wa matumizi unaodhinishwa ba bunge.

Kutofanya hivyo, ni kujenga mazingira ya kutumbua fedha zilizosalia kwenye akaunti ya EPA – fedha ambazo ni za umma; ikiwa ni pamoja na zile zinazodaiwa kurejeshwa – na katika mazingira yasiyo na uwazi.

Aidha, kuruhusu matumizi ya fedha kwa mtindo aliosema rais, itakuwa kukiuka misingi ya utawala fedha na hata kuongeza fedha kwenye mzunguko na huenda kusababisha mfumuko zaidi wa bei.

(Makala hii itachapishwa katika gazeti la MwanaHALISI toleo la Jumatano 27 Agosti 2008). Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa simu: 0713 614872; imeili: ndimara@yahoo.com)

Saturday, August 23, 2008

SERIKALI INAPOKIRI UPUNGUFU KWA UKALI

Wanajeshi, dalalada na manyanyaso

Na Ndimara Tegambwage

WAZIRI wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk. Hussein Mwinyi amekuwa mmoja wa mawaziri wanaosema ukweli.

Katika kipindi cha 1995 hadi 2000, mawaziri waliokuwa wasema ukweli walikuwa wakihesabika na tangu hapo kumekuwa na ukame.

Kazi ya mawaziri imekuwa kuficha ukweli, kunyamaza, kusema nusu uwongo au uwongo mkuu na kutetea serikali hata pale ambapo hapahitaji utetezi.

Miaka hiyo, walioongoza kwa kukiri makosa ya serikali, kutojua, kukubali kukosolewa au kusema ukweli, walikuwa Dk. Aaron Chiduo na Bujiku Sakila.

Dk. Chiduo alikuwa Waziri wa Afya na Sakila alikuwa Naibu Waziri wa Elimu. Hawakusita kutamka kuwa hilo serikali hailijui, haijalitenda na haina mipango ya kulifanya. Walikuwa wakweli.

Naye Dk. Mwinyi kajiunga na wasema ukweli wachache. Sikiliza kauli yake bungeni wiki iliyopita kuhusu askari wa Jeshi la Wananchi (JW) na usafiri wa daladala. Kapasua. Bila woga. Bila shinikizo.

Waziri amekiri kuwa wizara tayari imeandaa bajeti yake; haingewezekana kuirekebisha wakati huo alipokuwa akiwasilisha hoja bungeni ili kuweka fungu la nauli ya askari.

Kauli hiyo inaweza kuchambuliwa kama ifuatavyo: Kwamba serikali haina utaratibu wa kufikiria nauli ya askari. Kwamba si utamuduni wa serikali kupanga bajeti ya usafiri wa askari.

Kwamba wizara/serikali imezoea kusahau kuweka bajeti ya usafiri. Kwamba wizara haijawahi kuona umuhimu wa fungu la usafiri wa askari katika bajeti yake. Kwamba serikali haijui mazingira mabaya yanayowakabili askari.

Lakini inawezekana pia, kama anavyosema Dk. Mwinyi, kuwa wizara haina fedha. Amenukuliwa na vyombo vya habari akisema, wakati huu serikali haina hata uwezo wa “kuwaongezea askari fedha za kujikimu.”

Hili la ukosefu wa fedha ni jibu la kuchonga la serikali ambalo hufukuliwa mvunguni na kutolewa kwa kila anayedai utekelezaji unaohitaji fedha.

Ni hapo ambapo waziri alionekana kuunganisha mawili – ukosefu wa uwezo wa kuongeza fedha za kujikimu na ukosefu wa fungu la nauli – na kusema kuwa kujadili suala la nauli wakati huu ni “kuleta mkanganyiko katika jamii.”

Ni waziri anayeongeza kuwa serikali haina uwezo wa kujenga nyumba za kutosha kwa askari wake katika makambi yao au kutoa usafiri kwa askari kutoka walipo hadi sehemu zao za kazi na kurudi.

Hadi hapa, waziri amekiri upungufu, udhaifu, usahaulifu na pengine kutowajibika, katika mambo makuu yafuatayo:

Kwanza, kushindwa kwa serikali kuona umuhimu wa kupanga fungu maalum kwa ajili ya usafiri wa askari kutoka wanakoishi hadi vituo vya kazi na kurejea makazini kwao.

Pili, kushindwa kwa serikali kujenga nyumba za kutosha kwa askari katika makambi yao nchini.

Tatu, kushindwa kwa serikali kuongeza kiwango cha fedha za kujikimu kwa askari wa JW.


Mambo haya matatu aliyosema Dk. Mwinyi bungeni, mara nyingi huchukuliwa kuwa nyeti na siri. Lakini bunge ni mahali ambako lazima waziri amwage chozi ili kupata alichopanga kupata.

Hii ni fursa adimu kwa wananchi na hasa waandishi wa habari kumegewa taarifa hizi ambazo zinasaidia katika uchambuzi wa tabia na mwenendo wa serikali hata katika mambo yanayohusu ulizi wa nchi.

Ukweli unabaki palepale. Wananchi wanajua baadhi ya matatizo ya askari kwa kuwa askari ni watoto wao, ndugu zao, baba, mama, kaka na dada zao.

Bali katika suala la matumizi ya usafiri wa daladala, hata kama waziri hatataka wananchi waendelee kujadili; kule kuendelea kutumia usafiri huo hakika kunamomonyoa hadhi ya askari, jeshi na serikali yenyewe.

Mara nyingi mimi husafiri kwa mabasi ya daladala. Ndani ya basi kuna viti vitatu au vinne visivyo na abiria. Mnakaribia kituo kingine cha mabasi ambako kuna askari watatu na mwanafunzi mmoja.

Sikiliza kauli za yule wanayemwita kondakta wa basi: “Kuna nuksi hapo. Wanga hao. Simamia mbele kuleee,” anamweleza dereva. Mwanafunzi na askari wanaitwa nuksi. Wanaitwa wanga. Wanaitwa mikosi.

Askari anakimbiwa. Au askari anaonekana kama ombaomba kwa magari madogo, pikapu au malori. Anazomewa na wale ambao wasingeweza kumzomea maishani. Anachelewa kazini. Jumla: ananyanyasika.

Itabakia kuwa kweli kwamba askari ananyanyasika pale anapopanda magari kwa kubahatisha; kwa kuitwa majina machafu; kwa kuitwa “ombaomba wa lifti.”

Majeshi ni vyombo vya ulinzi vya dola. Vyombo vya dola haviwezi kutegemea kufanya kazi zake kwa fadhila za wafanyabiashara wakubwa na wadogo na kwa kubeuliwa na wale ambao wanategemea huduma ya majeshi hayohayo.

Vyombo vya ulinzi vya dola vikiwa na tabia ya kuomba au kutegemea “wema” wa mtu binafsi, vinaweza kupoteza ujasiri wake wa ulinzi na hata kutia hatarini usalama ambao vinatakiwa kuulinda.

Na askari anayesimamisha magari 10 hadi 20 ndipo apate wa kumbeba, huku mabasi madogo yakimpita na kummiminia kejeli nyembamba, atakuwa amechoka sana, kimwili na kisaikolojia, pindi afikapo eneo la kazi.

Hapa kuna mazingira yaliyojitokeza na kuruhusu jamii kujadili hadhi na heshima ya askari. Kuna mazingira pia yaliyosababisha waziri kutoa maelezo ya kweli juu ya kushindwa kwa serikali kukidhi mahitaji ya askari.

Muhimu ni kwamba sasa waziri na serikali wanatambua kuwa askari wananyanyasika. Raia na askari wanasubiri; wanataka kuona hatua zinazochukuliwa kuondoa hali hiyo mara moja.

(Makala hii itachapishwa katika gazeti la MwanaHALISI toleo la Jumatano, 27 Agosti 2008. Mwandishi anapatikana kwa simu: 0713 614872 na imeili: ndimara@yahoo.com)

0713 614872

UFISADI ULIOKUBUHU

EPA na watuhumiwa wasioonekana

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI kubishana na Rais Jakaya Kikwete kuhusiana na hatua aliyochukua kuhusu watuhumiwa wa ufisadi wasioonekana.Kwani mjadala ndio umeanza.

Pamoja na mambo mengine, Kikwete amesema amedaka watuhumiwa. Wamerudisha sehemu ya fedha walizokwapua. Amewanyang’anya pasipoti na kukamata nyumba na magari yao.

Aliliambia taifa na dunia, kupitia hotuba yake bungeni, Alhamisi wiki iliyopita, kuwa watuhumiwa wawe wamerejesha kiasi chote cha fedha walizokwapua kabla ya Oktoba 31, vinginevyo watapelekwa mahakamani.

Mpaka hapo nani hataki kumsikiliza rais? Masikio ya wengi yalikuwa yamejiandaa kusikia atasema nini juu ya wizi katika akaunti ya EPA ndani ya Benki Kuu (BoT).

Katika kupambana na rushwa na ufisadi, kile alichotangaza rais ni hatua ndogo sana, tena ya kutamanisha tu. Kuna hatua kubwa na shirikishi ambazo ni msingi wa mapambano haya.

Tujadili hatua moja ya msingi. Hii ni ile ya kutangaza majina ya watuhumiwa, makampuni yao, mahali wanakoishi, zilipo nyumba zao zinazoshikiliwa na serikali, biashara zao, magari yao yaliyokamatwa na mahali yalipoegeshwa.

Hatua hii ni muhimu kwa kuwa vita vyovyote dhidi ya rushwa na ufisadi ni vita vya umma; vinavyohusu jamii nzima. Hii ni kutokana na ukweli kwamba matokeo ya rushwa na ufisadi yanaathiri jamii nzima.

Jamii ingependa kuwajua watuhumiwa, tena kwa majina yao; lakini kubwa zaidi, jamii ingependa kuona “mapapa wa ufisadi” wakiburuzwa mahakamani na hatimaye kuona wanapewa adhabu kubwa ikiwa ni pamoja na kifungo.

Jamii ingependa kuona watuhumiwa hawakingiwi kifua kwa sababu zozote zile, hata visingizio vya “haki za binadamu.” Hakuna popote ambako haki za binadamu zinaruhusu wizi au aina yoyote ya ufisadi.

Mambo haya mawili, kutajwa hadharani kwa majina ya watuhumiwa na kufikishwa mbele ya sheria, huwapa imani wananchi kuwa serikali yao ipo, ni makini, inafanya kazi yake na haitavumilia ufisadi.

Hatua hii hufanya wananchi kuwa na hamu na nia ya kushiriki katika kutoa taarifa za kufichua mafisadi. Huamini kuwa wanaowahujumu wao na taifa lao, wakikamatwa watachukuliwa hatua.

Wananchi ni pamoja na asasi za kijamii. Asasi hizi zina nafasi kubwa katika kuangaza njia ya jamii na kuiongoza katika kufikiri na kutenda.

Asasi ambazo zinahusika na mapambano dhidi ya rushwa; zinazoshughulikia elimu na malezi; zinazojitambulisha na masuala ya demokrasi na utawala bora, ni sehemu nyingine ya jamii iliyoko vitani dhidi ya rushwa na ufisadi.

Kuongezeka kwa hamu ya kushirikiana na serikali katika mapambano haya; kukua na kupanuka kwa shughuli zao katika eneo hili; na kufumuka kwa fikra mpya juu ya mbinu na mikakati dhidi ya ufisadi, hutegemea wanavyoona serikali inawajibika.

Hakuna mahali popote duniani ambako serikali imefaulu kupambana na rushwa na ufisadi bila kushirikisha wananchi – mmojammoja na katika makundi na asasi za kijamii. Hakuna!

Vilevile hakuna popote pale ambako wananchi peke yao au na asasi zao, wamepambana na rushwa na ufisadi na kushinda bila kushirikisha serikali.

Utashi na mamlaka ya serikali ni muhimu katika mapambano haya na utashi utajidhihirisha kwenye hatua ambazo serikali inachukua.

Hatua hizo ni pamoja na kuweka wazi kila kitu: Nani mtuhumiwa wa ufisadi, yuko wapi, kachukua nini na wapi, kapelekwa mahakamani na kachukuliwa hatua gani.

Hakuna mahali ambako rais amewahi kushinda ufisadi kwa kutumia wapelelezi wake wa siri; kupata taarifa ya siri, kukamata watuhumiwa wa siri, kukusanya fedha za siri na kuzihifadhi kwenye akaunti ya siri. Hakuna.

Hakuna kokote duniani ambako rais amefaulu kupambana na ufisadi kwa yeye kuwa mkamataji watuhumiwa, mwendesha mahojiano, mkusanyaji fedha, mtoaji misamaha; tena kwa watuhumiwa wasioonekana. Hakuna.

Hatua kama hiyo haisaidii kukuza mapambano dhidi ya rushwa; haisaidii kujenga msingi wa mapambano, wala haionyeshi kuwa serikali ina nia nzuri.

Badala yake, hatua hiyo inachafua sura ya serikali katika mapambano haya. Inasaidia kujenga mazingira ya kuishuku serikali na watawala, kwamba huenda hata wao wanahusika katika ukwapuaji.

Vita vyovyote dhidi ya rushwa na ufisadi sharti vifanywe kwa uwazi na katika uwazi. Pasipo uwazi ni kukomaza rushwa, ufisadi na uhalifu. Kwa ufupi, ni kushiriki ufisadi. Mjadala ndio umeanza.

(Makala hii itachapishwa katika Tanzania Jumapili, 24 Agosti 2008. Mwandishi anapatikana kwa simu: 0713 614872 ma imeili: ndimara@yahoo.com)

AINA NYINGINE YA UFISADI

'MACHINGA COMPLEX' NA LONGOLONGO YA KISIASA

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI Machinga Complex kwa kuwa itazaa mgogoro utakaozaa migogoro itakayozaa migogoro isiyoisha na kuwa mfano mbaya kwa nchi nzima.

Machinga Complex ni kitu kikubwa kinachoitwa Jengo la Wafanyabiashara Wadogo lililoko Dar es Salaam ambalo Rais Jakaya Kikwete aliweka jiwe lake la msingi Ijumaa wiki hii.

Tunaambiwa ni machinga watakaokuwa katika jengo hilo la thamani ya Sh. 10 bilioni kutoka Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) na linalotarajiwa kukamilika Novemba mwaka huu.

Wazo la kujenga Machinga Complex lilitokana na mawazo ya watawala kwamba ‘Jiji la Dar es Salaam limechafuka.’ Limejaa takataka lakini pia limejaa uchafu unaotembea; maduka yanayotembea (machinga).

Wakati wageni wa kitaifa wanapotangaza kutembelea nchi, maganda ya mihogo na miwa, machinga, plastiki zilizotumiwa, ombaomba na mikokoteni, vyote hufagiwa kwa shabaha ya kusafisha jiji kabla wageni hawajawasili.

Swali likazaliwa. Uchafu ulioko sehemu moja unaweza kukusanywa haraka. Uchafu unaotembea je? Wazo likazaliwa: Ukusanyiwe kwenye jengo moja litakaloitwa Machinga Complex. Hapa ndipo tumefikishwa.

Takwimu zinasema jengo lina uwezo wa kuchukua wafanyabiashara wadogo wapatao 10,000. Hapo ndipo hoja zinapoanzia.

Wafanyabiashara ndogo ni akina nani? Biashara ndogo inaanzia shilingi ngapi? Nani anajua thamani ya biashara ya wafanyabiashara ndogo? Nani anajua idadi ya wafanyabiashara ndogo jijini Dar es Salaam na idadi imepatikana kwa vigezo vipi vya biashara ndogo?

Tunaambiwa Machinga Complex inajengwa kwa fedha za NSSF. Bila shaka hiki ni kitega uchumi. Kama hivyo ndivyo, hii ni biashara ya aina yake. Ni nipe nikupe.

Katika hali hii wafanyabiashara ndogo tunaowajua, wale wasaga lami kuanzia alfajiri ya saa 11 hadi usiku wa manane, watapata wapi fedha za kulipia pango kwenye jengo la ghorofa sita?

Hata kabla hawajafikiria suala la pango, nani atafikiria wasaga lami kuwa sehemu ya jengo la kisasa: wao na marapurapu yao; wao na jasho lao; wao na makatambuga yao au pekupeku – bila kiatu wala ndala?

Kuna mifano michache hapa ya kuangalia. Nenda soko la Kjitonyama, wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam. Hakuna ghorofa. Hakuna mmeremeto. Ni jengo na vituti vya kuuzia bidhaa. Nani hakumbuki kilichotokea pale lilipofunguliwa?

Wenye fedha walichukua karibu nafasi zote katika soko; wakilipa kiasi kilekile kinachohitajika kulipwa. Wakahodhi soko. Ndipo wakaanza biashara ya kuuza nafasi hizo kwa bei isiyoshikika.

Asitokee mtu akadai kuwa hajui kilichotendeka Soko la Sterio Temeke. Ni yaleyale ambayo yalitokea Kijitonyama. Hodhi ya karibu nafasi zote au zilizoko maeneo mazuri na baadaye kuziuza kwa bei ya juu.

Hayo ni madai hai hadi sasa. Waliokumbwa na mkasa huo bado wana la kusimulia. Na bado kuna wanaodai kuwa mabanda yaliyojengwa kuzunguka shule nyingi Dar es Salaam yamehodhiwa na wenye fedha na kuuzwa baadaye kwa kiwango cha kufuru.

Ndiyo maana maneno ya Machinga Complex hayawatui hata machinga wenyewe. Kama walikuwa sehemu ya takataka, na ‘dampo’ linalojengwa ni la dhahabu, wao watatupwaje katikati ya utajiri?

Kama wenzao, wauza mihogo na mboga, walishindwa kupata nafasi katika masoko ya pembezoni, kutokana na wenye fedha kuhodhi maeneo mengi na nyeti kibiashara, wao wataingiaje ghorofani hata kabla mtoto wa mkuu wa wilaya au mkoa hajapewa nafasi?

Ni maswali yanayotokana na mazingira na mazoea jijini na nchini kwa ujumla. Chukua mfano wa Benki ya Makabwela (NMB). Hakuna mkurugenzi au hata mfanyakazi wa benki hiyo anaweza akasema ile benki ni ya makabwela. Hayupo!

Sababu ni kwamba siyo ya makabwela. Basi. Ni benki ya biashara isiyokuwa na ukabwela wowote. Wenye akaunti humo ni wafanyabiashara, maofisa serikalini na makapuni mbalimbali binafsi.

Wengine wenye akaunti ni na wale ambao waajiri wao wamewaambia wafungue akaunti zao kule au wanaolazimika kuchukua mikopo kupitia benki hiyo. Ukabwela uko wapi?

Kabwela hana shati. Anaazima la rafikiye. Kabwela hana kitanda. Analala chini au kwa kugawana na mwenzie. Kabwela hana akaunti benki wala ajira. Kabwela gani anamiliki benki kama siyo dhihaka?

Machinga Complex itakuwa kama Benki ya Makabwela. Ni longolongo ya kisiasa ya kukidhi haja iliyopo tena kwa wakati uleule tu. Machinga – ule uchafu unaoleta kinyaa mitaani wakati wageni wanapotembelea jiji – utakaaje ghorofani?

Lakini tusiishie hapo. Ni machinga wangapi walioko jijini hivi sasa? Wanaingia wangapi jijini ambao watakuwa machinga kesho? Kiwango cha uingiaji mijini vijana wa kuwa machinga katika miaka mitano ni kipi?

Kuna wasioanza moja kwa moja na umachinga. Dereva na karani aliyefukuzwa kazi. Mfanyakazi wa nyumbani aliyepewa ujauzito na mwajiri na kutupwa mitaani. Ni wengi. Ni wengi.

Mradi wa machinga utasimama kwa miguu yote? Abbas Kandoro atakuwa shahidi.

(Makala hii ilichapishwa katika gazeti la MwanaHALISI la Alhamisi 20 Agosti 2008. Mwandishi anapatikana kwa simu: 0713 614872 na imeili: ndimara@yahoo.com)

Wednesday, August 13, 2008

UFISADI SOKONI NA MITAANI

Wanafunzi, mabasi na mafisadi

Na Ndimara Tegambwage

ANGALIA watoto hawa. Ni wanafunzi. Wasichana kwa wavulana. Umri wao ni mdogo. Baadhi yao wana matongotongo. Kuna waliobeba mikoba, madaftari mikononi na nyuso zisizotabirika. Lakini wana lengo moja.

Kuna waliobeba mabango na moja linalosomeka haraka linasema, “…maisha bora kwa kila fisadi.” Wamo katika maandamano jijini Dar es Salaam.

Vichanga hivi vya shule za msingi na sekondari vimevuka mstari. Vimeona wazazi wao wamebaki kimya. Vimeamua kusimama na kupaza sauti kutetea wazazi na kujitetea. Vinasema nauli ya Sh. 100 kwa safari moja kwa mtoto, katika mazingira ya sasa, ni mzigo usiobebeka.

Kama kawaida sauti zinagonga kwenye mwamba na kutoa mwangwi unaoendelea kwa muda mrefu: Nauli! Nauliii! Nnaul…! Nnnau…Nnnna…nnnnn…

Sauti za wanafunzi hao, zikiwakilisha maelfu ya vijana wa rika lao, zinapotelea katika mwangwi kama madai yao yanavyoyeyukia kwenye ahadi za watawala na ujanja wa wafanyabiashara.

Kwa vijana hawa, makali ya ufisadi yanaanzia pale wanaposhindwa kwenda shule au wanapochelewa; wanaposhindwa kutumwa sokoni au kwa ndugu; wanaposhindwa kutembeleana.

Sasa ujumbe wao kuwa maisha bora kwa kila Mtanzania yamechukuliwa na “maisha bora kwa kila fisadi,” hakika umepelekwa na umefika.

Walioandamana ni wanafunzi walewale wadogo, ambao wamekuwa wakishirikishwa katika magwaride, kusoma risala na kukimbiza mwenge. Kauli za maisha bora wamezidaka kwenye mdomo wa watawala na maisha yao ya kila siku.

Kwa nini tusikubali kuwa sasa wanafunzi wameanza kufundishwa kufikiri na kuoanisha maisha na matukio na kuacha kuwa kasuku wa vibandani?

Sasa jambo moja ni wazi: Kwamba tayari watoto wa shule, katika umri wao mdogo, wameanza kujifunza kwa kufikiri na siyo kuwa kama kasuku wa vibandani.

Mabango yao yanaonyesha jinsi ya kuunganisha matukio. Kwa mfano, uhusiano kati ya rushwa na kufifia au kukosekana kabisa kwa huduma za kijamii.

Wanajua ukosefu wa utawala bora unavyoweza kusababisha hata njaa kwa nchi nzima kwa kuwa wananchi hawana fursa za kutenda kwa uhuru.

Wanaelewa kuwa chakula ni suala la ulinzi wa nchi na kwamba kupungua au kukosekana kwa chakula, kama ilivyo kwa kukosekana kwa utawala bora, kunaweza kuzaa maafa ya vita vya muda mrefu vya wenyewe kwa wenyewe au kupinduliwa kwa serikali.

Leo hii wanafunzi wanajua kuwa kuwepo kwa mafisadi, wanaojipakulia mabilioni ya shilingi kutoka kwenye chungu cha taifa, kunadhoofisha uchumi na kuua fursa za elimu, tiba na miundombinu.

Wanaelewa kuwa ukwapuaji wa mabilioni ya shilingi, unaofanywa na wachache katika jamii, unachochea kukua kwa akili butu, zisizo na uwezo wa kufikiri isipokuwa kuiba, kula, kunenepa na kufa kwa magonjwa ya ulafi.

Aidha, wanafunzi wanajua sasa kwamba ukwapuaji huo pia ndiyo njia ya kuchimba makaburi ya mamilioni ya wananchi waliokamuliwa (sio wasionacho kwani wanaporwa kila kukicha); ambao lazima wafe kutokana na ujinga, maradhi na umasikini.

Siyo siri tena kwamba wakati kuna wanaokufa kwa magonjwa yatokanayo na ulafi; ulafi ambao ni uzao wa wizi mkubwa, unyanganyi na ufisadi; kuna wanaokufa kutokana na maradhi yaletwayo na ufisadi.

Wanafunzi pamoja na umri wao mdogo, sasa wanaweza kubaini kuwa mikataba ya kinyonyaji, kwa mfano ile ya nishati ya umeme, inaongeza ugumu wa maisha kwa baba au mama zao.

Wanaona hatua ya serikali ya kukimbia wajibu kwa visingizio vya “serikali haifanyi biashara,” imeacha soko la nishati ya mafuta mikononi mwa walafi – ambao huenda ni pamoja na maofisa wa serikali – na kusababisha mzazi kushindwa kununua hata fungu la mchicha ambalo bei yake imepaa.

Watoto wanasikitika sana. Wakilia wanaona na serikali inalia. Maana yake ni nini? Wanaona kwamba hawana ulinzi tena. Kwamba usalama wao umeyeyuka. Kwamba serikali waliyotarajia kuwa ngao yao nayo imetota.

Tena afadhali kilio cha wengi, wakiwemo wanafunzi, kinachoweza kuleta kisirani au simanzi kuliko kilio cha wachache serikalini ambao wamebainika kuwa miongoni mwa wakwapuaji wakubwa wa fedha za umma na raslimali za taifa.

Wanafunzi katika shule za msingi na sekondari, wanayaona yote haya. Wamezaliwa katika mazingira haya. Wanakulia humo. Hawahitaji kusimuliwa uchungu wake. Wanaujua vema. Wanahitaji nadharia tu ya mapambano ya kuondokana na hali hiyo.

Siku ya Ijumaa, tarehe 1 Agosti mwaka huu, wanafunzi wa Dar es Salaam, kwa niaba ya wenzao mkoani na nchi nzima, walitumia kauli na miguu hadi ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam kusisitiza kuwa wao na wazazi wao hawana uwezo wa kulipa nauli mpya.

Nauli haikupunguzwa. Lakini kesho wanaweza kujitokeza kutoa maoni kwa jambo jingine muhimu katika jamii. Ni ishara ya vijana hai; jamii hai inayotolea maoni kila jambo linaloihusu.

Bali duniani kote hakuna mahali ambako kuna mabasi pekee ya wanafunzi isipokuwa katika shule chache sana ambazo huwa na mabasi ambayo gharama yake huingizwa kwenye karo. Wengine wote hutumia usafiri wa umma.

Hapa kwetu kelele za “wanafunzi” zinaletwa na wenye shabaha ya kutaka kupendelewa ili wanunue magari na kuendesha miradi ya kubeba wanafunzi pekee au wanaofikiri serikali itanunua mabasi wapate mahali pa kufanyia ufisadi.

Leo tutafute jibu kwa swali moja: Nauli ya Sh. 100 siyo kwa wanafunzi peke yao. Ni kwa watoto wote. Yakinunuliwa mabasi kwa wanafunzi peke yao, na kufanya kazi siku za shule, watoto wengine watasafiri vipi? Wakati wa likizo wanafunzi watasafirije?

Halafu angalia uchovu huu wa aina yake. Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam anasema kwa kuwa wanafunzi watalipa Sh. 100, basi waketi kwenye viti!

Kwa wenye mipango mizuri ya usafiri mijini, viti vichache – kama 15 hivi katika basi kubwa – huwa vya wajawazito, wenye ulemavu, wagonjwa na vikongwe. Wengine hupanda, husimama na kushuka. Mwanafunzi atakaa vipi?


(Makala hii imechapishwa katika gazeti la MwanaHALISI la 13 Agosti 2008. Mwandishi anapatikana kwa simu: 0713 614872; imeili: ndimara@yahoo.com)

Saturday, August 9, 2008

WOGA WA WATAWALA

Vitisho kwa waandishi wa habari Iringa


Na Ndimara Tegambwage

SITAKI vitisho vya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Mrisho Said alivyomwaga mbele ya waandishi wa habari mjini Iringa, Jumanne ya 29 Julai mwaka huu.

Amina alikuwa akifungua mafunzo ya wiki moja ya Uandishi wa Habari za Uchunguzi katika Rushwa, Utawala Bora na Matumizi ya Sheria ya Ununuzi Serikalini ya mwaka 2004.

Ilikuwa baada ya mkuu huyo wa mkoa kuwapaka mafuta kidogo waandishi wa habari kwa kusema wao ni mhimili wa nne wa dola, ndipo aliwageukia na kumwaga nyongo.

Kwanza, Amina alilalamika kuwa mkoani mwake kuna waandishi wa habari ambao wanamkera sana kwa kuandika wanavyotaka na kudai kuwa hayo waliyoandika yamesemwa na yeye.

Pili, alisema baadhi ya waandishi wa habari wa mkoani Iringa, bila kutaja majina yao, wanajipachika ‘majina bandia’ na kutawanya habari zao katika vyombo vingi vya habari.

Tatu, Amina aliapa kupambana na waandishi wa aina hiyo kwa kusema, ‘serikali ina mkono mrefu. Mimi nawafahamu tu. Nikisoma habari hii na hii na ile, najua ameandika mtu mmoja kwa kubadili majina tu, lakini nasema, serikali ina mkono mrefu. Nikiwahitaji nitawapata.’

Kauli hii, mbele ya waandishi wa habari waliokusanyika kujifunza jinsi ya kuandika habari za uchunguzi; ukiwemo uchunguzi katika matumzi ya madaraka na dhamana za uongozi, ilikuwa kama kutangaza msiba katikati ya sherehe.

Kwa kuzingatia kauli aliyotoa, mahali alipoitolea, madhumuni ya kusanyiko hilo la waandishi wa habari na ujio wa ziara ya Rais Jakaya Kikwete – siku nne mbele – utaona kuwa mkuu wa mkoa alilenga kupanda mbegu ya woga.

Tukubali basi kwamba hakuna anayepinga mtu kuwa na haki ya kuwa na maoni. Kila mtu pia, ikiwa ni pamoja na mkuu wa mkoa, ana haki ya kusikitika, kukasirika, kulia, kucheka au kulalamika. Hizo pia ni baadhi ya njia za kujieleza.

Lakini kwa mkuu wa mkoa kusubiri darasa la kufundisha wachokonozi katika matumizi ya serikali, rushwa na utawala bora ndimo amwage malamiko na vitisho vya kutumia mkono mrefu wa serikali, hakika ni kwenda mbali.

Haishangazi basi kwamba waandishi wa habari aliotishia walisikika wakikejeli kuwa, ‘Mama huyu ni mwoga; ana mchecheto,” wakihusisha vitisho vyake na hali iliyomkumba siku moja kabla Rais Kikwete kuanza ziara mkoani Iringa.

Usiku wa manane wa mkesha wa siku ya kwanza ya ziara ya rais, Amina alilazwa hospitali kuu ya mkoa mjini Iringa akisumbuliwa na kile madaktari wawili walisema ni ‘matatizo katika kifua.’

‘Nadhani ni mchoko na vumbi,’ alieleza daktari mmoja bila kutaka kufafanua hasa kilichokuwa kinamsumbua mkuu wa mkoa.

Yawezekana ulikuwa mchanganyiko wa mambo mengi: Mchoko uliotokana na mzunguko mrefu kwenye sehemu ambazo rais angetembelea, vumbi, wasiwasi wa ujio wa rais katika mazingira ambayo hayajawekwa sawa, misuguano na malumbano miongoni mwa viongozi mkoani ambavyo vingeonekana wakati wa ziara ya rais.

Mambo mengine ambayo bila shaka yaliongeza mchecheto na huenda kuathiri afya ya Amina ni ‘jeshi’ la waandishi wa habari walioandamana na rais kutoka Dar es Salaam na mkoani wakidhamiria kuanika kila kitu katika ziara hii.

Lakini jingine muhimu ni kuwepo mkoani kwa waandishi wa habari aliowatishia kwa kusema serikali yake ina mkono mrefu wa kuwasaka kwa kuandika kinyume na kile alichosisitiza kuwa ‘maadili ya uandishi wa habari.’

Kwamba tayari Amina amepata afueni na alifanikiwa kuhudhuria angalau kikao cha majumuisho ya ziara ya Rais Kikwete, mengi ambayo yalimfanya awe na mchecheto yaweza kuendelea kuibuiliwa.

Kwa mfano, tayari taarifa zinazohitaji kuthibitishwa zinasema kuna maeneo ambayo hayakuwa katika ratiba ya awali ya ziara ya rais, lakini yaliingizwa baadaye. Haya ni pamoja na Shule ya Sekondari ya Anna Makinda iliyoko kijiji cha Ihanga, Njombe.

Makinda ni Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Eneo jingine ambalo limetajwa kuwa halikuwa katika ratiba lakini liliingizwa, ni ASAS Dairy Farm – shamba la mifugo linalomilikiwa na mfanyabiashara Salim Abri. Hili nalo Kikwete alilitembelea.

Lakini katika majumuisho yake, baada ya ziara ya karibu wiki nzima, Kikwete aliwataka viongozi wa mkoa, kwenye kikao pekee alichohudhuria Amina, ‘kuongeza ushirikiano’ na kuepuka malumbano ambayo alisema hayasaidii kuleta maendeleo.

Ukiweka pamoja yote yaliyotokea mkoani kabla na wakati wa ziara ya rais; na ukizingatia kile ambacho rais amebaini – kuwepo kwa malumbano na ukosefu wa ushirikiano – mchecheto wa mkuu wa mkoa mbele ya waandishi wa habari ni hali iliyotarajiwa.

Bali hakuna sababu yoyote kwa mkuu wa mkoa yeyote kuwa na mchecheto na hata kutishia waandishi wa habari kwa mkono mrefu wa serikali. Mkono mrefu wa serikali ukamate mafisadi ambao wapo pia mkoani Iringa.

Anachohitaji Amina ni kuweka wazi utendaji wake, kwa kila moja kuona na hata kutathmini na kutarajia waandishi wa habari kuheshimika kwa kuandika ukweli au kuumbuka kwa kuandika uwongo.

(Makala hii itachapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili, 10 Agosti 2008.Mwandishi anapatikana kwa simu: 0713 614872; imeili: ndimara@yahoo.com)