Saturday, May 24, 2008

Serikali na utata wa Ballali

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI serikali ijiingize kwenye utata wa kutoeleweka, kutoaminika na kutothaminiwa.

Kwa zaidi ya mwaka mmoja, ni serikali ambayo ilisema haijui aliko Dk. Daudi Ballali, yule aliyekuwa gavana wa Benki Kuu (BoT) na ambaye alifukuzwa kazi na Rais Jakaya Kikwete.

Mbali na kusema kwamba Ballali anaumwa na yuko kwenye matibabu nchini Marekani, serikali ilikataa kusema mambo mengi juu ya mtu muhimu katika jamii.

Ilikataa kusema yuko katika jimbo gani nchini Marekani. Ilikataa kusema amelazwa hospitali gani. Ilinyamazia ugonjwa unaomsubua gavana; ilikataa kutoa taarifa juu ya hali yake kadri ilivyoendelea na ilikataa kusema kifo chake kimetokana na nini.

Ukimya huu ulizaa mashaka. Ulizaa utata. Ilifikia mahali wananchi wakauliza, tena kwa kishindo na mfululizo, iweje serikali isijue wapi amelazwa mtu muhimu kama gavana wa benki.

Leo hii, Ballali hayupo. Amefariki. Taarifa zinasema alifariki Mei 16, Ijumaa ya wiki iliyopita. Lakini kauli ya serikali ilitoka siku tano (5) baada ya kifo cha Ballali.

Hata kauli ya serikali ilishinikizwa na waandishi wa habari watukutu walioizonga wakitaka itamke kama Ballali amefariki kweli au ulikuwa uvumi.

Ukimya huu unaendelea kuzaa utata na mashaka. Kifo cha Ballali kimekuja wiki mbili baada ya serikali kusema kuwa haimhitaji Ballali kwa sasa.

Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Salva Rweyemamu aliwaambia waandishi wa habari kuwa “serikali ikimhitaji Ballali utampata” na kwamba serikali ina mkono mrefu.

Sasa tuone ukimywa huu wa serikali ulivyo na athari kwa utawanyaji habari. Mmoja wa wasomaji wa safu yangu hii, ameniaandikia ujumbe wa simu. Unasema hivi:

“Jamani ninyi waandishi wa habari, hamjui wala kutafakari. Mwili utakaochomwa moto (wa Ballali) sio wa mtu halisi, lakini Ballali mwenyewe wala hayupo Washington. Hii ni njama imeandaliwa kwa muda mrefu na kwa gharama kubwa. Namba yangu (ya simu) msiitoe popote tafadhali. Baada ya kuisoma hii, uifute. Ni mimi raia mwema.”

Huyo ni msomaji mmoja. Wapo wengi walioandika juu ya Ballali na “madai” kuhusu kifo chake. Wakizingatia kuwa serikali imekuwa ikikataa kutoa taarifa, wana haki ya kupokea hata uvumi na kuuamini.

Lakini kama nilivyowahi kuandika katika kitabu changu, “Who Tells The Truth In Tanzania?” (Nani Msema Ukweli Tanzania), kila uvumi una asili na chimbuko lake.

Kwa wote waliofuatilia suala la wizi wa mabilioni ya shilingi kutoka BoT; walioshuhudia Rais Kikwete akiunda Kamati ya kurejesha mabaki ya mabilioni hayo na wanaofuatilia kauli za viongozi, kifo cha Ballali, kama kimetokea, kinaweza kutafsiriwa kwa njia nyingi.

Mhusika mkuu wa tafsiri nyingi za wananchi wengi ni serikali. Ni serikali iliyoficha ukweli wa mahali alipo Ballali kwa kudai kuwa haijui.

Ni serikali iliyokataa kumtafuta Ballali akiwa hai, kumrejesha nyumbani ili asaidie katika kutoa taarifa juu ya uchotaji wa mabilioni ya shilingi kutoka BoT.

Kauli kwamba Ballali siyo mtuhumiwa na wala hahitajiki kwa sasa, siyo tu zinazidisha utata, bali pia zinathibitisha kushiriki kwa, ama watendaji au serikali yenyewe katika ufujaji wa fedha za umma.

Na hapo ndipo vinapatikana viini vingi vya taarifa zisizorasmi. Kwamba kama Ballali angerudi nchini na kupewa kibano, angetaja nani alimwamuru kuvunja misingi na maadili ya kazi yake.

Kwamba walioko kwenye utawala na waliostaafu wangekumbwa na “tsumani ya ukweli” usiopingika kuwa walishiriki ufisadi usiomithilika.

Kwamba fedha zilizothibitika kukombwa, Sh. 133 bilioni, kweli ni “vijisenti” kwani hizo ni kutoka akaunti moja tu katika mwaka mmoja wa fedha.

Iwapo akaunti zote zingepitiwa, ungekuta ni mamilioni ya mabilioni ya shilingi ambazo zilikombwa. Mwenye taarifa hizo ni Ballali.

Kwamba huenda ni kweli Ballali alikuwa anaumwa na watawala waliona hawezi kupona; hivyo wakaamua wamwache “afe salama” bila usumbufu wa nyongeza.

Kwamba huenda kipindi cha miezi sita ambacho Kikwete alitoa kwa kamati yake kufuatilia mabilioni yaliyokwapuliwa benki, kilikuwa kinalingana na muda ambao Ballali alikuwa amebakiza kuaga dunia.

Kwamba kwa vyovyote vile, hakuna mtawala ambaye angekubali Ballali arejee nchini na kuruhusiwa kufungua kinywa chake. Ama angeapishwa kuwa atakaa kimya au angenyamazishwa kwa vyovyote vile.

Kwamba hakuna, miongoni mwa wanufaika wakuu wa ukwapuaji BoT, aliyetaka hata Ballali aendelee kuishi, kwani walijua kuwa iwapo ataendelea kuwapo, popote pale duniani, na katika utulivu wa akili na afya njema, angeweza kufikika na taarifa ambazo angetoa zingekuwa za madhara makubwa kwao.

Kwamba inawezekana kabisa kuwa ukimya wa Ballali, mke wake, watoto wao, ndugu zake, jamaa na marafiki zake, uliundwa rasmi na genge la mafisadi. Walinyamazishwa kwa vitisho, ahadi na “mishiko” hadi alipofariki.

Kwamba ndugu na jamaa hao walilishwa yamini, kuwa hata baada ya kifo chake, asitokee wa kuinua kidole au kichwa na kutoa kauli inayomwakilisha Ballali, yenye uwezekano wa kuwaangamiza wakwapuaji.

Yote haya yamesababishwa na ukimya wa serikali. Vyovyote vile ambavyo serikali ingetaka kufanya, ingekuwa vizuri kama ingekuwa inatoa taarifa, hata kama zisingekuwa zinakubalika moja kwa moja kwa wananchi.

Hakuna ubishi kuwa Ballali alifukuzwa kazi. Lakini alibaki hazina muhimu ya taarifa ambazo zingesaidia serikali kurejesha mabilioni ya shilingi za umma na angalau kuwa na ukweli juu ya waliozichota na kwa amri au pendekezo la nani.

Kama kweli Ballali amekufa na kuzikwa, basi amezikwa na hazina ya taarifa muhimu. Hii inatokana na jeuri na ubabe wa baadhi ya wale waliotakiwa kupata kauli yake kabla ya juzi.

Hapana. Labda siyo ubabe wala jeuri. Labda ni kwa kuwa wanaohusika ni wahusika pia katika ukwapuaji.

(Makala hii itachapishwa katika Tanzania Daima Jumapili ya 25 Mei 2008. Mwandishi anapatikana pia kwa simu: 0713 614872 na imeili: ndimara@yahoo.com)

Monday, May 12, 2008

‘Kochonkocho’ dhidi ya ufisadi

Vijiko, uma, sufuria silaha muhimu


Na Ndimara Tegambwage

WIKI iliyopita kulikuwa na taarifa katika vyombo vya habari juu ya vijana waliokamatwa kwa madai ya “kumtukana” rais mstaafu Benjamin Mkapa.

Kutukana ni kosa la jinai. Siyo kwa kumtukana rais au aliyekuwa rais peke yake, bali mtu yeyote. Lakini habari hizo hazikusema ni matusi yapi alitukanwa kiongozi wa zamani anayelindwa na askari na sheria za nchi.

Katika baadhi ya nchi duniani, rais aliyemaliza muda wake huendelea kuitwa rais; hata neno mstaafu halitumiki. Ni heshima ya kudumu. Marais hufa na urais wao hata baada ya kumaliza vipindi vyao vya utawala.

Hayo ni mema unayoishi nayo hadi kuzimuni. Lakini ukilikoroga, umati ukakuona, “aha, ni fulani kama mwingine,” basi utadonolewa kama ndege wadonoavyo hindi.

Taarifa za vyombo vya habari zinasema waliokamatwa walikuwa wakiimba, “Fisadi! Fisadi! Fisadi! (mara tatu) wakati rais mstaafu akipita eneo walikokuwa.

Hakuna maelezo iwapo walikuwa wameelekeza “nyimbo” hizo kwa Mkapa au walikuwa wakiziimba kabla hajafika au walikuwa wakifanya mazoezi kwa ajili ya kusanyiko tofauti.

Lakini katika mazingira ambamo rais mstaafu amekuwa akitajwa kukiuka maadili ya uongozi na amekataa kujitokeza kujibu tuhuma; basi inawezekana, nasema huu ni uwezekano tu, kwamba walikuwa wanapeleka ujumbe.

Ni suala la kusubiri hadi mahakama itoe uamuzi. Hiyo ni kama watashitakiwa.

Na ujumbe huu ni maoni binafsi. Hata kama ulikuwa umemlenga Mkapa, mtu haadhibiwi kwa maoni yake, tena ambayo yamejengeka kwa kipindi kirefu na bila ya kusahihishwa, kurekebishwa, kubadilishwa kwa kauli au vitendo, vya yule anayetuhumiwa.

Hata kutaja majina, ingawa taarifa hazisemi vijana hao walitaja jina la mtu yeyote, hakuna uzito. Katika mazingira huru, na mara hii wakati wa wiki ya uhuru wa kufikiri na kuwa na maoni, tendo la vijana hao linazusha mjadala wa maana kwa ustawi wa uhuru na haki ya kuwa na maoni na kujieleza.

Nchini Venezuela kuna mapambano kama yaliyopo nchini Tanzania. Ni mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi. Na rushwa na ufisadi wa Venezuela umejikita serikalini na katika biashara kubwa.

Vyombo vya habari vya nchi hiyo vimefanya kazi ya kuwataja watuhumiwa na wala rushwa na mafisadi wenyewe. Majina yao yanafahamika. Majina yao yanaimbwa asubuhi, mchana na usiku.

Hapa ndipo mwanzo wa “kochonkocho.” Kaeni ndani ya mgahawa au hoteli. Wakati ukiwa pale, acha aingie mtuhumiwa au yule ambaye amethibitika kuwa mwizi serikalini, katika jeshi au mwanasiasa mkwapuzi. Utashangaa.

Caracas, ambako ni mji mkuu wa nchi hiyo, ndiko kuna vimbwanga. Akiingia fisadi, wale wanaomtambua huanza mara moja mchezo wa kochonkocho. Huanza kugonganisha vijiko, uma na visu.

Ghafla, kila mmoja hustuka na kuuliza kuna nini. Ndipo zogo hukolea. Wengine huanza kugonga glasi, sahani na meza kwa kutumia vijiko, uma au visu.

Mchezo huu, ambao hasa siyo mchezo bali kazi takatifu, hufanywa kwa ustadi, bila kelele nyingine za mdomo na humfanya mtuhumiwa, ambaye ni mlengwa, ama kukaa kimya na “kuzimia kiofisa” au kutoka nje ya mgahawa au hoteli.

Zogo hilo ambalo huanzishwa na wenyeji wa miji husika, huungwa mkono mara moja na wageni katika mahoteli na migahawa ambao huwa wameambiwa kinachoendelea.

Mambo hayaishii hapo. Kuna kindumbwendubwe cha mitaani. Mtuhumiwa wa wizi au mwizi kweli aliyethibitika; mtuhumiwa wa ufisadi au fisadi aliyekubuhu aliyethibitika, hupata wakati mgumu.

Pindi mtuhumiwa au mthibitika anapoonekana mitaani, akina mama hupeana taarifa harakaharaka. Hutoka nje wakiwa na sufuria, madebe, ndoo na vikaango. Kazi huwa moja.

Akina mama hao hugonga vyombo hivyo kwa nguvu. Vyombo vitupu. Hakuna sauti ya mtu. Nkochonkocho ya vyombo hujaa mtaa mmoja; huenea hadi mtaa mwingine; husambaa mitaa mingine ambako mtuhumiwa au mthibitika anapita.

Hatua hiyo ambayo nchini Venezuela inaitwa Cacerolazo, ina shabaha ya kuonyesha kwamba muhusika ni mtu aliyekataliwa na jamii; asiyetakiwa, mwenye kasoro; aliyejaa hitilafu na duni kimaadili.

Huu ni mzigo mkubwa. Ni adhabu ya kijamii. Ni utashi wa jamii iliyochoka matendo ya wizi na ufisadi. Ni kumkataa mtu, familia yake na wote ambao wanatuhumiwa kushirikiana naye katika wizi na ufisadi.

Nchini Venezuela wazomewaji ni pamoja na mawaziri, wakurugenzi na maofisa wa ngazi ya juu serikalini, viongozi wa majeshi, watendaji wa ikulu na rais mwenyewe. Ukitajwa unaandamwa.

Nguvu ya umma ya mtaani ina uwezo mkubwa nchini Venezuela kuliko vyama vya upinzani. Vyama vikiandamana kueleza kutoroshishwa na serikali na vitendo vya ufisadi, wafuasi wa rais hufungulia kila silaha mitaani.

Silaha ambayo hadi sasa ni kubwa katika kukabiliana na wizi, rushwa na ufisadi; angalu inayowanyima usingizi watuhumiwa au wathibitika, ni umma ulioko mitaani; ukitumia vijiko, uma, visu, sufuria, ndoo na vyombo mbalimbali vya nyumbani.

Hii ni kazi moja ya kuzomea na kupeleka ujumbe mfupi wenye maana ndefu, kubwa na pana: Kwamba tayari tunawafahamu. Siku ya kuamua kuwasaka, tujaua mahali pa kuwapata.

Yawezekana Tanzania, na hasa Dar es Salaam na miji mingine inaelekea Caracas, Venezuela. Sauti za uma, vijiko na visu ni sauti za watu.

Sauti za sufuria, vikaango, glasi na sahani, siyo tena za vyombo vinavyovunjikia jikoni. Ni sauti ya umma usio na mahali salama pa kupitishia kauli zake.

Kukomaa kwa wizi na ufisadi kunazaa njia nyingine za mawasiliano za kupambana nao. Leo ni magazeti, televisheni na redio vinavyotangaza. Kesho huenda redio ikazimwa na televisheni ikawa mikononi mwa fisadi na magazeti kuangamizwa kwa ala.

Umma ulio hai mitaani, hata kama una njaa na kero kabakaba, ndio kimbilio la mwisho kuzomea na kusambaza kisirani kwa wezi wakubwa na mafisadi; kuwakosesha raha na kuwaahidi kimbunga cha mwisho ambapo sunami utakuwa mchezo wa ndimu.

Hakuna ajuaye kwa sasa iwapo vijana waliokamatwa walikuwa wakitukana rais mstaafu au walikuwa kwenmye kindumbwendubwe cha kutumia haki na uhuru wao wa kujieleza kusema kilichoko rohoni mwao. Tunasubiri dimba. Kitaeleweka tu.

(Makala hii itatoka katika gazeti la MwanaHALISI toleo la 14 Mei 2008. Mwandishi anapatikana kwa simu: 0713 614872 na imeili: ndimara@yahoo.com)

Thursday, May 8, 2008

Polisi wakigoma itakuwaje?

Polisi wanaogomea serikali

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI askari polisi na askari magereza waanze kufanya maandamano na migomo wakidai serikali iwasikilize na kuwalipa mishahara inayolingana na kazi yao. Sitaki!

Hata Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Khamis Kagasheki ameelezwa kuwa askari nao hawataki kugoma wala kuandamana kama wafanyavyo wafanyakazi wengine wa serikali.

Tatizo hapa ni kama Kagasheki amesikia; na kama amesikia, ameelewa na kama ameelewa, yeye na serikali yake, kama wana nia ya kubadili maisha ya askari polisi na magereza.

Fikiria unaamka asubuhi. Unakutana na msululu wa askari polisi na askari magereza waliobeba mabango. Wanakwenda ama kwa Waziri wa Mambo ya Ndani au Ikulu. Moja ya mabango waliyobeba linasomeka hivi: “Kwa kuwa sisi hatugomi ndio maana hatuongezwi mishahara!”

Kufumba na kufumbua unasoma mabango mengine. Hili linasema, “Tukiamua kugoma nchi itakuwa katika wakati mgumu,” na jingine linasema, “Tukistaafu, kazi pekee ni ukorokoroni.”

Haya ni maandamano, bado mgomo. Je, maandamano haya yameombewa kibali au yametolewa taarifa? Lakini taarifa itolewe wapi wakati wapokea taarifa ndio waandamanaji?

Hawa watu wenye magwanda wameruhusiwa na nani kuingia mitaani? Je, nani analinda waandamanaji? Au mara hii raia wanalinda maandamano ya askari? Hapo ndipo utashangaa. Unaweza kudhani unaota. Nani atamkamata nani na nani atamfunga yupi – polisi na magereza!

Lakini hakuna la kushangaa. Tayari maandamano yameanza. Yameanzia mjini Bukoba. Askari polisi na askari magereza walimwambia Naibu Waziri Mambo ya Ndani, Khamis Kagasheni mapema wiki hii kwamba serikali inapaswa kuboresha mishahara yao.

Mishahara ndiyo inaamua kiasi cha maslahi pale mfanyakazi anapostaafu. Sasa wanasema kutokana na maslahi kiduchu, wanalazimika kufanya kazi za korokoroni “kwenye maduka ya Wahindi,” mara baada ya kustaafu ili kulea familia zao.

Msemaji wa askari hao (tofauti kabisa na Msemaji wa Polisi), alimwambia waziri umuhimu wa serikali kuongeza mishahara yao bila kusubiri migomo kama wafanyakazi wengine.

Ili kuongeza uzito kwenye maelezo yao, msemaji wao aliongeza kuwa askari anafanya kazi kati ya siku 320 na 350 kila mwaka wakati wafanyakazi wengine wanafanya kazi kwa siku 196 (Mwaka moja una siku 365)!

Askari wanalalamika: Hawana nyumba. Hawana mishahara ya maana. Magereza wanatumia gari lililonunuliwa mwaka 1978. Kwa usafiri wako ulimwengu wa 10. Yote hayo yanamwagwa kwenye kikao na naibu waziri alipoamua kusikiliza kero za “usalama wa raia.”

Usalama wa raia utatoka wapi katika mazingira haya? Asiye salama atalindaje maisha ya raia? Kwa udhaifu huu, asiye salama atalindaje mwajiri wake na wabia wake wa ndani na nje?

Asiye na mahali pa kuishi au anayeishi katika kibanda cha ovyo, huku akichekwa na wananchi, kama askari alivyomweleza waziri, atalindaje maisha ya watu, serikali na mali zao?

Lakini hapa kuna mambo muhimu ya kuzingatia. Askari polisi au magereza amevaa sare ya dola – shati na suruali au blausi na sketi. Amevaa kofia yenye nembo ya mwajiri. Amevaa mkanda wenye rangi za taifa. Ni “chombo cha dola” kwa maana zote.

Huyu ndiye askari anayechekwa. Anayezomewa kwa kuwa katika hali mbaya ya maisha. Ndiye anasubiriwa kustaafu ili aanze kazi mpya ya kumlinda mfanyabiashara kwa kuwa hana njia nyingine yoyote ya kuziba pengo pale ambapo mshahara kiduchu uliacha makorongo.

Ni askari huyu anayepaswa kukimbiza wezi waliopora fedha, mikufu, shanga, saa na mali nyingine za raia. Ndiye huyuhuyu anayepaswa kulinda ofisi za serikali hadi ikulu. Ni huyuhuyu anayepaswa kupeleleza wizi wa kawaida na ufisadi uliofanywa na watumishi serikalini. Ataweza?

Mtu aweza kubisha kwamba polisi wa upelelezi wa mambo makubwa wanalipwa mishahara mizuri na wanaishi katika mazingira ya nafuu. Lakini nani asiyejua kwamba polisi wadogo ndio wako karibu sana na vyanzo vya taarifa kuliko walioko ghorofani?

Kuna wakati niliandika juu ya polisi wa laini ya Temeke, jijini Dar es Salaam; jinsi walivyokuwa wakipita madirishani kuingia ndani ya nyumba zao za vigae zinazovuja.

Nakumbuka kuandika juu ya polisi waliokuwa wakiishi katika mabanda yaliyojengwa kwa suti ya mabati matupu. Wakati wote ni jahanamu: Joto likija wanaungua na baridi ikija wanatetemeka kama vifaranga vya kuku.

Niliwahi kuandika juu ya askari walioishi katika mabanda yasiyo na vyumba kiasi kwamba pazia ndiyo ilitenganisha familia moja na nyingine. Nakumbuka sana.

Hili la Bukoba limenikumbusha yote hayo na nina uhakika kwamba Kagasheki atakuwa amepigwa na butwaa. Kama alikuwa anajua hali hiyo tangu zamani, basi alikwenda kukidhi haja ya matembezi ya waziri na kupata angalizo la baadaye kwa rais wake.

Waziri amenukuliwa akisema anasikitishwa na hali wanayokabiliana nayo na kwamba atawasilisha kero zao mahali panapohusika.

Hivi ni wapi huko panapohusika ambako wahusika hawahusiki kwa miaka 47? Na askari polisi na magereza hawawezi kugoma wala kuandamana. Ni “watoto wa nyumbani” kwa mzee.

Walie lita ngapi za machozi; wapige mayowe yaendayo umbali gani au wanyamaze kimya cha mauti na kunyanyasika ndipo waonwe na malaika wa huruma.

Na je, wanastahili huruma au haki yao? Kagasheki ataweza kusimamia hili? Wewe, mimi na askari, tunasubiri kuona mabadiliko.

(Makala hii itachapishwa katika toleo la 11 Mei 2008 la gazeti la Tanzania Daima Jumapili. Mwandishi anapatikana kwa simu: 0713 614872; imeili: ndimara@yahoo.com)

Monday, May 5, 2008

Statement by
Ndimara Tegambwage


Freedom of Expression

THE World Press Freedom Day provides us with an opportunity to restate and reaffirm our stand on Freedom of Expression.

Freedom of expression means a lot to all of us present here and to mankind. It is, among others, freedom to think and generate ideas and views. Freedom to speak out one’s mind. Freedom to seek information. Freedom to share that information with anyone. Freedom to differ, in opinion/views, with anyone including authority.

But in order for freedom of expression to be complete and fully enjoyed, such expression must be uttered, published in the press or broadcast. This means opinion that is not demonstrated in practice, uttered, printed or broadcast, remains as captive as its source. Therefore today is the day to restate our commitment to nurture free speech and to guard the same.

However, today’s event comes at the most opportune time in the history of Tanzania. It comes at a time when revelations have it that a businessman/woman and a government official are pressed cheek to cheek in a corruption tango.

The event comes at a time when the nation is submerged in total bewilderment resulting from massive siphoning of public funds for personal aggrandizement. It comes at a time when those in the upper echelons of leadership are alleged, and others proved, hardcore masterminds of fraudulence, which has milked public coffers dry.

This event therefore, comes at a time of heated discussion and arguments on what should be done to bring back to public coffers, funds stolen from banks and through dubious companies and satanic contracts. Indeed, it is at a time when information is flowing in, from all sides, to tell the story of who stole what, when, with whom; and who did not get his share of the loot of thousands of billions of shillings, enough to cause a halt on borrowing from countries abroad.

This is the time when even the dumb have their voices high on top of mountains; when every information bearer has a contribution to make; when citizens are seeking answers to questions hitherto unasked and demanding for authority’s action.

Fortunately, this is the time when a good number of media outlets have decided never to blink lest they lose the trend of events and stories of untold scandals resulting from grand corruption that has left the economy bleeding profusely.

As a trainer in anti-corruption, I know that if corruption is to be attacked, it must be exposed through giving necessary information and resources to citizens. That is, information supplied must be broad, in full context and bearing public relevance. Such information, does not only stimulate debate and action, but also provides long lasting knowledge on corruption and the way to fight the vice.

It is the work of serious media outlets; indeed of committed reporters, editors, publishers and broadcasters, that can provide the citizenry with authoritative data with which to widen their horizons and enhance their understanding on corruption and how to fight it. Again, it is media that can mercilessly expose authority’s conspiracy in corruption, its complacency and, or inability to tackle corruption, to a point of igniting a dormant giant into action.

Given the circumstances obtaining in the country today, especially the obscenity of money drawn at ease from public coffers; a kind of corruption speedily impoverishing the nation and its people; weakening government and becoming a potential source of conflict, the 3rd May of this year must necessarily leave us with a commitment to make Tanzania “a talking nation.”

A talking nation is an informed nation. It knows what is happening and why. It knows what links business with government and who facilitates corruption and malfeasance. But for the nation, say citizenry, to keep talking, it must
necessarily have the right conduits through which to exercise freedom of expression – media outlets.

Corruption, and especially grand corruption, cannot survive if the public is informed about the nature and extent of abuse of power. Here, the willing media can faithfully provide an avenue through which the entire citizenry can strongly address the leadership; instill fresh thinking, put forward their demands and cause to bring about change for the better.

However, it is unfortunate that Press Freedom Day this year finds some media outlets in the country divided. One part is keenly looking to expose corruption and the other part is avariciously aiding and abetting those who have been found to be grand looters. This is quite an unhealthy situation. As if that was not enough, political thuggery has taken root; attacking editors and media workers of effective media outlets from all corners – verbal threats, court cases, organized hit squads and directives as to how media must do its work. But there is neither slackness nor surrender; at least that is the message already communicated to the world.

As we pledge to remain firm to defend freedom of expression for the betterment of the nation and the entire world citizenry, let’s also pledge to support, in word and deed, all those who have vowed to expose corruption at all costs.

Thank you very much for paying attention as I read this message. I wish you a good observation of World Press Freedom Day this year – 2008.

(The statement was delivered in an imprompt version of Kiswahili at a gathering to commemorate Press Freedom Day on 3rd May 2008 at Courtyard Hotel in Dar es Salaam. The function was organised by the Media Institute of Southern Africa Tanzania Chapter (MISA-Tan), IPP media, UNESCO and UN information Offices in the country. An unofficial traslation into Kiswahili is available in a separate posting)

Ends

UHURU WA KUJIELEZA

Uandishi silaha dhidi ya ufisadi

JUMAMOSI iliyopita, 3 Mei 2008 Taasisi ya Habari Kusini mwa Afrika tawi la Tanzania (MISA-Tan), ikishirikiana na IPP Media, UNESCO, na Ofisi ya Habari ya Umoja wa Mataifa (UN) iliandaa kongamano la wadau katika hoteli ya Courtyard jijini Dar es Salaam, kuadhimisha Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani. Mshauri wa mambo ya habari nchini, NDIMARA TEGAMBWAGE, alitoa salaam zifuatazo ambazo zimetafsiriwa kutoka Kiingereza.

*************************************

SIKU ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani hutupa fursa nyingine ya kurejea na kuthibitisha msimamo wetu kuhusu Uhuru wa Kuwa na Maoni.

Uhuru wa kuwa na maoni una maana pana kwetu sote tulioko hapa na kwa binadamu kwa ujumla. Uhuru wa maoni una maana ya uhuru wa kufikiri na kuzalisha mawazo na maoni. Uhuru wa kusema kilichoko moyoni. Uhuru wa kukusanya/kutafuta habari/taarifa. Uhuru wa kugawana habari hizo na mtu/watu wengine. Uhuru wa kuwa na mawazo/maoni tofauti na mtu mwingine au hata utawala.

Lakini ili uhuru wa kuwa na kutoa maoni uwe kamili na ufurahiwe kikamilifu, sharti maoni hayo, mawazo hayo yatamkwe; yawe hadharani; yachapishwe katika magazeti na kutangazwa katika redio na, au televisheni. Hii ina maana kuwa maoni ambayo hayajawasilishwa kwa njia yoyote ile: kutamkwa, kuchapishwa au kutangazwa, yanabaki utumwani kama aliyo yule aliyeyatoa. Kwa hiyo, leo ni siku ya kuahidi tena kuendeleza msimamo wetu wa kukuza uhuru wa kuwa na maoni na kuulinda.

Hata hivyo, tukio la leo linakuja wakati muwafaka katika historia ya Tanzania. Ni wakati kuna ufunuo kwamba mfanyabiashara na ofisa wa serikali wako bega kwa bega katika “dansa la rushwa.”

Tukio la leo linakuja wakati taifa limezama katika mshangao kutokana na uporaji uliopindukia wa mabilioni ya shilingi kutoka hazina ya umma kwa ajili ya kukidhi matakwa na ulafi wa watu binafsi. Tukio linakuja wakati wale waliopo kwenye ngazi za juu za utawala wanatuhumiwa, na wengine wamethibitika kuwa wabunifu wakuu na wazoefu wa mikondo ya kugushi na wizi ambao umekomba hazina ya umma.

Kwa hiyo, tukio la leo linakuja wakati kuna mijadala mikali na ubishi juu ya kipi kifanyike kurejesha fedha za umma katika hazina; kurejesha fedha zilizokwapuliwa kutoka katika mabenki na nyingine kupitia makampuni bandia na mikataba ya kishetani.

Hakika, huu ni wakati ambapo taarifa zimetamalaki kutoka sehemu mbalimbali, zikieleza nani ameiba nini, lini, wapi na kwa ushirikiano na nani; na nani “alizikwa” (hakupewa mgawo wake) katika kukatiana maelfu ya mabilioni ya shilingi ambazo kwa wingi wake, zingefanya serikali iache ombaomba nchi za nje.

Ni wakati ambapo hata sauti za mabubu zinasikika kwenye vilele vya milima; wakati kila mwenye taarifa ana kitu cha kuchangia katika zogo hili, wakati raia nwanadai majibu kwa maswali ambayo yalikuwa hayajawahi kuulizwa hapo awali na wanataka serikali ichukue hatua.

Bahati nzuri, huu ni wakati ambapo vyombo vingi vya habari vimeamua kutopepeza kope ili visije vikapoteza mkondo wa matukio na taarifa za kashfa zisizomithilika kutokana na rushwa kubwa ambazo zimeacha uchumi wa nchi ukivuja kwa kiwango cha kutisha.

Nikiwa mwalimu katika nyanja ya kupambana na rushwa, ninajua kwamba ili kukabiliana na rushwa, sharti rushwa ianikwe kwa kutoa taarifa muhimu na njia nyingine za uwezeshaji kwa wananchi. Hii ina maana kwamba, taarifa zinazotolewa sharti ziwe pana na kamilifu; na zihusu maisha ya umma. Taarifa kama hizo, siyo tu zinaibua mijadala na kuchukuliwa kwa hatua, bali pia zinatoa elimu ya kudumu juu ya rushwa na njia za kupambana nayo.

Ni wajibu wa vyombo vya habari vilivyo makini, kuwapa raia taarifa na takwimu zisizo na shaka za kuwawezesha kupanua upeo na kuimarisha uelewa wao juu ya rushwa na jinsi ya kuikabili. Aidha, ni vyombo vya habari ambavyo, bila huruma, vinaweza kuanika ushirika wa watawala katika rushwa, uzembe au, na hata udhaifu wao katika kukabiliana na rushwa, hadi kuwatoa usingizini.

Kwa kuzingatia mazingira ya sasa nchini, hasa “uchafu” unaotokana na matumizi ya ovyo ya maelfu ya mabilioni ya shilingi yaliyokwapuliwa kiwepesi kutoka hazina ya umma; aina hii ya rushwa inayofukarisha haraka taifa na watu wake; rushwa inayodhoofisha serikali na kugeuka kuwa chanzo kikubwa cha migogoro, Mei 3 ya mwaka huu sharti ituache na ahadi ya kuifanya Tanzania kuwa “Taifa linaloongea.”

Taifa linaloongea ni taifa lenye taarifa. Linajua kinachotendeka na kwa nini. Linajua kitu gani kunaunganisha wafanyabiashara na maofisa au watawala na nani anasaidia kusimika miliki ya rushwa na ufisadi. Bali kwa taifa, tuseme wananchi wake kuendelea kuongea, sharti viwepo vyombo halisi na huru ambamo watatekelezea na kufurahia uhuru wa kuwa na maoni.

Rushwa na hasa rushwa kubwa, haiwezi kudumu iwapo umma utakuwa umeeleweshwa aina na viwango na matumizi mabaya ya madaraka. Hapa, vyombo vya habari vinaweza kukubali, kwa uaminifu kabisa, kuwa njia ambamo raia wanaweza kupitia ili kuwasiliana na uongozi wa nchi; kuingiza mawazo mapya katika jamii, kuwasilisha matakwa na madai yao na hatimaye kuwezesha kufikiwa kwa mabadiliko bora.

Hata hivyo, ni bahati mbaya kwamba Siku ya Uhuru wa Maoni Duniani mwaka huu imekuta baadhi ya vyombo vya habari vimegawanyika. Sehemu moja inatafuta kwa dhati kuanika rushwa na ufisadi wakati sehemu nyingine inatoa udenda ikitafuta kusaidia wale ambao wamebainika kuwa wakwapuanji wakubwa wa fedha za umma. Hii ni hali mbaya na ya kusikitisha.

Kana kwamba hiyo haitoshi, uhuni wa kisiasa nao umeota mizizi; unatumika kushambulia, kutoka sehemu zote, wahariri na wafanyakazi wa vyombo vya habari ambavyo ni makini – kwa kauli za vitisho, kutishia au kufungua mashitaka mahakamani, kuunda vikundi vya kihuni na vya kupiga na kujeruhi watendaji, na kutoa maelekezo jinsi vyombo vya habari vinapasa kufanya kazi zake.

Pamoja na yote hayo, hakuna kulegea wala kukata tamaa; angalau huo ndio ujumbe ambao tayari umepelekwa kwa walimwengu.

Tunavyoahidi kubaki imara katika kutetea uhuru wa maoni kwa manufaa ya taifa na raia wote wa dunia, basi na tuahidi pia kuunga mkono, kwa kauli na vitendo, wale wote walioapa kuanika rushwa na ufisadi kwa gharama yoyote ile.

Mwisho

Saturday, May 3, 2008

Serikali inayokimbia wajibu wake

Na Ndimara Tegambwage
SITAKI serikali ishindwe kuelewa ujumbe wa wafanyakazi wa Mei Mosi kwamba “Ajira Bora, Maisha bora, Uchumi imara na Maendeleo vinawezekana bila ufisadi.”

Huu ni ujumbe wa makusudi kabisa ambao wafanyakazi wameshona kwenye kaulimbiu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) wakati wa kampeni kwamba “Maisha bora kwa kila Mtanzania yanawezekana.”

Katika hili, hatua ya wafanyakazi siyo ndoto. Ni ukweli unaodhihirishwa na yanayotendeka serikalini. Iweje serikali inunue ndege moja kwa Sh. 40 bilioni na kushindwa kulipa mfanyakazi wake mshahara wa Sh. 150,000 kwa mwezi?

Na ndege yenyewe hairuki. Ikiruka haitui viwanja vya ndani ya nchi kwa kuwa vina vumbi na ikipata vumbi inaugua “mafua.” Ni ndege ya madoido katika nchi za wengine.

Ndege yenyewe ni ghali kuhudumia. Ikitumiwa kwenda Zanzibar sharti iruke hadi Madagascar, ndipo irudi kutua Zanzibar, kwani inapokuwa bado haijakaa sawa angani inakuwa imepita Zanzibar kwa masafa marefu sana.

Ni ndege ambayo ununuzi wake uliambatana na kauli za Waziri wa Fedha wakati huo, Basil Mramba kwamba ndege itanunuliwa hata kama wananchi “watakula nyasi.”

Hiyo ni lugha na mazingira ya rushwa kwa wachombezaji hata kama hadi sasa haijagundulika nani alichukua nini.

Iweje serikali ishindwe kulipa mfanyakazi wake lakini ijiingize katika ununuzi wa rada kwa zaidi ya Sh. 70 bilioni, ununuzi ambao baadaye umegundulika ulihusisha mlungula wa mabilioni ya shilingi?

Iweje serikali iruhusu, ishiriki au izembee uchotaji wa kifisadi wa mabilioni ya shilingi kutoka Benki Kuu (BoT) na ikae kimya hadi inapogunduliwa na wapitanjia, huku mfanyakazi akilia na kusaga meno?

Wanachoshuhudia wafanyakazi ni kusoma takwimu tu: Kampuni ya Kagoda Agriculture Ltd., imechota Sh. 38 bilioni; Meremeta imechotewa Sh. 10 bilioni; Tangold imechotewa Sh. 24 bilioni, Richmond na dada yake Dowans wanachotea zaidi ya Sh. 150 milioni kila siku.

Iweje serikali ishindwe kusitisha mikataba ya kinyonyaji ya makampuni ya umeme ya IPTL, Songas, Agreco, Richmond na sasa Tanpower Resources Limited, ili mfanyakazi wake angalau apate mshara unaoweza kumfikisha katikati ya mwezi?

Kama wazalendo walisimama imara, kushamirisha wananchi na kusitisha utawala wa kikoloni, nani anasema leo hii, kwamba haiwezekani kufuta mikataba ya kishetani inayofyonza mabilioni ya shilingi kila siku?

Wafanyakazi wanauliza kipi kizito: kuondoa ukoloni au kusitisha mikataba ya kinyonyaji ya makampuni ya madini ili “watoto wa taifa” hili waweze kuneemeka?

Ujumbe wa wafanyakazi ni mzito. Wanauliza iweje serikali ikae kimya wakati hazina ya nchi inakamuliwa na watu binafsi na makampuni ya kifisadi ambayo serikali inayajua; halafu wao waishi kwa kupiga mihayo?

Mwaka hadi mwaka, taarifa ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) huonyesha fedha zilizotumiwa vibaya, zilizoibwa, zilizopotea au zisizojulikana ziliko. Ni maelfu ya mabilioni ya shilingi.

Mvujo huo wa fedha za umma huwaacha wafanyakazi wakijiuliza vipi serikali inashindwa kudhibiti matumizi lakini inakuwa makini katika kutoongeza mishahara yao na kutoilipa kwa wakati?

Kinachosikitisha zaidi ni kwamba michango ya wafanyakazi imetumiwa kujenga vitegauchumi vingi na vikubwa vya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ambayo inameremeta kwa wingi wa fedha na ufahari wa miundombinu.

Fedha za mifuko hii hazitoki kuwaondoa wafanyakazi katika dhiki zao. Hata wanapokuwa wanastaafu, bado kuna mshololo mrefu sana wa kupata malipo yao kiasi cha kujuta kwa nini walikuwa katika mpango wa akiba.

Ujumbe wa wafanyakazi unatia moyo. Unaiambia serikali kwamba wafanyakazi wana macho, masikio, akili na hivyo, uwezo wa kufikiri. Wanasema wanajua kinachoendelea.

Ujumbe wa wafanyakazi unaonyesha wameanza kutambua kiini cha wao kupata mishahara kiduchu wakati baadhi ya viongzi wanaogelea katika mabilioni ya shilingi yaliyochotwa kwenye hazina ya umma.

Serikali ina jibu moja ililochonga na kuliweka kabatini. Kila ikiulizwa sawali, basi hulichomoa na kuliweka mezani. Jibu hilo ni, “Serikali haina fedha kwa wakati huu.”

Kila wafanyakazi wanapodai nyongeza ya mshahara, rais, waziri au kiongozi yeyote serikalini huharakisha kuchomoa jibu: “Serikali haina fedha kwa sasa.” Ni jibu lilelile la kizeme ambalo hutumika sana bungeni kila wabunge wanapouliza kwa nini miradi kadhaa haijatekelezwa. Ni jibu la kukimbia wajibu.

Sasa wafanyakazi wameamua kusema wazi: “Ajira Bora, Maisha bora, Uchumi imara na Maendeleo vinawezekana bila ufisadi.”

Ukiangalia mabilioni ya shilingi ambayo imebainika yanachotwa kutoka Hazina na BOT kwenda makampuni ya kifisadi, utaamini kuwa hakika maisha yasingekuwa hivi yalivyo.

Ukiona ripoti ya CAG juu ya hesabu za serikali na fedha ambazo zimetawanyika tu bila maelezo au kwa maelezo finyu lakini yaliyobeba mabilioni ya shilingi, utagundua mengi.

Lakini muhimu zaidi, utagundua kuwa wafanyakazi wa nchi hii wangekuwa na mishahara mizuri kuliko hata wa Botswana ambao mara baada ya kuthibtishwa kazini huruhusiwa moja kwa moja kukopa chombo cha usafiri.

Naafiki kauli ya wafanyakazi ya Mei Mosi. Kwa hiyo serikali ikiendekeza mafisadi itaangamiza wafanyakazi. Lakini ubora uliopo sasa ni kwamba wafanyakazi wameelewa hili na kulitamka bayana. Ujumbe wao umewafikia wengi wenye vilio vya aina hiyo.

Swali moja ni muhimu hapa: Je, wana uwezo wa kusimamia kauli yao ili iwe kitendo? Ikitokea hatutashangaa. Hawatakuwa wa kwanza. Utakuwa mwendelezo unaokubalika.

(Makala hii itachapishwa katika Tanzania daima Jumapili ya tarehe 4 Mei 2008. Mwandishi anapatikana kwa simu: 0713 614872; imeili: ndimara@yahoo.com)

SERIKALI INAYODUMU KWA VISINGIZIO

Na Ndimara Tegambwage

Waziri anayedanganya wananchi

SITAKI Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja apotoshe wananchi au awafiche ukweli. Angalau atambue basi kuwa si wote waliopumbazika au wasio na uwezo wa kufikiri.

Ngeleja anasema kupanda kwa gharama ya umeme nchini kunatokana na hatua ya serikali ya kusitisha ruzuku kwenye nishati hiyo kuanzia mwaka wa fedha 2007/2008 na kuagiza kuwa shirika la umeme (Tanesco) sasa liendeshe.

Tutakwenda hatua kwa hatua. Kwa nini serikali iliamua kuipa ruzuku Tanesco? Ni kwa kuwa iliona gharama ya umeme ilikuwa juu sana kiasi kwamba wananchi wengi wasingemudu kutumia nishati hiyo.

Kwa nini gharama ya umeme imepanda kiasi cha kutisha, kufikia hatua ya serikali kuamua kutoa ruzuku kwa Tanesco ili kukata makali kwa walaji?
Hii ni kutokana na gharama ya uzalishaji umeme kuwa juu.

Kwa nini gharama ya uzalishaji umeme imepanda kiasi cha kufanya watumiaji wake kufikiria kurejea kwenye vibatari? Ni kutokana na serikali kuingia mikataba na “mumiani wa kibiashara” walioamua kufyonza neema yote ya wananchi kwa kulipia umeme peke yake.

Nani alilazimisha serikali kuingia mikataba ya kinyonyaji, kama ule wa IPTL na mingine ya kuzalisha umeme, huku ikijua ni kulifukarisha taifa na kuwafunga wananchi katika utumwa mpya? Ni viongozi wote ikulu na wizarani, waliohusika na ukamilishaji mikataba.

Miongoni mwa washirika wao ni viongozi wa Tanesco, ambao walijua kinachofanyika na athari zake, lakini walilazwa usingizi au walizimwa, kwa njia mbalimbali, ili wasiseme, wasikemee, wasistue taifa bali watulie na kuneemeka wao na waliowapa kazi.

Kwa hali hiyo, waliosuka kitanzi cha gharama ya umeme ni baadhi ya viongozi serikalini. Ukitaka kulielewa hili vizuri, wahusika ni watawala, waliotumia watumishi wao ndani ya serikali na Tanesco.

Kuongezeka kwa gharama ya umeme kulikinzana na kauli na ahadi za watawala za kusambaza nishati hii ili kuliondoa taifa gizani; kuwezesha taifa kuzalisha kwa wingi na kwa njia za kisasa, kufanya maisha kuwa bora na hatimaye kuleta “maendeleo.”

Hapa, maslahi binafsi kwa wote waliokabidhiwa majukumu ya kutawala na kumulikia taifa yalizidi, kwa uzito, maslahi ya umma na ahadi lukuki wakati wa kutafuta ofisi za kisiasa.

Kwa hiyo, uamuzi wa serikali wa kutoa ruzuku kwa Tanesco kwa shabaha ya “kukata makali” ya gharama za umeme kwa mlaji, haukuwa na hauna uhusiano na serikali kuwahurumia wananchi. Hapana!

Huo ulikuwa uamuzi uliotokana na watawala kuona kuwa wameumbuka na wataendelea kuumbuka iwapo hawakuleta chochote cha kupoza, angalau kwa muda tu, makali ya gharama ya umeme kwa mlaji.

Ruzuku ya maana inaweza kutolewa kwa matarajio kwamba juhudi zinazofanywa zitazaa matunda na hali itakuwa nzuri. Ziko wapi juhudi hizo? Kilichopo ni kuendelea kuingia mikataba mipya ya kinyonyaji na kuendelea kumwangamiza mtumiaji wa umeme.

Sasa Waziri Ngeleja anasema Tanesco imekuwa ikipata hasara ya kati ya Sh. 107 bilioni na 189 bilioni kila mwaka tangu 2004 hadi 2007.

Anasema hiyo inatokana na kuuza umeme kwa Sh. 96 kwa yuniti wakati gharama ya kuzalisha na kusambazwa umeme hadi kwa mlaji ni Sh. 164 kwa yuniti moja. Hivyo Tanesco inadaiwa kupata hasara ya Sh. 68 kwa yuniti.

Lakini kinachoitwa hasara ya Tanesco kiliundwa na watawala na Tanesco yenyewe. Ni hawa walioingia mkataba wa IPTL, Songas, Agreco, Richmond na Dowans na TanPower Limited.

Kwa mikataba hii ya kinyonyaji, ambapo mitambo ya makampuni haya, iwe inatoa umeme au imesimama, sharti yalipwe, ndimo Tanesco imekwama kama inzi kwenye mtandao wa buibui.

Ni wazi sasa kwamba Tanesco ina mapato ya Sh. 37 bilioni kila mwezi; lakini malipo kwa makampuni tata ya “kuzalisha umeme” ni Sh. 29 bilioni kila mwezi. Tanesco inabakia na Sh. 8 bilioni tu kila mwezi kwa shughuli zake.

Watawala walioingia mikataba mumiani wanajua unyonyaji huu. Tanesco na wataalam wake wa ufundi na uchumi, wanajua ulafi ulioshonana na biashara ya umeme. Miaka inakuja na kuondoka na hakuna anayebadili mfumo huu unaokamua wananchi.

Mfumo haubadilishwi kwa kuwa miongoni mwa waliopaswa kuubadili au kuufuta kabisa, kuna wanaonufaika na ukwapuaji huu. Na asitokee mtu akadai kuwa hanufaiki au amekashifiwa!

Sasa hatua ya serikali ya kufuta ruzuku, nayo ni ishara ya mchoko; ni ghadhabu tupu – olukana – inayotokana na kugundua kuwa wananchi wameelewa kinachoendelea na watawala “wamekamatwa wakiwa uchi.”

Uchi? Si wachawi, si vichaa. Wameumbuka. Wako tayari kukana sura zao; kila mmoja akisema “siyo mimi,” kumbe ni yeye – yuleyule mfuga nyoka ndani ya chumba cha kulala.

Uwezo wa kuondoa adha ya gharama kubwa za umeme – kuanzia kuunganisha hadi kulipia matumizi – umo mikononi mwa watawala ambao, bahati mbaya, kila kukicha, wanaleta mkataba mpya wa umeme na kampuni ya kinyonyaji.

Hadi hapa Waziri Ngeleja hana budi kujua kuwa umeme siyo ghali. Umeme unafanywa kuwa ghali ili zipatikane fedha za kugharimia miradi ya watoa maamuzi na watia saini kwenye mikataba ya kinyongaji.

Bahati mbaya sana kwa waziri, wananchi tayari wanajua yote haya. Hawakubaliani na kilio chake kinachojaribu kuficha ukweli wa chanzo halisi cha gharama kubwa ya umeme. Ataumbuka.

(Makala hii ilichapishwa katika Tanzania Daima Jumapili ya tarehe 27 Aprili 2008. Mwandishi anapatikana kwa simu: 0713 614872 na imeili: ndimara@yahoo.com)