SITAKI
Na Ndimara Tegambwage
SITAKI mwandishi wa habari anayeficha habari. Huyu ni rafiki yetu wa siku nyingi, Said Nguba ambaye amekuwa mwandishi wa habari wa Waziri Mkuu kwa miaka miwili sasa.
Katikati ya wiki hii, Nguba alinukuliwa na vyombo vya habari akikiri kutoalikwa waandishi wa habari kwenye makabidhiano ya ofisi kati ya Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa na yule wa sasa, Mizengo Pinda.
Eti hakukuwa na habari katika tukio hilo ndio maana hakuita waandishi, lakaini alipeleka picha ya tukio hilo ikionyesha Lowasss ana Pinda wamekumbatiana; tena kwa kicheko cha “pasua mbavu.”
Katika hili, mwandishi mwenzetu Said Nguba ametuonea. Ametuficha “dhahabu ya habari.” Ametunyima fursa kuu katika maisha ya kisiasa. Ametuweka gizani – waandishi, wasomaji, watazamaji na wasikilizaji wa vyombo vya habari.
Kwa ujumla, Nguba ametupokonya haki yetu ya kuwa mashahidi wa tendo la kihistoria. Lakini lisilokubalika hata kidogo ni kile kitendo cha kufanya shughuli za serikali katika kiza nene.
Mawaziri na naibu mawaziri walikabidhiana kwa uwazi kabisa na hotuba zao kutangazwa. Kwa nini waziri mkuu wa zamani anyimwe au akoseshwe fursa ya kusema lolote alitakalo mbele ya kadamnasi anapokuwa anakabidhi ofisi kwa waziri mku mpya?
Inawezekana wahusika wakuu hawakutaka “kuvamiwa” na waandishi wa habari; hivyo waliamuru wasiitwe. Hapo ndipo penye udhaifu.
Waandishi wa habari wanaoteuliwa au wanaopelekwa kufanya kazi serikalini, wakiwa waandishi wa rais, waziri mkuu, makamu wa rais au idara yoyote ile, kama waandishi wengine, wanapaswa kuwa wataalam.
Utaalam wao hauishii kwenye kuandika tu habari za wakubwa zao, bali hata kuwashauri juu ya jinsi ya kusema wanachotaka kukisema, lini kisemwe ili kipate uzito unaostahili; na kisemwe katika mazingira yapi ili kiwe na uzito uliolengwa.
Muhimu zaidi, waandishi hao wa “wakubwa” huwa na kazi nyingine, na labda muhimu kuliko kuandika habari za wakubwa; nayo ni kuelimisha na kushawishi wakubwa zao kuelewa umuhimu wa vyombo vya habari wakati wote.
Hili ni jukumu la kuwatoa kizani watawala, kwa kuwafundisha na kuwafafanulia polepole na hatua kwa hatua, kwamba ofisi zao ni ofisi za umma na kamwe hazipaswi kutenda kizani.
Kwamba kufanya mambo kwa uficho wakati umo katika ofisi ya umma, ni kujiingiza katika vitendo vya ushirikina ambavyo havipaswi kufanyiwa katika ofisi za umma.
Kuelimisha na kushawishi kwamba kwa kuwa macho ya umma ni vyombo vya habari, na kazi zinazotakiwa kufanywa ni za umma, basi vyombo hivyo viitwe wakati wote; viwepo na kushuhudia kila kinachotendeka.
Natumia neno “viitwe” kutokana na kutokuwepo uhuru wa kutosha wa waandishi kutoka vyombo mbalimbali vya habari “kuparamia” ikulu wakati wowote wanapotaka habari.
Tumeona mara kadhaa, ikulu au ofisi ya waziri mkuu, ikibagua waandishi pale kunapokuwa na suala la kueleza wananchi kupitia vyombo vya habari. Ofisi hizi zimeshiriki kujenga “matabaka” ya waandishi kwa matumizi na manufaa ya watawala.
Aidha, hakuna utaratibu wa kuwa na waandishi kutoka vyombo mbalimbali ambao ni wawakilishi wakazi wa ikulu na ambao hudonoa kila kinachodondoka kutoka mdomoni na mikononi mwa watawala.
Inawezekana hatujafikia hatua hiyo kutokana na watawala kuogopa vyombo vya habari au kufanya mambo mengi yaliyo kinyume na yanayotakiwa ofisini; au kutokana na kutojua au uzembe wa washauri kuhusu masuala ya habari pindi wanapoteuliwa.
Lakini, hata baada ya kusema hayo yote, iko wapi nafasi ya mwandishi wa waziri mkuu kusema kwamba “hakukuwa na habari” katika tukio la kukabidhiana ofisi – kati ya Lowassa na Pinda?
Sitaki kumrudisha darasani mwandishi wa waziri mkuu. Kwa hiyo nitasema machache. Kwamba tayari mwandishi wa mkubwa amekuwa mkubwa na anatenda kama “wakubwa” wanavyotenda.
Anaamua na kuwaamulia wengine kwamba hapa kuna habari na pale hakuna habari. Hili ndilo kosa kubwa; ndiyo hujuma kuu ya mwaka huu kwa wananchi, vyombo vya habari na waandishi wa habari.
Kila ninapoingia darasani kufundisha waandishi wa habari wanafunzi, na hata wakongwe, naanza kwa kuwaambia umuhimu wa kuona zaidi ya wengine wanavyoona; kusikia zaidi ya wengine wanavyosikia; na kupaanza sauti kutawanya kilio cha wengi kuliko wengine wanavyofanya.
Hii ina maana moja kuu; nayo ni kwamba siyo kila mmoja ataona jambo lilelile kwa njia ileile na msisitizo uleule. Tuchukue mfano wa makabidhiano ya Lowassa na Pinda.
Wote wataona wawili wakikabidhiana mafaili; wakiwa wamesimama. Wataona wanakumbatiana kama picha ambayo Nguba alituma kwenye vyombo vya habari. Wataona “tabasamu za kisiasa.” Watasikia hotuba za wahusika.
Lakini kuna watakaoona zaidi: Jicho jekundu la mmoja wa wahusika. Kusitasita wakati wa kutoa kauli yake. Chozi lililoning’inia katika jicho la kulia. Mgegemo wa midomo na mashavu. Haraka ya kumaliza tukio.
Si hayo tu. Macho ya huruma ya mmoja wao. Uchangamfu au mdhoofiko. Mashaka. Woga. Aibu. Tabasamu ya kutunga. Ung’avu wa macho na uso kwa ujumla kunakoashiria kupata au kukosa. Mataumaini au kukata tamaa.
Wengine wataona ujasiri usiomithilika machoni mwa wote au mmoja wao. Watatunga yote haya na kuandika habari kwa ujazo unaostahili. Kwa mtazamo wa chombo chao cha habari. Kwa mtindo wa uandishi wautakao. Hiyo ndiyo kazi na utamu wa uandishi.
Kukimbia waandishi wa habari, au kushauriwa kuwaficha tukio kubwa kama la makabidhiano ya ofisi ya waziri mkuu, kwa madai kwamba hakukuwa na habari, ni kuusaliti uandishi wa habari.
Zaidi ya hapo, ni kuendeleza utamaduni wa serikali kufanyia kazi zake gizani. Ukitaka ongeza hili: Ni kukataa kufanya kazi ya kuelimisha watawala juu ya umuhimu wa habari.
(Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa simu: 0713 614872; imeili: ndimara@yahoo.com) Makala itachapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili ya 24Februari 2008)
Saturday, February 23, 2008
Monday, February 11, 2008
WAZIRI MKUU MIZENGO PINDA ATAYAWEZA HAYA?
Na Ndimara Tegambwage
HAKUNA anayetaka kumfundisha kazi waziri mkuu mpya, Mizengo Pinda. Ninachojua ni kwamba amekubali uteuzi na anajua anachotakiwa kufanya. Akiboronga, tunaye!
Bali kuna mambo kadhaa ya kumkumbusha ili ayaweke karibu na orodha ya majukumu yake ya kila siku na hasa baada ya kuthibitika kwa ufisadi katika mkataba kati ya serikali na kampuni ya "kubuni" ya Richmond Development Corporation.
Kwamba waziri mkuu, pamoja na mambo mengine, ahakikishe serikali yake inatambua, inaheshimu na kulinda uhuru wa mtu mmojammoja au vikundi, wa kuwa na maoni tofauti na watawala. Asijiingize katika kutaka tuwe na sare ya fikra.
Kwamba serikali yake itambue na kulinda uhuru wa watu wa kutoa maoni yao bila woga wala aibu, na kwamba serikali ijifunze kuheshimu mawazo ya wananchi, mmojammoja au vikundi, hata kama haina nia ya kuyafanyia kazi.
Kwamba waziri mkuu mpya atambue uhuru wa habari; na katika eneo hili, tusisitize uhuru wa wananchi kupata taarifa na uhuru wa vyombo vya habari kukusanya na kutawanya habari/taarifa bila kushinikizwa kwa njia ya vitisho au hongo za fedha au ahadi za vyeo.
Katika hili, ule mtindo wa kukusanya waandishi wa habari, kuwauliza wataandikaje habari za waziri mkuu na hata kufikia hatua ya kuwaelekeza jinsi ya kumpamba, utokomezwe kabisa na katika nafasi yake ijengeke tabia ya Mizengo Pinda kujiamini na kuacha waandishi na wananchi wamwone Pinda kama anavyoonekana.
Kwamba serikali ina wajibu wa kuchangia elimu pana ya waandishi wa habari. Hii ni elimu katika nyanja mbalimbali na katika taaluma ya habari ambayo itajenga jeuri ya waandishi, kuwaondolea woga na kuwashikisha zana za vita dhidi ya ufisadi.
Kwamba Mizengo Pinda atasimamia, pamoja na mambo mengine, kupatikana kwa jamii inayoongea bila woga wala aibu; inayotunga kidole jichoni mwa viongozi na watawala na kusema, “Hili siyo sahihi.”
Umuhimu wa mazingira huru ya aina hii umedhihirika wakati wa mapambano ya kuthibitisha kuwa mkataba kati ya serikali na Richmond ulighubikwa na upendeleo na vitendo kadhaa vya kifisadi; na kwamba hata waliotarajiwa kulinda maslahi ya umma walizama katika kutafuta maslahi binafsi na kuzamisha zaidi wananchi katika dimbwi la ufukara.
Kwamba waziri mkuu mpya atapokea, kama alivyokwishakiri, mchango maridhawa wa vyombo vya habari katika kupigania haki, uwazi na ukweli; na kushiriki kwa njia ya uwezeshaji – hasa kielimu – wa waliomo katika taaluma ili kulinda ujasiri huo usimomonyoke.
Kwamba, kwa waziri mkuu mpya kutambua umuhimu wa uhuru wa habari na waandishi wa habari, atahakikisha kwamba serikali inaweka mazingira ambamo waandishi wazalendo, wanaopigania ukweli, haki na maslahi ya taifa, hawamwagiwi "tindikali" wala kukatwa mapanga wakiwa katika vyumba vya habari au popote pale kutokana na habari wanazoandika au staili ya uandishi wao.
Kwamba Mizengo Pinda ataheshimu uhuru wa wananchi wa “kujenga mashaka” juu ya mwenendo wa watawala wao; na kwamba ni mashaka hayo yaliyowezesha ufuatiliaji hadi ikagundulika kuwa mkataba kati ya Richmond na serikali ulikuwa kaburi jingine la jasho na damu ya walipakodi wa nchi hii.
Kwamba serikali itaanza kufikiria upya utoaji wa matangazo yake kwa magazeti na vyombo vingine vya habari vya watu binafsi.
Matangazo ni chanzo muhimu cha mapato katika kuendesha vyombo vya habari. Kwa serikali kuvinyima matangazo vyombo binafsi; imekuwa ikivijengea mazingira ya kufa wakati fedha hizo za serikali zinatokana na kodi ya wananchi ambayo ulipaji wake haubagui wananchi kwa misingi ya vyama vya siasa, itikadi wala jinsia.
Kifo cha vyombo vya habari, viwe vya serikali au vya watu na mashirika binafsi, ni kifo cha uhuru wa maoni na uhuru wa kutoa mawazo. Kwani uhuru wa habari na uhuru wa kutoa mawazo hukamilika pale mawazo yanapochapishwa au kutangazwa na kutawanywa.
Kwamba Mizengo Pinda, baada ya kutambua mchango wa kauli za wananchi, waandishi na vyombo vya habari, atakwenda mbele zaidi na kufaya yafuatayo, hasa kuhusu kampuni ya Richmond:
Kwanza, kuhakikisha kuwa serikali inaanzisha mchakato wa kusimamisha mkataba kati yake na kampuni ya Richmond kwa msingi mkuu kwamba wahusika katika kampuni hiyo walisema uwongo na waliingia katika ubia na wananchi ili kukamua uchumi wa nchi hii.
Madai kwamba mkataba ukisitishwa serikali itafikishwa mahakamani, ni kama kumtishia mtu mzima kwa nyau. Woga wa kushitakiwa ni sehemu kubwa ya mkakati wa ufisadi; na serikali haina budi kukataa kutishiwa.
Pili, wananchi wanatarajia kuona waliohusika na ujambazi huu wa kiuchumi wakichukuliwa hatua za kisheria. Hatua hizi ni pamoja na kuwakamata, kuwahoji na kuwafikisha mahakamani kujibu mashitaka ambayo mpaka sasa ni wazi kabisa.
Kinachohitajika hapa pia ni kutaka kurejesha serikalini, fedha zote ambazo serikali iliishaweka kwenye mradi huu unaoendelea kueleweka, kila kukicha, kuwa wa kitapeli.
Hatua nyingine ni kutathmini mali za wote waliohusika katika uchafu huu wa kuangamiza taifa, zinazoshukiwa na, au zilizothibitika kutokana na mradi wa Richmond Development Corporation na kuzitaifisha.
Tatu, kuhakikisha kwamba mapendekezo yote ya Kamati Teule ya Bunge kuhusu kampuni ya Richmond yanatekelezwa. Hili litampa waziri mkuu, heshima mbele ya wananchi, serikali yake na jumuia ya kimataifa.
Nne, waziri mkuu mpya ajifunze kuwa “kikulacho kinguoni mwako.” Kwamba waliobuni au walioshinikiza au waliopendelea kile kinachoitwa kampuni ya Richmond kupata mkataba na serikali ni baadhi ya viongozi serikalini.
Vilevile wanaoongoza Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), iliyosema “hakuna hasara iliyopatikana kwa upande wa serikali” kutokana na kutoa mkataba kwa kampuni ya Richmond, nao ni wateule wa rais.
Hilo la uteule lisiwape kinga. Wananchi wanasubiri kuona, kwamba katika mapambano dhidi ya rushwa, angalau kwa mara ya kwanza, anakamtwa sangara na kukaangwa kwa mafuta yake mwenyewe. Kazi hii Pinda anaiweza.
Kwa msingi huo, kitu muhimu hapa, mbali na sheria za udhibiti, ni kuweka mazingira yatakayohakikisha kwamba mambo yote yanayohusu serikali yanafanywa kwa uwazi na, au yanapohitajiwa na wananchi, yanawekwa wazi.
Sitarajii kuwa haya ni mengi ya kumchosha Mizengo Pinda. Bali wananchi wanaangalia serikali itafanya nini leo kuwadhihirishia kuwa iko makini na inastahili kuendelea kuwatawala.
(Makala hii imeandaliwa kwa ajili ya gazeti la MwanaHALISI toleo la 13 Februari 2008. Mwandishi anapatikana kwa simu: 0713 614872; imeili: ndimara@yahoo.com)
HAKUNA anayetaka kumfundisha kazi waziri mkuu mpya, Mizengo Pinda. Ninachojua ni kwamba amekubali uteuzi na anajua anachotakiwa kufanya. Akiboronga, tunaye!
Bali kuna mambo kadhaa ya kumkumbusha ili ayaweke karibu na orodha ya majukumu yake ya kila siku na hasa baada ya kuthibitika kwa ufisadi katika mkataba kati ya serikali na kampuni ya "kubuni" ya Richmond Development Corporation.
Kwamba waziri mkuu, pamoja na mambo mengine, ahakikishe serikali yake inatambua, inaheshimu na kulinda uhuru wa mtu mmojammoja au vikundi, wa kuwa na maoni tofauti na watawala. Asijiingize katika kutaka tuwe na sare ya fikra.
Kwamba serikali yake itambue na kulinda uhuru wa watu wa kutoa maoni yao bila woga wala aibu, na kwamba serikali ijifunze kuheshimu mawazo ya wananchi, mmojammoja au vikundi, hata kama haina nia ya kuyafanyia kazi.
Kwamba waziri mkuu mpya atambue uhuru wa habari; na katika eneo hili, tusisitize uhuru wa wananchi kupata taarifa na uhuru wa vyombo vya habari kukusanya na kutawanya habari/taarifa bila kushinikizwa kwa njia ya vitisho au hongo za fedha au ahadi za vyeo.
Katika hili, ule mtindo wa kukusanya waandishi wa habari, kuwauliza wataandikaje habari za waziri mkuu na hata kufikia hatua ya kuwaelekeza jinsi ya kumpamba, utokomezwe kabisa na katika nafasi yake ijengeke tabia ya Mizengo Pinda kujiamini na kuacha waandishi na wananchi wamwone Pinda kama anavyoonekana.
Kwamba serikali ina wajibu wa kuchangia elimu pana ya waandishi wa habari. Hii ni elimu katika nyanja mbalimbali na katika taaluma ya habari ambayo itajenga jeuri ya waandishi, kuwaondolea woga na kuwashikisha zana za vita dhidi ya ufisadi.
Kwamba Mizengo Pinda atasimamia, pamoja na mambo mengine, kupatikana kwa jamii inayoongea bila woga wala aibu; inayotunga kidole jichoni mwa viongozi na watawala na kusema, “Hili siyo sahihi.”
Umuhimu wa mazingira huru ya aina hii umedhihirika wakati wa mapambano ya kuthibitisha kuwa mkataba kati ya serikali na Richmond ulighubikwa na upendeleo na vitendo kadhaa vya kifisadi; na kwamba hata waliotarajiwa kulinda maslahi ya umma walizama katika kutafuta maslahi binafsi na kuzamisha zaidi wananchi katika dimbwi la ufukara.
Kwamba waziri mkuu mpya atapokea, kama alivyokwishakiri, mchango maridhawa wa vyombo vya habari katika kupigania haki, uwazi na ukweli; na kushiriki kwa njia ya uwezeshaji – hasa kielimu – wa waliomo katika taaluma ili kulinda ujasiri huo usimomonyoke.
Kwamba, kwa waziri mkuu mpya kutambua umuhimu wa uhuru wa habari na waandishi wa habari, atahakikisha kwamba serikali inaweka mazingira ambamo waandishi wazalendo, wanaopigania ukweli, haki na maslahi ya taifa, hawamwagiwi "tindikali" wala kukatwa mapanga wakiwa katika vyumba vya habari au popote pale kutokana na habari wanazoandika au staili ya uandishi wao.
Kwamba Mizengo Pinda ataheshimu uhuru wa wananchi wa “kujenga mashaka” juu ya mwenendo wa watawala wao; na kwamba ni mashaka hayo yaliyowezesha ufuatiliaji hadi ikagundulika kuwa mkataba kati ya Richmond na serikali ulikuwa kaburi jingine la jasho na damu ya walipakodi wa nchi hii.
Kwamba serikali itaanza kufikiria upya utoaji wa matangazo yake kwa magazeti na vyombo vingine vya habari vya watu binafsi.
Matangazo ni chanzo muhimu cha mapato katika kuendesha vyombo vya habari. Kwa serikali kuvinyima matangazo vyombo binafsi; imekuwa ikivijengea mazingira ya kufa wakati fedha hizo za serikali zinatokana na kodi ya wananchi ambayo ulipaji wake haubagui wananchi kwa misingi ya vyama vya siasa, itikadi wala jinsia.
Kifo cha vyombo vya habari, viwe vya serikali au vya watu na mashirika binafsi, ni kifo cha uhuru wa maoni na uhuru wa kutoa mawazo. Kwani uhuru wa habari na uhuru wa kutoa mawazo hukamilika pale mawazo yanapochapishwa au kutangazwa na kutawanywa.
Kwamba Mizengo Pinda, baada ya kutambua mchango wa kauli za wananchi, waandishi na vyombo vya habari, atakwenda mbele zaidi na kufaya yafuatayo, hasa kuhusu kampuni ya Richmond:
Kwanza, kuhakikisha kuwa serikali inaanzisha mchakato wa kusimamisha mkataba kati yake na kampuni ya Richmond kwa msingi mkuu kwamba wahusika katika kampuni hiyo walisema uwongo na waliingia katika ubia na wananchi ili kukamua uchumi wa nchi hii.
Madai kwamba mkataba ukisitishwa serikali itafikishwa mahakamani, ni kama kumtishia mtu mzima kwa nyau. Woga wa kushitakiwa ni sehemu kubwa ya mkakati wa ufisadi; na serikali haina budi kukataa kutishiwa.
Pili, wananchi wanatarajia kuona waliohusika na ujambazi huu wa kiuchumi wakichukuliwa hatua za kisheria. Hatua hizi ni pamoja na kuwakamata, kuwahoji na kuwafikisha mahakamani kujibu mashitaka ambayo mpaka sasa ni wazi kabisa.
Kinachohitajika hapa pia ni kutaka kurejesha serikalini, fedha zote ambazo serikali iliishaweka kwenye mradi huu unaoendelea kueleweka, kila kukicha, kuwa wa kitapeli.
Hatua nyingine ni kutathmini mali za wote waliohusika katika uchafu huu wa kuangamiza taifa, zinazoshukiwa na, au zilizothibitika kutokana na mradi wa Richmond Development Corporation na kuzitaifisha.
Tatu, kuhakikisha kwamba mapendekezo yote ya Kamati Teule ya Bunge kuhusu kampuni ya Richmond yanatekelezwa. Hili litampa waziri mkuu, heshima mbele ya wananchi, serikali yake na jumuia ya kimataifa.
Nne, waziri mkuu mpya ajifunze kuwa “kikulacho kinguoni mwako.” Kwamba waliobuni au walioshinikiza au waliopendelea kile kinachoitwa kampuni ya Richmond kupata mkataba na serikali ni baadhi ya viongozi serikalini.
Vilevile wanaoongoza Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), iliyosema “hakuna hasara iliyopatikana kwa upande wa serikali” kutokana na kutoa mkataba kwa kampuni ya Richmond, nao ni wateule wa rais.
Hilo la uteule lisiwape kinga. Wananchi wanasubiri kuona, kwamba katika mapambano dhidi ya rushwa, angalau kwa mara ya kwanza, anakamtwa sangara na kukaangwa kwa mafuta yake mwenyewe. Kazi hii Pinda anaiweza.
Kwa msingi huo, kitu muhimu hapa, mbali na sheria za udhibiti, ni kuweka mazingira yatakayohakikisha kwamba mambo yote yanayohusu serikali yanafanywa kwa uwazi na, au yanapohitajiwa na wananchi, yanawekwa wazi.
Sitarajii kuwa haya ni mengi ya kumchosha Mizengo Pinda. Bali wananchi wanaangalia serikali itafanya nini leo kuwadhihirishia kuwa iko makini na inastahili kuendelea kuwatawala.
(Makala hii imeandaliwa kwa ajili ya gazeti la MwanaHALISI toleo la 13 Februari 2008. Mwandishi anapatikana kwa simu: 0713 614872; imeili: ndimara@yahoo.com)
Friday, February 8, 2008
RAIS KIKWETE NA 'WAFANYABIASIASA'
Na Ndimara Tegambwage
RAIS Jakaya Kikwete ametangaza nia ya kuwa na sheria ya “Wafanyabiasiasa.” Hii ni sheria kizibo. Inalenga kuzuia tabia ya “mshika mbili.”
Kama unataka uongozi wa kisiasa, basi ukabidhi biashara yako kwa wadhamini hadi mwisho wa kipindi cha uongozi wako. Kama unataka biashara, usubiri ukomo wa kipindi chako cha uongozi kisiasa ndipo uanze kufukuzia shilingi.
Leo hii serikali yake imejaa hao tunaowaita “wafanyabiasiasa” – wale wanaochanganya biashara na madaraka ya kisiasa kwa wakati mmoja.
Ni hoja nzuri. Lengo ni muafaka, bali uwezekano wa kuziba udenda wa siasa kuvujia kwenye biashara; na kuzuia mtononoko wa tamaa ya biashara kuvujia kwenye siasa, ni mdogo sana.
Katika mazingira ya sasa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambacho Kikwete anaongoza, wafanyabiashara ndio “tajiri wa chama.” Tuseme “wenye fedha” ndio roho ya chama kiuchumi.
Mieleka iliyoendeshwa kwa mabilioni ya shilingi katika chaguzi tatu kuu zilizopita na majigambo ya “ushindi wa kishindo,” vimeingiza taifa katika mashindano ya fedha na siyo siasa kwa misingi ya itikadi, sera na ajenda za maendeleo.
Katika mazingira hayo, mwenye fedha, awe mfanyabiashara wa kweli au “mwizi” aliyethibitika machoni mwa wengi, anaweza kushika uongozi. Kaidi wa kuelewa hili aulize mwananchi mmojammoja.
Nasema wenye fedha kwa kuwa hakuna anayetaka kujua fedha zimetoka wapi. Popote zilikotoka, halali au haramu, zikitawanywa kama njugu, mtawanyaji anashinda uchaguzi na huweza kuambulia madaraka zaidi, kwa mfano uwaziri.
Aliyekuwa na biashara akipata uongozi serikalini anakuza biashara yake; aliyekuwa na fedha akipata uongozi, anaanzisha biashara, kwani chanzo chake cha fedha za awali kinaweza kukauka. Hapa ndipo kuna ugumu wa kazi anayojipa Kikwete.
Rais anasema anataka afanyie marekebisho ile sheria ya maadili ya viongozi ili kuzuia walioko katika uongozi kuendelea kufanya biashara na wanaoingia kwenye uongozi kuanza kufanya biashara.
Kwanza, hadi sasa kauli ya rais ni kauli tu. Inaweza kutumika kwenye mijadala mirefu na isiyoisha. Baadhi ya wanasiasa wanaweza kupendekeza kuwa kuwepo utaratibu wa kutafuta maoni ya wananchi juu ya suala hilo. Miaka inaweza kuja na kupita.
Pili, kauli tu ya rais tayari imezaa “roho mbaya.” Wenzake ambao walikuwa naye katika mbio za kutafuta urais wake, wameanza kusema, “Rais anataka kutusaliti.” Wengine wanasema tayari amewatelekeza.
Miongoni mwa wale ambao aliwateua kushika uongozi serikalini na walioko bungeni, Rais Kikwete anajua nani ana biashara ipi. Anajua nani ana mali au fedha kiwango gani. Zaidi ya yote, anaweza kuwa anajua nani alimchangia kiasi gani.
Aidha, rais anajua ni akina nani wenye kilio kikubwa kuhusiana na biashara, mali au fedha zao. Akiona huruma au akiogopa kuchukua hatua, kwa misingi ya kutotaka kusaliti au kutelekeza “wenzake,” basi atavuta miguu.
Hapo ndipo tutashuhudia mchakato wa kuleta mabadiliko ya sheria ukikawia kuanza; au hata kama utaanza, siyo leo wala kesho; au hata kama utaanza kesho, utakwenda goigoi au vitazaliwa visingizio; hatimaye hoja itazeeka na kufa kabla ya wakati wake.
Hapa Kikwete atalazimika kuamua kati ya mawili: “Kusaliti” agano na wafayabiashara ambao sasa ni wafanyabiasiasa wenye nafasi za utawala au kusaliti umma wa nchi hii unaotarajia utawala usio na doa.
Tatu, Kikwete ameanza kusikia sauti, aghalabu za chinichini, ndani ya chama chake, zinazosuta na kukemea mwenendo wa jeuri ya wafanyabiasiasa, hasa mawaziri na watumishi wengine serikalini. Kutosikiliza sauti hizo kunaweza kumnyang’anya kete muhimu kisiasa.
Nne, rais hajapata shinikizo la kutosha kutoka nje ya chama chake kuhusu umuhimu wa kuondokana na wafanyabiasiasa. Shinikizo hilo linatarajiwa kutoka kwa wafanyabiashara waaminifu, asasi za kijamii na vyama siasa.
Iwapo rais atasubiri kushinikizwa na sehemu hizo za jamii, atakuwa amepoteza fursa mwanana kwa kiongozi wa nchi kuchukua hatua bila kushinikizwa kwa migomo, kauli kali na hata maandamano.
Kwa mfano, mgomo wa aina yake ulioendeshwa na wabunge wa Bunge la Jamhuri mjini Dodoma, wa kukataa kumsikiliza waziri na kukataa kujadili hoja kuhusu umeme, ni moja ya majanga ya kisiasa yawezayo kumpata rais anayeogopa kuasi wafanyabiasiasa.
Tano, inawezekana kabisa rais alikuwa na malengo maalum katika kuwateua wafanyabiashara kuingia serikalini na alikuwa akijua kuwa nafasi zao zitaleta mgongano wa maslahi. Je, sasa malengo hayo yametimizwa?
Lakini rais anaweza kuwa ameemewa na katika hilo anataka kuonyesha kuwa ana mamlaka ya kutenda kile ambacho wananchi wanatarajia kutoka kwake.
Kwa hiyo, shinikizo ndani ya chama chake, malalamiko ya wananchi, mgomo bungeni, utendaji wa mashaka wa watuhumiwa na woga wa kimbunga cha upinzani, vinaweza kumsukuma rais kuchukua hatua.
Bali katika mazingira ya sasa, siyo rahisi marekebisho ya sheria ya maadili peke yake kuwa dawa ya kukabililiana na ufisadi, mgongano wa maslahi na rushwa vitokanavyo na wafanyabiasiasa.
Kwani hata kabla rais hajafanya marekebisho ya sheria, wafanyabiasiasa wanafahamika kuwa na makampuni mengi, biashara nyingi na mali nyingi chini ya majina ya watoto wao, wake/waume zao, ndugu zao na marafiki zao.
Tayari kuna uhusiano wa aina ya kipekee miongoni mwa wafanyabiasiasa. Aliyeko wizara ya nishati aweza kusaidiwa na aliyeko Kilimo, wakati wa Elimu aweza kumwinua aliyeko Tawala za Mikoa na serikali za Mitaa. Ni nikune hapa nitakukuna pale.
Marekebisho ya Kikwete hayawezi kuona hili. Anayeng’olewa kwa ufanyabiasiasa, tayari amejenga mkondo – kuanzia kwa rais, hadi waziri mwenzake, hadi katibu mkuu wa wizara, hadi mbunge ambaye ni mjumbe wa bodi ya wakurugenzi, hadi mtendaji wa kata ambako anataka kipande kikubwa cha ardhi.
Tuchukulie kwamba sheria imeyataja maeneo yote. Hoja mpya inakuja: Nani anafuatilia kuona haya yanatendeka? Mbona hata sheria inayotakiwa kurekebishwa imeshindikana kusimamiwa na imekaa kama kolokoloni mwenye rungu na ambaye pia amelala usingizi wa pono?
Ni kweli Kikwete ameogopesha wengi kwa kauli yake, lakini waliokaribu naye wanajua la kufanya, wakati waliombali naye wanatafuta pa kuanzia.
Sheria ya Kikwete haitafanikiwa hadi watawala wametambua, kuhesimu, kuthamini na kulinda uhuru wa jamii wa kufikiri na kutoa maoni. Huko ndiko chimbuko la taarifa na mamlaka ya kukabiliana na ufisadi.
Ninazungumzia jamii huru inayozungumza bila woga wala aibu. Asasi huru za kijamii zenye uwezo wa kuibua hoja na taarifa. Vyombo huru vya habari vyenye macho, masikio na midomo ya nyongeza; na vyama vya siasa vinavyojua wajibu wake kwa jamii katika maandalizi ya kuleta mabadiliko.
Hapa sharti pia uwe na serikali sikivu. Inayopokea taarifa na kuchukua hatua. Iliyo tayari kukosolewa na kulinda watoa habari. Inayokiri mamlaka ya wananchi.
(Makala hii ilichapishwa katika gazeti la MwanaHALISI toleo la 6 Februari 2008. Mwanndishi anapatikana kwa simu: 0713 614872 na imeili: ndimara@yahoo.com)
RAIS Jakaya Kikwete ametangaza nia ya kuwa na sheria ya “Wafanyabiasiasa.” Hii ni sheria kizibo. Inalenga kuzuia tabia ya “mshika mbili.”
Kama unataka uongozi wa kisiasa, basi ukabidhi biashara yako kwa wadhamini hadi mwisho wa kipindi cha uongozi wako. Kama unataka biashara, usubiri ukomo wa kipindi chako cha uongozi kisiasa ndipo uanze kufukuzia shilingi.
Leo hii serikali yake imejaa hao tunaowaita “wafanyabiasiasa” – wale wanaochanganya biashara na madaraka ya kisiasa kwa wakati mmoja.
Ni hoja nzuri. Lengo ni muafaka, bali uwezekano wa kuziba udenda wa siasa kuvujia kwenye biashara; na kuzuia mtononoko wa tamaa ya biashara kuvujia kwenye siasa, ni mdogo sana.
Katika mazingira ya sasa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambacho Kikwete anaongoza, wafanyabiashara ndio “tajiri wa chama.” Tuseme “wenye fedha” ndio roho ya chama kiuchumi.
Mieleka iliyoendeshwa kwa mabilioni ya shilingi katika chaguzi tatu kuu zilizopita na majigambo ya “ushindi wa kishindo,” vimeingiza taifa katika mashindano ya fedha na siyo siasa kwa misingi ya itikadi, sera na ajenda za maendeleo.
Katika mazingira hayo, mwenye fedha, awe mfanyabiashara wa kweli au “mwizi” aliyethibitika machoni mwa wengi, anaweza kushika uongozi. Kaidi wa kuelewa hili aulize mwananchi mmojammoja.
Nasema wenye fedha kwa kuwa hakuna anayetaka kujua fedha zimetoka wapi. Popote zilikotoka, halali au haramu, zikitawanywa kama njugu, mtawanyaji anashinda uchaguzi na huweza kuambulia madaraka zaidi, kwa mfano uwaziri.
Aliyekuwa na biashara akipata uongozi serikalini anakuza biashara yake; aliyekuwa na fedha akipata uongozi, anaanzisha biashara, kwani chanzo chake cha fedha za awali kinaweza kukauka. Hapa ndipo kuna ugumu wa kazi anayojipa Kikwete.
Rais anasema anataka afanyie marekebisho ile sheria ya maadili ya viongozi ili kuzuia walioko katika uongozi kuendelea kufanya biashara na wanaoingia kwenye uongozi kuanza kufanya biashara.
Kwanza, hadi sasa kauli ya rais ni kauli tu. Inaweza kutumika kwenye mijadala mirefu na isiyoisha. Baadhi ya wanasiasa wanaweza kupendekeza kuwa kuwepo utaratibu wa kutafuta maoni ya wananchi juu ya suala hilo. Miaka inaweza kuja na kupita.
Pili, kauli tu ya rais tayari imezaa “roho mbaya.” Wenzake ambao walikuwa naye katika mbio za kutafuta urais wake, wameanza kusema, “Rais anataka kutusaliti.” Wengine wanasema tayari amewatelekeza.
Miongoni mwa wale ambao aliwateua kushika uongozi serikalini na walioko bungeni, Rais Kikwete anajua nani ana biashara ipi. Anajua nani ana mali au fedha kiwango gani. Zaidi ya yote, anaweza kuwa anajua nani alimchangia kiasi gani.
Aidha, rais anajua ni akina nani wenye kilio kikubwa kuhusiana na biashara, mali au fedha zao. Akiona huruma au akiogopa kuchukua hatua, kwa misingi ya kutotaka kusaliti au kutelekeza “wenzake,” basi atavuta miguu.
Hapo ndipo tutashuhudia mchakato wa kuleta mabadiliko ya sheria ukikawia kuanza; au hata kama utaanza, siyo leo wala kesho; au hata kama utaanza kesho, utakwenda goigoi au vitazaliwa visingizio; hatimaye hoja itazeeka na kufa kabla ya wakati wake.
Hapa Kikwete atalazimika kuamua kati ya mawili: “Kusaliti” agano na wafayabiashara ambao sasa ni wafanyabiasiasa wenye nafasi za utawala au kusaliti umma wa nchi hii unaotarajia utawala usio na doa.
Tatu, Kikwete ameanza kusikia sauti, aghalabu za chinichini, ndani ya chama chake, zinazosuta na kukemea mwenendo wa jeuri ya wafanyabiasiasa, hasa mawaziri na watumishi wengine serikalini. Kutosikiliza sauti hizo kunaweza kumnyang’anya kete muhimu kisiasa.
Nne, rais hajapata shinikizo la kutosha kutoka nje ya chama chake kuhusu umuhimu wa kuondokana na wafanyabiasiasa. Shinikizo hilo linatarajiwa kutoka kwa wafanyabiashara waaminifu, asasi za kijamii na vyama siasa.
Iwapo rais atasubiri kushinikizwa na sehemu hizo za jamii, atakuwa amepoteza fursa mwanana kwa kiongozi wa nchi kuchukua hatua bila kushinikizwa kwa migomo, kauli kali na hata maandamano.
Kwa mfano, mgomo wa aina yake ulioendeshwa na wabunge wa Bunge la Jamhuri mjini Dodoma, wa kukataa kumsikiliza waziri na kukataa kujadili hoja kuhusu umeme, ni moja ya majanga ya kisiasa yawezayo kumpata rais anayeogopa kuasi wafanyabiasiasa.
Tano, inawezekana kabisa rais alikuwa na malengo maalum katika kuwateua wafanyabiashara kuingia serikalini na alikuwa akijua kuwa nafasi zao zitaleta mgongano wa maslahi. Je, sasa malengo hayo yametimizwa?
Lakini rais anaweza kuwa ameemewa na katika hilo anataka kuonyesha kuwa ana mamlaka ya kutenda kile ambacho wananchi wanatarajia kutoka kwake.
Kwa hiyo, shinikizo ndani ya chama chake, malalamiko ya wananchi, mgomo bungeni, utendaji wa mashaka wa watuhumiwa na woga wa kimbunga cha upinzani, vinaweza kumsukuma rais kuchukua hatua.
Bali katika mazingira ya sasa, siyo rahisi marekebisho ya sheria ya maadili peke yake kuwa dawa ya kukabililiana na ufisadi, mgongano wa maslahi na rushwa vitokanavyo na wafanyabiasiasa.
Kwani hata kabla rais hajafanya marekebisho ya sheria, wafanyabiasiasa wanafahamika kuwa na makampuni mengi, biashara nyingi na mali nyingi chini ya majina ya watoto wao, wake/waume zao, ndugu zao na marafiki zao.
Tayari kuna uhusiano wa aina ya kipekee miongoni mwa wafanyabiasiasa. Aliyeko wizara ya nishati aweza kusaidiwa na aliyeko Kilimo, wakati wa Elimu aweza kumwinua aliyeko Tawala za Mikoa na serikali za Mitaa. Ni nikune hapa nitakukuna pale.
Marekebisho ya Kikwete hayawezi kuona hili. Anayeng’olewa kwa ufanyabiasiasa, tayari amejenga mkondo – kuanzia kwa rais, hadi waziri mwenzake, hadi katibu mkuu wa wizara, hadi mbunge ambaye ni mjumbe wa bodi ya wakurugenzi, hadi mtendaji wa kata ambako anataka kipande kikubwa cha ardhi.
Tuchukulie kwamba sheria imeyataja maeneo yote. Hoja mpya inakuja: Nani anafuatilia kuona haya yanatendeka? Mbona hata sheria inayotakiwa kurekebishwa imeshindikana kusimamiwa na imekaa kama kolokoloni mwenye rungu na ambaye pia amelala usingizi wa pono?
Ni kweli Kikwete ameogopesha wengi kwa kauli yake, lakini waliokaribu naye wanajua la kufanya, wakati waliombali naye wanatafuta pa kuanzia.
Sheria ya Kikwete haitafanikiwa hadi watawala wametambua, kuhesimu, kuthamini na kulinda uhuru wa jamii wa kufikiri na kutoa maoni. Huko ndiko chimbuko la taarifa na mamlaka ya kukabiliana na ufisadi.
Ninazungumzia jamii huru inayozungumza bila woga wala aibu. Asasi huru za kijamii zenye uwezo wa kuibua hoja na taarifa. Vyombo huru vya habari vyenye macho, masikio na midomo ya nyongeza; na vyama vya siasa vinavyojua wajibu wake kwa jamii katika maandalizi ya kuleta mabadiliko.
Hapa sharti pia uwe na serikali sikivu. Inayopokea taarifa na kuchukua hatua. Iliyo tayari kukosolewa na kulinda watoa habari. Inayokiri mamlaka ya wananchi.
(Makala hii ilichapishwa katika gazeti la MwanaHALISI toleo la 6 Februari 2008. Mwanndishi anapatikana kwa simu: 0713 614872 na imeili: ndimara@yahoo.com)
Saturday, February 2, 2008
DK. NGASONGWA NA MACHOZI YA PAPA
SITAKI Na Ndimara Tegambwage
SITAKI Dk. Juma Ngasongwa, yule Waziri wa Mipango, Uchumi na Uwezeshaji astuke leo hii kwamba uchumi wa nchi umeshikwa na wawekezaji kutoka nje.
Kwani ushikwe na nani? Kwa miaka kumi sasa
Watanzania wameshuhudia kasi isiyomithilika ya watawala kuuza kila kitu kilichoitwa “mali ya umma” kana kwamba wametumwa kufuta msamiati huo na chochote kile kilichosimamia dhana hiyo.
Damu ya walipakodi na jasho la wananchi wote kwa ujumla, vimechuruzikia katika mabenki, maofisi, mifuko na midomo ya watu binafsi kutoka nje ya nchi.
Hili halikufanyika kwa misingi linganifu ya kibiashara, bali kwa taratibu zinazoonyesha kana kwamba watawala walikuwa wanajiondolea kero. Uuzaji damu na jasho la wananchi uliwekewa kalenda kana kwamba usipofanyika katika kipindi maalum, basi watawala wataadhibiwa.
Ubinafsishaji nchini ulifanyika mithili ya uuzaji nguo kuukuu sokoni au mitaani. Kwa mtindo huo, mashirika na makampuni ya umma – yale mazao ya damu na jasho la wananchi – yakawa kama matambara yawezayo kununuliwa kwa bei yoyote ile iliyotamkwa na mnunuzi, hata kama ni ndogo kukaribia kuwa bure.
Leo hii, Waziri Ngasongwa anasema, “Tulibinafsisha kwa nia njema,” na kuharakisha kuongeza kuwa ubinafsishaji huohuo umefanya watu wa nje, siyo tu kushika bali hata kutawala “uchumi wa nchi.”
Kuuza mali ya umma kwa watu kutoka nje ya nchi, ni kuuza damu na jasho la wananchi. Ni kuuza mali iliyochumwa na wananchi; na mara hii bila kuwashirikisha katika maamuzi.
Kuuza mali ya umma hadi hatua ya kutambua kuwa sasa uchumi wa nchi, kupitia nyanja ya uwekezaji, uko mikononi mwa wageni, ni kuuza nchi na kufanya watawala wetu kubakia na kazi ya kuchunga mali ya wawekezaji.
Ubinafsishaji wa aina ya Tanzania umekuwa wa aina ya kusaidia uporaji wa mali ya umma na raslimali za nchi, kwa kasi ambayo ilikuwa haijawahi kuonekana nchini. Ni ubinafsishaji unaopaswa kujengewa mashaka; kama kweli wahusika walilenga kuneemesha taifa au walitaka kuchuma kwa mkondo huo.
Leo hii Dk. Ngasongwa ndio anakumbuka “wazawa.” Alisema Alhamisi wiki hii kwamba serikali inaandaa mipango ya kuwezesha wananchi wawekezaji ili waweze kushika uchumi wa nchi yao. Alisema hiyo inafanywa kupitia Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC).
Kauli ya Ngasongwa ina maana gani katika mazingira ya sasa? Kwamba serikali ndiyo imezinduka? Kwamba serikali ya sasa inasikitishwa na hatua ya serikali iliyopita ambayo iliuza nchi kwa kasi ya moto wa kiangazi?
Ngasongwa anamsemea nani? Mipango hiyo ipo kweli au anatangaza hisia zake? Je, yawezekana kuna aina ya kujirudi serikalini na kwamba mawaziri sasa waweza kukiri, kutubu na kuomba msamaha?
Katika suala la ubinafsishaji, ilitazamiwa kwamba serikali ingekaa chini na kuangalia jinsi ya kukuza uwezo wa uwekezaji wa ndani kabla ya kuita wawekezaji kutoka nje.
Wawekezaji kutoka nje, wanaokuja kwa kasi tuliyoshuhudia nchini na ambayo waziri anaanza kustukia, wana uwezo wa kuchochea au kuendeleza rushwa, kufinyaza ajira, kulaghai juu ya mapato na hivyo kutolipa kodi kamili au kutolipa kabisa; au kuishia kwenye kulipa mirabaha.
Baya zaidi, wawekezaji wengi wa aina ya wale walioingia Tanzania, na kwa kasi na mfumo walioingilia, waweza kushirikiana na waliowawezesha kuingia, kudumaza na hata kufuta kabisa uwezekano wa kuibuka na kukua kwa uwekezaji wa ndani ambao ungekuwa endelevu na mkombozi wa taifa.
Ni baada ya serikali kuuza makampuni na mashirika ya umma yaliyochangiwa na kila raia kwa njia mbalimbali, ndipo inastuka na kusema kwamba ilisahau wazawa. Ni leo inasema kuwa inataka kuwaandalia mpango chini ya NDC.
Hii ni aibu. Lakini pia ni jinai. Wazawa wamenyang’anywa chao; hicho walichopata kwa damu na jasho lao na kwa pamoja kama taifa. Wameachwa kwenye mwamba wa ufukara na matarajio haba.
Siyo rahisi kuamini kwamba NDC itafanya maajabu. Shirika hili limekuwepo kwa miaka mingi. Ubinafsishaji wa kasi umelikuta na kasi imeisha na kuliacha palepale.
Kama ni kujenga nguvu na uwezo wa Shirika la Taifa la Maendeleo, kwa maana halisi ya jina hilo, uimarishaji wake ndio ungetangulia ubinafsishaji ambao umeweka uchumi mikononi mwa wageni.
Nguvu za uwezeshaji NDC zinatoka wapi wakati mashirika na makampuni ambayo lingesimamia ili yajenge nguvu ya ndani ya nchi ama ni mizoga au yako mikononi mwa wageni?
Sitaki kusema serikali haiwezi kubadili mkondo wake. Nasema imechelewa. Sitaki kusema anayosema waziri hayawezekani. Nasema mazingira ya sasa ni magumu mno kuliko ilivyokuwa na leo hii hakuna cha kusalimisha.
Sitaki kusema wazawa hawawezi kuinuka na kuchukua nafasi yao. Nasema utawala wa sasa hauonekani kuwa na lengo, shabaha na sera hiyo. Uzawa unakuwa mtamu kuimba majukwaani lakini wakati ukiwadia mwekezaji wa nje anakumbatiwa.
Mashirika, makampuni na raslimali nyingine za taifa vimeuzwa kwa watu wa nje. Serikali imekataa au imeshindwa kusaidia wazawa hadi maziwa na asali vyote vimekombwa na wageni.
Tunachoshuhudia ni mamilioni ya Watanzania na watawala wao kuwa katika nyarubanja: wanalima, wanapalilia, wanavuna na kuhifadhi. Wanasubiri mwenye shamba aje kuchukua mazao; labda na kuwaachia bakshishi.
Huo ndio utumwa tuliomo. Ngasongwa anajua hili vema. Je, NDC iliyopuuzwa kwa miaka mingi itaweza?
(Makala hii itachapoishgwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili, 03 Februari 2008. Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa simu: 0713 614872; imeili: ndimara@yahoo.com)
SITAKI Dk. Juma Ngasongwa, yule Waziri wa Mipango, Uchumi na Uwezeshaji astuke leo hii kwamba uchumi wa nchi umeshikwa na wawekezaji kutoka nje.
Kwani ushikwe na nani? Kwa miaka kumi sasa
Watanzania wameshuhudia kasi isiyomithilika ya watawala kuuza kila kitu kilichoitwa “mali ya umma” kana kwamba wametumwa kufuta msamiati huo na chochote kile kilichosimamia dhana hiyo.
Damu ya walipakodi na jasho la wananchi wote kwa ujumla, vimechuruzikia katika mabenki, maofisi, mifuko na midomo ya watu binafsi kutoka nje ya nchi.
Hili halikufanyika kwa misingi linganifu ya kibiashara, bali kwa taratibu zinazoonyesha kana kwamba watawala walikuwa wanajiondolea kero. Uuzaji damu na jasho la wananchi uliwekewa kalenda kana kwamba usipofanyika katika kipindi maalum, basi watawala wataadhibiwa.
Ubinafsishaji nchini ulifanyika mithili ya uuzaji nguo kuukuu sokoni au mitaani. Kwa mtindo huo, mashirika na makampuni ya umma – yale mazao ya damu na jasho la wananchi – yakawa kama matambara yawezayo kununuliwa kwa bei yoyote ile iliyotamkwa na mnunuzi, hata kama ni ndogo kukaribia kuwa bure.
Leo hii, Waziri Ngasongwa anasema, “Tulibinafsisha kwa nia njema,” na kuharakisha kuongeza kuwa ubinafsishaji huohuo umefanya watu wa nje, siyo tu kushika bali hata kutawala “uchumi wa nchi.”
Kuuza mali ya umma kwa watu kutoka nje ya nchi, ni kuuza damu na jasho la wananchi. Ni kuuza mali iliyochumwa na wananchi; na mara hii bila kuwashirikisha katika maamuzi.
Kuuza mali ya umma hadi hatua ya kutambua kuwa sasa uchumi wa nchi, kupitia nyanja ya uwekezaji, uko mikononi mwa wageni, ni kuuza nchi na kufanya watawala wetu kubakia na kazi ya kuchunga mali ya wawekezaji.
Ubinafsishaji wa aina ya Tanzania umekuwa wa aina ya kusaidia uporaji wa mali ya umma na raslimali za nchi, kwa kasi ambayo ilikuwa haijawahi kuonekana nchini. Ni ubinafsishaji unaopaswa kujengewa mashaka; kama kweli wahusika walilenga kuneemesha taifa au walitaka kuchuma kwa mkondo huo.
Leo hii Dk. Ngasongwa ndio anakumbuka “wazawa.” Alisema Alhamisi wiki hii kwamba serikali inaandaa mipango ya kuwezesha wananchi wawekezaji ili waweze kushika uchumi wa nchi yao. Alisema hiyo inafanywa kupitia Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC).
Kauli ya Ngasongwa ina maana gani katika mazingira ya sasa? Kwamba serikali ndiyo imezinduka? Kwamba serikali ya sasa inasikitishwa na hatua ya serikali iliyopita ambayo iliuza nchi kwa kasi ya moto wa kiangazi?
Ngasongwa anamsemea nani? Mipango hiyo ipo kweli au anatangaza hisia zake? Je, yawezekana kuna aina ya kujirudi serikalini na kwamba mawaziri sasa waweza kukiri, kutubu na kuomba msamaha?
Katika suala la ubinafsishaji, ilitazamiwa kwamba serikali ingekaa chini na kuangalia jinsi ya kukuza uwezo wa uwekezaji wa ndani kabla ya kuita wawekezaji kutoka nje.
Wawekezaji kutoka nje, wanaokuja kwa kasi tuliyoshuhudia nchini na ambayo waziri anaanza kustukia, wana uwezo wa kuchochea au kuendeleza rushwa, kufinyaza ajira, kulaghai juu ya mapato na hivyo kutolipa kodi kamili au kutolipa kabisa; au kuishia kwenye kulipa mirabaha.
Baya zaidi, wawekezaji wengi wa aina ya wale walioingia Tanzania, na kwa kasi na mfumo walioingilia, waweza kushirikiana na waliowawezesha kuingia, kudumaza na hata kufuta kabisa uwezekano wa kuibuka na kukua kwa uwekezaji wa ndani ambao ungekuwa endelevu na mkombozi wa taifa.
Ni baada ya serikali kuuza makampuni na mashirika ya umma yaliyochangiwa na kila raia kwa njia mbalimbali, ndipo inastuka na kusema kwamba ilisahau wazawa. Ni leo inasema kuwa inataka kuwaandalia mpango chini ya NDC.
Hii ni aibu. Lakini pia ni jinai. Wazawa wamenyang’anywa chao; hicho walichopata kwa damu na jasho lao na kwa pamoja kama taifa. Wameachwa kwenye mwamba wa ufukara na matarajio haba.
Siyo rahisi kuamini kwamba NDC itafanya maajabu. Shirika hili limekuwepo kwa miaka mingi. Ubinafsishaji wa kasi umelikuta na kasi imeisha na kuliacha palepale.
Kama ni kujenga nguvu na uwezo wa Shirika la Taifa la Maendeleo, kwa maana halisi ya jina hilo, uimarishaji wake ndio ungetangulia ubinafsishaji ambao umeweka uchumi mikononi mwa wageni.
Nguvu za uwezeshaji NDC zinatoka wapi wakati mashirika na makampuni ambayo lingesimamia ili yajenge nguvu ya ndani ya nchi ama ni mizoga au yako mikononi mwa wageni?
Sitaki kusema serikali haiwezi kubadili mkondo wake. Nasema imechelewa. Sitaki kusema anayosema waziri hayawezekani. Nasema mazingira ya sasa ni magumu mno kuliko ilivyokuwa na leo hii hakuna cha kusalimisha.
Sitaki kusema wazawa hawawezi kuinuka na kuchukua nafasi yao. Nasema utawala wa sasa hauonekani kuwa na lengo, shabaha na sera hiyo. Uzawa unakuwa mtamu kuimba majukwaani lakini wakati ukiwadia mwekezaji wa nje anakumbatiwa.
Mashirika, makampuni na raslimali nyingine za taifa vimeuzwa kwa watu wa nje. Serikali imekataa au imeshindwa kusaidia wazawa hadi maziwa na asali vyote vimekombwa na wageni.
Tunachoshuhudia ni mamilioni ya Watanzania na watawala wao kuwa katika nyarubanja: wanalima, wanapalilia, wanavuna na kuhifadhi. Wanasubiri mwenye shamba aje kuchukua mazao; labda na kuwaachia bakshishi.
Huo ndio utumwa tuliomo. Ngasongwa anajua hili vema. Je, NDC iliyopuuzwa kwa miaka mingi itaweza?
(Makala hii itachapoishgwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili, 03 Februari 2008. Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa simu: 0713 614872; imeili: ndimara@yahoo.com)
ULAFI NA TATIZO LA USAFIRI WA WATOTO TANZANIA
SITAKI Na Ndimara Tegambwage
SITAKI kuandika kwa kujirudia lakini ninaolenga kuelimisha wakionyesha kuwa hawajaelimika, nitarudia, kurudia na kurudia. Hivi ndivyo nifanyavyo sasa.
Somo lenyewe ni dogo: Ni usafiri wa wanafunzi katika jiji la Dar es Salaam na miji na majiji mengine. Ni somo lililochukua saa nzima ya kipindi cha Kipima Joto cha Independent Televisheni (ITV), juzi Ijumaa usiku.
Kipindi hiki kilitawaliwa na maswali: Nani anawajibika kusafirisha wanafunzi kwenda na kutoka shuleni na hatua gani zinachukuliwa kumaliza tatizo hilo.
Kipindi kilimalizika kwa msiba mkubwa. Hakuna jibu lililotolewa. Hata Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Ludovick Mwananzela hakuwa na maelezo muwafaka.
Washiriki wote waliogelea katika nauli ya Sh. 50 kwa mwanafunzi kuwa ni kiasi kidogo kisicholeta faida; na umuhimu wa kuwa na kampuni za kusomba wanafunzi peke yao. Huu ni mkasa.
Katika nchi zenye mipango mizuri ya uchumi, na ambamo huduma au biashara ya usafiri na usafirishaji inaitwa “usafiri wa umma,” hakuna msamiati uitwao “mwanafunzi.” Msamiati pekee unaotumika na kuheshimika, ni “abiria.”
Katika mazingira hayo, mwanafunzi ni abiria. Mwanamke ni abiria. Mwanaume ni abiria. Mnene ni abiria. Mwembamba ni abiria. Mfupi ni abiria. Mstaafu ni abiria. Mfanyakazi ni abiria. Mwenye ulemavu wa aina yoyote ile ni abiria.
Lakini katika Tanzania, mwanafunzi siyo abiria. Ni mwanafunzi tu; kitoto cha kusumuka huku na kule; kupiga, kufukuza, kuchania vitabu au ikiwezekana, kuacha vituoni ili kuepuka “hasara.”
Hiyo ndiyo dini ya madereva na makondakta wa mabasi ya daladala na huenda baadhi ya wamiliki wake. Ni: Achana na watoto wa shule, wanaleta hasara kwa kulipa nauli ya shilingi 50.
Na hii ni kutokana na mfumo wa sasa wa umuliki wa mabasi. Kila mwenye fedha ya kununulia basi, kubwa au dogo, ananunua na kuliweka barabarani. Huyu aweza kuwa tajiri mwenye mtaji mkubwa, askari, mfanyakazi, mstaafu, mporaji “aliyetajirika jana,” mjane, yatima au hata aliyeokota fedha jana au aliyeshinda bahati nasibu.
Kila mwenye gari anatafuta kondakta na dereva anayemfahamu na kumkabidhi chombo. Kilichobaki ni kukinga mkono na kupokea mavuno ya barabarani. Basi.
Katika ushindani huu, wafanyakazi wa gari la “tajiri” wanataka nauli kubwa inayokamilisha haraka kiwango walichowekewa na tajiri. Kwa hiyo mwanafunzi anayelipa Sh. 50, ni balaa, ni kero. Kondakta anataka nauli ya mtu mzima.
Kwa kuwa mabasi ya daladala yanaongozwa na kusimamiwa na tabia binafsi ya mmiliki, dereva na kondakta, lazima mwanafunzi atakuwa ukoma au uchuro au kero ya kudumu.
Ni hivi: Kama mabasi ya daladala, au vyovyote vile yatakavyoitwa mabasi yanayotoa huduma ya umma, yangekuwa chini ya usimamizi mmoja, msamiati wa “mwanafunzi” ungekuwa umekufa na kuzikwa zamani.
Mabasi yote yangechomekwa chini ya mamlaka moja; kwa mikataba maalum inayozingatia ubora wa gari, muda wa kutoa huduma chini ya mamlaka na viwango vya mapato kila mwezi, suala la “mwanafunzi” lisingekuwepo.
Kungekuwa na masuala ya kisera na utekelezaji tu, kwamba watoto wa umri fulani hulipa nauli kiasi gani na wakubwa hulipa kiasi gani. Basi. Kwa msingi huo, kusingekuwepo msamiati wa wanafunzi na unyanyasaji tuuonao leo, kwani kuna hata watoto wasioenda shule ambao wanastahili kusafiri.
Kwa maana hiyo, gari likibeba wanafunzi wengi au wachache, haitakuwa ajabu wala hasara; ni basi la mamlaka ya usafirishaji. Aliyebeba watu wazima watupu na aliyebeba watoto kwa bei iliyowekwa kisera, wote wameingiza mapato katika mamlaka hiyohiyo.
Umiliki wa aina hii, wa kampuni moja au mbili; wa ushirika au utawala wa jiji au mji, ndio pekee uwezao kurejesha hadhi na kulinda haki ya watoto wanaokwenda na kutola shuleni au wanaokwenda sehemu yoyote ile.
Katika kipindi cha Kipima Joto, Naibu Waziri alisema kuna mwekezaji mmoja ambaye ameanzisha kampuni ya kusafirisha watoto peke yao kwenda shule na kurudi makwao na kwamba wizara yake imemsaidia katika maeneo kadhaa.
Kampuni hii au mengine yenye lengo kama hilo, hayataondoa tatizo la unyanyapaa wa wanafunzi kwa misingi ya viwango vya nauli.
Kampuni hizo zitakuwa zimelenga kuchuma mahali penye ushindani mdogo lakini zitakuwa zimewatenga wanafunzi na watoto wengine. Je, wasiosoma lakini ni watoto watasafiri vipi?
Niliwahi kuandika kwamba mabasi ya daladala “hayana mwenyewe,” kwa maana ya kutokuwa na utawala wa pamoja. Kila mwenye shughuli huweza kuchomoa gari lake na kwenda zake, huku abiria wakitaabika.
Magari ya daladala yaweza kunufaika na mpango wa kuwa chini ya mamlaka moja; kubeba abiria na siyo “wanafunzi,” na kwa njia hiyo kusitisha unyanyasaji wa watoto. Hii ni iwapo yatakuwa chini ya mamlaka kwa njia ya mikataba.
Faida nyingine ya kuwa chini ya mamlaka ni kwamba magari yakiharibika, mamlaka inayatengeneza; yanapangiwa madereva stadi na makondakta wenye ujuzi; yanalazimika kufuata kanuni na sheria na hivyo kujenga utamaduni bora wa matumizi ya barabara.
Leo hii ni vurugu mechi. Kuendelea na utaratibu huu au ule wa “kusomba wanafunzi peke yao,” ni kuendeleza unyanyapaa wa watoto na wanafunzi. Ni kuvunja haki za binadamu.
(Makala hii ilichapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili, 28 Januari 2008. Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa simu: 0713 614872; imeili: ndimara@yahoo.com)
SITAKI kuandika kwa kujirudia lakini ninaolenga kuelimisha wakionyesha kuwa hawajaelimika, nitarudia, kurudia na kurudia. Hivi ndivyo nifanyavyo sasa.
Somo lenyewe ni dogo: Ni usafiri wa wanafunzi katika jiji la Dar es Salaam na miji na majiji mengine. Ni somo lililochukua saa nzima ya kipindi cha Kipima Joto cha Independent Televisheni (ITV), juzi Ijumaa usiku.
Kipindi hiki kilitawaliwa na maswali: Nani anawajibika kusafirisha wanafunzi kwenda na kutoka shuleni na hatua gani zinachukuliwa kumaliza tatizo hilo.
Kipindi kilimalizika kwa msiba mkubwa. Hakuna jibu lililotolewa. Hata Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Ludovick Mwananzela hakuwa na maelezo muwafaka.
Washiriki wote waliogelea katika nauli ya Sh. 50 kwa mwanafunzi kuwa ni kiasi kidogo kisicholeta faida; na umuhimu wa kuwa na kampuni za kusomba wanafunzi peke yao. Huu ni mkasa.
Katika nchi zenye mipango mizuri ya uchumi, na ambamo huduma au biashara ya usafiri na usafirishaji inaitwa “usafiri wa umma,” hakuna msamiati uitwao “mwanafunzi.” Msamiati pekee unaotumika na kuheshimika, ni “abiria.”
Katika mazingira hayo, mwanafunzi ni abiria. Mwanamke ni abiria. Mwanaume ni abiria. Mnene ni abiria. Mwembamba ni abiria. Mfupi ni abiria. Mstaafu ni abiria. Mfanyakazi ni abiria. Mwenye ulemavu wa aina yoyote ile ni abiria.
Lakini katika Tanzania, mwanafunzi siyo abiria. Ni mwanafunzi tu; kitoto cha kusumuka huku na kule; kupiga, kufukuza, kuchania vitabu au ikiwezekana, kuacha vituoni ili kuepuka “hasara.”
Hiyo ndiyo dini ya madereva na makondakta wa mabasi ya daladala na huenda baadhi ya wamiliki wake. Ni: Achana na watoto wa shule, wanaleta hasara kwa kulipa nauli ya shilingi 50.
Na hii ni kutokana na mfumo wa sasa wa umuliki wa mabasi. Kila mwenye fedha ya kununulia basi, kubwa au dogo, ananunua na kuliweka barabarani. Huyu aweza kuwa tajiri mwenye mtaji mkubwa, askari, mfanyakazi, mstaafu, mporaji “aliyetajirika jana,” mjane, yatima au hata aliyeokota fedha jana au aliyeshinda bahati nasibu.
Kila mwenye gari anatafuta kondakta na dereva anayemfahamu na kumkabidhi chombo. Kilichobaki ni kukinga mkono na kupokea mavuno ya barabarani. Basi.
Katika ushindani huu, wafanyakazi wa gari la “tajiri” wanataka nauli kubwa inayokamilisha haraka kiwango walichowekewa na tajiri. Kwa hiyo mwanafunzi anayelipa Sh. 50, ni balaa, ni kero. Kondakta anataka nauli ya mtu mzima.
Kwa kuwa mabasi ya daladala yanaongozwa na kusimamiwa na tabia binafsi ya mmiliki, dereva na kondakta, lazima mwanafunzi atakuwa ukoma au uchuro au kero ya kudumu.
Ni hivi: Kama mabasi ya daladala, au vyovyote vile yatakavyoitwa mabasi yanayotoa huduma ya umma, yangekuwa chini ya usimamizi mmoja, msamiati wa “mwanafunzi” ungekuwa umekufa na kuzikwa zamani.
Mabasi yote yangechomekwa chini ya mamlaka moja; kwa mikataba maalum inayozingatia ubora wa gari, muda wa kutoa huduma chini ya mamlaka na viwango vya mapato kila mwezi, suala la “mwanafunzi” lisingekuwepo.
Kungekuwa na masuala ya kisera na utekelezaji tu, kwamba watoto wa umri fulani hulipa nauli kiasi gani na wakubwa hulipa kiasi gani. Basi. Kwa msingi huo, kusingekuwepo msamiati wa wanafunzi na unyanyasaji tuuonao leo, kwani kuna hata watoto wasioenda shule ambao wanastahili kusafiri.
Kwa maana hiyo, gari likibeba wanafunzi wengi au wachache, haitakuwa ajabu wala hasara; ni basi la mamlaka ya usafirishaji. Aliyebeba watu wazima watupu na aliyebeba watoto kwa bei iliyowekwa kisera, wote wameingiza mapato katika mamlaka hiyohiyo.
Umiliki wa aina hii, wa kampuni moja au mbili; wa ushirika au utawala wa jiji au mji, ndio pekee uwezao kurejesha hadhi na kulinda haki ya watoto wanaokwenda na kutola shuleni au wanaokwenda sehemu yoyote ile.
Katika kipindi cha Kipima Joto, Naibu Waziri alisema kuna mwekezaji mmoja ambaye ameanzisha kampuni ya kusafirisha watoto peke yao kwenda shule na kurudi makwao na kwamba wizara yake imemsaidia katika maeneo kadhaa.
Kampuni hii au mengine yenye lengo kama hilo, hayataondoa tatizo la unyanyapaa wa wanafunzi kwa misingi ya viwango vya nauli.
Kampuni hizo zitakuwa zimelenga kuchuma mahali penye ushindani mdogo lakini zitakuwa zimewatenga wanafunzi na watoto wengine. Je, wasiosoma lakini ni watoto watasafiri vipi?
Niliwahi kuandika kwamba mabasi ya daladala “hayana mwenyewe,” kwa maana ya kutokuwa na utawala wa pamoja. Kila mwenye shughuli huweza kuchomoa gari lake na kwenda zake, huku abiria wakitaabika.
Magari ya daladala yaweza kunufaika na mpango wa kuwa chini ya mamlaka moja; kubeba abiria na siyo “wanafunzi,” na kwa njia hiyo kusitisha unyanyasaji wa watoto. Hii ni iwapo yatakuwa chini ya mamlaka kwa njia ya mikataba.
Faida nyingine ya kuwa chini ya mamlaka ni kwamba magari yakiharibika, mamlaka inayatengeneza; yanapangiwa madereva stadi na makondakta wenye ujuzi; yanalazimika kufuata kanuni na sheria na hivyo kujenga utamaduni bora wa matumizi ya barabara.
Leo hii ni vurugu mechi. Kuendelea na utaratibu huu au ule wa “kusomba wanafunzi peke yao,” ni kuendeleza unyanyapaa wa watoto na wanafunzi. Ni kuvunja haki za binadamu.
(Makala hii ilichapishwa katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili, 28 Januari 2008. Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa simu: 0713 614872; imeili: ndimara@yahoo.com)