Wednesday, November 28, 2007

UJINGA UNAPOKUWA NGOME

Fasheni ya kukiri ujinga Tanzania

Na Ndimara Tegambwage

KATIKA siasa za Tanzania, kukiri ujinga imekuwa fasheni. Lakini siyo fasheni peke yake. Kukiri ujinga hadharani imekuwa njia ya kueneza ghiliba, kujikosha na kutaka kuhurumiwa.

Waziri Mkuu Edward Lowassa amenukuliwa akisema mjini Morogoro mwishoni mwa wiki iliyopita kwamba serikali haiwajui mafisadi na “vigogo” wauza dawa za kulevya nchini.

Gazeti moja, katika toleo la juzi Jumatatu lilimnukuu Lowassa akisema, “Nasema watajeni na ninaahidi tutawashughulikia bila kujali cheo cha mtu au nafasi aliyonayo katika taifa hili…”

Lowassa amefuata nyayo za Rais Jakaya Kikwete ambaye miezi miwili iliyopita aliwaambia waandishi wa habari akiwa Ufarasa kwamba hajui sababu za Tanzania kuwa masikini wakati ina maliasili na raslimali nyingi.

Hata Kikwete alikuwa akirudia yaliyosemwa na Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye ambaye alinukuliwa akisema, Juni mwaka huu, kwamba kabla ya kupata elimu katika Chuo Kikuu cha Harvard, Marekani, alikuwa hajui kwa nini Tanzania ni nchi masikini.

Katika hili, ujinga wa Kikwete unaweza kulinganishwa na ule wa Sumaye. Kwamba viongozi hawa, pamoja na kuwa serikalini kwa miaka mingi, hawakuweza kupata nyenzo za kuwasaidia kufikiri na kuchambua.

Wamekuwa wakitazama lakini hawaoni. Kuona ni kutambua. Kutambua kunahitaji elimu iliyolenga muhusika kujenga tabia ya kufikiri, kuuliza maswali na kujenga mashaka. Kupita madarasani kwa kukariri bila kufikiri, hakuzai elimu; kunazaa kasuku na makasha.

Sumaye anakiri kuwa elimu imemwondoa katika kiza nene. Hakuweza kujua kwa kuwa alikuwa hajapata elimu ya kumwezesha kufikiri, kuuliza maswali na kudai majibu sahihi na kupembua.

Kikwete bado anashangaa kwa nini nchi bado ni masikini wakati ina utajiri wa maliasili na raslimali nyingi. Bila shaka anahitaji kufumbuliwa macho kwa kuambiwa au kufunzwa kufikiri na kung’ang’aniziwa tabia ya kufikiri kwa kuzingatia mazingira na nyakati.

Lakini hili la Lowassa la kuwataka wananchi wataje mafisadi na vigogo wauza dawa za kulevya, linahitaji zaidi ya darasa la kufikiri.

Lowassa ni mmoja wa wale waliotajwa kwenye orodha ya mafisadi 11. Jina lake linaonekana bila wingu lolote. Naye, kwa miezi mitatu sasa tangu orodha iwekwe hadharani, hajakana kuwa fisadi. Hata serikali haijajitokeza na orodha yake ya mafisadi.

Kilichosikika sana kutoka kwa baadhi ya viongozi serikalini na katika na Chama Cha Mapinduzi (CCM), ni kauli kwamba wanaotaja “mafisadi” sharti wawe na “ushahidi.”

Hii siyo mara ya kwanza kusikia kauli hizo ambazo, bila shaka yoyote, zimelenga kunyamazisha watoa fununu juu ya ufisadi.

Lakini Lowassa anayo orodha. Kila kiongozi wa ngazi ya juu katika serikali ana orodha hiyo. Tatizo ni kwamba karibu wote wanasema, “madai hayo siyo mapya.” Wanaongeza kuwa hayo ni malalamo ya wapinzani.

Hii ina maana gani? Kwamba tuhuma za ufisadi zinazowahusu wao siyo mpya. Kwa hiyo hazipaswi kushughulikiwa. Kwa hiyo wanataka tuhuma mpya dhidi ya watu tofauti na siyo wao!

Mazingira ambamo Lowassa alitolea kauli yake yalikuwa mazuri kwake kukana au kukiri kuwa ni mmoja wa mafisadi. Lolote kati ya hayo, ama lingekuwa ungamo au kanusho ambalo lingepata nguvu ya askofu mpya, Jacob ole Mameo aliyekuwa anatiwa wakfu kuwa Askofu wa Dayosisi ya Morogoro.

Hakufanya hivyo. Hakupata ushauri wa kufanya hivyo. Aliwaambia wananchi, wengi wa madhehebu yake ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), kwamba wampe orodha ya mafisadi na vigogo wa dawa za kulevya.

Kumbe waumini hao na wananchi wengine waliohudhuria ni sehemu ya jamii ambayo tangu Septemba 15 mwaka huu imehubiriwa orodha ya mafisadi ambamo jina la Lowassa linasomeka bila utata.

Tendo la waziri mkuu kujiunga na “klabu” ya viongozi wenye fasheni ya kukana kujua hili au lile kutokana na ama kutokuwa na elimu au kwa ghiliba tu na kutaka kuonewa huruma, halijamshangaza yeyote mjini Morogoro na katika taifa zima.

Kikwete na Lowassa wamekuwa serikalini kwa zaidi ya miaka 20 sasa. Hakuna awezaye kusema hajui kilio cha wananchi juu ya watu wanaofanya ufisadi na kuuza dawa za kulevya, lakini hawakamatwi na kama wakikamatwa hawafikishwi mahakamani.

Na hili halihitaji kuhubiriwa kanisani wala misikitini. Serikali iliyo makini huandaa utaratibu wa kuondoa kero za ufisadi na dawa la kulevya. Huomba wananchi watoe taarifa bila kuwatishia kwa kudai ushahidi.

Baada ya hapo serikali huchukua fursa hiyo, kwa kutumia vyombo vyake, kuchunguza na kupata ushahidi na hatimaye kuwaswaga wahusika mahakamani.

Lakini sivyo ilivyo. Kila anayeingia madarakani anaanza kusema “nipe majina ya mafisadi na wauza dawa za kulevya.” Rais Kikwete amewahi kukiri kupewa orodha ya wauza dawa za kulevya. Kwa nini Lowassa anakataa kutumia orodha hiyo?

Leo hii pia kuna orodha ya mafisadi iliyotolewa hadharani na kuhubiriwa nchi nzima. Rais anayo. Waziri Mkuu na viongozi wengine serikalini wanayo. Kwa nini Lowassa hataki kutumia orodha hiyo na badala yake anadai mpya?

Tayari wananchi wameanza kuelewa kinachoendelea. Kuna kukiri ujinga ambao hakika ni wazi; kwamba muhusika alikuwa hana nyenzo za kutumia kufikiri, kuchambua na kupambanua.

Lakini hata katika hilo, ghiliba ni wazi. Je, muhusika hakuwa na wasaidizi; wataalam wenye uwezo wa kufikiri? Je, kama kweli alikuwa hajui, kwa nini aliendelea au anaendelea kukaa madarakani bila kwanza kujifunza anachopaswa kufanya?

Hapa pia kuna chembe ya rushwa. Kung’ang’ania kuchukua nafasi ya utawala ya ngazi ya juu, kwa kishindo na mbwembwe, wakati hujui unachopaswa kufanya ili kulinda watu na maliasili na raslimali zao, ni rushwa ya aina yake.

Hata hivyo, kuna kukiri ujinga kulikolenga kulegeza mishipa ya fahamu ya wananchi; ili waseme kwa sauti ya unyenyekevu, “Jamani, kumbe hata rais wetu na waziri mkuu nao hawajui hili?

Hili nalo ni sehemu ya ufisadi. Ni njia ya udanganyifu usiomithilika wa kuchota mawazo ya wananchi na kuwafanya wakubaliane na hoja dhaifu, lakini zilizolenga kuwatakasa watawala ili wadumu madarakani.

Hebu soma hili: “Jamani kwa muda mrefu nimekuwa nasikia wanaokamatwa kwa dawa za kulevya na rushwa eti ni watu wadogowadogo huku vigogo wakitazamwa, tatizo ni kuwa mnasema tu vigogo, vigogo, hamuwataji.”

Hivyo ndivyo alivyonukuliwa Lowassa akisema mjini Morogoro. Anasema hawajui mafisadi wala vigogo wa dawa za kulevya na amesikia malamiko “kwa muda mrefu.” Na kwa muda mrefu, yeye na serikali yake
wamechukua hatua gani?

Kuna kila haja ya kuondoa uwezekano wa wananchi kuamua kwamba watawala wote nao ni mafisadi. Kwa kuwa watakuwa wameamini kuwa mafisadi hawawezi kukamata mafisadi, basi watafanya watakavyofanya kwani kukiri ujinga sasa hakuwaondolei adha.

(Makala hii imechapishwa katika gazeti la MwanaHALISI, 28 Novemba 2007)
ndimara@yahoo.com
Simu: 0713 614872

Monday, November 26, 2007

UHURU WA MAWAZO KATIKA KILA NYANJA

Kisumo asivyopenda uhuru wa kufikiri

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI wanasiasa wachovu wabeze maoni ya baadhi ya wanajamii na kuyaita ya “kitoto” kama alivyonukuliwa Peter Kisumo akisema.

Alikuwa akirejea mjadala uliopo sasa iwapo mbunge wa Kigoma Kaskazini Zitto Kabwe awemo kwenye Kamati ya Madini ya watu 12 iliyondwa na Rais Kikwete.

Kwa hali yoyote ile, kauli ya Peter Kisumo ina ushawishi ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambamo yeye ni mkongwe. Lakini ni kauli chafuzi inayolenga kuziba mifereji ya fikra.

Kwanza, kuziba, kuzuia au kuweka ugumu wowote ili watu wasijadili jambo lolote linalohusu maisha yao kijamii, kisiasa, kiuchumi na hata kiimani, ni kuingilia uhuru wao wa mawazo.

Huko ndiko kuvunja haki na uhuru wao wa kuwa na maoni na kutoa maoni hayo hadharani. Na Kisumo amenukuliwa akisema kwamba mjadala huo ni mabishano ya “kitoto.”

Pili, kwa mtu yeyote mwenye nafasi ya Kisumo katika jamii, kudiriki kuita mjadala hai juu ya maisha ya watu na taifa lao, kuwa ni wa “kitoto” ni kuendesha ugaidi kifikra na kutaka kunyamazisha sauti na hoja zinazogongana na zake au chama chake.

Kisumo anataka kusema kwamba kama rais kasema, basi inatosha. Hakuna haja ya kutafakari. Hakuna sababu ya kutofautiana. Hakuna muda wa kuhoji. Hizo ndizo nyakati za “zidumu fikra za mwenyekiti” ambazo huwezi leo hii, kuzitumia hata katika darasa la chekechea.

Mjadala kuhusu Zitto kuwemo au kutokuwemo katika Kamati ya Kikwete ya Madini (KKM) umeibuka wakati muwafaka. Kilichouibua ni ujasiri wa kuhoji na tabia ya kujenga mashaka.
Haitoshi kugegema na kutokwa udenda juu ya tendo la rais kuunda kamati ya kuchunguza mikataba na sheria zinazotawala uchimbaji madini. Haitoshi.

Rais ameunda kamati wakati gani? Katika mazingira yapi? Kufuatia matendo yapi? Chini ya shinikizo lipi na kutoka kwa nani? Kama ni kwa utashi wake binafsi, lini rais aligundua umuhimu wa kamati kama hiyo? Ina maana rais siyo mwepesi wa kutambua maslahi ya nchi yake?

Hayo ni baadhi ya maswali ambayo mwananchi anatafuta majibu yake kupitia mijadala hai; katika magazeti, redio, televisheni, mikutano na semina. Ni maswali yenye kujenga kiungo thabiti kati ya wazo (fikra) na tendo.

Kuna maswali mengine. Nani mwingine aliyeteuliwa kuingia kamati hii? Anatoka wapi? Amekuwa wapi? Tabia yake ni ipi – katika maeneo ya ukweli, uadilifu na uwajibikaji? Amefanya nini maishani mwake hadi sasa kinachompa sifa za kuingia kamati hii?

Hayo pia ni maswali muhimu. Yanalenga kuibua majibu yenye kutaka kuondoa mashaka juu ya kile ambacho rais anataka kamati ifanye. Hata hivyo, ni majibu kwa maswali haya, ambayo yanaweza kuonyesha mwelekeo na hata hatima ya kazi ya kamati.

Bado kuna maswali mengine. Je, mteuliwa ana uhuru wa kufikiri na kutenda au amefungwa kama boya? Je, ikibidi anaweza kutofautiana hata na aliyemteua? Je, mteuliwa anachukulia uteuzi huu kama ajira, asante, njia ya kumlinda aliyemteua au kujikosha nafsi yake kwa machafu aliyowahi kutenda?

Maswali haya yanalenga kuimarisha hoja kuu iliyosababisha kuundwa kwa kamati. Yanatekenya nafsi za watakaofanya kazi na kupembua hata fikra zao ili kuona iwapo kweli watafanya kazi ambayo wananchi wenyewe wanataka kuamini kuwa ni muhimu kwao na nchi yao.

Ni maswali kama haya ambayo yanaweza kukupa majibu juu ya nia safi ya rais katika kuunda kamati; au ni tendo la kukidhi “utetezi” wa nafasi yake dhidi ya shinikizo kutoka pande zote.

Maswali yote haya na mengine ya aina hii, ndiyo yanaunda hoja za mjadala juu ya nani hasa alipaswa kuingia katika kamati inayopewa jukumu kubwa la kuangalia jinsi raslimali za taifa zinavyopaswa kuvunwa kwa maslahi ya wananchi.

Hapa hoja siyo Zitto awemo au asiwemo katika kamati. Hoja kuu ni je, rais ana dhamira ya kweli ya kujua sheria na mikataba inasemaje kuhusu uchimbaji madini? Ni kweli hakujua hayo kwa karibu miaka 20 aliyokuwemo serikalini na je, utaratibu aliotumia ni sahihi?

Kama rais ana dhamira ya kweli, ni watu wa aina gani wanastahili kuwa katika kamati yake ya kutafuta ukweli? Je, waliokwishanufaika na mikataba hiyo, hata kwa hila, bado wana sifa ya kuwa katika kamati hii?

Mjadala huu ni mzuri na mpana. Unalenga kuwa darasa kwa rais, serikali na wananchi. Unapanua wigo wa mawazo na kuambukiza hamu na sharti kuu la kufikiri.

Kuita mjadala huu kuwa ni wa “kitoto” ni kukiri kuwa mtoto katika utu uzima. Na hiyo ni hatari kwa afya ya taifa na watu wake. Sitaki!

(Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa simu: 0713 614872; imeili: ndimara@yahoo.com. Ilichapishwa katika gazeti la Tanzania Daima la 25 Novemba 2007)

Saturday, November 17, 2007

MATATIZO YA USAFIRI WA WANAFUNZI TANZANIA

Nauli, wanafunzi na serikali bubu

Na Ndimara Tegambwage

SITAKI wadau wa usafirishaji abiria Dar es Salaam wafikiri kuwa kila Mtanzania au kila mtu, hana uwezo wa kuona, kusikia wala kufikiri.

Siyo siri kwamba wadau wengi katika tasnia hii, ni wenye magari ya usafirishaji abiria. Hata walioko serikalini, mashirika, kampuni na taasisi za mafunzo; wana magari ya kusafirisha abiria.

Kila pendekezo wanalotoa linalenga kuonyesha kwamba wao wana uchungu sana na wanafunzi na wasafiri mijini; kwamba wao hawapati faida au wanapata hasara; kwamba wao wanajitoa muhanga; kwamba wao ni wema sana isipokuwa “hali ya kiuchumi” inauma sana.

Inapotokea mjadala unaohusu kupanda kwa nauli umetokana na kile wanachoita “utafiti” wa taasisi, tena ya serikali, basi wadau hawa wenye magari hushangilia na kuona kwamba “huu ndio wakati wa mavuno.”

Na ndivyo ilivyokuwa jijini Dar es Salaam, Ijumaa wiki iliyopita. Baada ya kufanya kile kilichoelezwa kuwa mjadala, wadau wengi wameripotiwa kujiridhisha kuwa “hali ya maisha ni ngumu,” kwa hiyo wanafunzi walipe nauli ya Sh. 100 badala ya Sh. 50 za sasa.

Hii ina maana kwamba nauli ya Sh. 100 ndiyo itatoa motisha kwa kondakta na dreva kubeba wanafunzi; tofauti na sasa ambapo wanaachwa vituoni kwa kuwa wanalipa Sh. 50.

Huu ni uzandiki wa hali ya juu. Nani amesema nauli ya mtu mzima itaendelea kuwa Sh. 250 au 300 au 350 wakati wote? Hivi hawa wanaojiita watafiti hufanyia wapi utafiti wao? Vyumbani? Kwenye kompyuta tu?

Nenda kituo cha mabasi cha Mwenge. Nauli hutegemea wakati au muda maalum. Asubuhi inaweza kuwa Sh. 300 kwa safari ya Mwenge kwenda Tegeta. Inakuwa 250/- kati ya saa saba na saa 10. Kuanzia saa 12.30 hadi saa 2 usiku, inapanda na kuwa Sh. 500 au hata 1,000 kwa kichwa.

Hii ni kwa baadhi ya magari madogo. Magari makubwa ambayo yamekatisha njia katika sehemu nyingine, hutoza kati ya Sh. 300 na 500.


Je, kunapokuwa na “mavuno” makubwa kwa njia ya unyang’anyi, mbona bado wanafunzi wanaendelea kunyanyaswa? Asubuhi wanaachwa vituoni kwa kuwa hawana nauli “kubwa.” Jioni wanaachwa kwa kuwa magari yanabeba walio tayari kulipa zaidi ya nauli inayofahamika.

Leo nauli ni Sh. 300 (kituo hadi kituo) na wanafunzi au watoto wanatozwa Sh. 100. Je, nani kasema nauli haitapanda zaidi? Je, nauli kwa wakubwa ikiwa Sh. 500, si wenye mabasi watataka mwanafunzi alipe Sh. 250 au 300, vinginevtyo wataendelea kumwacha kituoni?

Tasnia ya usafirishaji abiria, hasa jijini Dar es Salaam, ni soko holela lisilokuwa na mpangilio maalum. Miongoni mwa wasafirishaji ni mawaziri, makatibu wakuu, watendaji wakuu wengine serikalini, wakurugenzi wa kila ngeli katika mashirika na kampuni.

Humohumo kuna magari ya wafanyabiashara wakubwa, mainjinia, maprofesa wafunza vyuoni, makarani, walimu, watunza hesabu, wajane, polisi wa vyeo vya juu, askari wa ngazi za juu jeshini na yeyote yule aliyewahi kupata fedha, kwa njia yoyote ile, za kununulia gari la abiria.

Kila aliyeweka gari barabarani anataka kupata faida isiyomithilika. Dereva na kondakta wake hawatajali sheria wala kanuni za barabarani. Watajali kasi inayowawezesha kufika waendako haraka na kukusanya kiasi kikubwa cha fedha.

Na hao matajiri – wenye magari – wameyatupa magari yao barabarani na kusubiri mapato mwishoni mwa siku. Lakini sikiliza mjadala wa kondakta na dereva, tena mbele ya abiria.

Dereva atasema, “Nakwambia, huyu hata akinitia kidole jichoni, sitaondoka. Lakini nikija kutoka hapa, tayari nina gari langu mwenyewe.” Kondakta atadakia, “Eh, kama alivyofanya Juma. Sasa ana magari mawili ingawa moja linampa matatizo kidogo.”

Hizo siyo kauli za soga. Wanaambizana ukweli. Wanachuma. Wanatafuta panono. Wanabeba wenye nauli kubwa. Wanaomba kila siku nauli ipande ili waweze kuchuma.

Hivyo kuna wachumaji wa aina mbili katika biashara moja ya gari moja. Mwenye gari anachuma anachopelekewa. Dereva na kondakta wanachuma wanachoweza kusogeza nje ya kile walichoagizwa kuleta. Ni biashara ya ua nikuue. Anayeumia ni abiria.

Hapa ndipo zinaingizwa kauli za kipuuzi, lakini za kimaslahi kwa wanaozitoa, ambao ni baadhi ya viongozi nchini, kwamba ili kuwapunguzia wanafunzi matatizo ya usafiri, waende shule zilizoko karibu na wanapoishi.

Shule ninapoishi haijawahi kutoa mwanafunzi hata mmoja wa kwenda sekondari kwa zaidi ya miaka 15 sasa. Hapo ndipo unaambiwa upeleke mtoto wako. Hapo, kwenye kituo cha kujifunzia umbeya, uvutaji bangi na hata ukabaji!

Jijini Dar es Salaam, kama ilivyo katika baadhi ya sehemu nyingi nchini, kuna shule ambazo huwezi kutamani kuweka mtoto wako, hata kama ni kwa kukulia hapo tu.

Shule hizo ni chafu kwa maana ya ukosefu wa walimu, madarasa, madawati, vitabu, vifaa mbalimbali na kutokuwepo mazingira ya kupata elimu.

Mzazi atapenda kulipa zaidi kwa njia ya nauli, ili mtoto wake asake elimu mbali na nyumbani. Lakini kwa kuwa hakuna mpango mahususi wa usafirishaji jijini, nia na shauku ya kuwapa watoto elimu, inakandamizwa na kudidimizwa; na ulafi wa wenye magari unaneemeshwa usiku na mchana.

Serikali Kuu na serikali ya Dar es Salaam zimekataa kuweka utaratibu muwafaka wa usafirishaji. Zimefanya kila mwenye gari kuliingiza barabarani na kufanya anavotaka.

Serikali hizi zimekataa kuweka magari chini ya usimamizi mmoja wa kampuni, shirika au ushirika ambako magari yatachunguzwa uimara wake, yatawekewa ratiba, yatasimamiwa kitaaluma na madereva na makondakta watakuwa watu wenye ujuzi huo.

Nchi hii ina Vyuo Vikuu, Chuo cha Usafirishaji cha Taifa (NIT), Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra); ina Idara ya Usalama Barabarani na wadau wengine katika tasnia hii.

Kwa hali hiyo, leo kusingekuwa na watendaji serikalini, ambao ni pamoja na Waziri Mkuu, wanaolialia juu ya “tatizo la usafiri wa wanafunzi” au msongamano wa magari barabarani. Kusingekuwa na wanaotoa sababu kiwete kwamba wanafunzi wakilipa nauli ya Sh. 100 tatizo lao la usafiri litaisha.

Serikali ikikubali kila mwenye gari alisajili katika kampuni au ushirika mmoja, na asubiri malipo yake kwa mujibu wa mkataba wake, kile kinachoitwa tatizo la usafiri wa wanafunzi kitaisha.

Magari yatakuwa katika ubora unaotakiwa; ajali zitokanazo na uchakavu zitaisha; uzembe uletao ajali utapungua; heshima kwa abiria itatunzwa; viwango vya nauli vitalindwa; njia za mabasi zitaheshimiwa, utamaduni wa matumizi bora ya barabara utaanzishwa na mwanafunzi atakuwa abiria kama abiria mwingine.

Lakini kwa kuwa serikali kuu na serikali ya Dar es Salaam zinaendeshwa na baadhi ya viongozi wenye maslahi katika uholela wa usafirishaji Dar es salaam, kilio cha watoto na wazazi wao kitaendelea hadi wahusika watakapovuliwa mamlaka na madaraka.

(Mwandishi wa makala hii itakayochapishwa katika Tanzania Daima, Jumapili 18 Novemba 2007, anapatikana kwa simu: 0713 614872, imeili: ndimara@yahoo.com)

Tuesday, November 13, 2007

MAHAKAMA YA KADHI TANZANIA


Kikwete asikimbie hoja

Na Ndimara Tegambwage

RAIS Jakaya Kikwete hataki kuhusishwa na kilichomo katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2005 kuhusiana na Mahakama ya Kadhi nchini.

Anasema chama chake na serikali yake havina sera ya kuwa na mahakama ya kadhi. Aidha, anasema hilo siyo suala lake binafsi.

Mahakama ya kadhi ni kilio cha waislamu nchini kwa miaka mingi sasa; karibu tangu mara baada ya uhuru. Waislamu wamekuwa wakiitaka serikali irejeshe mahakama ya kadhi iliyokuwepo nchini kabla ya uhuru na muda mfupi baada ya uhuru.

Kwa ufupi, mahakama ya kadhi hushughulikia mambo ambayo yanahusiana na imani na taratibu za madhehebu ya kiislamu. Kupeleka mambo hayo mbele ya mahakama ya sheria za nchi, hufikirika kuwa muhali.

Kwa upande mwingine, kumekuwa na hoja kwamba mahakama ambayo ni moja ya nguzo za dola, inakidhi matakwa ya watu wa imani zote, kwani katiba ya nchi haina madhehebu wala dini.

Katika hili, hakuna mwanzilishi wa jana au juzi wa madai ya mahakama ya kadhi. Ni maombi, matakwa na shinikizo la kisirisiri na la wazi, la muda mrefu. Linaibuliwa leo kutokana na kujitokeza kwa hoja ya “kushughulikia suala la mahakama ya kadhi” katika Ilani ya CCM ya mwaka 2005.

Hii ilikuwa mbinu ya kisiasa ya kukumbia kura za walioamini kuwa mahakama ya kadhi ni muhimu na ingekidhi kiu yao.

Sasa Rais Kikwete anakana kusimamia kifungu hicho katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM. Anadiriki kusema kwamba hakushirikishwa kuandika ilani.

Hakuna anayesema mahakama ya kadhi ni sera ya CCM au serikali. Bali yaliyomo kwenye ilani ni matakwa ya CCM ambayo huweza kutungiwa sera pindi uamuzi wa utekelezaji wake unapokuwa umechukuliwa.

Rais Kikwete hastahili kukimbia ilani ya chama chake. Hata kama hakushiriki kuiandika; huo ndio ukweli au ghiliba ya chama chake. Hayo ndiyo mahubiri yaliyosambazwa kumtafutia urais na akaupata.

Sasa kama Kikwete anasema hakuandika ilani ya uchaguzi ya CCM, wakati kila kukicha anasema nchi nzima inatekeleza ilani ya chama kilichoko madarakani, ni ilani ipi itekelezwe na ipi itelekezwe?

Kauli ya rais ni ya kukwepa wajibu; na kwa kauli hiyo pekee, anapaswa kuadabishwa na chama chake. Atakana mangapi katika ilani hiyo?

Ameishayavulia. Sharti ayaoge.

(Makala hii itachapishwa katika gazeti la MwanaHALISI la Jumatano, 14 Novemba 2007)