Friday, September 28, 2007

Tabloid under fire of political misile in Tanzania

Hali Halisi Publishers Limited

The new war against
freedom of information

PRESS RELEASE
27th September 2007

MwanaHALISI, a weekly tabloid published by Hali Halisi Publishers Limited (HHP) of Dar es Salaam, Tanzania, has information about a conspiracy, by individuals and groups, to suffocate and kill the citizens’ freedom to seek and receive information.

There is an underground movement by individuals and groups, currently sowing fear among media outlets, especially MwanaHALISI, its publishers, printers, editors, reporters, correspondents and individual private contributors.

Such machinations against MwanaHALISI, are not new. For nearly a year now, there have been threats through a number of ways, including attack letters from either the government or individual citizens, threatening to arraign us in court for our style of reporting and analysis. We have managed to arrest their desires by our continued reporting of truth and by categorically stating that we unwaveringly stand by our style and reports.

But since last week, especially after a loose-cooperation of opposition political parties released a list of eleven alleged corrupt individuals in public office, conspiracies to wipe out the people’s outlet have been more distinct.

The alleged corrupt persons in public office include the current president Jakaya Kikwete and former president Benjamin Mkapa. Others are Premier Edward Lowassa, Governor of the Central Bank Daudi Balali, ruling Chama Cha Mapinduzi (CCM) party’s national treasurer Rostam Aziz, government ministers Andrew Chenge, Basil Mramba and Nazir Karamagi. Also alleged are principal secretaries Gray Mgonja and Patrick Rutabanzibwa and lawyer-m businessman cum member of parliament, Nimrod Mkono.

Simply because our newspaper did its professional duty; that of making public all names of alleged corrupt leaders and their position in the malfeasance, just as they were read out at a public rally at a Dar es Salaam suburb, now everyone who wants to discount the allegations does it in widely publicized manner and concludes by promising to go to court to sue, among others, MwanaHALISI, and our printers, Printech.

A series of vows, real or empty threats, to sue the outlet and its printers – for alleged defamation – is a new, calculated move to sow fear among publishers, printers and journalists. The move is intended to mar interest and initiative in continued exposure as more information on the alleged malfeasance unfolds and spill faster.

It is very unfortunate that the detractors fail to appreciate the fact that it is this very vehicle – MwanaHALISI – which is poised to report correctly, fairly and truthfully on findings about the allegations. To have this outlet smashed is, indeed a calamitous grieve to them and society as a whole.

It’s a relief that advocate Nimrod Mkono has said he would not sue MwanaHALISI because the outlet has no money to pay him. Here, he has put himself on the side of the winner of the case well before he goes to court. But the truth is that we indeed do not have money to give to the opulent. The only money we have is already planned for promotion of people’s freedoms and right to information.

The fastest way to kill an information medium, and here I am referring to MwanaHALISI, is to build blocks along its way to a printing press.

Already the management at Printech has been threatened in two ways: First, by being told blatantly that the press will be “ordered” to close because of their insistence on printing MwanaHALISI. Secondly, it is through threats to sue them in court for defamation. MwanaHALISI is also under the same threats.

There are two important points to observe as regards to this issue: First, Printech is not a government printing press nor does it belong to those facing allegation of corruption. This is an independent private company. It uses printing machines donated for one major purpose: To promote media development in Tanzania and Africa.

Second, it is not secret that such printing presses have been donated to, and are in operation in, Zambia, Lesotho, Botswana and Zimbabwe. Plans are underway to have the same machines installed in Mozambique for the same purpose.

This important project for the development of media aims to give capacity to up-coming publishers with the clear view of promoting democratic values and freedom of the press. The project is under SAMDEF – Southern Africa Media Development Fund with its headquarters in Botswana.

To this effect, this is not a project whose management can very easily be twisted and threatened by anybody who wants to do so. We print with Printech because we value the assistance of those who value freedom and quality of information and media as a whole.

Donors to Printech, who include George Soros, founder of Open Society Institute (OSI), with branches all over the world, will be struck with astonishment to see this country wants to ditch this grand assistance through Printech; the assistance whose main objective is to bring about development for the entire citizenry.

At MwanaHALISI we try hard to report and strictly record what society and its people say, how they say what they say, how they are addressed and how the communicators were heard and even interpreted by audiences. And in this, we don’t find any unpleasantness, fault or criminality. Indeed, herein we find pride and pleasure.

It is our ardent hope that management at Printech will not shift its stand and that it will perform its duty without fear or favour.

We have a contract with Printech. We are guided by the principle that views expressed in the outlet are not necessarily those of the printer. If that principle is adhered to, and at the same time MwanaHALISI adheres to professionalism, truth and faithfulness, none will derail us from our objectives.

I have been heartened by a statement by the General Manager of Printech which was communicated to MwanaHALISI on 26/09/2007 pertaining to threats resulting from the continued printing of our newspaper. He has said he will never back down on threats in the execution of his responsibility.

However, this remains a big war between the two parties: Those who want to suppress information about them, more especially when they are and remain in public offices, on one hand; and those sworn recorders of all that is said so that wananchi get to read, understand, analyze and decide on information given, on the other. In this, when supported by communities, we shall definitely win the war. Our message to everyone is that, we don’t want your communication vehicle smashed to debris.

Saed Kubenea
Managing Director

Distribution list:
- General Manager, Printech
- Executive Officer, SAMDEF – Botswana
- Director, MAELEZO
- Media Council of Tanzania
- MISA-Tanzania
- Media institutions
- Diplomatic Missions
- NGOs, CSOs, CBOs

Thursday, September 27, 2007

VYOMBO VICHACHE VYA HABARI VINAJARIBU

KAULI YA BALOZI WA MAREKANI

Balozi wa Marekani nchini Tanzania, Mark Green, amemwambia mwandishi wa gazeti la Tanzania Daima (27 Sept. 2007), Peter Nyanje, kuwa kuibuliwa kwa tuhuma za ufisadi kumethibitissha ni jinsi gani vyombo vya habari vya Tanzania vilivyo na uwezo na uhuru wa kufuatilia na kuripoti masuala ya ubadhilifu wa mali ya umma kwa uwazi.

“Kuna baadhi ya nchi ambako vyombo vua habari haviwezi kuripoti kama ambavyo inafanyika hapa Tanzania sasa. Katika nchi kama hizo, unaweza ukadhani hakuna rushwa, wakati ukweli ni kwamba ipo, ingawa vyombo vya habari havifichui hali hiyo,” Balozi amenukuliwa akisema.

Amesema, “Hapa inaonekana kuwa vyombo vya habari na waandishi wa habari wana nguvu za kutosha kusema mambo haya…” amesema balozi.

Mwandishi amemnukuu balozi akisema kwamba tuhuma za ufisadi zisigeuzwe kuwa uhasama “kati ya waliozitoa na waliotuhumiwa.”

UHURU WA HABARI KITANZINI

Hali Halisi Publishers Limited

VITA VIPYA VYA KUUA UHURU WA HABARI

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
27 Septemba 2007

MwanaHALISI, gazeti linalochapishwa na Hali Halisi Publishers Ltd., lina taarifa juu ya kuwepo njama, za mtu mmojammoja na, au makundi, za kuangamiza uhuru wa wananchi wa Tanzania wa kutoa na kupokea habari.

Kuna mienendo ya chinichini, ya kusambaza vitisho kwa vyombo vya habari, hususan MwanaHALISI, wachapishaji wake, wahariri, waandishi na wachangiaji makala na taarifa mbalimbali.

Kwa MwanaHALISI, hilo halikuanza jana. Kwa karibu mwaka mmoja sasa kumekuwa na vitisho kwa njia ya barua za kutukemea, ama kutoka serikalini au kwa watu binafsi, ambao wamekuwa wakitishia kutupeleka mahakamani. Hao tumekabiliana nao kwa kuendelea kuandika ukweli na kutamka kwamba tunashikilia kile tulichoandika na bila kutetereka.

Lakini tangu wiki iliyopita, hasa baada ya vyama vya upinzani kutuhumu viongozi 11 kushiriki ufisadi, njama za kutaka kuangamiza “mdomo” wa wananchi zimekuwa wazi zaidi.

Kwa kuwa gazeti hili lilifanya kazi yake kitaaluma, ile ya kutaja majina ya watuhumiwa wote kwa majina na tuhuma zao kama zilivyowasilishwa na upinzani, sasa karibu kila mmoja anayetaka kujikosha au “kujitetea,” anatishia kushitaki aliyesoma majina hadharani (Dk. Willibrod Slaa), gazeti la wananchi la MwanaHALISI na kampuni ya uchapaji ya Printech.

Mlolongo wa ahadi, na huenda azma, za kweli au za kutishia tu gazeti na wachapishaji wake, ni njia mpya ya kutaka ujengeke woga miongoni mwa wachapishaji na wachapaji, ili kadri mambo yanavyoendelea kufumuka, pasiwepo wa kuyaweka wazi kama tuhuma zilivyowekwa wazi.

Hawa wanashindwa kuelewa kwamba ni chombo hikihiki ambacho kitaandika ukweli mweupe pale madai yatakapokuwa yamethibitika au yamekanushwa. Kukipoteza chombo hiki ni msiba mkubwa kwao na jamii; lakini bahati mbaya hawajui.

Afadhali wakili Nimrod Mkono amesema hatashitaki MwanaHALISI kwa kuwa hatuna fedha za kumlipa. Hapa yeye aliishajiamulia kushinda na sisi kushindwa hata kabla hajaenda mahakamani. Lakini ukweli unabaki palepale, kwamba hatuna fedha za kuwapa wenye fedha. Fedha tulizonazo ni kwa ajili ya kuendeleza haki na uhuru wa wananchi wa kupata habari.

Hatua ya haraka ambayo inaweza kuzima uhuru wa chombo cha habari, na katika hili najadili MwanaHALISI, ni kuliwekea gazeti pingamizi ili lisichapwe.

Tayari uongozi wa Printech umepokea vitisho kwa njia mbili: Njia ya kwanza ni kuambiwa moja kwa moja kwamba kiwanda chao kitafungwa. Njia ya pili ni kutishiwa kushitakiwa mahakamani. Yote hayo mawili yanaikabili pia MwanaHALISI.

Kuna mambo mawili muhimu katika kuangalia hali hii: Kwanza, Printech siyo kiwanda cha serikali wala cha watuhumiwa. Ni kampuni inayojitegemea. Imepewa na wafadhili mitambo ya uchapaji kwa shabaha moja kuu ambayo ni: Kukuza vyombo vya habari katika Tanzania na Afrika.

Pili, siyo siri kwamba mashine za uchapaji kama iliyoko Printech, ziko pia katika nchi za Zambia, Lesotho, Botswana na Zimbabwe. Mipango iko njiani kuweka mashine kama hizo nchini Msumbiji.

Mradi huu muhimu wa kuinua uwezo wa wachapishaji wachanga kwa shabaha ya kukuza demokrasia, uko chini ya uangalizi wa Mfuko wa Kuendeleza Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika (SAMDEF – Southern Africa Media Development Fund).

Kwa vyovyote vile, Printech siyo mradi wa kutishiwa na yeyote anayetaka kufanya hivyo. Tunachapa MwanaHALISI katika kampuni hiyo kwa kuwa tunathamini msaada wa wanaothamini uhuru na ubora wa habari na vyombo vya habari kwa ujumla.

Wafadhili wa Printech, akiweno George Soros ambaye ni mwanzilishi wa asasi ya Open Society Institute (OSI), yenye matawi mengi duniani, watashangaa nchi hii kuona inataka kuharibu hata msaada mzuri kama huu, uliolenga kuleta ustawi na maendeleo kwa watu wote.

Katika MwanaHALISI tunajitahidi kunukuu jamii na watu wake kama wanavyotamka; kama wanavyoambiwa na kama wasemaji walivyosikika. Na katika hili hatuoni ubaya, kosa wala jinai. Tunaona fahari na faraja.

Ni matumaini yetu kwamba Printech haitayumba katika kufanya kazi iliyoundiwa na kutekeleza wajibu wake bila woga wala upendeleo.

Tuna mkataba wa kuchapa gazeti Printech. Tuna kanuni kwamba yaliyomo humo siyo lazima yawe maoni ya wachapaji. Msingi huo ukizingatiwa, na MwanaHALISI ikazingatia taaluma, ukweli na uaminifu, hakuna wa kuweza kutuyumbisha.

Nafarijika na kauli ya Meneja wa Printech, Richard Seni aliyoitoa kwa MwanaHALISI jana (26/09/2007), kuhusiana na vitisho kwake kutokana na kuchapa gazeti letu. Alisema kwamba hatasikiliza vitisho katika kutekeleza wajibu wake.

Hata hivyo bado hivi ni vita vikubwa kati ya pande mbili: Wale wanaotaka kuzima habari juu yao, wakati wakiwa katika ofisi za umma; na wale walioapa kuweka kwenye rekodi kila kinachosemwa ili wananchi wasome, waelewe, watafakari na waamue wenyewe. Katika hili, tukiungwa mkono pia na jamii, tutashinda. Ujumbe wetu kwa kila mmoja ni kwamba hatutaki chombo chenu kife.


Saed Kubenea
Mkurugenzi Mtendaji
Hali Halisi Publishers,
Dar es Salaam.

Nakala kwa:
- Meneja Mkuu Printech
- Mtendaji Mkuu SAMDEF – Botswana
- Mkurugenzi – MAELEZO
- Baraza la Habari Tanzania
- MISA-Tanzania
- Vyombo vya habari
- Ofisi za mabalozi wa nchi za nje
- Asasi za kijamii

Monday, September 24, 2007

Kandoro na ujenzi wa 'matundu' 822


(Makala hii itatoka katika gazeti la MwanaHALISI, Jumatano 26 Septemba 2007)
Na Ndimara Tegambwage

ABBAS Kandoro, mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam amejitafutia kibarua kikubwa. Naona ni kinene na kizito pia. Anataka kujenga matundu 822.

Kandoro anatafuta msaada kwa wakazi wa Dar es Salaam. Anataka wachange Sh. 10 bilioni ili aweze kukamilisha ndoto yake. Anataka kuthibitisha kuwa ameitikia kwa vitendo wito wa “kukuza elimu.”

Matundu ya Kandoro ni “madarasa.” Anataka kuhakikisha kwamba wanaomaliza Darasa la VII mwaka huu wanapata mahali pa “kuingia.” Anasema madarasa yaliyopo mkoani mwake hayatoshi.

Je, kwa kibarua hiki, Kandoro amepata au amepatikana? Tutajadili. Lakini kwanza tupate nukuu kutoka kwa Mwalimu Julius Nyerere. Alisema yafuatayo:

“Tunapoongelea kupanua elimu ya sekondari tunaharakisha sana kusema kwamba watu watachangia ujenzi kwa juhudi zao. Lakini majengo hayana umuhimu wa kwanza; vitu muhimu katika elimu ni walimu, vitabu na kwa sayansi, ni maabara.”

Je, Kandoro aliishasoma nukuu hii ya Mwalimu? Kusoma kunaweza kuwa kugumu. Je, aliishaisikia popote ikitajwa? Kumbuka hapa si Kandoro peke yake.

Je, Waziri Mkuu Edward Lowassa amewahi kukumbana na nukuu hii? Inawezekana ni zamani sana na sasa amesahau? Je, Baraza la Mawaziri ambako maamuzi makuu yanapita, linajua lolote juu ya matamshi ya Mwalimu?

Je, wataalam washauri katika masuala ya elimu nchini wamewahi kukumbana na kauli ya Mwalimu? Tukubali kwamba hawajawahi kusoma hayo. Je, utaalam walionao haujawahi hata siku moja kuwaelekeza kuwa “matundu” siyo elimu?

Je, inawezekana kadri miaka inavyopita, uwezo wa kufikiri wa viongozi unaendelea kushuka na kupotea kiasi kwamba hawawezi kuona na kuelewa hekima ya wazi?

Kandoro na timu yake wanataka kujenga matundu 822 katika mkoa wa Dar es Salaam. Mkuu wa mkoa anasema wanafunzi 58,304 wamefanya mtihani wa Darasa la VII na kwamba kati ya hao, 36,557 wanatarajiwa kuingia sekondari!

Mpaka hapa, hata kabla usahihishaji wa mitihani haujakamilika, tayari Kandoro na wenzake “wamepitisha” wanafunzi 36,557 kwenda sekondari; na sekondari zenyewe ndizo anatafutia fedha hivi sasa.

Sasa tujadili. Kuna mambo kadha wa kadhaa ya kuzingatia. Ujenzi wa matundu ambao Kandoro anautafutia fedha hauna tofauti na ujenzi wa awamu ya kwanza hapa Dar es Salaam na mikoani kote nchini.

Ni ujezi wa dharura. Ni ujenzi wa pupa. Ni bandika bandua. Ni kati-pa, kati-bandu! Umakini haba. Baadhi ya matundu yameanza kupata nyufa, miezi mitano tu tangu yajengwe.

Ni ujenzi wa matundu. Yale ambayo wanaoyajenga wanayaita madarasa. Nani hajasikia kilio cha wanafunzi jijini Dar es Salaam hivi sasa kwamba shule zao hazina vyoo na kwamba wanapiga foleni kwenda haja, tena na walumu wao?

Kandoro anasema fedha ziwe zimepatikana ifikapo Oktoba 31 mwaka huu. Ndipo waanze kujenga kwa kasi ya vibarua wa malkia wa nyuki. Mapema mwaka kesho, wanafunzi waanze shule.

Kandoro? Waanze shule bila walimu; alimradi watateua mwalimu mmoja na kumfanya Mwalimu Mkuu. Anachokulia kiko wapi? Bila vitabu. Bila madawati. Bila maabara.

Wiki iliyopita, wanafunzi kutoka Shule ya Sekondari Katende iliyoko Chato, Biharamulo mkoani Kagera, walimfuata Waziri Mkuu ziarani Geita, mkoani Mwanza, kumwambia kwamba tangu waende sekondari hawajapata mwalimu wa kuwafundisha.

Katende ziko nyingi; ziko kila kata, wilaya na mkoa, ambako ujenzi wa shule kwa pupa ya kuongeza idadi ya waenda sekondari umepewa jina la “kukuza elimu.”

Ongezeko la shule haliendani na ongezeko la walimu, vitabu, maabara na hata vyoo. Ni matundu tu ili kukidhi idadi wanayotaka watawala; idadi ya kupigia kampeni ili wapenda elimu waweze kuleta au kuongeza misaada. Basi.

Hii ina maana kwamba hapa hakuna elimu. Zinazoitwa shule panakuwa mahali pa kupigia soga. Ni “vijiwe” vya watoto ambao wangekuwa watu wa manufaa kwa nchi lakini wanashindia hadithi za kwenda “Bondeni” na “Majuu” – Afrika Kusini na Ulaya.

Na takwimu hizi za wingi wa matundu yanayoitwa madarasa, zinasambazwa dunia nzima kiasi kwamba hata juzi, Rais Jakaya Kikwete akiwa Marekani, alikabidhiwa Tuzo na asasi moja ya New York kwa, pamoja na mambo mengine, “mchango wa Tanzania katika kuboresha elimu.”

Akina Kandoro wanamdaganya nani? Mbona uwongo umevuka mipaka kiasi kwamba wao walioutunga, ukiwarudia wanaanza kuuamini?

Watawala wanajua mazingira ya kusoma hayapo na katika shule hizi hawawezi kupeleka watoto wao. Mtoto wa Kandoro hawezi kupelekwa katika shule iliyozungukwa na wavuta bangi kiasi kwamba walimu na wanafunzi wanavuta moshi na harufu ya bangi wakati wote wakiwa shuleni.

Na matundu wanayojenga kwa kasi, bila mazingira ya kuchochea hamu ya kusoma na bila zana, hayana tofauti na magenge ambako kila tabia ambayo jamii inaita “mbaya” inagawiwa bure kwa kila muhitaji.

Kinachoitwa elimu ni maangamizi. Kulundika watoto wa umri kati ya miaka 12 na 20, katika eneo ambako hakutolewi elimu na usimamizi wake hauashirii kuwepo nidhamu itokanayo na kazi, ni kuwaangamiza wakiwa na umri mdogo.

Lakini kinacholeta matumaini ni kwamba hata wazazi wameanza kuelewa. Mwaka jana, wazazi katika mikoa ya Shinyanga na Mara walikataa watoto wao kupanda darasa kwa madai kwamba hawakushinda.

Wakati watawala wanasema watoto wamefaulu, hivyo waendelee na masomo, wazazi wanasema watoto hawakushinda. Wanatoa hoja ambazo serikali haiwezi kuzipangua.

“Utasemaje watoto wetu wamefaulu na sasa waendelee na madarasa ya juu wakati hawajui kusoma na kuandika?” Wazazi wamehoji. Walimu wamebaki wameduwaa. Serikali imeziba macho kwa aibu.

Na Kandoro hataki kulaumiwa peke yake. Anataka wewe na mimi tushiriki maandalizi ya maangamizi kwa kizazi kijacho.

Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam anasema wakazi wa Dar es Salaam, wachangie ujenzi wa chapuchapu wa matundu 822 kukidhi mahitaji ya wanafunzi ambao tayari amesema lazima watakwenda sekondari.

Mtawala huyu wa Dar es Salaam amelenga hadi kwenye kaya ambako watawala wa serikali za mitaa watapita na kapu kuchangisha fedha kwa ajili ya mradi wake.

Bahati nzuri Kandoro hajataja adhabu atakayotoa au hatua atakazochukua kwa atakayekataa au kushindwa kuchangia mradi wake. Bado anasema ni hiari na watu wote wanajua serikali huwa haina hiari. Hiari iko kwenye asasi za kijamii.
Bali kuchangia ujenzi wa matundu; ambako walimu watakuwa wameokwa kwa wiki sita tu; pasipo na vitabu, madawati, maabara na vifaa vingine; kama ilivyo katika shule zake nyingi; hakika inataka moyo!

ndimara@yahoo.com
www.ndimara.blogspot.com
Simu: +255 (0) 713-614872

Friday, September 21, 2007

Wahujumu wa mbuga ya Serengeti

SITAKI

SITAKI watawala na matajiri wachache kutoka nje waangamize maliasili za Watanzania na jamii ya kimataifa, kwa kugeuza mbuga za wanyama kuwa miji.

Huu ni mpango wa kuua au kuhamisha au kufukuza wanyama, ndege, wadudu na hata kuharibu mazingira katika mbuga za wanyama.

Wasomaji, kupitia safu ya barua, katika magazeti mbalimbali, wamekuwa wakiuliza, “barabara za lami za nini katika mbuga za wanyama.”

Tujadili mbuga ya wanyama ya Serengeti. Mbuga hii ni tajiri sana wa wanyama. Humu kuna aina nyingi za wanyama na na baadhi ambao hawapatikani kokote kwingine duniani.

Serengeti ni maliasili ya taifa na dunia kwa ujumla; ni urithi wa vizazi na vizazi unaotokana na nguvu za asili. Bali, na ndivyo ilivyo, ni kivutio kikubwa cha watalii na chanzo cha mapato ya fedha kwa Tanzania.

Watu wa mafaifa mbalimbali wamekuwa wakija nchini kuona wanyama katika mbuga hii; na kila anayetoka huko anakuwa balozi wa Serengeti na Tanzania.

Sasa serikali imeamua kuruhusu matajiri kutoka nje kuingia Serengeti na kujenga hoteli kubwa kwa madai ya kuhudumia watalii.

Kuna walioanza kujenga hoteli. Kuna wenye mipango ya kujenga barabara za lami. Serikali imesema itaita matajiri wengine kuwekezaji katika hoteli katika mbuga.

Kana kwamba hiyo haitoshi, matajiri wanasemekana kuwa wameanza kujenga viwanja vya ndege ndani ya mbuga. Wanadai kuwa hiyo itarahisisha usafiri kwa wamiliki wa hoteli na watalii.

Huu ndio msiba mkubwa. Mbuga yetu, Serengeti, imevamiwa. Wanyama, ndege, wadudu na mandhari ya Serengeti, vimevamiwa.

Ni serikali iliyoruhusu uvamizi wa urithi wa Tanzania na dunia nzima. Kwa hatua hiyo, chanzo kingine cha mapato ya taifa kimevamiwa pia.

Matokeo ya uvamizi uliohalalishwa na serikali ni haya: Wakati wa ujenzi wa hoteli kunakuwa na mwingiliano mkubwa kwenye mbuga.

Magari makubwa, yaliyobeba vifaa vya ujenzi hupiga kelele nyingi na zinazofika mbali. Kelele hizi huwastua wanyama, ndege na hata wadudu waliomo katika mbuga.

Kelele hizi hutishia amani ya wanyama na uhai wao; husababisha watawanyike kwa hofu, na huweza kwenda mbali na hata wasiweze kurudi katika maeneo yao ya asili.

Kelele za binadamu, wale wajenzi wa hoteli ambao mara nyingi hupenda kufanya kazi zao kwa kuimba au kutoa sauti kubwa katika kuhimizana, ni tishio kwa wanyama.

Ujenzi wa barabara za lami huchukua muda mrefu. Kwa kipindi chote, huwa kuna mwingiliano wa magari na kelele zisizo za kawaida.

Shughuli zote hizi za ujenzi, ikiwa ni pamoja na ujenzi wa viwanja vya ndege husababisha wanyama kutawanyika na wasiweze kurudi walipokuwa.

Hawawezi kurudi walipokuwa awali kwa vile sasa kuna watu, kuna hoteli, kuna barabara zenye wingi wa magari; kuna wingi wa wasafiri na mazingira yamebadilika kabisa.

Lakini kuna tishio kubwa zaidi. Hili ni mingurumo ya ndege wanaotua kwenye viwanja. Kelele kali wakati wa kutua na kuondoka, hutishia wanyama na kuwasambaza zaidi wasiweze hata kurudi katika maeneo ya awali.

Uvamizi huu kwa wanyama na makazi yao unasababisha washindwe kutulia na kustawi; washindwe hata kuingiliana ipasavyo na kuzaliana. Hili linaweza kuchangia katika kupungua kwa idadi yao.

Ukweli mwingine ni kwamba wanyama wanaweza kutawanyika na kwenda nchi nyingine ya jirani; na Tanzania ikawa imepoteza, mara moja na milele, utajiri wake wa asili.

Hoja kubwa hapa ni kwamba watalii kutoka nje ya nchi wamekuwa wanakuja nchini kuona wanyama. Hawaji kulala kwenye hoteli kubwa na za kisasa kama zile zilizoko mijini.

Hapa kuna njama. Watawala na wawekezaji wanaharibu mifumo ya maisha ya wanyama; wanawatishia na kuwaondoa kwenye makazi yao; wanawahamishia hata nchi nyingine; halafu wanadai kuwa wanaendeleza utalii.

Waongo! Hakuna utalii. Kuna uharibifu wa makazi ya wanyama na mazingira kwa ujumla. Na hii haiwezi kuwa bure.

Mtu analazimika kuuliza, “Watawala wamelipwa nini na kwa kiasi gani ili waharibu maliasili ya nchi na dunia kwa ujumla?”

Sitaki kuamini kwamba penye barabara za lami; hoteli nyingi na kubwa na viwanja vya ndege na mingurumo angani, bado panaitwa mbuga ya wanyama.

Sitaki kuamini kuwa penye mwingiliano wa watu wengi wanaofanya shughuli mbalimbali, na siyo kuona wanyama katika utulivu wao, bado panaweza kuitwa mbuga ya wanyama.

Serikali na wawekezaji waroho wanaua maliasili ambayo ni urithi wa binadamu wote.

Kuna haja ya kuwaambia hapana! Sababu zipo: Wanayama hawahitaji barabara za lami, magari wala hoteli. Na watalii hawaendi Serengeti kuona barabara za lami, hoteli wala ndege. Wanakwenda kuona wanyama.

Kinachofanyika ni ukatili kwa wanyama, uchafuzi wa mazingira na uhujumu kwa maliasili ya Tanzania na binadamu wote. Tukatae hili.

(Itachapishwa Sept. 23 2007 katika Tanzania Daima Jumapili katika safu ya SITAKI)

Thursday, September 20, 2007

Jamii itatulinda

HOJA iko mezani. Viongozi 11 wametuhumiwa na vyama vya upinzani nchini kuwa wametenda, au wamesaidia kutenda au wamenyamazia hujuma na ufisadi nchini kwa kipindi cha miaka saba sasa.

Mwandishi wa habari wa gazeti hili alikuwa kwenye mkutano wa hadhara ambako wapinzani walitaja majina ya watuhumiwa wote, mmoja baada ya mwingine; bila kunong’ona bali kwa sauti ya juu na kwa kupitia vipaza sauti.

Kazi yetu kama chombo cha habari ni kusambaza taarifa hiyo, kama tunavyosambaza habari nyingine; kwa kuwaeleza wasomaji wetu nani alisema, alisema nini, alisemea wapi, alimsema nani na alikuwa akimwambia nani.

MwanaHALISI limefanya hivyo. Hii ni kwa kuzingatia msingi wa kuandika ukweli; kuandika kwa usahihi; likitekeleza haki na wajibu wake kwa jamii.

Lakini tangu tulipoandika majina ya watuhumiwa, tumekuwa tukipokea simu nyingi zikiuliza: Kwa nini mmemtaja mkubwa huyu? Ninyi hamuogopi? Mbona magazeti mengine yanasema watu hao hawapaswi kutajwa hadharani? Mbona yanadai sheria inakataza?

Ni kweli baadhi ya magazeti yameandika, tena siyo mara moja, kwamba hawataji majina ya watuhumiwa kutokana na misingi ya “taaluma na sheria.”

MwanaHALISI linaamini kwamba aliyetajwa Temeke, Dar es Salaam ndiye huyohuyo ambaye Mtwara, Pemba, Kyaka na Kigoma wanataka kujua. Kukataa kutaja jina ni kuendesha ushirikina katikakati ya teknolojia ya habari.

Wananchi waliokuwa kwenye mkutano jana; wakasikia majina yakitajwa na kurudiwa na leo wanaambiwa vyombo vya habari havipaswi kuyataja, wataelewaje vyombo hivyo?

Tunaamini kwamba wananchi wana haki ya kujua na vyombo vya habari vina haki ya kuwapa, kwa usahihi, kile kilichotendeka.

Kama kuna maadili ambayo yanazuia kuandika ukweli ni maadili ya wasiopenda ukweli na siyo uandishi wa habari. Kama kuna sheria inayozuia kuadika ukweli, basi hiyo ndiyo sheria ya kuasi haraka na mapema.

Taaluma ya habari ikifunikwa na siasa, kwa ngonjera na nyimbo za wasifu; na waandishi wa habari wakageuzwa mawakala wa mwanasiasa mmojammoja, haki ya watu ya kupata habari na taarifa itakuwa imezikwa.

MwanaHALISI halitaki kushiriki ushirikina wala njama za kuua haki, uhuru na wajibu wa mwandishi na jamii. Atakayetajwa hadharani ataandikwa. Na katika hili, jamii itasimama nasi.

(Tahariri ya gazeti la MwanaHALISI, toleo maalum juu ya ufisadi – kesho 21 Septemba 2007. Gazeti hili lilitaja majina yote 11 ya viongozi waliotuhumiwa ufisadi yakiwemo ya rais wa sasa Jakaya Kikwete na aliyestaafu, Benjamin Mkapa).

Wednesday, September 19, 2007

Rushwa inapokuwa mbeleko CCM

SITAKI kuamini kwamba rushwa ndiyo imekuwa mbeleko ya kubebea wagombea katika uchaguzi unaoendelea wa viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa ngazi zote.

Taarifa za vyombo vya habari zimejaa ripoti za utoaji rushwa kuanzia ngazi ya chini kabisa ya uongozi katika chama kilichoko ikulu, hadi nafasi za juu.

Kinachoendelea hivi sasa katika uchaguzi ni “nipe-nikupe” au “mzee kanituma” au “pokea salaam za Waziri au Waziri Mkuu” au “Mwenyekiti wa Taifa kanituma.”

Kwa hali ilivyo, hata wanaoogopa kuulizwa ushahidi, wanaweza kutoa kauli iliyo salama kabisa kuwa, “Tunaona wanachama, wagombea na mawakala wao wakigawa fedha katikati ya pilikapilika za uchaguzi.”

Lakini hakuna haja ya kukimbia neno “rushwa” kwani hutolewa na kupokelewa kwa aina na njia mbalimbali.

Rushwa inaweza kuwa kauli kwa njia ya ahadi; takrima kwa njia ya chakula na pombe; zawadi kwa njia ya nguo, baisikeli au hata gari; na fedha kwa maelekezo ya kujikwamua kiuchumi.

Yote haya yameonekana. Yamethibitika. Yamelalamikiwa. Mahali pengine yamezomewa na kulaaniwa. Ni rushwa.

Kilicho kigumu kuamini ni iwapo wanaotafuta uongozi kwa njia hii ya milungula, ndio haohao wanaotaka kuendelea kukaa ikulu na kutawala nchi hii. Hicho ndicho sitaki kuamini.

Nani hajasikia majigambo ya CCM, kila kukicha, kwamba “sera tunayotekeleza ni ya Chama Cha Mapinduzi ambacho kilipata ushindi wa kishindo?”

Tuulize taratibu, nani sasa, baada ya taarifa za kuaminika juu ya matumzi ya rushwa, ataweza kuchagua uzao wa mlungula kwa kishindo na kuukabidhi utawala?

Nani hajasikia CCM, sema viongozi wake, wakijigamba na kujitutumua mbele ya halaiki, kuwa watapambana na rushwa na kukariri msemo “rushwa ndiyo adui wa haki?”

Leo na kesho, baada ya ushahidi wa wazi, na ule wa kimazingira, juu ya utoaji na upokeaji wa rushwa, nani ataamini tena kuwa CCM inakiri kuwa “rushwa ndiyo adui wa haki?”

Na kukiri hakutoshi, kwani kunaweza kuishia kwenye kauli. Katika mazingira haya, nani atategemea CCM itende kufuatana na kauli yake ya kupambana na rushwa?

Kama uongozi wa chama kilichoko ikulu, utapatikana kwa njia ambayo wanachama na viongozi wake wengi wanajua au wanaamini, kuwa ni kwa rushwa, nani atatarajia mabadiliko kwa maana halisi ya maendeleo ya wananchi?

Nani atatarajia amani katika minyukano ya kupora raslimali za taifa; kuuza maliasili za wananchi na kunyang’anyana madaraka katika kuhudumia wawekezaji wa nje?

Kilio cha sasa cha rushwa hakitoki nje ya CCM. Kinatoka ndani ya chama hicho. Wenye nacho au wenye wajomba, wanatamba na kutesa. Wasionacho na mashabiki wao, wamenywea kama gugu lililong’olewa wakati wa kiangazi.

Na huu ni wakati mbaya sana kwa chama kilichoko ikulu kupata hata harufu ya rushwa. Hii ni kutokana na madai ya rushwa yaliyozagaa katika mikataba ya serikali, utendaji na maamuzi makuu ya watendaji serikalini.

Kwa uchaguzi uliojaa madai ya rushwa na hivyo kuleta watuhumiwa wakuu wa rushwa, nani sasa atachunguza IPTL, ule mradi ambao kutajwa kwake tu, hufanya waliokuwa wizarani na ikulu wakati huo, kupata tumbo la kuhara.

Kama viongozi waliochaguliwa na wanaoendelea kuchaguliwa wanapatikana kwa mtindo wa rushwa, nani atachunguza baba, mama na dada wa Richmond?
Nani, miongoni mwa watakaokuwa wamepatikana kwa rushwa anaweza kupendekeza uchunguzi juu ya matumizi mabaya ya ikulu; kule kuigeuza “meza ya sokoni?”

Nani, kati ya waliopatikana kwa mlungula, anaweza kupendekeza uchunguzi katika ununuzi wa ndege za jeshi zisizo za kijeshi; rada ya ndege iliyozeeka na ndege ya rais iliyoko “likizo?”

Atatoka wapi, miongoni mwa hao, ambaye atachunguza harufu ya rushwa katika mikataba ya madini, iliyosainiwa ndani na nje ya nchi?

Yuko wapi, miongoni mwao, atakayechunguza matumizi ya serikali, madai dhidi ya Benki Kuu (BoT), miliki ya maliasili kama misitu na mbuga ambavyo vyote vinaonekana kuwa mikononi mwa watu kutoka nje?

Nani atanyosha kidole kumtetea mkazi wa mwaloni Mwanza, Bukoba na Musoma ambaye hawezi kupata samaki kutoka Ziwa Viktoria, bali anaambulia mapanki?

Kilio cha wana-CCM wengi dhidi ya rushwa ndani ya chama chao, kina ujumbe mkubwa; kwani hakuna kilicho cha wana-CCM peke yao. Uporaji uliorasimishwa na uongozi uliotokana na rushwa, utaua wote – waliomo na wasiokuwamo.

Kinacholeta matumaini ni kwamba sauti nyingi za wanaolia, wanaolalama, wanaosuta na kulaani kinachotendeka sasa katika uchaguzi unaoendelea, ni za wanachama wa CCM.

Kwenye mtaji huu, ukiongeza sauti zilizoko nje ya chama hiki, hoja ya kukataa rushwa inaimarika katika jamii. Panapatikana mahali pa kuanzia kusema “Hapana” kwa rushwa na waliopatikana kwa rushwa.

Sitaki mtu adharau hatua hii kwa kusema ni ndogo tu. Ndio, ni ndogo, lakini ni hatua; tena hatua kwenda mbele.

(Imechapishwa katika Tanzania Daima, Jumapili 02 Septemba 2007)

Uchumi wa Tanzania utakua lini?

SITAKI kuamini sababu za watawala wa Tanzania za kutotaka kuingia haraka katika Shirikisho la Afrika Mashariki.

Ni kwa sababu hizo Uganda inasema wanaotaka na walio tayari waendelee na shirikisho. Hii ina maana kwamba wenye woga, mashaka na kutojiamini, watajiunga na shirikisho hapo baadaye.

Na sababu za Tanzania kutojiunga na shirikisho katika mpango wa kasi ni dhaifu sana. Eti Tanzania “inapenda sana kujiimarisha kwanza kiuchumi” ndipo isonge mbele.

Maswali: Nani alichelewesha Tanzania kuimarika kiuchumi? Nani ana uhakika kwamba uchumi wa Tanzania utaimarika leo, kesho au keshokutwa? Kuimarika kiuchumi kuna maana gani; ni kufikia viwango vya Kenya au Uganda?

Lakini swali na suala kubwa hapa ni: Nani anajua kuwa uchumi wa Tanzania haujawa imara? Ni rais na mawaziri wake au hata wananchi kwa ujumla wao wanajua hivyo?

Je, wananchi wanajua nchi yao ilipofikia katika maendeleo kwa kulinganisha na Uganda na Kenya au wanaambiwa na rais na wanasiasa, tena kwa kauli zinazotafuta kuungwa mkono?

Je, katika kura ya maoni, wananchi waliposema hawataki shirikisho lije haraka, walikuwa wanajua shirikisho la kisiasa ni nini au maoni yao yalikuwa juu ya kukataa kile ambacho hawakijui?

Nani alitegemea wakazi wa miji midogo na vijiji, ambao hawajui wala hawajawahi kuelezwa lolote juu ya jumuiya, kukubali kuingizwa katika kile ambacho walikuwa hawajui?

Je, si kwa kukataa shirikisho kwa njia ya haraka, wananchi walikuwa wanawaeleza watawala kuwa watawala hawajafanya kazi ya kuelimisha umma juu ya shabaha na matunda ya shirikisho?

Nani atakataa kwamba maoni juu ya shirikisho ulikuwa mtihani wa watawala kwa watahiniwa, ambao ni wananchi; lakini wanaoleta mtihani walikuwa hawajawahi kufundisha hata kidogo?

Kama hujafundisha, lakini umetunga mtihani, kwa nini usieleweke kuwa umedhamiria watahiniwa wote washindwe isipokuwa wale waliokuwa na mawasiliano nawe au wenye uwezo wa kupata elimu kwa njia tofauti?

Lakini katika hili, mawaziri wa serikali ya Rais Jakaya Kikwete walizunguka nchi nzima kueleza umuhimu wa kuingia katika shirikisho haraka.

Je, mawaziri waliokuwa wakiendesha kampeni kuwataka wananchi wakubali mpango wa haraka, hawakubaliani na Rais Kikwete?

Je, mawaziri hao hawajui au hawakujua hali ya uchumi wa Tanzania kiasi kwamba wanapingana na rais wao? Na kama mawaziri wanapigana na rais, wanatafuta nini katika nafasi zake za uteuzi?

Kama kweli Rais Kikwete anajua, anaamini na kukiri kuwa sharti Tanzania ijiimarishe kwanza kiuchumi ndipo iingie shirikisho, kwa nini bado anakumbatia mawaziri waliokuwa wanapingana naye?

Au tudadisi zaidi, ni lini Kikwete alijua kwamba Tanzania haijaimarika kiuchumi; kabla ya kuagiza maoni na kutoa ajira kwa wakusanyaji maoni au baada ya maoni kutangazwa?

Rais Kikwete alikuwa mmoja wa viongozi wa Afrika Mashariki walioketi na kuamua wananchi waulizwe juu ya shirikisho la haraka au la polepole.

Kama kweli utawala wake unasema kile unachoamini, kwa nini hakujua au hata kushauriwa mapema, kwamba uchumi wa Tanzania haujaimarika na hivyo hakuna haja ya shirikisho kwa njia ya haraka?

Ukichunguza kwa makini, utaona kwamba kuna sababu nyingine, na tofauti kabisa, za Rais Kikwete kukataa shirikisho kwa njia ya haraka. Zipo. Aziseme mwenyewe. Hakuna wa kumsemea.

Tuulize tena: Hivi kigezo kikuu cha kuingia Shirikisho la Afrika Mashariki ni kuwa na uchumi ulioimarika na siyo kuunganisha wananchi na hali zao za kiuchumi za wakati uliopo?

Shirikisho la kisiasa hujenga mazingira sare kisiasa kwa wanachama husika ambayo huchochea uhuru, utashi na kutoa fursa sawa kwa watu na taasisi zao kujituma na kujiendeleza ili kujenga na kuimarisha uchumi.

Shirikisho, katika hali yoyote ile ya kiuchumi, linaweza kukuza na kuimarisha uchumi wa nchi na watu wake, wakati jeuri ya uchumi imara peke yake inaweza kuleta mgawanyiko.

Hapo ndipo Rais Yoweri Museveni wa Uganda anaona arudie maoni yake ya awali kabisa, kwamba walio tayari kwa shirikisho waanze; wasio tayari watakuja baadaye.

Sitaki wanaotaka shirikisho wasubiri wale ambao hawana kalenda ya kuwa na uchumi imara.

Mara baada ya vita dhidi ya dikiteta Idi Amin Dada, rais alitangaza miezi 18 ya “kufunga mikanda” ili kurejesha uchumi katika hali nzuri.

Miezi hiyo ilipomalizika, serikali ikatangaza miezi mingine 18. Hali iliposhindikana kubadilika, watawala wakaacha kusema lolote juu ya miezi ya kufunga mikanda. Mikanda ikafungwa hadi leo.

Katikati ya ubadhilifu, ufujaji wa maliasili na raslimali za nchi, mikataba ya kinyonyaji, wizi wa moja kwa moja wa fedha za umma, rushwa na ukosefu wa ajira, hakuna awezaye kutabiri lini uchumi imara utapatikana.

Acha wanaotaka haraka Shirikisho la Kisiasa la Afrika Mashariki waanze. Wenye mikongojo wataingia siku watakapowasili mjini, mradi milango iko wazi, lakini huenda kwa gharama zaidi.

Na ubishi kuhusu hili unaweza kupandikiza mbegu ya chuki miongoni mwa mataifa ya Afrika Mashariki na hatimaye uhasana ambao utakuwa mgumu kuung’oa.

(Safu ya STAKI huandikwa na Ndimara Tegambwage na huchapishwa na Tanzania Daima, Jumapili. Makala hii ilichapishwa 16 Septemba 2007)

Mchango wa msomaji
Hongera sana kwa makala. Swali la nyongeza: Wakati Tanzania inaimarisha uchumi wake je, Kenya na Uganda watakuwa wamekaa wanaisubiri ijiimarishe? Je, ni haki uzembe wetu uwacheleweshe wao? Je, uchumi wetu usipoimarika mapema itakuwaje? Na je, uchumi wetu ukipanda wa kwao ukashuka, itakuwaje?

By Maswi, Bunda, Mara
Simu: +255 (0) 784477900

Saturday, September 1, 2007